domingo, 15 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 33 YA MWAKA-B

JUMAPILI WIKI YA 32 YA MWAKA-B
15/11/2015
Somo I: Dan 12:1-3
Zab: 16:5, 8, 9-10, 11
Somo II: Ebr 10:11-14, 18
Injili: Mk 13:24-32
Nukuu:
Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile,” Dan 12:1

Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele,” Dan 12:2 

Na walio na hekima watang'aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang'aa kama nyota milele na milele,” Dan 12:3

Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake,” Ebr 10:12-13 

Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa,” Ebr 10:14

Lakini siku zile, baada ya dhiki hiyo, jua litatiwa giza, na mwezi hatautoa mwanga wake. na nyota za mbinguni zitakuwa zikianguka, na nguvu zilizo mbinguni zitatikisika. Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni kwa nguvu nyingi na utukufu,” Mk 13:24-26

Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatimie,” Mk 13:30 

Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Mk 13:31 

Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba,” Mk 13:32 

TAFAKARI: “Mwisho wako utategemea ishi yako leo na sasa.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 33 ya Mwaka “B” wa Kanisa. Masomo yote matatu yanatupa viashirio vya nyakati za mwisho na hukumu yake. Kama tunavyokaribia kumaliza mwaka “B” wa Kanisa ni vyema pia kutafakari ukweli kuhusu mwisho wa nyakati, na hukumu ya kila mmoja wetu mbele ya Mungu aliye Upendo, Haki, Msamaha, Huruma, na Uvumilivu. Sifa zote hizi za Mungu hazionekani tu mwisho wa nyakati, bali zipo na zinaonekana kila sekunde, dakika, saa, siku, wiki, mwezi, na  mwaka hadi mwaka unapoivuta pumzi aliyokupa kwa kukupenda, kukuchagua, na kukuumba uwe kwa sura na mfano wake mwenyewe. Hakika sidhani kama kuna upendo na upendeleo wa Mungu kwetu kama huu.

Hivyo wapendwa katika Kristo, jambo la kwanza leo Mama Kanisa anatutaka kwa upendo huo huo wa Mungu, tuelewe kwamba muda tuliopewa kuishi ni leo na sasa, mwisho wake ni siri ya Mungu mwenyewe. Na kama mwisho wa muda huo ni siri yake Mungu mwenyewe nasi hatuna ufahamu juu yake, jambo la pili na la muhimu ni kwamba, mwisho wako utategemea ishi yako leo na sasa. Mungu wetu ni Upendo na haki, Msamaha, huruma na Uvumilivu. Kwa mantiki hii, Mungu wetu hawezi kamwe kutuwazia lililo baya. Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Tunahitaji hekima hii ya Mungu kujua ukweli huu. Na hekima ya Mungu wetu ni kule kuwa na hofu naye. Hofu hii ya Mungu itatuongoza katika pendo na haki ya Mungu, Msamaha, Huruma na Uvumilivu wa Mungu. Wenye kusimama katika kweli hii hadi mwisho ndiyo watakao ng’ara mbele za Mungu. Na walio na hekima watang'aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang'aa kama nyota milele na milele,” Dan 12:3. Je, unahitaji kwenda chuo kikuu kujua ukweli huu? Ni nani basi kati yetu asiyekuwa hata na chembe ya upendo wa Mungu ndani yake?

Wapendwa wana wa Mungu, habari za nyakati za mwisho zinatisha sana kwa yule asiyejua matumizi ya muda wake, yaani, leo na sasa, na malengo mazima ya maisha yake hapa duniani. Nabii Danieli anatuambia hali ya mambo itakavyokuwa siku hiyo ya mwisho. Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile,” Dan 12:1. Atakayeokolewa ni yule ambaye jina lake lipo kwenye kitabu cha uzima. Kitabu hiki cha uzima kipo Mbinguni, ila nakala yake unayo, na unatembea nayo kila siku. Kitabu hiki cha uzima yanaandikwa yale mazuri tu uyafanyayo kila upewapo pumzi ya kupumua na aliye kuumba kwa kukupenda na kukuchagua. Na kitabu hiki ulipewa siku ile ya ubatizo wako kabla ya kupewa mshumaa uwakoa na kuzibuliwa masikio ili usike neno lake na mdomo ili uungame imani ya Kristo.

Pia kitabu hiki ulipewa mara baada ya kumwagiwa maji ikiwa ni ishara ya kuvushwa kuelekea nchi ya ahadi (kufa na kufufuka na Kristo), na baadaye kupakwa mafuta ya Krisma ili uunganike na taifa lake Mungu kuwa kiungo cha Kristo; kuhani, nabii, na mfalme, hadi upate uzima wa milele mbinguni. Mbatiza wako alipokupa kitabu hiki aliyatamka maneno haya: “F…(Edgar) umekuwa sasa kiumbe kipya na kumvaa Kristo. Nguo hii nyeupe iwe ishara ya cheo chako. Nawe ukisaidiwa kwa maneno na mifano ya jirani zake, ukaifikishe safi katika uzima wa milele mbinguni,” Misale ya Waamini, toleo la 1996, uk 933.

Nabii Danieli anaendelea kutupa ukweli kuhusu siku ya mwisho kwa kusema, Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele,” Dan 12:2. Waliolala katika mavumbi ya nchi wataamka, yaani makaburi yatafunguka na watayaacha makaburi yao na kuingia uzima wa milele. Mimi na wewe tunayeyapuuzia haya na kuona ni kama hadithi tu za akina Abunuasi, tutaingia katika aibu ya kudharauliwa milele kwa sababu tu ya kutokuwa makini kwa yale tuliyoyapokea siku ya ubatizo wetu, yaani kuishi ahadi zetu za ubatizo.

Jambo hili alisemalo Nabii Danieli halina tofauti na ukweli anaotuambia Yesu leo katika Injili, yaani, habari njema ya wokovu wetu. Yesu anatuambia leo, Lakini siku zile, baada ya dhiki hiyo, jua litatiwa giza, na mwezi hatautoa mwanga wake. na nyota za mbinguni zitakuwa zikianguka, na nguvu zilizo mbinguni zitatikisika. Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni kwa nguvu nyingi na utukufu,” Mk 13:24-26. Je, Mwana wa Adamu ni nani katika hukumu hii? Ni kwa makusudi makubwa kabisa ‘NENO’ aliyefanyika mwili na kukaa kwetu, yaani Yesu, awe mpatanishi wetu na Mungu. Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni,” Kol 1:19-20. Huu ndio uwezo na mamlaka aliyokuwa nayo Mwana wa Adamu, yaani Kristo Yesu. Je, waweza kukwepa hukumu hii?

 Wapendwa katika Kristo, mara nyingi tunapoambiwa habari hizi hufikiri hazituhusu na wapo wanaoambiwa na siyo sisi. Twafanya hivyo kwa sababu tunajihesabia haki pasipo haki. Yesu anaweka bayana ukweli huu na kusema, Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatimie,” Mk 13:30. Kwa maana hiyo, Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Mk 13:3. Je, ndugu yangu utabadili njia yako mbaya kwa kusikia maneno haya kutoka mbinguni na kwa malaika? Ukweli wa lini litatokea jambo hili hakuna anayejua, ila mwisho wa nyakati lazima utafika. Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba,” Mk 13:32. Kama jambo hili limefichwa kwetu na ufahamu wetu hauwezi kujua, tufanye nini sasa ili tuwe njia salama?

Ndugu zangu, kwanza kabisa ili niwe njia iliyo salama itanipasa kila sekunde ninayopewa pumzi na Mungu nihesabu nimepewa hiyo tu kwa kujiandaa na umilele. Jambo la pili, inanipasa kuanzia sasa nitazame upya mahusiano yangu na Mungu, Wenzengu, hasa jirani zangu,  na Mazingira yanayonizunguka. Swali la kujiuliza katika jambo hili la pili ni hili; Je, kwa uhusiano huu nilionao kuna mwelekeo wa kuifikia mbingu?

Mtume Paulo anatupa namna ya kuishi kuielekea mbingu na uzima wake. Naye anasema, Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu,” Flp 3:12. Kila siku uliyopewa na Mungu ni siku ya kuimarisha uhusiano wako na Mungu, jirani zako, na mazingira yako. Huku ndiko kukaza mwendo ukiyachuchumilia yaliyo mbele, yaani, uzima wa milele, kwenye mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo. Paulo Mtume anatuambia,  “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu,” Flp 3:13-14. Je, una haki au sababu yoyote ya kujihesabia haki mbele ya Mungu kwa mazingira na hali uliyo nayo sasa? Ni Mungu tu ndiye atuhesabiaye haki kadiri ya Upendo na Huruma yake kwa sababu ndicho alicho.

Ndugu zangu katika Kristo Yesu, tunalo kimbilio moja tu katika mkwamo huu wa sintofahamu kuelekea uzima wa milele. Yesu Kristo ndiye jibu letu. Yesu ananiambia mimi na wewe kwamba, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Kumbe bado haujachelewa kufanya mabadiliko katika maisha yako. Kubadili njia yako mbaya ni leo na sasa. Mimi na wewe yatupasa kujenga uhusiano mzuri na Kristo Yesu “Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake,” Rum 5:10. Kwa sadaka yake pale msalabani sote tumehesabiwa haki na kuwa warithi wa ufalme wa Mungu. Kwa sababu, huyu alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake,” Ebr 10:12-13. Leo sadaka hiyo ni adhimisho la Ekaristi Takatifu. Mama Kanisa kama Sakramenti ya wokovu wetu anaadhimisha Sakramenti hii ya Misa Takatifu kwa wokovu wangu na wako na wale wote wanaomridhia Mwana wa Mungu. Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa,” Ebr 10:14. Je, hutaki kutakaswa kwa adhimisho hili la Ekaristi Takatifu? Je, walichukuliaje adhimisho hili la Ekaristi Takatifu unapopata nafasi ya kushiriki? Ndugu yangu, uwe mlei, mtawa, mtawa na mkleri, au mkleri, usifanye jambo hili kwa mazoea. Ni nafasi ya pekee sana katika maisha yako.

Theresia Midu alikuwa mhudhuriaji mzuri sana wa Misa Takatifu kila siku na Jumapili. Adhimisho la Misa kwake lilikuwa na maana tu kwenye kushiriki mwili na damu ya Yesu. Mara baada ya tendo hili huondoka na kuelekea kwenye biashara yake ya kuuza genge sokoni. Neno la Mungu, na Baraka ya mwisho wa Misa baada ya Matangazo haikuwa na maana yoyote kwake kiibada.

Muda ulipita na mwisho wa maisha yake ulifika. Kwa jinsi alivyoishi hapa duniani na hasa moyo wake wa kuudhuria Misa kila siku hakuwa na shaka ya kuiona mbingu. Je, mambo yalikuaje huko mbele ya safari?

Mbele ya kiti cha hukumu akiwa Mungu na Yesu Mthibitisho wa kila aliyepita kwenye hukumu hii, na msema neno la mwisho kwa vile alitujua kama tulivyo, na Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake. Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake,” 1Pet 2:21-22
.
Hivyo ilipofika zamu ya Theresia, Malaika Michaeli alitumwa alilete kalabrasha lake. Kwa kawaida kwenye kalabrasha hili huandikwa yale mema tu uliyofanikiwa kuyafanya wakati wa uhai wako. Kwa bahati mbaya kuanzia mwanzo wa ukurasa wa kwanza hadi wa mwisho hakuna kilichokuwa kimeandikwa zaidi ya nukuu ya angalizo. Nayo ilikuwa inasema hivi: “alihudhuria sadaka ya Misa Takatifu kama wajibu na alimpokea Mwana wa Adamu kwa kipindi kile kile alichokuwa Kanisani na baada ya hapo alimwacha kule kule Kanisani. Hakuondoka naye kwa sababu hakuisubiri Amani na Baraka ya mwisho ambacho ndicho kielelezo cha upatanisho wa wanadamu na wewe Mungu Baba kwa kupitia Mwanao Yesu Kristo. Kwa mantiki hii hana mastahili yoyote kwenye uzima huu wa milele. Zaidi rejea kwenye kitabu cha uzima kwa taarifa zake zaidi.” mwisho wa kunukuu. Malaika Michaeli alilifunga kalabrasha lile.

Basi kitabu cha uzima kililetwa, na Yesu alikifungua. Kwenye kitabu kile walikuwa akina Theresa wengi, mfano Theresa wa Calcuta, Theresa wa Mtoto Yesu, ila Theresa Midu hakuwepo kwenye Kitabu hiki cha uzima. Ndipo Mwana wa Adamu, yaani Yesu akamwambia, “Theresa Midu, tatizo lako hukuishi ahadi zako za ubatizo. Ulipewa muda wa kutosha kabisa, na kila mara niliingia ndani yako uliposhiriki mwili na damu yangu, ila hukupenda nibaki nawe. Uliniacha na kuwahi biashara zako na genge lako. Vyumba vipo vingi kama unavyoona katika ufalme huu. Akina Theresa wote wamepata vyumba katika ufalme huu ila wewe huna nafasi mahali hapa,” Yesu alimweleza yote bila kuficha neno. “Je, niende wapi, au wapi nilipoandaliwa?” Theresa Midu alimuuliza Yesu. Fuata njia hiyo yenye watu wengi na barabara yake ni pana huko ndipo kwenye kulia na kusaga meno, Mt 13:50. Wapendwa wana wa Mungu, hii ndiyo adhabu ya kudharauliwa milele.

Tumsifu Yesu Kristo!


Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo nililolinena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho,” Yoh 12:48

No hay comentarios:

Publicar un comentario