domingo, 22 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 34 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 34 YA MWAKA-B
23/11/2015
Somo: Dan 1-6, 8-20
Zab: Dan 3:52, 53, 54, 55, 56
Injili: Lk 21:1-4
Nukuu:
Naye mfalme akazungumza nao; na miongoni mwao wote hawakuonekana waliokuwa kama Danielii, na Hanania, na Mishaeli, na Azaria; kwa hiyo wakasimama mbele ya mfalme,” Dan 1:19

Na katika kila jambo la hekima na ufahamu alilowauliza mfalme, akawaona kuwa walifaa mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake,” Dan 1:20

Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo,” Lk 21:3-4 

TAFAKARI: “Kuwa kile ulicho na jitoe bila kujibakiza, ndivyo apendavyo Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, Danielii, Hanania, Mishaeli na Azaria ni vijana waliowekwa katika majaribia kama kweli wanaweza kutumika katika ufalme wa Mfalme Nebukadreza. Kama ilivyokawaida, wale waliokuwa viongozi katika nyumba za kifalme walikuwa matoashi wa kufanywa, yaani waliasiwa ili walishikwe na ashiki ya kutamani wake wa mfalme. Ndugu hawa, yaani Danielii, Hanania, Mishaeli na Azaria walikuwa Wayahudi ambao waliishika vyema torati. Hivyo mapendekezo ya Mfalme kwa wao kula chakula cha kifalme ikiwa ni pamoja na divai aliyokunywa ilikuwa ni najisi kwao. Hivyo wanaomba kula mtama tu. Vijana hawa wanaishinda tamaa yao na kuwa kile walicho. Afya yao iliboreka na kupendeza machoni mwa Mfalme.

Vijana hawa wanakuwa huru juu ya ushawishi si kwa vile hawapendi kushawishika, ila kwa vile wameamua kusimama katika kweli. Kweli ya Mungu utufanya kuwa huru. “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh 8:32. Kweli hii inawafanya vijana hawa wawe kile walicho na kumpendezesha mfalme. Naye mfalme akazungumza nao; na miongoni mwao wote hawakuonekana waliokuwa kama Danielii, na Hanania, na Mishaeli, na Azaria; kwa hiyo wakasimama mbele ya mfalme,” Dan 1:19. Hakuna aliyekuwa kama vijana hawa kwa vile hawakuisaliti kweli.

Wapendwa wana wa Mungu, ukiwa mpenda kweli Mungu atakupigania hata pale watesi wako watakapoonekana kutokutenda haki juu yako. Mungu uigeuza midomo lenye kulaani na kuwa midomo ya baraka unaposimama katika kweli. Mfano mzuri ni maisha ya shujaa wa Afrika ya Kusini, Nelson Mandela. Vinywa vile vilivyomwona kuwa ni gaidi na muhaini na kumfunga kwa miaka 27, ni vivyo hivyo hivyo vilivyosadiki kuwa mtu huyu ni shujaa na anastahili kuwa huru. Hivyo, Na katika kila jambo la hekima na ufahamu alilowauliza mfalme, akawaona kuwa walifaa mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake,” Dan 1:20. Vijana hawa wanaonekana washindi si kwa uzuri wa mwono wao, bali kwa vile walisimama katika kweli bila kudondoka. Mungu aliye hai anakuwa mtetezi wao.

Kusimama katika kweli na kujitoa bila kujibakiza ndiyo mfumo aupendao Kristo hasa pale tunapoishi katika mazingira ya kubaguana kutoka na hali na historia zetu. Katika utoaji wa sadaka, mwanamke mjane anahesabiwa haki kwa tendo la kujitoa bila kujibakiza. Yesu Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo,” Lk 21:3-4. Je ndugu yangu umejitoa vilivyo? Ni katika kutoa bila kujibakiza kunakuwa silaha za haki. Hivyo, “wala msiendelee kuvitoa viungo vyenu kuwa silaha za dhuluma kwa dhambi; bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa, na viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha za haki,” Rum 6:13. Ndugu yangu, “kuwa kile ulicho na jitoe bila kujibakiza, ndivyo apendavyo Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mt 20:28


No hay comentarios:

Publicar un comentario