JUMATATU WIKI YA 27 YA MWAKA-B
5/10/2015
Somo: Yon 1:17, 2:10
Zab: Yon 2:3-5, 8
Injili: Lk 10:25-37
Nukuu:
“Ondoka,
uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukapige kelele juu yake; kwa maana uovu wao
umepanda juu mbele zangu,” Yon 1:2
“Naye
akawaambia, Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari itatulia; kwa maana najua
ya kuwa ni kwa ajili yangu tufani hii imewapata,” Yon 1:12
“Bwana
akaweka tayari samaki mkubwa ili ammeze Yona, naye Yona akawa ndani ya tumbo la
samaki yule muda wa siku tatu, mchana na usiku. Bwana akasema na yule samaki,
naye akamtapika Yona pwani,” Yon 1:17, 2:10
“Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” Lk
10:25
“Akajibu akasema, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako
wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na
jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27
“Akamwambia, Umejibu vema; fanya hivi nawe utaishi,” Lk 10:28
“Akasema, Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia,
Enenda zako, nawe ukafanye vivyo hivyo,” Lk 10:37
TAFAKARI: “Fanya hivi nawe utaishi
milele.”
Wapendwa wana wa Mungu,
pamoja na mbwembwe zote za mwanadamu hapa duniani, ni wajibu wa kila mmoja wetu
kujiuliza swali hili la msingi alilouliza mwana-sheria mmoja wa Kiyahudi kwa
Yesu kuhusu uhai. Mwana-sheria huyu anamuuliza Yesu hivi; “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”
Lk 10:25. Msingi wa swali hili haupo kwenye uhai tu wa leo na kesho, bali uhai
katika umilele wake. Tuelewe kwamba mwanadamu ameumbwa kuishi milele, na hayo
ndiyo makusudi ya Mungu katika uumbaji wa mwanadamu. Tatizo kubwa la mwanadamu
ni mbwembwe nyingi alizokunazo akisahau kuwa muda aliopewa hapa duniani
hausimami kumsubiri. Mhubiri anatuwasa na kusema, “ mwanadamu hadumu katika
heshima, bali amefanana na wanyama wapoteao,” Zab 49:12. Fahari ya mwanadamu ni
yule aliyemuumba, yaani Mungu wake. Mengine yote ni mbwembwe tu! “Mche Bwana, Mungu wako, umtumikie yeye; ambatana naye, na kuapa
kwa jina lake. Yeye ndiye fahari
yako, na yeye ndiye Mungu wako, aliyekutendea mambo haya makubwa, ya kutisha,
uliyoyaona kwa macho yako,” Kum 10:20-21. Ndugu unayesafiri nami katika
tafakari hii, elewa kwamba utajiri wako, ufahamu wako (kiwango cha elimu ulicho
nacho), umaarufu wako, nk, bila Mungu ni bure kabisa.
Yesu
kabla ya kumjibu vizuri mwana-sheria yule wa kiyahudi alitaka kujua uelewa wake
wa Maandiko Matakatifu (Torati) yanasema nini kuhusu uhai wa Milele.
Mwana-sheria yule akamjibu kwa staha, “Mpende
Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako
zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako,” Lk 10:27. Yesu
anaridhika na jibu hili na amamwambia hivi; “Umejibu vema; fanya hivi nawe
utaishi,” Lk 10:28. Kuishi kwetu hapa duniani ambapo kunatupelekea kuishi
milele baada ya kifo kama wanadamu kwatuwajibisha kufanya kwa weledi mkubwa
mambo makuu mawili.
Moja, mpende Mungu wako kwa moyo wako wote, roho yako yote,
na nguvu zako zote. Kwa maana nyingine ni kutumia vyote Mungu alivyokujalia ili
umpende na ubaki kumpenda daima. Afya yako njema, akili yako ya pekee, utajiri
wako, na umaarufu wako hapa nduniani isiwe sababu ya kujitenga na upendo huu wa
Mungu. Hayo Mungu aliyokujalia kwa namna ya pekee isiwe sababu ya kuwakejeli
wenzako ambao kwa mtazamo wako wa kibinadamu waona hawastahili mema yoyote
mbele ya uso wa Mungu. Ndugu yangu, hata yale tunayoyaona kwa macho yetu kama
udhaifu wa mtu na wengine, Mungu wakati mwingine utumia udhaifu huo
kutufundisha siri ya maisha na uhai tuliopewa na Mungu mwenyewe. Maisha na uhai tuliyonayo ni mali na zawadi yake
Mungu. Mimi na wewe tumepewa uhai huu na kuazimwa kwa muda tu hapa duniani kama
sababu ya kuutumia vyema uhai huu ili tuishi milele baada ya muda ambao kila
mmoja wetu kapewa kadiri ya mapenzi yake Mungu. “Maana siku zangu zinatoweka
kama moshi, Na mifupa yangu inateketea kama kinga,” Zab 102:3.
Pili, nimpende jirani yangu kama nafsi yangu. Jirani yangu
ni yeyote yule ninayekutana naye na wale wote wanaonizunguka, yaani, wahitaji
na wasio wahitaji. Jirani yangu ni kama kioo cha kujitazama ukamilifu wangu
mbele ya Mungu. Je, udhaifu wa jirani yangu unasema nini kuhusu maisha yangu
mimi niliyejiinua na kujiona safi na mwema kuliko wengine? Yesu, anakemea hali
hii kwa Mafarisayo na Waandishi, na kwetu pia. “Waandishi na
Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi,
yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo
yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi,” Mt 23:2-3. Mtazamo huu wa
ugeugeu na kujiinua mbele za Mungu pasipo mastahili yoyote ndio sababu ya mfano
wa Msamaria mwema. Wafarisayo ambao kwa kiasi kikubwa walijiinua na kuwa wepesi
kuwahukumu wengine, wanashindwa kuokoa uhai ambao ni mali na zawadi ya Mungu
kwa vile tu muhitaji huyu mhusika hakuwa Myahudi. Wakati mwingine tunashindwa
kusimama katika kweli kwa vile tu mhusika siyo kutoka familia yetu, ukoo wetu,
kabila letu, au kutoka Kanda yetu. Wenye mitazamo kama hii ilihali wanajiita
wafuasi wa Kristo, basi Kristo huyo huendelea kusulubiwa kwa matendo yao.
Kristo huyo siyo fahari ya maisha yao. Mimi na wewe kama wafuasi wa Kristo
hatuna kitu kingine cha kujivunia zaidi ya Msalaba wa Kristo. “Lakini mimi, hasha,
nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo,
ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14.
Je, tusikemee maovu? La hasha! Mkemeapo “Basi, wekeni mbali uovu wote na hila yote, na unafiki na husuda
na masingizio yote. Kwa sababu
ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia
kielelezo, mfuate nyayo zake. Yeye
alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi
kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye
mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa
mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa,”
1Pet 2:1, 21, 23-24. Je, nauona udhaifu wangu ninapoutazama udhaifu wa mwingine?
Wapendwa
wana wa Mungu, Yesu anapomwambia mwana-sheria yule afanye tathimini kati ya
wale wayahudi na yule Msamaria aliyetoa msaada kwa mhitaji yule aliyepata
kipigo na wanyang’anyi, mwana-sheria anaelewa soma lile na kumjibu Yesu, “Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia, Enenda
zako, nawe ukafanye vivyo hivyo,” Lk 10:37. Wapendwa yatupasa kusimama katika
kweli na haki, hivyo tutende yote kwa upendo na huruma ya kweli. Tusipolifanya
jambo hilo basi tujiandae kusutwa na dhamiri zetu katika umiele wote.
Tunaona Nabii Yona anasutwa na dhamiri yake pale anapokataa
kusimama katika kweli na haki kuupeleka ujembe wa wokovu kwa watu wake. Baada
ya kugundua yeye ndiye tatizo la kuchafuka kwa baharí anakiri udhaifu huo na
kuhamuri haki ya Mungu itendeke. Naye anatoa suluhu la tatizo na kuwaambia, “Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari
itatulia; kwa maana najua ya kuwa ni kwa ajili yangu tufani hii imewapata,” Yon
1:12. Ukweli wa Mungu, haki ya Mungu, na upendo wake kwetu hatuwezi kuubadili
kama kweli Mungu anapenda kumtumia mmoja kati yetu licha ya udhaifu wa mtu
huyo. Haki hii, kweli hii, na upendo huu wa Mungu unajidhihirisha katika agizo
hili analopewa Nabii Yona. “Ondoka,
uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukapige kelele juu yake; kwa maana uovu wao umepanda
juu mbele zangu,” Yon 1:2. Hili ni agizo la Mungu. Mungu huweza kumtumia ye
yote kati yetu licha ya udhaifu wa mtu huyo mbele ya macho ya wanadamu.
Anachotaka Mungu tuwe na furaha ya kweli. Haya ndiyo mabadiliko katika nyanja
za mwili na roho. Kwa kukaidi kwake Yona, “Bwana
akaweka tayari samaki mkubwa ili ammeze Yona, naye Yona akawa ndani ya tumbo la
samaki yule muda wa siku tatu, mchana na usiku,” Yon 1:17. Kwa vile Mungu wetu
ni UPENDO, na baada ya Yona kupata somo juu ya kile alichoamuriwa na Bwana wa
Majeshi, “Bwana akasema na yule samaki, naye akamtapika Yona pwani,” Yon 2:10.
Tusipo ukiri udhaifu wetu na kufanya kadiri ya matakwa ya Mungu, hatutawezwa
kutapikwa, yaani, kunusuriwa kutoka katika majanga yanayotushikilia. Je, hutaki
kutapikwa?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Hakuna aliye
mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba
kama Mungu wetu,” 1Sam 2:2
No hay comentarios:
Publicar un comentario