JUMAPILI
YA 27 YA MWAKA-B
4/10/2015
Somo
I: Mwa 2:18-24
Zab:
127:1-5
Somo
II: Ebr 2:9-11
Injili:
Mk 10:2-16
Nukuu:
“Bwana Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala;
kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake,” Mwa 2:21
“na ule ubavu alioutwaa katika Adamu Bwana Mungu akaufanya
mwanamke, akamleta kwa Adamu,” Mwa 2:22
“Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na
nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika
mwanamume,” Mwa 2:23
“Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye
ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja,” Mwa 2:24
“Kwa kuwa ilimpasa
yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote vimekuwapo, akileta
wana wengi waufikilie utukufu, kumkamilisha kiongozi mkuu wa wokovu wao kwa
njia ya mateso,” Ebr 2:10
“Maana yeye atakasaye
na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita
ndugu zake,” Ebr 2:11
“Yesu akawaambia, Kwa
sababu ya ugumu wa mioyo yenu aliwaandikia amri hii,” Mk 10:5
“Lakini tangu mwanzo
wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke,”Mk 10:6
“Kwa sababu hiyo mtu
atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja;
hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,” Mk 10:7-8
TAFAKARI:
“Yesu Kristo haoni haya kutuita ndugu zake hata kama tunaishi kinyume cha
maagano yetu kimaisha kwa sababu kwa neema ya Mungu ameonja
mauti kwa ajili ya kila mtu.”
Wapendwa sana wana wa
Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 27 ya mwaka “B” wa Kanisa. Kwa
namna ya pekee Mama Kanisa kupitia masomo yote matatu ya leo anatutaka tuonje
upendo wa Mungu kupitia mwanaye Yesu Kristo, hasa kwenye maagano yetu ya
Maisha, hususani Sakramenti ya Ndoa Takatifu. Sakramenti ya ndoa Takatifu ina
upekee wake kwa mtazamo huu: ni Sakramenti ambayo wahusika wote wawili ndiyo
wakufunzi wa ndoa hiyo. Ni maajabu ya Mungu katika upendo na makusudio yake
kwamba muunganiko huu wafanywa imara licha ya tofauti za kimalezi na makuzi ya
kila mwanandoa.
Siri na fumbo la
sakramenti hii Takatifu ipo kwenye makusudio ya uumbaji wa mwanaume na
mwanamke. Mungu baada ya kuumba vitu vyote na katika uzuri wake, aliona bado
kuna kitu ambacho si sawa. Hivyo kwa upendo wa ajabu wa Mungu Baba anayafanya
haya; “Bwana Mungu akamletea Adamu usingizi
mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali
pake,” Mwa 2:21. Kilichotolewa kwa Adamu, yaani upavu, ndiyo uwepo wa Mwanamke.
Kwa maana hiyo mwanamke ni kile kilichotoka wa Adamu. Tendo hili ndilo
linalowaweka pamoja na kuwa mwili mmoja. Hivyo, “na ule ubavu alioutwaa katika Adamu
Bwana Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu,” Mwa 2:22. Wataalamu wa
hesabu wanatuambia kwamba moja jumlisha na moja ni mbili, ila kwa hesabu hii,
Mungu katika fumbo hili ya ndoa, anatufundisha kwamba moja jumlisha moja ni
moja. “Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye,
ataambatana na mkewe; na hao
wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja,”
Mk 10:7-8. Umoja huu ni wa ajabu sana unaotuelekeza kutafakari upendo wa Mungu katika
Sakramenti hii na fumbo zima la Sakramenti ya ndoa.
Katika
dunia hii walitokea watunzi wazuri sana wa tenzi mbalimbali hata leo bado wapo
watunzi wa tenzi hizi, ila haijatokea mtuzi mzuri wa tenzi za rohoni kama
Adamu. Fumbo hili la mwanamke kutoka kwa mwanaume lina ibua hisia za ndani za
Adamu na yeye bila kujizuia anayasema
haya ya moyoni: “Sasa huyu ni mfupa
katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa
maana ametwaliwa katika mwanamume,” Mwa 2:23. Hakuna neno lingine zaidi ya
maneno haya ya Adamu yanayoweza kuonyesha furaha aliyokuwa nayo Adamu baada ya
kupewa msaidizi wake. Kama huu ni ukweli, iweje basi tunaona leo ndoa hazidumu?
Kwa nini basi ndoa zimekuwa za majaribio? Nafasi ya Baba na Mama katika ndoa
leo ipo wapi? Mbona tunaona kila mmoja akijifanyia mambo yake hata kama ndoa
hiyo bado yaesabika kuwepo?
Wapendwa tatizo kubwa leo katika ndoa ni kwamba NDOA
halichukuliwi katika UTAKATIFU wake bali kama mazoea na mfumo wa kawaida wa
kijamii, kwamba muda ukifika na jamii ikiona inafaa basi yanipasa kuona kuwa na
mke, au kuolewa kuwa na mume. Mambo yamekuwa ya KIMWILI zaidi kuliko KIROHO.
Ndoa nyingi leo zinapofungwa Makanisani au sehemu nyingine kwenye vyombo vya
sheria kama mahakamani, zimekuwa maigizo
makubwa. Ni maigizo makubwa katika mtazamo huu wa kiroho: anayefunga ndoa,
yaani kuoa au kuolewa unakuta kesha kuwa na mahusiano hayo kimkataba na wanaume
wengi au wanawake wengi. Huyu anayefunga naye ndoa sasa ndiye anayejulikana
rasmi katika jamii kwa sababu kaamua kujulikana hivyo kutokana na matakwa ya
jamii husika na siyo maisha ya ndani ya kiroho. Ndoa hii haiwezi kudumu kwa
sababu inaingia katika mgogoro wa kimahusiano kiroho uliokwishwa kufanywa awali
na wanaume au wanawake wengi. Madhara ya kufanya uzinifu kabla ya ndoa kama
Sakramenti ni tatizo kubwa kwa maisha ya ndoa husika.
UZINZI ni:-Kufanya tendo la ndoa kabla ya
ndoa na nje ya ndoa baada ya ndoa au ni kufanya ngono na mtu asiyekuwa mke au
mume wako. Unapozini ni sawa na kuuchukua mwili wako na kuunganisha na mwili wa
mtu mwingine “nao watakuwa mwili mmoja” (Mwa. 2:24b). Kwa hiyo kadri
unapozini na watu wengi ndivyo unavyozidi kuugawa mwili wako na unajijeruhi
zaidi. “Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na
kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja,”
1Kor 6:16. Hiki ni chanzo kikubwa sana cha maumivu ya ndani kwa wanandoa.
Hivyo aliye zini kabla ya kuoa au kuolewa, katika ulimwengu
wa kiroho anakuwa ameugawa mwili wake kwa hao aliozini nao. Na hivyo ndani ya
mwili wake anakuwa amebeba miili ya watu wengine. Sasa wakati mtu huyu anapooa
au kuolewa, ndoa yake inakuwa ya shida na ugomvi mwingi kwa sababu anakuwa si
mkamilifu kimwili na anakuwa tayari amejigawa sehemu mbalimbali na amebeba
miili ya watu wengine. Hapa ndipo tunaposhangaa na kuona mwanamme anamwacha mke
wake mzuri na wa kuvutia na kutembea na vigaragosi vya ajabu. Vile vile hapa
ndipo tunaposhangaa kumwona mwanamke anatoka kwenye ndoa yake na kutembea na
vibaka wa ajabu kusimuliwa. Je hatujui kwamba, “kila
mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na
mtu mwingine, azini?”
Wapendwa
wana wa Mungu, pamoja na mapungufu hayo kibinadamu bado tunao uponyaji
tunapojisalimisha ndani na katika Kristo. Kama vitu vyote vimekuwepo kupitia
Kristo ni kwa njia yake vitu hivyo hutakaswa kupita yeye mwenyewe. Hivyo
uponyaji wetu upo kwa Kristo peke yake. “Kwa kuwa ilimpasa
yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote vimekuwapo, akileta
wana wengi waufikilie utukufu, kumkamilisha kiongozi mkuu wa wokovu wao kwa
njia ya mateso,” Ebr 2:10. Je, tupo tayari kuona ukweli huo ndani yetu ili
tuponwe na Kristo? Mara nyingi
kinachozuia uponyaji wetu ni pale tunapoona aibu kujipokea kama tulivyo. Hakuna
maana yoyote kuendelea kujipulizia uturi ili hali ndani yetu kuna ufundo wa
harufu kali sana. Yesu pamoja na kubeba aibu yetu, haoni haya kutuita ndugu
zake. “Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa
mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake,” Ebr 2:11. Waswahili wana
sema hivi, “msificha uchi hazai.”
John na
Mary walikuwa na wakati mzuri sana na ndoa yao ya miaka minne. Hakika Mary
alijiona mwanamke aliyependwa sana na mme wake na kubarikiwa sana na Mungu.
Hivyo siku moja alitaka kumfanyia
“surprise” mume wake. Aliamua kununua “line” nyingine tofauti ya simu ili akiwa
nyumbani ampigie mume wake.
Kama
ilivyokuwa kawaida, Mume wake, yaani John baada ya kurudi kazini njioni huwa
sebuleni akitazama mpira au tamthilia huku mkewe Mary akiwa jikoni anaandaa
chakula cha jioni.
Mara Mary
akampigia mmewe siku kwa namba ile mpya. “Hello Mpenzi wa moyo wangu. Mbona leo
upo kimya sana? Kulikoni?” Mary aliongea kwa sauti nyororo kupita kiasi. “Ok,
nimekuelewa Darling. Nipo nyumbani na “Asha Ngedere” kanibana mbaya sana.
Nitakutafuta baadaye honey wangu.” John alikata simu haraka kwa woga kwamba mke
wake aliyekuwa jikoni angesikia mazungumzo yale.
Mary
hakuamini masikio yake, hivyo alimtumia ujumbe wa maneno, “Message,” nao
ulikuwa hivi, “MBONA SIKUELEWI?” Mara John akajibu, “nimekuwambia nipo na mke
wangu kanibana kama mpira wa kona. Nitakutafuta baadaye baby.”
Basi,
baada ya kula na wakiwa kitandani, wote wakiwa simu zao zipo “silence,” John
alimtumia ujumbe yule aliye mpigia na kumtumia ujumbe. “Bila shaka naongea na
Monica. Mbona tulishamalizana ile “issue” ya gari? Please baby, usiniharibie ndoa yangu.
Nipo naye kitandani. Kesho jioni tutaonana pale pale Corner Bar,” John alituma
ujumbe.
Mara
baada ya dakika tano hivi, Mary mkewe John, aliamka kitandani na kuwasha taa.
John alishtuka kwa sababau haikuwa kawaida ya Mary kufanya hivyo. “Embu niambie
mume wangu mpenzi, huyu Monica ni nani?” Mary alitaka kujua ukweli wa huyo
Monica huku akimuonyesha mumewe zile “message.”
John macho yalimtoka kama mjusi
aliyebanwa na mlango! Kisha John alimdondokea miguuni mke wake na kumwomba
msamaha huku akisema, “hapa sina cha kujitetea mke wangu. Kama kukamatwa
umenikamata vizuri. Naomba unisamehe na kesho nitakuonyesha huyo Monica na
baada ya hapo ndio utakuwa mwisho wa mimi na Monica,” Mary akamjibu, “Basi
tulale mme wangu ila sina furaha nawe kwa sana!”
Wapendwa wana wa Mungu, ndoa ni fumbo na
yawapasa wana ndoa kusomana tabia kila siku hadi mwisho wa maisha yenu. Na
msamehane kweli pale mmoja wenu anapokiri udhaifu wake. Msaidie kweli mwenzako
wa ndoa kuwa imara unapoona ni dhaifu katika mambo fulani ndani ya ndoa yenu.
Mpe moyo mwenzako wa ndoa kufanya vizuri zaidi pale anaposhindwa kufikia
malengo yake sawa sawa.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi;
kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” Ebr 13:4
No hay comentarios:
Publicar un comentario