lunes, 5 de octubre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 27 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 27 YA MWAKA-B
6/10/2015
Somo: Yon 3:1-10
Zab: 129:1-4, 7-8
Injili: Lk 10:38-42
Nukuu:
Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa; ukaihubiri habari nitakayokuamuru,” Yon 3:2

Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa,” Yon 3:4

Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo,” Yon 3:5

Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu,” Yon 3:6 

“Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake,” Yon 3:7b-8

Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende,” Yon 3:10

Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi,” Lk 10:41 

lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa,” Lk 10:42

TAFAKARI: “Usalama wa maisha yetu baada ya kukengeuka ni kufanya toba ya kweli.”

Wapendwa wana wa Mungu, kukengeuka kiimani ni kuiacha njia ya Mungu, kuacha mafundisho na miongozo ya maisha ya kiroho. Ni maisha ambayo mtu anajichagulia na kujifanya yeye kuwa yote katika yote. Kwa maneno mengine ni kuasi Imani yako. Kuasi au kugeukia njia mbaya kiimani, mtu anaweza kufanya kwa kujua kabisa na kuliko wazi, yaani kuikana imani yake hiyo hadharani, au kwa kutokujua na pole pole kujidhihirisha katika matendo na namna yake ya kuishi. Kwa kuishi kwake mtu huyu siyo tu haamini, bali hataki hata kusikia habari hizo.

Hivyo katika somo letu leo kutoka Nabii Yona tunaona ni kwa namna gani watu wa Ninawi walivyokengeuka na kuishi visivyompendeza Mungu. Yona anatumwa kwa watu hawa kufikisha ujumbe wa Mungu. Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa; ukaihubiri habari nitakayokuamuru,” Yon 3:2. Habari yenyewe ni kuacha njia zao mbaya na kumrudia Mungu. Mara nyingi binadamu anapokataa uwepowa Mungu katika maisha yake, mwisho wa usalama wake unakuwa matatani. Yapo mambo mengi binadamu kafichwa kuhusu uhai na maisha yake kwa ujumla. Mfano; ukweli kuhusu kifo, ukweli kuhusu sintofahamu ya maisha yake hata kwa sekunde moja ijayo, ukweli kuhusu matukio ya kutisha yanayotokana na nguvu za asili “Nature,” nk. Pasipo na shaka yoyote ile hali hii inataka kutuambia kitu kuhusu nguvu fulani iliyopo nje ya uwezo wa mwanadamu na yale yote yanayomzunguka. Hapana shaka pia kwa jicho la Imani, nguvu hii ni uwepo wa Mungu anayeyaratibisha yote kadiri ya uwezo ma mamlaka yake.

Kujirudi au kurudi kutoka njia mbaya ni kufanya ukiri wa kweli. Kujitambua huku kiimani ni kufanya toba ya kweli. Kwa kufanya tendo hili Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, ambayo tangia mwanza ni kuwa na uhusiano mzuri na viumbe vyake. Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba,” 2Pet 3:9. Baada ya kuupokea ujumbe wa Yona, watu wa Ninawi waliifanya toba yao kama ifuatavyo, Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo,” Yon 3:5. Ishara zote zinazobeba tendo hili la toba zinatuelekeza kwenye huruma ya Mungu baada ya ukiri wa ndani wa yale yaliyopelekea kuvunjika uhusiano wetu na Mungu.

Kilio cha toba licha ya kwamba chaweza kufanywa na yeyote kwa kujifahamu baada ya kufuata njia zake na hasara zake, tendo hili linapofanywa na jamii nzima linakuwa na nguvu sana. “Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao,” Mt 18:20. Kwa uzito wa jambo hili, Mfalme wa Ninawi anahamasika na kutoka katika kiti chake cha ufalme. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu,” Yon 3:6. Kama kiongozi kujitoa katika kiti cha enzi ni kukubali mabadiliko yanayopelekea usalama wa wale unaowaongoza. Ni kukubali kama kiongozi umechangia tatizo, na upo tayari kuanza upya na watu wako katika yale yaliyomema na kwa manufaa mapana ya Taifia lako.

Ni viongozi wachache sana wanaojitambua hasa pale wanapoambiwa mambo hayapo sawa, na watu wanateseka. Kwa upande wa nchi zetu za Afrika bado hatuna utaratibu wa viongozi kukubali kuchoka kwao na kuwa sababu ya mateso ya watu wao. Wapo tayari kufa na tai zao shingoni, yaani, kutokuachia madaraka, licha ya kwamba hali ni mbaya sana kwa kila nyanja. Hawa ni viongozi wanaochukua nafasi ya Mungu na kuwa sababu ya mateso na dhiki kwa wananchi wao. Mfalme wa Ninawi aliposikia ujumbe ule wa Mungu kupitia Nabii wake Yona, alitoa tamko kwa watu wake: “Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake,” Yon 3:7b-8. Huku ndiko kuwa na maarifa kama kiongozi wa watu. Kukosa maarifa kumewatesa wengi sana, hata sasa watu wa Mungu wanateseka kwa viongozi wao na wale wanaongozwa kukosa maarifa. Naye Mungu anasema, “kwa sababu hiyo watu wangu wamechukuliwa mateka, kwa kukosa kuwa na maarifa; na watu wao wenye cheo wana njaa, na wengi wao waona kiu sana,” Isa 5:13. Kujielewa ni hatua muhimu sana kuelekea njia iliyo njema na salama. Ni pale tu wana wa Ninawi walipojielewa Mungu akaurudisha uhusino wake nao uliovunjika kutokana na kukengeuka kwao. Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende,” Yon 3:10. Huku ndiko kujisalimisha kwa kujielewa. Hapa ndipo iliposalama yetu inayojengwa na ufahamu wetu wa kweli wa Mungu yule tunayemtumikia.

Katika somo la Injili ya leo, Mariamu ndugu yake Martha anajielewa na kumfahamu yule anayemtumikia aliye kweli katika yote, na mwisho anajisalimisha kwake. Yawezekana mimi na wewe tumeyapa maisha yetu kipaumbele chake cha kwanza katika kujishughulisha katika mambo mengi yasiyo na mwelekeo. Maisha yetu hayajengwi kwa wingi wa vitu tunavyofanya, bali uelewa wa yale tunayoyafanya, na kwa nini tunafanya kama tunavyoyafanya. Martha kama tulivyo wengi anajilinganisha na yale anayofanya na kukosa muda wa kujua chanzo ya yale yote tunayoyafanya na kwa nini tunayafanya kwa namna hiyo, na ni nani anayeyaratibisha. Martha anamlalamikia Yesu kwa nini Mariaumu ndugu yake hamsaidii. Yesu anamkumbusha Martha jambo la muhimu na kusema, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi,” Lk 10:41. Furaha yetu haitokani na vitu tunavyofanya. Kujishughulisha huku katika maana ya kufanya hivyo tu, kutatuletea mfadhaiko mkubwa sana.

Maisha yetu yanamaana kwanza kabisa tunapojitambua na mwisho kujisalimisha muda wote kwa yule atupaye uzima wa milele. Huyu ndiye chanzo cha furaha yetu na umilele wa maisha yetu. Kwake yatupasa kutumia muda mwingi naye. Huyu ndiye Kristo; njia, ukweli, na uzima wetu, Yoh 14:6. Kuwa na Kristo ni kuchagua fungu lililo jema ambalo kwalo hatuwezi ondolewa. Ukweli huu ndio Yesu anaomwambia Martha na sisi leo kwamba pamoja na yote tuyafanyayo, lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa,” Lk 10:42. Kukaa chini ya miguu ya Yesu ni ule utayari wa kulishwa neno la uzima, na kujazwa ufahamu na kufunuliwa siri ya uzima wa milele. Tumeumbwa tuishi Milele.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE BWANA TUFUNULIE KWELI YAKO KILA SIKU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario