JUMATANO WIKI YA 29 YA MWAKA-B
21/10/2015
Somo:
Rum 6:12-18
Zab:
124:1b-3, 4-6, 7-8
Injili:
Lk 12:39-48
Nukuu:
“Basi, dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti,
hata mkazitii tamaa zake,” Rum 6:12
“Kwa maana dhambi haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya
sheria, bali chini ya neema,” Rum 6:14
“Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa
watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni
utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki,”
Rum 6:16
“na mlipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mkawa watumwa wa
haki,” Rum 6:18
“Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana
wa Adamu,” Lk 12:40
“Heri mtumwa yule, ambaye
bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo,” Lk 12:43
“Na mtumwa yule aliyejua
mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa
sana,” Lk 12:47
“Na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa
kidogo,” Lk 12:48a
“Na kila aliyepewa vingi,
kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo
watataka na zaidi,” Lk 12:48b
TAFAKARI: “Jiwekeni tayari, kesheni mkiyatenda
mapenzi ya Mungu.”
Wapendwa
wana wa Mungu, injili yetu ya leo inakazia sana kuwa tayari muda wote kwa
sababu hatujui siku ya kutoka kwenye ulimwengu huu. Hivyo kuwa katika mikono
salama ni kukesha katika utumishi wa haki katika kutenda mapenzi ya Mungu. “Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana
wa Adamu,” Lk 12:40. Jambo la msingi kupita yote katika kesha letu ni kuishi
katika hali ya neema, yaani, kutokuwa na hatia juu ya dhambi. Mtume Paulo
anakazia sana swala hili ikiwa ndiyo njia pekee ya kupata kibali mbele ya Mungu
na kuhesabiwa haki. “Basi, dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti,
hata mkazitii tamaa zake,” Rum 6:12. Maisha ya mtu wakati mwingine huongozwa na
tamaa za mwili wake pale nafsi yake inapoegemea zaidi katika mwili.
Wapendwa wana wa Mungu,
nafsi inapoegemea mwenye mwili mtu huyo huongozwa na matendo ya mwili. Matendo
hayo ya mwili hayampi mtu fursa ya kuurithi ufalme wa Mungu. “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu,
ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi,
uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana
na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba
watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21.
Hata hivyo mtu huwa kwenye mikono salama pale nafsi yake inapoegemea katika
Roho. Tunda la Roho hakuna sheria katika maana ya kufuata mambo yetu ya
kibinadamu ikiwa ni pamoja na mila na desturi zetu zisizokuwa njema. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu
wema, fadhili, uaminifu, upole,
kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23. Tuelewe kwamba mtu
mzima ni mwili, nafsi, na roho.
Wapendwa katika Kristo, mwili ni nyumba ya
nafsi na roho. Kwenye nafsi
ndipo penye magonjwa yenyewe kwani ni katikati ya Roho na Mwili. Ni kwenye
nafsi mtu hudumu katika madhara ya dhambi na kuendelea kuhifadhi moyoni. Hapa
ndipo kwenye hifadhi ya matukio mabaya yanayomsononesha mtu. Kwenye nafsi ndipo
kunapomfanya mtu kutosamehe kwa muda mrefu. Nafsi hupata maumivu kutoka roho,
hasa dhambi. Nafsi pia hutawaliwa na; Hofu, Chuki, Hasira, Kujihukumu,
Kujikataa, Kukosa furaha, Kukosa upendo, na Kukosa amani.
Ili
uisalimishe nafsi yako yakupasa kuishi katika hali ya neema, yaani, kuishi
katika hali ya utakaso kila wakati. Mtume Paulo anawasihi watu wake na hasa
kuwaonya juu ya matendo ya sheria. Matendo ya sheria ni uhalali waliojiwekea
baada ya kuishakachua Torati na hivyo kuishi kutokana na tafsiri ya torati na
mapokea ya mababu zao. Kwa namna nyingine walichokuwa wanakishikilia kilikuwa
ni ukweli wa Mungu uliopotoshwa. Hiki ndicho kile kilichojulikana kama TALMUD.
Kwa mantiki hii, mtu hawezi kuhesabiwa haki kwa matendo ya sheria. “Hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya
sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo Yesu ili
tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria; maana kwa
matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki,” Gal 2:16. Tuelewe
kwamba Mtume Paulo hasemi kwamba kwa kumwamini Kristo Yesu hakuna haja ya
sheria katika maana ya Torati. “Kwa maana wale wote
walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa
kila mtu asiyedumu katika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati,
ayafanye,” Gal 3:10. Kinachopingwa hapa
ni kile nilichokisema juu ya ukweli wa TALMUD. Hapa waliyafanya tu yale
yaliyozipendezesha nafsi zao na kuacha yale yaliyozisuta dhamiri zao.
Mtu akiwa chini ya Neema,
yaani hali ya utakaso, hawezi kutawaliwa na dhambi. “Kwa maana dhambi
haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria, bali chini ya neema,”
Rum 6:14. Tunazipata neema hizo tunapojijengea uhusiano mzuri na Kristo Yesu
aliyeshinda dhambi kwa sadaka yake pale msalabani. “Hamjui ya kuwa kwake yeye
ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa
wake yule mnayemtii,” Rum 6:16a. Sisi tu
watumwa wa Kristo kwa sababu utumishi wa utii unaleta haki. “Ni utumishi wa
utii uletao haki,” Rum 6:16c. Yesu ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6. Ila
mauti uletwa na utumishi wa dhambi. “Ni kweli kwamba ni utumishi wa dhambi
uletao mauti,” Rum 6:16b.
Injili inakazia jambo hili
la kuwa watumwa katika utumishi wa utii uletao haki. Yesu anasema heri ya
mtumwa huyu anayekesha kwa utumishi wa utii na kufanya mapenzi ya Mungu. “Heri
mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo,” Lk 12:43. Kwa
kuiongoza nafsi katika kweli na neema tuipatayo kwa sakramenti ya upatanisho,
ndipo tunapoiokoa na kuhesabiwa haki kadiri ya mapenzi yake Mungu. Kwa
kutokufanya mapenzi ya Mungu huku ukijua ukweli huo, itakupasa kipigo kutoka
kwa Mungu. “Na mtumwa yule aliyejua mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari,
wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana,” Lk 12:47. Ni kwa namna hiyo hiyo kwamba, “Na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa
kidogo,” Lk 12:48a. Hivyo maisha yetu hapa duniani na fursa tulizojaliwa na
Mungu vinatualika kuwa mawakili wazuri na waaminifu. Mwisho wa siku itakupasa
kutoa hesabu yake kwa namna ulivyotumia fursa hizo. “Na kila aliyepewa vingi,
kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo
watataka na zaidi,” Lk 12:48b. Ni wakati wa
kila mmoja wetu kujitazama vyema ili usije anguka katika mtego huu wa
kutokukesha katika utumishi wa haki uliotukUKA katika kuyafanya mapenzi ya
Mungu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Tusiwe kwazo la namna
yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; bali katika kila neno tujipatie sifa
njema, kama watumishi wa Mungu,” 2Kor 6:3-4a
No hay comentarios:
Publicar un comentario