JUMAMOSI WIKI YA 26 YA MWAKA-B
3/10/2015
Somo: Bar 4:5-12, 27-29
Zab: 68:33-37
Injili: Lk 10:17-24
Nukuu:
“Jipeni moyo, watu wangu, Israeli mnaokumbukwa! Mliuzwa kwa
mataifa, lakini hamkuangamia, kwa kuwa mlimtia Mungu ghadhabu mlitolewa kwa
adui zenu,” Bar 4:5-6
“Kwa sababu ya dhambi za wanangu nimeachwa ukiwa, kwa kuwa
walikengeuka na kuiacha sheria ya Mungu,” Bar 4:12b
“Jipeni moyo, wanangu, mlilieni Mungu! Maana Yeye
aliyewapatiliza mambo haya atawakumbuka,” Bar 4:27
“Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni
kama umeme,” Lk 10:18
“Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na
n’nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru,” Lk 10:19
“Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii;
bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni,” Lk 10:20
“Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo
haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam,
Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:21b
TAFAKARI: “Furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”
Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka binadamu yeyote yule
katika mahangaiko yake ya kila siku anaitafuta furaha na anataka kuwa na
furaha. Furaha hii ambayo ndiyo kielelezo cha yote ayafanyayo mwanadamu kwa
bahati mbaya au nzuri furaha hiyo hukatishwa na yeye mwenyewe, mazingira
anayoyaishi, au na watu wengine. Pamoja na mazingira hayo iliyosema, maisha ya
mtu yasiyo na malengo ni chanzo kikubwa sana cha kutokuwa na furaha ya kweli.
Malengo ya mtu ndiyo dira ya kuyafikia yale anayoyatamani. Maisha yenye malengo
hubeba mafiga manne: wewe mwenyewe, uhusiano wako na Mungu, uhusiano wako na
jamii inayokuzunguka, na uhusiano wako
na mazingira yanayokuzunguka. Maisha ya mtu hujengwa na kulindwa na mafiga
hayo. Moja ya mafiga haya yasipozingatiwa, binadamu huyu aweza kuwa utumwani au
akawa hatarini kuwa utumwani.
Utumwa kwa namna nyingine ni hali yo yote ile isiyokuwa
huru au uwezo wa kufanya chochote hata kama uwezo huo, yaani wewe mwenyewe binafsi, jamii, na Taifa upo.
Utumwa huu ni hali ili ya kujisalimisha pasipo hiari yako. Vile vile
kutokujielewa na kukosa ufahamu wa mambo yaliyo ya kawaida kabisa ni utumwa
mbaya sana kuliko ule wa kutumikishwa. Ni kwa namna hii wewe mwenyewe unaweza
kuwa mtumwa. Uhusiano wako na wengine au jamii inayokuzunguka usio na uwiano
sawa, kweli, na haki waweza kukufanya wewe mtumwa, au Taifa kama dola huru
likawa utumwani hata kama kijeografia wapo pale pale. Utumwa wa namna hii
tunauona sana katika mataifa mengi ya Afrika na Tanzania ikiwemo. Uhusiano wako
na Mungu katika hali ya uasi wakufanya kuwa mtumwa wa dhambi. Tunakuwa watumwa
wa dhambi kwa kukataa waziwazi upendo wa Mungu na kujifanyia yetu, kusiko haki,
upendo, kweli, na Amani. Na mwisho, uhusiano wako na mazingira yako ukiwa mbovu
mwisho wa siku unakuwa mtumwa katika mazingira yako. Mfano, tunahitaji hewa
safi na maji yenye usalama kwa afya zetu. Tunapoyaharibu mazingira
yanayotuzunguka tunajiweka hatari kuwa watumwa wa afya zetu, na mwisho wa siku
ni janga kubwa la maisha.
Wapendwa wana wa Mungu, katika hali hizo, binadamu hawezi
kuwa na furaha hata kama kwa asili binadamu hutafuta furaha hiyo. Wana wa
Israeli wanajikuta hatiani kwa vile tu hawakuwa na uhusiano mzuri na Mungu.
Hivyo kutokuwa na furaha kama taifa na kujikuta wakiwa utumwani kunatokana na
kutozishika sheria za Mungu. Hivyo, “Kwa
sababu ya dhambi za wanangu nimeachwa ukiwa, kwa kuwa walikengeuka na kuiacha
sheria ya Mungu,” Bar 4:12b. Utumwa wa mtindo huu, binadamu anaweza kujinasua
tu kwa kujijengea ufahamu wa kutosha. Kuwa tayari kuzisoma alama za nyakati na
kuzitafsiri kadiri ya wakati. Mungu hawezi kumwacha mja wake katika hatua hii
muhimu ya kujitoa kwenye mkwamo huu. “Jipeni moyo, watu wangu, Israeli
mnaokumbukwa! Mliuzwa kwa mataifa, lakini hamkuangamia, kwa kuwa mlimtia Mungu
ghadhabu mlitolewa kwa adui zenu,” Bar 4:5-6
Je, hali hii ya wana wa Israeli inasema nini kuhusu Taifa
letu leo? Je sisi leo tunapoangalia uhusiano wetu na mataifa yanayotuzunguka
hata ng’ambo ya bara letu tupo salama? Kijeografia bado tupo kwenye ardhi yetu.
Je, kiuchumi, kijamii, kisiasa, utamaduni bado tupo salama? Bila shaka kwa hali
ilivyo leo jibu utakua nalo. Hata hivyo hatuna sababu ya kukata tamaa. Bado
tuna nafasi ya kufanya vizuri zaidi endapo tutaisikiliza sauti ya Mungu ndani
mwetu, na yale yote Mungu anayotufunulia kupitia watu mbali mbali. “Jipeni
moyo, wanangu, mlilieni Mungu! Maana Yeye aliyewapatiliza mambo haya
atawakumbuka,” Bar 4:27. Ni wakati wa kujipa moyo kwamba tunaweza na ni wakati
wa kufanya maamuzi magumu kwa manufaa mapana ya taifa letu na vizazi vijavyo. Mtindo wa kufanya mambo kwa
mazoezi hauna nafasi tena katika maisha ya leo.
Wanafunzi wa Yesu wale sabini, wanarudi katika utume wao na
kustajabia mambo makuu ya Mungu aliowatendea. Uhusiano wetu mzuri na Mungu ni
chanzo kikubwa sana cha furaha yetu ya kweli. Lakini Yesu anawaambia wasiwe na
furaha tu kwa sababu walimwana shetani akianguka kutoka mbinguni kama umeme,
bali ndani yao Mungu aweza kufanya mambo makubwa zaidi ya hayo. “Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na
n’nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru,” Lk 10:19. Huu ndio msingi wa furaha ya kweli kwa wale wote
wenye hofu ya Mungu. Mahusiano mazuri na Mungu, hutujengea uwezo mkubwa sana wa
kupambana na uovu.
Mara
tuyaonapo haya makuu yakifanyika ndani mwetu tusibweteke. Dunia hii tunapoishi
pomoja na uzuri wake na mambo yake, siyo mahali petu pa kudumu. Hapa ni mahali
tu pa maandalizi ya umilele. Ni jukumu la kila mmoja wetu kupafanya hapa
duniani kuwa sehemu nzuri zaidi ya kuishi huku tukijua siyo sehemu ya mwisho na
ya umilele. Maandalizi mazuri ya hapa duniani ndiyo jibu la uhakika wa maisha
hayo ya umilele. Hivyo furaha yetu kwa yote tutakayoyapata hapa duniani itupe
taswira halisi ya maisha baada ya haya. Kuhusu ukweli huu Yesu anawaonya
wanafunzi wake nasi pia kwa kusema, “Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini
kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni,” Lk 10:20. Furaha yetu isiwe tu ya
leo na kesho, bali furahi hii ipewe kibali na Mungu Baba wa Mbinguni. Tufurahi na
Mungu milele mbinguni.
Wapendwa wana wa Mungu, ufahamu wa siri na ukweli huu, Mungu anautoa wa wanyenyekevu wake wa moyo.
Wanyenyekevu wa moyo hufunuliwa siri za Mungu kwa sababu wapo tayari kusikia,
kufanya, na kuishi kadiri ya mpango wa Mungu. Hivyo Yesu anamshukuru Mungu kwa
niaba ya wanyenyekevu wote wa Moyo na kusema, “Nakushukuru, Baba, Bwana wa
mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili;
umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk
10:21b. Ni uchanga wetu kama watoto tupo tayariwa kujifunza, kusikiliza,
kufanya, na kuishi kadiri ya matakwa ya Mungu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mpatane nia zenu
ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge.
Msiwe watu wa kujivunia akili,” Rum 12:16
No hay comentarios:
Publicar un comentario