JUMAPILI
YA 30 YA MWAKA-B
25/10/2015
Somo
I: Yer 31:7-9
Zab:
126:1-2, 2-3, 4.6, 6
Somo
II: Ebr 5:1-6
Injili:
Mk 10:46-52
Nukuu:
“Maana Bwana asema hivi, Mwimbieni Yakobo kwa furaha,
mkampigie kelele mkuu wa mataifa, tangazeni, sifuni, mkaseme, Ee Bwana, uwaokoe
watu wako, mabaki ya Israeli,” Yer 31:7
“Watakuja kwa kulia, na kwa maombi nitawaongoza; nitawaendesha
penye mito ya maji, katika njia iliyonyoka; katika njia hiyo hawatajikwaa;
maana mimi ni baba wa Israeli, na Efraimu ni mzaliwa wa kwanza wangu,” Yer 31:9
“Maana kila kuhani
mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo
yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi,” Ebr 5:1
“awezaye kuwachukulia
kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali
ya udhaifu,” Ebr 5:2
“na kwa sababu hiyo
imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe,
kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi,” Ebr 5:3
“Na hapana mtu
ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni,”
Ebr 5:4
“Mwana wa
Daudi, Yesu, unirehemu,” Mk 10:47
“Yesu akasimama
akasema, Mwiteni. Wakamwita yule kipofu, wakamwambia, Jipe moyo; inuka,
anakuita,” Mk 10:49
“Yesu akamjibu,
akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu,
nataka nipate kuona,” Mk 10:51
“Yesu akamwambia,
Enenda zako, imani yako imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani,” Mk
10:52
TAFAKARI:
“Mungu huwaridhia watu wake nyakati zitimiapo. Msife Moyo.”
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, karibuni kwa pamoja leo Dominika ya 30 ya mwaka “B” wa Kanisa
tulitafakari neno hili, “Mungu huwaridhia watu wake nyakati zitimiapo. Msife
Moyo.” Dominika hii ya 30 ya mwaka “B,” masomo yote matatu yanalenga kwenye
dhana hii ya Mungu; Huruma, Upendo, na Haki kwa watu wake walioonewa. Mungu
wetu siyo kama mtengeneza saa ya ufungua, na baada ya tendo hilo huiacha saa
hiyo ijiendeshe yenyewe. Ukimya wa Mungu katika mahangaiko ya mwanadamu siyo
kwamba hamjali mwanadamu, bali husubiri nyakati zifaazo ili alitendapo jambo
hilo alitende katika ukamilifu na utimilifu wake mwenyewe. Ukimya wa Mungu
kwetu katika mahangaiko ni nafasi pia kwetu ya kuyatafakari kwa kina yatupatayo
ili nyakati zikitimia tufanye uamuzi sahihi kwa kile apendacho Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu,
hakuna uovu wowote ule utakao dumu milele. Wema na Upendo wa Mungu ndivyo
vitakavyodumu milele. Imani na matumaini yetu yatafikia kikomo chake. “Basi, sasa inadumu imani, tumaini,
upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” 1Kor 13:13. Mungu
hawezi kamwe kufuta mahusiano na mwanadamu aliyechagua kumuumba kwa sura na
mfano wake. Ni kwa namna hii ya ajabu, “Naye
alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi
yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi
yao; ili wamtafute Mungu,
ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja
wetu,” Mdo 17:26-27. Mahangaiko na mateso ya watu kwa namna yoyote ile, iwe
utumwani au kwenye inchi yao wenyewe, Mungu hawezi kuyafumbia macho. Hakuna
mwanadamu yeyote juu ya uso huu wa dunia ambaye yupo kwa sababu yake au kwa
bahati mbaya. Kila mmoja wetu yupo kama alivyo kwa sababu ya upendo wa Mungu na
furaha ya Mungu.
Wapendwa
wana wa Mungu, kilio cha muda mrefu cha wana wa Israeli kinasikika mbele ya
Mungu, naye Mungu wakati ulipotimia alisema basi inatosha. Mungu asemapo
inatosha, kweli inatosha kwa sababu, “kwa
kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu,” Mhu
3:1. Ni kwa kusudi hilo na kuridhia kwake Mungu na watu wake anatuma ujumbe wa
furaha kwa Yakobo kupitia Nambii Yeremia na kusema, “Mwimbieni Yakobo kwa
furaha, mkampigie kelele mkuu wa mataifa, tangazeni, sifuni, mkaseme, Ee Bwana,
uwaokoe watu wako, mabaki ya Israeli,” Yer 31:7. Mungu analitenda jambo hili
kwa wakati ulipotia. Tukiwa na Mungu hatuna sababu ya kuwa na hofu wala Mashaka
licha ya vitisho vingi vitakavyo uzunguka ukweli huo. Kama sote tuliumbwa kwa
sura na mfano wa Mungu, hakuna binadamu mwenye haki zaidi ya mwingine, wala
mwenye haki zaidi za umiliki kuliko mwingine.
Ni kwa maana hiyo hiyo
kwamba hakuna kikundi chochote kinachoweza kujihesabia haki katika umiliki
wowote ule. Kwa kufanya hivyo kwa nguvu na mabavu ni kujaribu kuchukua haki na
kibali ya Mungu iliyopo ndani ya kila mmoja wetu. Hili ni kosa kubwa sana
binadamu kulifanya. Kisicho kibali na haki ya wengi kwa maridhiano hasa katika
swala zima la utawala ni haramu, na hapo Mungu hawezi kuwepo. “Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika
kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao,” Mt 18:20. Sauti ya watu ni
sauti ya Mungu. Kuipuuza sauti ya wengi iliyosima katika haki na kweli ni
kumpuuza Mungu, na katika hali hiyo Mungu hawezi kufumba macho yake. Mtume
Paulo anasema, “bali kama vile tulivyopata kibali kwa Mungu tuwekewe amana
Injili, ndivyo tunenavyo; si kama wapendezao wanadamu, bali wampendezao Mungu
anayetupima mioyo yetu,” 1The 2:4. Lolote lile lisilokuwa na hofu ya Mungu
ndani yake halina uhalali wa kuwepo na mwisho wake ni majanga makubwa. Mzaburi
anasema, “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana
asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure,” Zab 127:1
Wapendwa wana wa Mungu, vita ya kweli na haki hasa pale
mwanadamu anapojaribu kujimilikisha haki za watu, kuuondoa utawala huo wa uovu
si jambo rahisi kwa binadamu fanya kwa nguvu zake mwenyewe. Tunahitaji nguvu ya
sala pamoja na maharifa aliyotujalia Mungu. Hata leo katika Taifa letu kama
ilivyokuwa Taifa la wana wa Israeli tunahitaji sala na uwezo wa Mungu ili
kuvuka vita hivi vya haki dhidi ya uovu. Naye Mungu anasema nasi leo, “mtakuja kwa kulia, na kwa maombi nitawaongoza;
nitawaendesha penye mito ya maji, katika njia iliyonyoka; katika njia hiyo
hamtajikwaa; maana mimi ni baba wa Israeli, na Efraimu ni mzaliwa wa kwanza
wangu,” Yer 31:9. Leo Taifa letu la Tanzania lipo katika hali hii ya wana wa
Israeli. Mungu peke yake ndiye wa kutuvusha katika mtego huu wa haki dhidi ya
uovu. Tumwamini Mungu pasipo shaka kwa sababu Mungu hawezi kuumba jiwe kubwa
ambalo mwisho wa siku akashindwa kulinyanyua. Mungu aliyetuumba kwa kutuchagua
na kutupenda kwa namna ya pekee hatoshindwa kututoa kwenye mkwamo huu wa leo.
Mungu kwa nafasi yake atamtumia mmoja wetu kutimiza nia na
matamanio yetu. Mpango wa Mungu kwetu ni wa ajabu sana kuuelewa. Ila historia
ya wokovu wetu inatuonyesha wazi ukweli huu kwamba, Mungu hutumia vile vilivyo
dhaifu kufifisha vile vinavyojionyesha na kujipendekeza kuwa shupavu na hodari.
Mama Bikiria Maria alipohesabiwa haki mbele ya Mungu anatuambia ukweli huu kwa
kusema, “Amefanya
nguvu kwa mkono wake; Amewatawanya walio na kiburi katika mawazo ya mioyo yao; Amewaangusha wakuu katika
viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:51-52. Huyu ndiye Mungu
anayesimama kutetea haki za wangonye na kuwa sauti kwa wale wasio na sauti
katika jamii. Kwa kutimiza jambo hili Mungu huchagua kile kinachoonekana dhaifu
machoni mwa watu hasa upande ule unaojihesabia haki. Jambo la ajabu licha ya
udhaifu wetu kibinadamu, kwa sakramenti ya ubatizo, Mungu anatushirikisha mambo
makuu matatu; Ukuhani wake, Unabii, na Ufalme. Ni kwa namna hii ya ajabu “kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili
ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili
ya dhambi,” Ebr 5:1. Hivyo yote tuyafanyayo si kwa mastahili yetu binafsi, bali
yale yanayomhusu Mungu na Taifa lake.
Wapendwa
katika Kristo, Mungu anayempenda na kumchagua
ayafanye yale anayoyataka ana sifa hizi tatu kadiri ya somo letu la pili
leo: Kwanza kabisa, “awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea,
kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu,” Ebr 5:2. Mungu hatuambii mtu
huyo lazima awe Mtakatifu kama Yeye alivyo, bali mtu huyo aweza kutumika vyema
kwa sababu naye ana hali ya udhaifu kama atakao wahudumia. Waswahili wanasema,
‘zimwi likujualo halikuli likakwisha.’ Sifa ya pili ni kuwajali wale atakao
watumikia licha ya udhaifu wake. “Na kwa sababu hiyo
imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe,
kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi,” Ebr 5:3. Ni kwa kupitia wajibu huu aliopewa
ndipo atakapo tumia dhamana hiyo aliyopewa ya juu kabisa kujisahihisha makosa
yake, na kujitakasa dhambi zake kwa sadaka ya utumishi wake na huruma ya Mungu.
Na sifa ya mwisho mtarajiwa huyo asiwe mtu wa kujikweza na kujihesabia haki,
bali Mungu awe hofu yake. “Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye
na Mungu, kama vile Haruni,” Ebr 5:4. Sifa hizo tatu kadiri ya somo letu la
pili leo zituongoze katika ufahamu wa kweli kutambua ni yupi anayetufaa kuwa
kiongozi wetu. Tumwombe Mungu kwa namna ya pekee atuongoze vyema katika chaguzi
hii ya viongozi wenye kuhesabiwa haki na kupewa kibali mbele zake Mungu.
Injili
yetu ya leo inakazia swala lile lile la Mungu kuwaridhia watu wake nyakati
zitimiapo. Jambo la pekee katika Injili ya leo ni hili la uponyaji wa Bartimayo
mwana wa Timayo. Nyakati za
kuponywa kwake zinatimia pale alipopaza sauti yake na kusema inatosha Bwana,
niondoe katika mahangaiko na shida hii niliyokuwa nayo kwa muda mrefu. Kumbe
neema na baraka hazikufuati kama haupo tayari kujifungua na kujiweza wazi
kuzipokea neema na baraka hizo. Ndiyo yako ya kutoka ndani, ndiyo pona yako
kutoka mateso yako. Bartimayo ambaye alikuwa mwombaji kipofu anapomsikia Yesu
anapita anasema kwa sauti kuu, “Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu,” Mk 10:47. Ni
ukweli mwamba Bartimayo alichoshwa na hali yake ya kuomba omba, na umasikini
uliokuwa unamzunguka. Bartimayo alichoshwa na kutokuona kwake, hivyo alipenda
kuona ‘kweli’ na ‘haki’ zikitendeka. Sehemu kubwa ya Watanzania leo hawana
tofauti na hali aliyokuwa nayo Bartimayo. Wengi tu masikini wa kutupwa na
ombaomba ilhali Mungu katupatia kila kitu kama Taifa. Yesu anamjibu Bartimayo,
mimi na wewe, “Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu,
nataka nipate kuona,” Mk 10:51. Bartimayo ametoa jibu sahihi juu ya mahangaiko
na mateso yake. Je, wewe na mimi tunajibu gani juu ya hatima ya maisha yetu na
Taifa letu? Baada ya Bartimayo kutoa
ombi lake, Yesu analitimiza kwa kusema, “Enenda zako, imani yako
imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani,” Mk 10:52. Je, una imani ya
kutosha ili upate uponyaji? Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii
usipoteze nafasi uliyopewa leo kufanya maamuzi sahihi ya maisha yako na Taifa
lako kwa vizazi vingi vijavyo.
Napenda
nikuache na maswali haya yafuatayo yakusaidie:
1.
Masomo ya leo yanasema
chochote kuhusu Tanzania yako ya kesho?
2.
Somo la pili leo kutoka
waraka kwa Waebrania linasema chochote kuhusu wagombea nafasi mbalimbali za
uongozi hasa kwa Rais umtakaye?
3.
Kama somo hilo la
Waebrania lina sema kitu kuhusu swali hilo la pili, bado umebaki na uelewa ule
ule wa mwanzo uliojikita kwenye ushabiki?
4.
Mwisho, somo la kwanza na
Injili linasema chochote kuhusu ukomo wa mahangaiko na mateso yako wewe, na
Taifa kwa ujumla?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Usinifiche
uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu,
usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu,” Zab 27:9
No hay comentarios:
Publicar un comentario