JUMAPILI
YA 28 YA MWAKA-B
11/10/2015
Somo
I: Hek 7:7-11
Zab:
89:12-17
Somo
II: Ebr 4:12-13
Injili:
Mk 10:17-30
Nukuu:
“Naliichagua
kuliko fimbo za enzi na vitu vya enzi, wala mali sikuifananisha na kitu cha
thamani; mradi dhahabu yote ya nchi ni kama mchanga kidogo,” Hek 7:8-9
“Maana Neno la Mungu
li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili,
tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani
yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo,” Ebr 4:12
“Yesu akamwambia, Kwa
nini kuniita mwema? Hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu,” Mk 10:18
“Yesu akamkazia macho,
akampenda, akamwambia, Umepungukiwa na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo navyo
vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate,” Mk
10:21
“Walakini yeye akakunja
uso kwa neno hilo, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi,”
Mk 10:22
“Ni rahisi ngamia
kupenya katika tundu ya sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu,”
Mk 10:25
“Yesu akawakazia
macho, akasema, Kwa wanadamu haiwezekani, bali kwa Mungu sivyo; maana yote
yawezekana kwa Mungu,” Mk 10:27
“Yesu akasema, Amin,
nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au
mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia
sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na
mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk
10:29-30
TAFAKARI:
“Kwa maana kuishi kwetu ni Kristo, na kufa
kwetu ni faida kwa wengine.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 28 ya mwaka “B” wa Kanisa. Dominika
hii Mama Kanisa anatualika sote tutafakari juu ya sababu ya maisha yetu hapa
duniani na msingi unayobeba maisha yote. Napenda tutafakari maneno ya Mtume
Paulo ambayo yanafanana na ujumbe wetu wa leo, yaani, “kwa maana kuishi kwangu
ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21. Kama tumeumbwa kwa sababu na lengo
mahususi la Mungu, ni kwa maana hiyo hiyo tupo hapa duniani kwa sababu maalumu
ya Mungu. Ni kweli isiyotia shaka kwamba uumbaji wetu umelenga katika ukombozi
wa ulimwengu mzima. Hivyo uwepo wako hauna maana yoyote kama hauna uhusiano na
mwingine aliyeumbwa kwa mfano wake Mungu. Tupo hapa duniani kwa kufaidiana na
kutaabikiana.
Jambo la msingi kupita
yote ni kulijua neno la Mungu na kulishika kikamilifu. Hii ndiyo hekima ya
kwanza kabisa inayolenga sababu ya kuumbwa kwetu na kuwa katika ulimwengu huu.
Uzima huu tunaupata katika neno la Mungu. Neno la Mungu ndiyo kirutubisha na
kijenga kinga ya mwili na roho. Tukikosa kirutubisho hiki, hakika afya yetu
itakuwa katika mashaka na tuupatapa ugonjwa wowote ule hatutakuwa salama kwa
sababu hatuna kinga. Hivyo kulichagua neno la Mungu ni muhimu kuliko fimbo za
enzi na vitu vya enzi, wala mali sikuifananisha na kitu cha thamani; mradi
dhahabu yote ya nchi ni kama mchanga kidogo,” Hek 7:8-9. Katika neno vyote
vilikuwa kama Mungu alivyoamuru. Mungu aliumba kwa neno na vyo vilifanyika kama
tunavyoviona. Hivyo “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali
kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na
roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo
na makusudi ya moyo,” Ebr 4:12. Wapendwa wana wa Mungu, je tunashiriki neno
hili kikamilifu katika jumuiya zetu? Mbona leo jumuiya zetu zimekuwa za kina
mama na watoto tu? Vijana wa kike na wakiume mpo wapi?
Neno hili
ambalo ni uzima na uhai ndani kwetu, ndiye Kristo mwenyewe. Yesu leo anakutana
na kijana aliyejaa shauku ya uzima wa milele huku akikabiliwa na changamoto ya
mali na malimwengu. Uzima wa milele upo kwa kila mmoja wetu, ila yatupasa kuwa
tayari na matakwa yake. Kijana huyu anajinasibu mbele ya Yesu kwa mbwembwe
nyingi na hata kumwita Yesu MWEMA. Kwa mbwembwe hizi Yesu anampa somo la kwanza
na kumweka sawa.
Yesu anatoa angalisho mapema kabisa kwa kusema, “Kwa nini kuniita mwema?
Hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu,” Mk 10:18. Wema katika maana halisi
ya neno hilo u na Mungu. Kama wema u na Mungu, yote tuyafanyayo hayawezi lingana
na wema wa Mungu.
Ndugu zangu katika
Kristo, yapo mambo mengi yanayotutia matumaini na heri hapa duniani. Ila kwa
mambo hayo hatuwezi kufananisha na uzuri na wema wa Mungu. Tukirejea falsafa ya
Plato, twaweza kusema kwamba, yote tuliyonayo yanaakisi tu wema na uzuri halisi
alionao Mungu peke yake. Ni katika hali hii, Yesu anampa changamoto kijana yule
aliyejiona mkamilifu na hasa amri za Mungu. Jambo hili kwake halikuwa matatizo
kabisa kwani amri hizi alizishika vizuri tangu utoto wake. Hivyo Yesu anamwambia
baada ya kumkazia macho na kumpenda, “Umepungukiwa
na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo navyo vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na
hazina mbinguni; kisha njoo unifuate,” Mk 10:21.
Ndugu yangu, yawezekana
hauna mali katika maana ya vitu vya kuonekana na kushikika, ila umejaliwa mali
za kiroho kama; akili nzuri, uwezo wa kusikiliza na kutatua matatizo yaani
busara na hekima, na hata maisha ya ukaribu na watu. Haya pia Yesu anatuambia
tuenende tukayauze na kuwapa maskini. Kuyauza haya hasa katika maana ya utajiri
wa Kiroho, ni kutoshikamanana nayo na kujifananisha nayo kama kielelezo cha utu
wetu mbele za watu na kujitofautisha mbele za wengine na haya yanayoonekana
pekee mbele za watu. Kuwapa maskini kunamaanisha kwamba haya yote tumepewa ili
tuyatoe kwa wahitaji. Kila mmoja wetu hapa duniani ni mwitaji. Hivyo kila mmoja
wetu ni masikini katika hali ya kuhitaji kile asichokua nacho. Hivyo kuishi
kwetu hapa duniani kama wana wa Mungu na wenye hofu ya Mungu, ni kuishi katika
kufaidiana kuliko kwa kweli, yaani niwe kwaajili ya mwingine.
Wapendwa wana wa Mungu,
kuyaona maisha katika mtazamo huu ni sawa na kujikana mwenyewe. Hivyo hatuoni
ajabu kwa kijana yule kuondoka mbele ya Yesu baada ya kupewa maana ya pili ya
sababu ya maisha yake hapa duniani. Kwa maana hiyo, “yeye
akakunja uso kwa neno hilo, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali
nyingi,” Mk 10:22. Kwa maana nyingine kijana huyu alikuwa na vipaji vingi, au
uwezekano mwingi kimaisha. Jambo hili linamtia hofu ya kuishi kwa sababu
aliishi kwa ajili yake tu. Kuishi kwetu hapa duniani si kwaa ajili yako tu.
Ubinadamu wetu, kama ulivyo katika kitabu cha mwanzo juu ya uumbaji, tumepewa
mamlaka ya uumbaji shirikishi na Mungu. Hivyo tupo hapa duniani kwa ajili ya
wengine pia waone na kutambua uso wa Mungu. Ukweli huu juu ya uumbaji wetu na
sababu zake, tusipoutilia maanani hatutaona wajibu wa kuwa matajiri. Hii ndiyo
sababu ya Yesu kusema hivi juu ya matajiri wasiojua wajibu huo katika dhana
nzima ya kufaidiana, “Ni rahisi ngamia
kupenya katika tundu ya sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu,”
Mk 10:25. Ndugu yangu, chunguza utajiri wako.
Jambo hili si rahisi
kulifanya kwa sababu sote kama binadamu tunayo silika ya umimi. Ila Mtu kuwa
huru na kuishi katika umilele yampasa kuushinda umimi wake. Kinachohitajika
hapa ni utashi wa kweli wa kufanya yaliyo mema na yenye mtazamo wa kimungu kila
siku. Tukiwa katika mwelekeo huu kimaisha, hakuna cha kutushinda. Hivyo Yesu
anasema katika hali hii ya kibinadamu; “Kwa
wanadamu haiwezekani, bali kwa Mungu sivyo; maana yote yawezekana kwa Mungu,”
Mk 10:27. Ndugu yangu, kwa Mungu yote yanawezekana. Chukua hatua. Hivyo kinga
hii yatupasa kuichangua
Mzee Mathayo na Mamsoro
walibariki ndoa yao wakiwa tayari wana watoto wanne. Mzee Mathayo alikuwa
mfanya biashara mzuri sana. Hakupata muda wa kusali na wana jumuiya wenzake
kila siku ya jumamosi asubuhi, kwani alidamka mapema sana kwenda kwenye
biashara zake. Kitendo hiki kilimkera sana mke wake na familia nzima. Kila mara
alipoulizwa na mke wake kwa nini hatengi muda wake na kusali nao kwenye
jumuiya, Mzee Mathayo alimjibu mkewe na kusema, “Mke wangu haujua tulipofunga
ndoa tumekuwa kitu kimoja? Unapokwenda wewe kwenye jumuiya nami nipo. Shida
yako nini? Somo hili hata Paroko analijua.” Mzee Mathayo alijitetea kila mara
kwa maneno haya.
Kwa upende mwingine kwa
michango ya Kanisa na mengineyo kama harambee, Mzee Mathayo alikuwa mstari wa
mbele kabisa. Kwa tendo hili alijulikana sana Parokiani mwake. Miaka ilipita na
wote wawili yaani, Mzee Mathayo na Mama Mamsoro walifariki. Je siku ya ufufuo
ilikuaje?
Mungu hakuchelewa
kuliona jina la Mamroso, na tendo lilifuata ni kumfufua kama alivyobatizwa,
yaani, ‘Mamroso nakufufua kwa jina langu (Mungu), na la mwana (Yesu Kristo) na
la Roho Mtakatifu.’ Mamroso aliposhtuka akajikuta yupo peponi na Watakatifu
wote, Malaika na Mungu. “Je, Mume wangu yupo wapi,?” Mamsoro alimwiliza Mungu.
“Niliwaunganisha kwa sakramenti ya ndoa ili msaidiane wote kuwa wakamilifu ila
mumeo alikataa kwa nafsi yake mwenyewe licha ya wewe kumshauri kila siku hasa
kulisikia neno langu kupitia jumuiya. Hivyo hapa kalabrasha lake halipo. Na
kama halipo hakuna ufufuo kwake,” Mungu alimjibu. “Mbona tuliambiwa tumekuwa
kitu kimoja katika sakramenti ya ndoa?” Mamroso alimuuliza Mungu. “Sakramenti
hiyo mmeunganishwa ili msindikizane na kusaidiana katika utakatifu na mwisho wa
siku kila mmoja wetu atafufuliwa kwa jina lake kama ilivyokuwa siku ya ubatizo
wetu. Wewe ulifanya nafasi yako vyema. Yeye alichagua fungu lake na kwa hilo
anastahili kuwa pale alipo, yaani motoni,” Mungu alimjibu.
Wapendwa wana wa Mungu,
tutakuwa pale tulipojiandalia. Ni vyema tukawa makini kwa kile tulicho leo
katika hali zetu zote. Kuishi kwetu kuna maana tukiwa na Kristo na kufa kwetu ni faida kwa wengine.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nchi na vyote
viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab 24:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario