JUMATATU
WIKI YA 28 YA MWAKA-B
12/10/2015
Somo:
Rum 1:1-7
Zab:
97:1-4
Injili:
Lk 11:29-32
Nukuu:
“ambaye katika yeye tulipokea neema na utume ili mataifa yote
wapate kujitiisha kwa imani, kwa ajili ya jina lake,” Rum 1:5
“ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule
wa Yesu Kristo,” Rum 1:6
“Na makutano
walipokuwa wakimkusanyikia, alianza kusema, Kizazi hiki ni kizazi kibaya;
kinatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona,” Lk 11:29
“Watu wa Ninawi
watasimama siku ya hukumu pamoja na kizazi hiki, nao watakihukumu kuwa na
hatia; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona, na hapa pana mkubwa kuliko
Yona,” Lk 11:32
TAFAKARI:
“Maisha bila Mungu ni sawa safari bila kuijua njia.”
Wapendwa wana wa Mungu,
ulimwengu wetu wa leo pamoja na maendeleo yake, binadamu amefikia hatua ya
kufikiri na kuishi bila Mungu. Watu walio wengi leo sio kwamba hawataki kuamini
kuwa Mungu yupo bali hawataki kusikia kabisa kuhusu Mungu. Leo walio wengi
uweka umuhimu wao katika kazi zao, namna ya kupata pesa, namna ya kupata
umaarufu, na mwisho wa siku namna ya kuyafurahia maisha. Tupo kwenye ulimwengu
wa vitu na kuviabudu vitu hivyo ndiyo imekuwa
sanamu ya kila siku.
Maisha ya mwanadamu
bila Mungu hayana maana yoyote. Uwepo wako hapa duniani ni kwa sababu Mungu
alipenda uwe hivyo na alikuwa na mpango nawe hata kabla ya kutungwa mimba
kwako. Hivyo hakuna mtu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe. Kwa maana,
“mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni
jiwe kuu la pembeni,” Efe 2:20. Yesu Kristo ndiyo msingi wa yale yote
tuyafanyayo kwa sababu kwa kupitia Yeye yote tuyaonayo kwa macho yetu
yalifanyika. “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho
chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Hapa ndipo tunapouona Umungu wa Yesu na uwezo
wake juu ya vitu vyote.
Hivyo katika Injili ya
leo Yesu anawakaripia wale wasioamini uwepo wake na kubakia tu katika Ishara.
Ujumbe anaotupa Yesu leo ni kwamba Yeye ni zaidi ya Ishara zile tuzionazo.
Ishara utusaidia tu kuelewa na kuamini mambo yale yaliyopita ufahamu wetu. Ila
kwa ishara hizo kama zilivyo haziwezi kulingana na Kristo ambaye katika mambo
yote yaliweza kuwa kupitia yeye mwenyewe. Hivyo msingi wa imani yetu haupo
kwenye Ishara. Yesu anawaambia makusanyiko ya watu na sisi pia katika ulimwengu
wetu leo kwamba, “Kizazi hiki ni kizazi kibaya;
kinatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona,” Lk 11:29.
Ishara ya Yona ilikuwa kwamba baada ya kukaidi kwenda Ninawi alimezwa na samaki
na kukaa ndani ya tumbo la samaki kwa siku tatu. Kwa Ishara hii, Yesu aliwafunulia kusanyiko
lile Ishara ya ufufuko wake uliotokea siku ya tatu baada ya mateso, kusulubiwa
msalabani na kufa. Hii ndiyo Ishara kubwa kupita zote na kielelezo cha uzima wa
milele.
Wapendwa wana wa Mungu, tusipoyaona maisha yetu katika mtazamo
huu wa umilele, maisha na fahari yake yote hapa duniani hayana maana yoyote.
Ninawi walikengeuka na kumwasi Mungu, ila walitubu na kupata msamaha wa Mungu
kupitia Nabii Yona. Hawa walioamini na kumsadiki Mungu pasipo shaka ndio
watakao kuwa mahakimu wetu siku ya kiama. “Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na kizazi
hiki, nao watakihukumu kuwa na hatia; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya
Yona, na hapa pana mkubwa kuliko Yona,” Lk 11:32. Miongoni mwetu hata leo wapo
watu ambao kwa maisha yao na wongofu wao Mungu anasema nasi kupitia wao. Hawa
pia siku ya mwisho watakuwa mahakimu wetu. Mara nyingi tumekuwa vinara wa
kuwanyanyapaa kwa mabadiliko yao ya kiroho kwa kuzidi kuwafananisha na maisha
yao ya zamani. Hili ni kosa kubwa sana kiimani. Hakuna mwenye hati miliki ya
maisha ya umilele. Sote tunaitaji upendo na huruma ya Mungu katika kuhesabiwa
haki na kuwa warithi wa maisha hayo ya umilele.
Je, wa mwamini Yesu Kristo? Mtume Paulo anatuambia wazi
kwamba, ni katika Yesu Kristo, “ambaye katika yeye tulipokea neema na utume ili mataifa yote
wapate kujitiisha kwa imani, kwa ajili ya jina lake,” Rum 1:5. Katika jambo
hili la msingi, Yesu Kristo ndiye njia ya safari yetu ya maisha ya umilele na
hakuna mbadala wake. Kwa kuuishi ukweli huu, na kuufanya wengine wauishi kwa
kujitoa kwetu pasipo kujibakiza ndiko kunakotufanya sisi kuwa wateule wa
Kristo. Hivyo kwa kupitia hawa tuliojitoa kwao bila kujibakiza ili wamjue
Mungu, wampende, wamtumikie na mwisho warudi kwake kwenye uzima wa milele, “katika
hao ninyi mmekuwa wateule wa Yesu Kristo,” Rum 1:6. Usifikiri hata mara moja
unapoteza muda wako kwa kuwalisha neno watu wa Mungu. Usisikitike hata mara
moja unapotumia muda wako kwa ajili ya wokovu wa watu. Kuna furaha kubwa sana
kwa Mungu ikiwa kwa kupitia kwako mtu mmoja alipata wokovu na kwenda Mbinguni
kwenye maisha ya umilele. Ndugu yangu uliyesafari nami katika tafakari hii,
maisha bila Kristo Yesu ni sawa na safari bila kuijua njia.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Maana,
ijapokuwa naihubiri njili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole
wangu nisipoihubiri njili!” 1Kor 9:16
No hay comentarios:
Publicar un comentario