JUMANNE WIKI YA 28 YA MWAKA-B
13/10/2015
Somo: Rum 1:16-25
Zab: 18:2-5
Injili: Lk 11:37-41
Nukuu:
“Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu
uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia,” Rum
1:16
“Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao,
waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao,” Rum 1:24
“Bwana akamwambia, Ninyi Mafarisayo mwasafisha kikombe na
sahani kwa nje, lakini ndani yenu mmejaa unyang'anyi na uovu,” Rum 11:39
“Lakini, toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote huwa
safi kwenu,” Rum 11:41
TAFAKARI: “Injili ni uweza wa
Mungu uletao wokovu. Na hii ndiyo habari njema kwetu”
Wapendwa
wana wa Mungu, ni kweli kwamba binadamu leo amefanikiwa kwa kiasi kikubwa
katika fani ya habari ikiwa ni wepesi wa kupata habari hizo na hata
kuzitengeneza, na kuzisambaza. Pamoja na mafanikio haya, mwanadamu hajawa na
amani ya kutosha na usalama wake katika ulimwengu huu wa leo wa sanyansi na
maendeleo yake. Wepesi wa kupata habari na kusambaa kwake kumekuwa ndiyo sababu
kubwa ya kumwongezea hofu. Kwa maana nyingine tumefanikiwa katika mawasiliano
kiiujumla na sio kwa kile tunachowasiliana (ujumbe). Ujumbe wa mawasiliano yetu
bado haujawa habari njema kwetu. Neno la Mungu ni habari njema kama lilivyo,
uzima, na wokovu wetu. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu na kama mbatizwa
kuliishi neno la Mungu na kutolionea haya. Kwa maana nyingine kila mbatizwa
apaswa kuwa habari njema kwa wengine. Mtume Paulo anatuambia, “Kwa maana siionei haya
Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa
Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia,” Rum 1:16. Neno hili ni uzima na wokovu kwa
kila mmoja wetu tunapolishika na kuliishi.
Leo ni
wachache sana kati yetu tunaochukua hata muda kidogo kulisoma neno la Mungu.
Hatulipendi neno hili kwa sababu huzisuta nafsi zetu. Ulimwengu tunaoishi kila
na kila tunapopita unatupa ujumbe huu, “maisha bila Mungu yanawezekana. Hivyo
weka umuhimu katika maisha yako na hasa utazame mwili wako.” Tunapolipiga
kisogo neno la Mungu basi maisha yetu ya kiroho huwa hatarini. Mwili uinuliwa
kupita kiasi na mwisho wa siku tunakosa yote. Maisha ya mtindo huu hayatupi
amani yoyote zaidi ya hofu na mashaka muda wote. Hivyo, “kwa ajili ya hayo Mungu
aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima
miili yao,” Rum 1:24. Tuelewe kwamba miili yetu ni mitakatifu kwa sababu ndilo
hekalu la Roho Mtakatifu. “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho
Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu
wenyewe,” 1Kor 6:19. Kama mwili ni nyumba ya Roho na Nafsi, nyumba hii
inapokuwa chafu huathiri pia Nafsi na Roho, hasa pale nafsi inapoegemea katika
mwili. “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu
iwe dhabibu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye
maana,” Rum 12:1. Wito huu ni wa kila mmoja wetu kadiri ya wito wake.
Tatizo
kubwa la kutokufikia malengo mazuri ya kuishi maisha ya kiroho kadiri ya mpango
wa Mungu ni pale tunapoweka umuhimu wa vitu pasipo kuwa na umuhimu. Mfumo wa
maisha unaobeba falsafa hii utuzeesha kabla ya wakati na kupotea muda bure.
Katika Injili ya leo Yesu analiona hilo kwa Mafarisayo na analikemea kwa nguvu
zake zote. “Ninyi Mafarisayo mwasafisha
kikombe na sahani kwa nje, lakini ndani yenu mmejaa unyang'anyi na uovu,” Rum
11:39. Huku ni sawa na kufunga bandeji kwanye paji la uso kusikokuwa na kidonda
ukaacha kufunga kidonda kinachotoa usaa mguuni. Kwa upande mwingine hili ni
tatizo la kutokujipokea kama ulivyo na kuanzia hapo ulipo ndipo uweze kusonga
mbele kuliko kuzuri zaidi. Kuyagusa maisha yako ya ndani na usiyopenda
kuyazungumza ndipo kuliko na ufunguo wa maisha yako. Tunapenda sana kuangalia
tamthilia za watu mbalimbali maarufu ulimwenguni na mwisho wa siku tunasahau
kuwa tamthilia nzuri na ya pekee ni kuhusu maisha yako. Yatazame maisha yako ya
ndani utagundua unafiki wako mbele ya Mungu na kwako mwenyewe. Eneo hili ni
muhimu sana kuligusa kwani ndiyo wewe mwenyewe. Wokovu wa mtu huanzia hapa kama
hatua ya ndani na ya mabadiliko kiroho.
Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, yale yote
tuyatoayo nje na kuyafanya huakisi maisha yetu ya ndani. Ni kweli unaweza
kuficha hali na ukweli wako wa ndani na kutenda kwa kuwapendezesha watu au
kutenda kwa kadiri ya mazingira fulani. Ukweli ni kwaba huwezi kuificha hali
hii kwa muda wako wote. Zawadi yako
kubwa kwa Mungu ni kuyatoa yale yaliyo ndani mwako kwake kwani ndani humo kuna
chapa yake. Kumbuka umeumbwa kwa sura na mfano wake. Chapa hii ya Mungu ndani kwako
hufifishwa na dhambi zako. Unapoishi katika hali ya neema na utakaso, taswira
hii ya Mungu ndani yako hung’ara na kufanywa upya siku kwa siku. Hivyo, “toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote
huwa safi kwenu,” Rum. Wapendwa wana wa Mungu, hivyo vya ndani ndivyo
vimpendezavyo Mungu kwa sababu vina chapa yake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Basi wewe, mwanangu, uwe hodari katika neema iliyo katika
Kristo Yesu,” 2Tim 2:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario