martes, 20 de octubre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 29 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 29 YA MWAKA-B
20/10/2015
Somo: Rum 5:12, 15b, 17-19, 20b-21
Zab: 40: 7-8a, 8b-9, 10, 17
Injili: Lk 12:35-38
Nukuu:
“kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi,” Rum 5:15b

Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima,” Rum 5:18

“Na dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi; ili kwamba, kama vile dhambi ilivyotawala katika mauti, vivyo hivyo kwa njia ya haki neema itawale hata uzima wa milele kwa Yesu Kristo Bwana wetu,” 5:20b-21

Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka,” Lk 12:35 

nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara,” Lk 12:36

 Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha,” Lk 12:37a

TAFAKARI: Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo yanatuelekeza kutafakari kuhusu muda wetu wa kuishi hapa duniani na mahusiano yetu na Kristo. Ni kweli kwamba kifo bado ni tishio na hakizoeleki. Pamoja na ukweli huo, kifo hakiwezi kuepukika kama mimi na wewe tu hai leo. Ndugu yangu ipo siku tutakakufa iwe tunapenda au hatupendi. Leo sina lengo la kukutisha kuhusu kifo, ila ni vyema kuuzungumza ukweli huu ambao mara nyingi hatupendi kuusikia. Kunatofauti kubwa sana kati ya yule anayemwamini Kristo na asiyemwamini juu ya ukweli kuhusu Kifo. Ndani na katika Kristo kifo hakina nguvu tena. Katika Injili ya leo, pamoja na ukweli huu juu ya kifo, Yesu anatuwasa kwamba, Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka,” Lk 12:35. Kuvifunga viuno ni kuwa tayari katika maana ya kujiandaa vyema kwa lolote lile ukilenga lililo salama zaidi. Ni kuishi maisha yenye kumpendeza Mungu kwa gharama zote. Jambo la pili katika maana hiyo ya kuvifunga viuno ni kwamba taa zetu ziwe zinawaka, ikimaanisha kuishi maisha yasiyo na hatia. Ni kuishi maisha ya kuuchuchumilia ukamilifu ingawa udhaifu upo. Kila siku upewayo na Mungu iwe nafasi ya kuongoka kwako. Ukweli huu unatupelekea kuyaona maisha hapa duniani ni JUKUMU LA MUDA MFUPI. Je, unamtazamo gani kuhusu maisha yako?

Ndugu unayesafiri nami katika tafakari hii, ni ukweli usiofichika kwamba maisha hapa duniani ni jukumu la muda mfupi. Je, unabisha? Maandiko Matakatifu hufundisha na kutukumbusha maisha yetu duniani yalivyo mafupi na yasiyodumu. Maisha yanaelezwa kama ukungu, mkimbiaji, pumzi, na mvuke.  "Kwani sisi tu wa jana tu, wala hatujui neno, kwa kuwa siku zetu duniani ni kivuli tu." Ayu 8:9

Ndugu, ili kutimiza vizuri maisha yako hupaswi kusahau ukweli wa aina mbili: Kwanza, yakilinganishwa na umilele, maisha ni mafupi sana. Hivyo, nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara,” Lk 12:36. Pili, dunia ni makazi ya muda tu. Hatuwezi kukaa hapa kwa muda mrefu, hivyo usijishikamanishe sana nayo. Yesu leo anatuambia,  Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha,” Lk 12:37a. Tumwombe Mungu atusaidie kuyaona maisha ya duniani kama anavyoyaona yeye mwenyewe. Mfalme Daudi aliomba, "Bwana, nijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; nijue jinsi nilivyo dhaifu," Zab 39:4

Ndugu yangu hapana shaka wa mfahamu vizuri "inzi!" Mdudu huyu kadiri ya utafiki wa kisayansi huishi siku saba tu. Ni wiki moja kati ya wiki 52 katika mwaka mmoja. Tazama fujo na papara za inzi. Hutua kila mahali kwa siku hizo saba; kwenye vyakula (vilivyo chacha na visivyo chacha), kwenye vinjwaji, kwenye vidonda, kwenye vinyesi, nk. Tazama anavyoongea kwa ishara akiwa amenyanyua miguu yake ya nyuma na kusema, "yaliyopita yeshapita." Na anapoinua miguu ya mbele husema hivi, "yajayo na yaje, ponda mali, furahia yote, haya ndiyo maisha."

Ndugu, tulio wengi leo maisha yetu hayana tofauti na haya ya inzi. Hutaka kufanya yote na kujaribu yote katika maisha. Hakuna muda wa maandalizi wala tafakari kuhusu umilele wetu kama zawadi ya pekee tuliyopewa sisi wanadamu. Maisha yetu leo yana maana sana “kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi,” Rum 5:15b. Yesu Kristo katurudishia hadhi ya kuwa tena wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake wa mbinguni.

Jambo la ajabu ona tunavyoishi na jirani zetu! Unaweka wigo "fence" kiasi kwamba unamzuiya hata jirani yako kufungua mlango. Ona! tusivyo wajali wengine afya zao! Tunaelekeza maji taka kwenye makazi yao bila huruma. Eti kwa vile unapesa, na unajulikana hadi usalama wa Taifa. Eti kwa vile wewe ni kiongozi wa ngazi za juu kwenye utawala dhalimu. Eti kwa vile wewe ni mfanya biashara maarufu nchini. Je, hili ndilo kusudi la Mungu kwa maisha yako hapa duniani?

Ndugu yangu, usisahau kuwa maisha ya hapa duniani ni sawa na kuwa ugenini. Haya si makazi yako ya kudumu, au hatma yako ya mwisho. Unapita tu!  Unatembea tu duniani. Mfalme Daudi anatukumbusha, "Mimi ni mgeni katika nchi, usinifiche maagizo yako," Zab 119:19, na Mtume Petro anasema,  "na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni." 1Pet 1:17. Waamini wa kweli wanafahamu wazi kwamba kuna mambo mengi ya maisha kuliko hii miaka michache tunayoishi hapa duniani. Uhakika huu tunapewa na Kristo mwenyewe baada ya kukishida kifo kwa sadaka yake pale msalabani. Sote tumehesabiwa haki kwa kifo cha Kristo. Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima,” Rum 5:18

Ndugu, kitambulisho chako kiko katika umilele, na nchi yako ni mbinguni kwa sadaka ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyekubali kuutoa uhai wake ili mimi na wewe tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi. “Na dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi; ili kwamba, kama vile dhambi ilivyotawala katika mauti, vivyo hivyo kwa njia ya haki neema itawale hata uzima wa milele kwa Yesu Kristo Bwana wetu,” 5:20b-21. Yote haya yawezekana kwako na kwangu kwa neema tu ya Mungu. Unapofahamu ukweli huu, utaacha kuwa na wasiwasi wa "kupata kila kitu" hapa duniani. Mungu yupo wazi kabisa kuhusu habari za kuishi kwa ajili ya "hapa" na "sasa" tu huku ukijifananisha na watu wa dunia hii katika kipaumbele na mtindo wa maisha.

Tunapochezacheza na majaribu ya dunia hii, Mungu anaita hali hiyo uzinzi wa kiroho.  "Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki ya dunia ni kuwa adui wa Mungu?" Yak 4:4. Karipio hili kwa maana nyingine la tuambia kwamba 'twajidanganya mbele za Mungu iwapo tunachotaka ni mambo yetu, kuchezacheza na ulimwengu kwa kila nafasi tunayopata mwisho wetu ni kuwa maadui wa Mungu na njia yake.' Rejea mfano wa inzi hapo juu. "Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo..." 2Kor 5:20. Cha kusikitisha, wakristo wengi tumemsaliti mfalme wetu na ufalme wake. Katika hali ya upumbavu tumeamua kwamba kwa sababu tunaisha hapa duniani, basi hapa ndiko nyumbani kwetu. "Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipinganazo na roho." 1Pet 2:11.

Mungu pia anatuonya tusijishikamanishe sana na vitu vinavyotuzunguka kwa kuwa si vya kudumu. "Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita." 1Kor 7:31. Ni wazi yatupasa kufanya kazi na kujipatia mahitaji yetu ya kila siku. Ila yote hayo tuyapatayo hatupaswi hata mara moja kujilinganisha nayo. Utu wetu na watu wengine ni zaidi ya mali hizo. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19

Ndugu, ni ukweli usiotia shaka kwamba kwa mivuto ya hali ya juu, na vyombo vya mawasiliano vyenye kutia upofu, na mambo mengi ya anasa yaliyopo siku hizi, ni rahisi kusahau kwamba maisha si kufanya raha tu. Ndugu sikuonei gele bali nakukumbusha tu!

Ni pale tu tunapokumbuka kuwa maisha ni majaribu, dhamana,  na jukumu la muda mfupi ndipo mvuto wa mambo ya anasa utakapokosa nguvu maishani mwetu. Hili likifikiwa twaweza kujiandaa kwa jambo jingine ambalo ni bora zaidi. "Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele. "2Kor 4:18b.

Ukweli ni kwamba dunia si makazi yetu ya kudumu huelezea kwa nini, kama wafuasi wa Kristo, tunapatwa na magumu, huzuni, na kukataliwa (Yoh 15: 18-19; 16:20; 16:33). Ukweli huu pia hueleza kwa nini baadhi ya ahadi za Mungu huonekana kutotimizwa, baadhi ya sala hazijajibiwa, na baadhi ya mazingira kuonekana kutokuwa na haki. Huu si mwisho wa mambo.

Ili kutufanya tusijifungamanishe na ulimwengu sana, Mungu huruhusu tusikie hali fulani ya kutokuridhisha na kutosheka katika maisha-hitaji ambalo "haliwezi" kutoshelezwa kamwe hapa duniani. Hatuna furaha kabisa hapa kwa sababu hatutakiwi! Dunia si makazi yetu ya milele, tumeumbwa kwa ajili ya kitu bora zaidi.

Ndugu yangu, samaki hawezi kuwa na furaha kuishi nchi kavu, kwa sababu ameumbwa kwa ajili ya kuishi majini. Tai kadhalika asingefurahi kama asingeruhusiwa kupaa angani. Hatuwezi kamwe kujisikia kutosheka kabisa hapa duniani, kwa sababu tumeumbwa kwa mambo mengine zaidi. Utakuwa na vipindi vya furaha hapa, lakini hakuna cha kufanana na kile Mungu amepanga kwa ajili yako.

Kwa kutambua kwamba maisha ni jukumu la muda mfupi tu ni lazima kubadili kabisa mambo unayoyaona ya muhimu maishani mwako. Mambo ya milele, yasiyo ya muda mfupi, yapasa yawe vigezo vya maamuzi yako. Kama C. S. Lewis anavyosema, "Kila kisicho cha milele hakifai milele.” Naye Mtume Paulo anatuambia, "Tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele," 2Kor 4:18.

Ndugu, ni kosa kubwa kudhani kuwa mpango wa Mungu kwa ajili ya maisha yako ni mafanikio ya mali au mafanikio ya siku hizi, katika ulimwengu unavyoyaona. Maisha tele hayana uhusiano na mali tele, na uaminifu kwa Mungu hautuhakikishii kuwa na mafanikio ya kazi au huduma, usitazamie taji zisizodumu (1Pet 2:11). Pia, "usiogope mtu atakapopata utajiri, na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua chochote; utukufu wake hautashuka ukimfuata," Zab 49:16-17.

Paulo Mtume baada ya kuongoka kwake alikuwa mwaminifu lakini alijikuta gerezani. Yohane Mbatizaji alikuwa mwaminifu lakini alikatwa kichwa. Mamilioni ya watu waaminifu wameuawa, wamepoteza kila walichokuwa nacho, au maisha yao yamekoma wakiwa hawana kitu. Lakini mwisho wa maisha haya si mwisho, bali mwanzo wa maisha mapya ya umilele. Kifo kwa njia ya haki ndani na katika Kristo ni kuzaliwa katika maisha ya umilele. Hapa kifo huwa njia, au daraja la kuvuka kwenda kwenye umilele.

Ndugu niliyesafiri nawe katika tafakari hii, naomba nisikuchoshe.  Katika macho ya Mungu, mashujaa wa imani sio wale waliopata mali, wenye mafanikio na nguvu katika maisha haya, bali ni wale wanaoyaona maisha kama jukumu la muda mfupi na kutumia muda huo kwa uaminifu, wakitumaini kupokea thawabu yao katika umilele. "Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao, maana amewatengenezea mji," Ebr 11:13, 16. Asante kwa kusafiri nami. Tafakari na chukua hatua.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Maana miaka elfu machoni pako ni kama siku ya jana ikiisha kupita, na kama kesha la usiku,” Zab 90:4


“Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu,” Lk 21:36

No hay comentarios:

Publicar un comentario