IJUMAA WIKI YA 29 YA MWAKA-B
23/10/2015
Somo: Rum 7:18-25a
Zab: 119:66, 68, 76, 77, 93, 94
Injili: Lk 12:54-59
Nukuu:
“Kwa maana lile jema
nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo,” Rum
7:19
“Basi kama lile
nisilolipenda ndilo nilitendalo, si mimi nafsi yangu nilitendaye, bali ni ile
dhambi ikaayo ndani yangu,” Rum 7:20
“Kwa maana naifurahia
sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini
katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya
akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo
vyangu,” Rum 7:22-23
“Enyi wanafiki, mwajua
kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira
haya?” Lk 12:56
“Maana, unapofuatana
na mshitaki wako kwenda kwa mwamuzi, hapo njiani fanya bidii kupatanishwa naye,
asije akakuburuta mpaka mbele ya kadhi; yule kadhi akakutia mikononi mwake
mwenye kulipiza, na yule mwenye kulipiza akakutupa gerezani,” Lk 12:58
TAFAKARI: “Kwa maana lile jema
nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.”
Wapendwa
wana wa Mungu, ni kweli kwamba kwa asili ya binadamu kama alivyoumbwa na sura
na mfano wake Mungu, si asili yake kutenda uovu. Kwa nini basi lile jema
alipendalo halifanyi, na lile baya asilolipenda hulifanya? Kadiri ya mafundisho
ya Mt. Augustino anasema hivi; “Hata baada ya maanguko ya mwanadamu Mungu
hakumuondolea mwanadamu ule uhuru wake. Angefanya hivyo basi Mungu asingekuwa
na haki ya kumuhukumu mwanadamu kwa sababu mwanadamu huyu angekuwa hana utashi wake
mwenyewe na hivyo kosa au dhambi isingekuwepo wake. Hata hivyo Mungu kwa upendo
wake mkuu alimwachia mwanadamu uhuru wake, na kwa njia hiyo mwanadamu huweza
kuziacha njia zake mbaya na kumrudia Mungu.”
Tukirudi
kwa Mtume Paulo, anamwona mtu katika hali hii: Mwili, Nafsi, na Roho. Mtu huyu
husukumwa na kutenda kadiri na mwitikio wa nafsi yake. Kwenye nafsi ya mtu
ndipo penye dhamiri yake. Nafsi ni kama mnara wa kuongoza ndege. Nnara huu
ukiegemea mwili basi matendo ya mwili tunayajua kama tusomavyo, Gal 5:19.21. Na
nafsi ikiegemea Roho, tunaona matunda ya roho kama tusomavyo, Gal 5:22-23. Hata
hivyo, kama asemavyo Mt. Augustino, mwanadamu bado ananafasi ya kufanya vizuri
hasa ataamua na kutumia uhuru uliopo ndani mwake wa kuchagua jema na kuacha
baya. Hivyo ni kwa mantiki hii Paulo anasema, “Kwa maana lile jema
nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo,” Rum
7:19. Je, hapa wa kulaumiwa ni nani? Je, tumalaumu Mungu aliyetupa uhuru huu,
au sisi wenyewe kwa kutokutumia uhuru wetu vyema?
Sheria ya
Mungu katika utu wa ndani, ni UHURU aliyopewa mwanadamu umsaidia katika mambo
mazuri kumwelekea Yeye na ufalme wake. Kufurahia uhuru huu katika ubaya ndilo
anguko la mwanadamu. Sheria ya utu huu wa ndani, yaani uhuru ulionao
unapoifanya nafsi yako kuegemea mwili, ndipo mtu anapodondoka kwenye dhambi
iliyo katika viungo vyake. Hii ni sawa na nafsi kupigwa mwereka na uhuru huu
ambao ndiyo sheria ya ndani ya utu wako. “Kwa maana naifurahia
sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini
katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya
akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo
vyangu,” Rum 7:22-23. Kujinasua katika mtego huu ni kutambua na kuyafanya
matendo ya Roho ambayo ndani kwayo yamejaa uhai na uzima, Gal 5:22-23.
Unapotambua
hali hiyo na usifanye chochote ndicho anachosema leo Yesu katika Injili. “Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu;
imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?” Lk 12:56. Ni kuujua ukweli kama ulivyo nawe ukabaki katika ubishi na ung’ang’anizi
usio na uzima ndani yake. Watesi wa Yesu nyakati zake, hasa Waandishi,
Mafarisayo na Wanasheria, waliujua ukweli lakini waliupindisha kwa makusudi
kukidhi haja zao na maslahi yao.
Yesu anawashauri na kutushauri
sisi leo kwamba, kama tunaufahamu ukweli basi tuufuate na kuufanya tungali hai
kwani hakimu wetu Mungu yupo anasafiri nasi kuelekea kwenye kiti hukumu. “Maana, unapofuatana na mshitaki wako kwenda kwa mwamuzi, hapo
njiani fanya bidii kupatanishwa naye, asije akakuburuta mpaka mbele ya kadhi;
yule kadhi akakutia mikononi mwake mwenye kulipiza, na yule mwenye kulipiza
akakutupa gerezani,” Lk 12:58. Kumbe kabla ya kutupwa gerezani, yaani kwenye
mateso yasiyo na mwisho, Mama Kanisa anatushirikisha huruma ya Mungu kwa
kupitia sakramenti ya upatanisho. Sote tunahitaji toba na kupatanishwa na Mungu
kila tunapodondoka katika dhambi.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Basi
zaeni mtunda yapasayo toba,” Mt 3:8
No hay comentarios:
Publicar un comentario