ALHAMISI WIKI YA 30 YA MWAKA-B
29/10/2015
Somo: Rum 8:31b-39
Zab: 109:21-22, 26-27, 30-31
Injili: Lk 13:31-35
Nukuu:
“Mungu
akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” Rum 8:31b
“Ni nani atakayewashitaki wateule wa
Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki,” Rum 8:33
“Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo
Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko
mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea,” Rum 8:34
“Lakini katika mambo hayo
yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda,” Rum 8:37
“Kwa maana nimekwisha
kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye
mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini,
wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio
katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 8:38-39
“Akawaambia, Nendeni,
mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa,
siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32
“Ee Yerusalemu,
Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi
nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake
chini ya mbawa zake, wala hamkutaka,” Lk 13:34
“Angalieni, mmeachiwa
nyumba yenu! Nami nawaambia, Hamtaniona tena kamwe, hata mtakaposema,
Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana,” Lk 13:35
TAFAKARI: “Mungu akiwapo upande wetu,
ni nani aliye juu yetu?”
Wapendwa wana wa Mungu, Mwana falsafa Spinoza aliwahi kusema
“kifo hakiwezi kuepukika. Ni lazima tutakukufa. Kinachotusumbua ni hofu kuhusu
kifo. Hivyo yatupasa kuishinda hofu. Na hivyo ni vizuri kufikiri kuhusu uhai.”
Mpendwa, je wamwamini Kristo Yesu? Kama unamwamini Kristo Yesu hakuna sababu ya
kuwa na hofu kuhusu kifo. Kristo Yesu kwa maisha yake, mateso, kifo, na ufufuko
wake ni jibu kuhusu aina zote za uovu na kifo. Kristo Yesu ndiye kielelezo
chetu kama wafuasi wake. Kristo Yesu ametupatia mfano na jibu kwamba hakuna
uovu wowote unaoweza kudumu katika umilele wake. Yesu haogopi vitisho wala
kifo.
Yesu anapoambiwa aondoke kwa kuwa Herode anataka kumuua
aliwajibu, “Nendeni, mkamwambie yule mbweha,
Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,”
Lk 13:32. Mnyama huyu Mbweha alitafsiriwa kama mtu asiye na msimamo, kigeugeu
na mwongo. Kristo hawezi kutishiwa na
mtu wa hali hii na kuacha kutoa huduma kwa watu ikiwa ndiyo sababu na mpango
kazi wake kwa watu wote. Ni kwa kupitia Kristo “vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma
wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa
habari njema,” Mt 11:5. Kristo pia anaufunua utukufu wake mara baada ya
kuushinda uovu anaposema, ‘siku ya tatu nakamilika.’
Mateso tunayoyapata leo au tuliyokwisha yapata kupia wazazi
wetu, siyo kwamba historia hiyo ya uovu Mungu haioni. Wakati utimiapo vyote
vitafanywa upya. Yesu anapoutazama mji wa Yerusalemu anayakumbuka na kuyaona
mateso na uovu wa manabii wake walifanyiwa na kusema, “Ee Yerusalemu,
Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi
nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake
chini ya mbawa zake, wala hamkutaka,” Lk 13:34. Huu kwetu ni wito wa kuongoka na kuacha njia zetu
mbaya na kujisalimisha kwa Kristo. Tusisubiri hadi siku ya Mwisho kwani
hatutakuwa na muda tena wa kujisalimisha kwake. Utakuwa muda wa kupokea ukumu
yetu kila mmoja kadiri alivyotenda. Yesu anasema, “Angalieni, mmeachiwa nyumba yenu! Nami nawaambia, Hamtaniona
tena kamwe, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana,” Lk 13:35.
Je, kuna sababu ya kusubiri hadi siku ya mwisho? Ndugu yangu natuanze kuishi
maisha ya ufufuko kabla ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.
Maisha baada ya ufufuko ni maisha yaliyokamili. Tunayaishi
maisha haya ya ufufuko kwa kuhesabiwa haki na kwa kuzaliwa mara ya pili kwa
Roho Mtakatifu. Hivyo “si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa
rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho
Mtakatifu; ambaye alitumwagia kwa
wingi, kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu; ili
tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate kufanywa warithi wa uzima wa milele,
kama lilivyo tumaini letu,” Tit 3:5-7. Je, una sababu yoyote ya kuwa na hofu
juu ya maisha yako ukiwa na Kristo?
Tukiwa
ndani na katika Kristo tu wateule wa Mungu na hakuna wa kutushitaki kwa sababu
Mungu kwa kupitia mwanaye Mpenzi ndiye anayetuhesabia haki. Basi “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye
kuwahesabia haki,” Rum 8:33. Katika hali hii hakuwa wa kutuhukumia adhabu kwa
sababu tumeshayasalimisha maisha yetu kwa Kristo mwenyewe aliyekubali kufa kwa
ajili yetu. “Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake,
kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake,” Rum 6:5. Hapa adhabu ya
kifo na hofuzimebatilishwa kwa kifo chake Kristo. Hivyo “Ni nani
atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka
katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea,” Rum
8:34.
Ndugu yangu, Kristo akupende vipe tena uamini
anakupenda? Huku ndipo Kristo alipotupenda upeo na wakati ulipofika aliyatoa
maisha yake kwa sababu yako na yangu. “Basi,
kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika,
atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake
katika ulimwengu, aliwapenda upeo,” Yoh 13.1. Upendo huu hadi leo Kristo
anauthibitisha kwetu tunapoutazama msalaba akiwa ameifungua mikono yake na
kusema, ‘tazama ninavyokupenda nimekubali kufa kwa sababu yako.’
Tunapo jisalimisha kwa Kristo hakika nguvu za giza na uovu
wa aina yoyote ile hauwezi ukashinda kwa sababu Kristo anatupenda. “Lakini katika mambo
hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda,” Rum 8:37.
Kutokuwa na Imani pamoja na kutengemea vitu vingine mfano pesa na mamlaka
fulani ni moja ya vizuizi vinavyotufanya kushindwa kujisalimisha kwa Jemedari
wetu Yesu Kristo.
Wapendwa
wana wa Mungu, tunapojisalimisha kwa Kristo hakuna
kitu wala kiumbe chochote kinachoweza kututenganisha na upendo wake. Paulo
anasema, “kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala
uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo,
wala wenye uwezo, wala yaliyo
juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na
upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 8:38-39. Ndugu yangu
tunayesafiri wote kwenye tafakari hii, bado tu hujakata shauri la kujisalimisha
kwa Kristo? Kama bado anza sasa taratibu. Wengine inawachukua muda mrefu na
wengine ni rahisi tu. Moja ya njia ya kujisalimisha kwa Kristo ni kuwa tayari
kufanya atakayo na apendayo Kristo hata pale tusipotaka kufanya hivyo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Sasa, basi, hakuna
hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu,” Rum 8:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario