jueves, 22 de octubre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 29 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 29 YA MWAKA-B
22/10/2015
Somo: Rum 6:19-23
Zab: 1:1-2, 3, 4, 6
Injili: Lk 12:49-53
Nakuu:
Nasema kwa jinsi ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu. Kwa kuwa kama mlivyovitoa viungo vyenu vitumiwe na uchafu na uasi mpate kuasi, vivyo hivyo sasa vitoeni viungo vyenu vitumiwe na haki mpate kutakaswa,” Rum 6:19

Lakini sasa mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele,” Rum 6:22 

Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 6:23

Je! Mwadhani ya kwamba nimekuja kuleta amani duniani? Nawaambia, La, sivyo, bali mafarakano,” Lk 12:51 

Kwa kuwa tokea sasa katika nyumba moja watakuwamo watu watano wamefarakana, watatu kwa wawili, wawili kwa watatu,” Lk 12:52 

Watafarakana baba na mwanawe, na mwana na babaye; mama na binti yake, na binti na mamaye; mkwe mtu na mkwewe, mkwe na mkwe mtu,” Lk 12:53

TAFAKARI: “Lenga kwenye ukamilifu ingawa kuna udhaifu pia.”

Wapendwa wana wa Mungu, moja ya njia ya kukua kiroho ni ule utayari wa kujisahihisha makosa. Asiyependa kujisahihisha makosa yake na kuwa tayari kufuata njia iliyo sahihi, ni vigumu kwa mtu huyo kubadilika na kukua kiroho. Ukweli huu ni kwa kila mwenye hofu ya Mungu, na kwa namna ya pekee wale wenye dhamana ya uongozi. Utayari wa kujisahihisha makosa ni moja ya sifa ya kiongozi bora na makini. Na kwa kupitia yeye wengi huona mwanga kwa sababu yeye ni kioo cha jamii husika.

Katika shughuli zetu za kila siku si kila mara mambo yatakwenda vema. Tunaweza kukosea hapa na pale. Basi tuwe tayari kusahihishwa na kujisahihisha. Tujisahihishe kweli. Tunajifunza kutoka makosa yetu na ya wenzetu. Zaidi ya hayo tusiyaache makosa yatokee kwa makusudi. Tujitahidi kuzuia makosa na mapungufu mengine yoyote yasitokee. Tulenge kwenye ukamilifu ingawa kuna udhaifu pia.

Masomo yetu ya leo yanalenga katika fundisho hili la ukamilifu ingawa kuna udhaifu kama wanadamu. Nasema kwa jinsi ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu. Kwa kuwa kama mlivyovitoa viungo vyenu vitumiwe na uchafu na uasi mpate kuasi, vivyo hivyo sasa vitoeni viungo vyenu vitumiwe na haki mpate kutakaswa,” Rum 6:19. Kila mmoja wetu naujua udhaifu wake, na anajua ni kiungo gani cha mwili wake kinachomtatiza kuufikia huo ukamilifu. Pamoja na binadamu kuwa na viungo vingi, embu tuutazame kiungo ULIMI. Kiungo hiki ulimi kimezungumzwa mara 85 katika Maandiko Matakatifu. Mtume Yakobo anatuambia hivi kuhusu ulimi: Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum,” Yak 3:6. Mbaya zaidi ulimu kwa kiasi kikubwa ulimi huu haujazungumziwa vizuri kadiri ya Maandiko Matakatifu. Ulimi unaweza kufarakanisha kila kitu, iwe imani, dini, siasa, umoja wetu kama Taifa, na hata mahusiano ya karibu kwa wapendanao. Ni muhimu sana mtu kuutumia ulimi wake vizuri hasa pale tunapotaka kutoa ujumbe wowote ule. Hivyo, Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai,” Yak 1:26. Ndugu yangu, kama kweli wewe una hofu ya Mungu, iweje basi umnenee binadamu mwenzako mabaya ilihali nawe unaelekea huko huko unapomnenea mabaya mwenzako? Kwa nini basi unakata tawi ulilolikalia mwenyewe?

Wapendwa wana wa Mungu, lengo la kujisahihisha katika madhaifu yetu ni kuupata huo utakaso ili tuweze kuufikia huo uzima wa milele tulioandaliwa. Huko ndiko kuwekwa huru kutoka utumwa wa dhambi, na kuhesabiwa haki kadiri ya mapenzi yake Mungu. Lakini sasa mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele,” Rum 6:22. Je, mwenzangu hupendi faida hiyo itokanayo na kuushinda udhaifu wako? Basi anza sasa kujichunguza ni wapi kila mara wajikuta unadondoka katika dhambi. Anzia hapo hapo kujisahihisha na kupata huo utakaso. Kama wewe ni Mkristo Mkatoliki baada ya kujichunguza na kuona mkwamo wa wewe kukua kiroho, usichoke kujongea sakramenti ya upatanisho. Kajipatanishe na Mungu, hakimu mwenye haki na upendo wa kweli.

Mpendwa mwenye hofu ya Mungu, wakati ndiyo sasa. Tatizo kubwa la kutokujisahihisha na kujisalimisha kwenye utakaso ni pale mtu anapofikiri bado anao muda wa kutosha kufanya hivyo. Muda kamwe haumsubiri mtu. Unapoguswa na ujumbe huu chukua hatua mara. Hakuna kesho kama hakuna leo. Na unaloweza kulifanya leo lisingoje kesho. Kudumu katika hali ya dhambi kwa muda mrefu kuna madhara mengi sana katika maisha yako ya kiroho. Moja ya dhara kubwa ni kuwa katika hali hatarishi ya umauti. Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 6:23. Je ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii hupendi karama ya Mungu, yaani, uzima wa milele tuupatao katika Kristo Yesu Bwana wetu?

Uzima huo wa milele ndani na katika Kristo Yesu tunausikia leo kutoka katika kinywa chake mwenyewe hasa kwa maneno haya ya kuchukua hatua tukiwa tunajitathimini maisha yetu ya kiroho. Naye anatuambia, Je! Mwadhani ya kwamba nimekuja kuleta amani duniani? Nawaambia, La, sivyo, bali mafarakano,” Lk 12:51. Ni mafarakano katika maana ya vita dhidi ya ubinadamu wetu. Kumfuata Kristo katika ukamilifu yakupasa kuushinda ubinadamu wako kwa kulenga ukamilifu ingawa udhaifu upo. Ni kwa kupitia Kristo aliyeushinda uovu kwa wema, yaani kuwa tayari kufa kwa ajili yangu na wewe weweza kuishinda vita hii. Msalaba ni ishara ya huo ushindi wa wema dhidi ya uovu. Mimi na wewe,  nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14.  Je, watambua nguvu ya msalaba katika maisha na wokovu wako?

Wapendwa kama upo tayari kufanywa upya katika ukamilifu ndani na katika Kristo Yesu, uwe tayari kupokea sintofahamu kwako na wale walikuwa nawe karibu kwa sababu ya ubinadamu wako na yale waliyokuwa wakiyafurahia kutoka kwako. Ukiwa rafiki wa kweli na karibu wa Yesu, giza la uovu litakuwa na vita kubwa na mwanga wa Kristo ndani ya maisha yako. Hivyo Yesu anatupatia changamoto hii kwa kusema, Kwa kuwa tokea sasa katika nyumba moja watakuwamo watu watano wamefarakana, watatu kwa wawili, wawili kwa watatu,” Lk 12:52. Hii ni vita Takatifu ya kiroho yenye kulenga ukamilifu wa kweli utupelekao kwenye uzima wa milele. Yesu hakuishia hapo tu. Anatuambia vita hii huenda hata kwa ndugu zetu wa damu. Je, upo tayari kufarakana na familia yako, Baba, Mama, na ndugu zako katika kweli na haki juu ya Kristo Bwana na mwokozi wako?

Katika ukweli huo wa kuelekea ukamilifu na uzima wa milele, Yesu anatuambia, watafarakana baba na mwanawe, na mwana na babaye; mama na binti yake, na binti na mamaye; mkwe mtu na mkwewe, mkwe na mkwe mtu,” Lk 12:53. Unapoamua kumfuata Kristo hakuna mbadala wake ikiwa ni pamoja na kutazama nyuma. Ni heri kuwa baridi au moto kuliko kuwa vuguvugu katika Imani. Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mt 10:22. Kwa maana nyingine, hakuna utukufu pasipo msalaba. Mtihani mkubwa kupita yote kwa mwanadamu ni kushindwa kufanya maamuzi ya kina kuhusu hatma ya maisha yake. Pale tunaposhikwa kigugumizi cha kuacha mazoea yetu na kufuata njia mpya na mwelekeo mpya katika maisha, mwanadamu huishia masikini wa mwili na roho.

Tumsifu Yesu Kristo!


Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?” Zab 27:1

No hay comentarios:

Publicar un comentario