JUMATANO WIKI YA 27 YA MWAKA-B
7/10/2015
Somo: Yon 4:1-11
Zab: 85:3-6, 9-10
Injili: Lk 11:1-4
Nukuu:
“kwa maana nalijua ya kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa
huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, nawe waghairi mabaya,” Yon
4:2c
“Basi, sasa, Ee Bwana, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana
ni afadhali nife mimi kuliko kuishi,” Yon 4:3
“Akawaambia, Msalipo, semeni, Baba [yetu uliye mbinguni],
Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, [Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani
kama huko mbinguni.]” Lk 11:2
“Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila
tumwiaye. Na usitutie majaribuni [lakini tuokoe na yule mwovu],” Lk 11:4
TAFAKARI: “Mungu anakupenda
kama ulivyo kwani ni mwingi wa huruma, rehemu, hughairi mabaya.”
Wapendwa
wana wa Mungu, bila shaka ulishajikuta una ukavu wa sala na kutokuona uwepo wa
Mungu na wakati mwingine kama umesahaulika kwa sababu tu yawezekana unaishi
katika hali ya hatia. Kuishi katika hatia fulani ni sawa na kujiweka mwenyewe
katika gereza na kushindwa kutoka ilhali ufunguo unao.
Mtu anayeisha katika
hatia, hutumia muda wa maisha yake yote kupekua lawama na kuficha aibu. Hivyo
watu wanaoongozwa na hatia wanaonewa sana na kumbukumbu. Wanaruhusu mambo
yaliyopita kutawala mambo yao ya usoni.Wanajiadhibu bila kujua kwa kuharibu
mafanikio yao. Kaini alipotenda dhambi, hatia yake ilimtenga na Mungu, na Mungu
akasema, "utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu
asiye na kikao duniani," Mwa 4:12. Hii inawaeleza jinsi watu wengi walivyo
siku hizi-wanatangatanga katika maisha bila lengo. Mfano mzuri angalia katika
vyama vyetu vya kitume. Wapo walio wengi huama chama kimoja cha kitume kwenda
kingine na mwisho huishia katika nyumba za sala. Nyumba za sala hapa
ninamaanishisha vijikanisa vinavyojiibua na kujiinua kwa wachungaji wao kuwa
manabii.
Ndugu yangu, sisi ni
matokeo ya muda wetu uliopita lakini hatupaswi kuwa wafungwa wa muda huo.
Kusudi la Mungu halifungwi na muda wako uliopita. Ona! Alimbadilisha muuaji
Musa na kuwa kiongozi mzuri; akambadilisha Gidioni aliyekuwa mwoga akawa shujaa
na hodari; anaweza kufanya mambo ya ajabu na maisha yako yaliyobaki. Tazama pia
maisha ya Mt. Augustino wa Hippo kabla na baada ya kuongoka kwake.
Mungu ni mtaalam wa
kutupa mawazo mapya. "Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa
yake," Zab 32:1. Kwa maana nyingine twaweza kusema, "wana furaha
kubwa wale waliosamehewa hatia zao. Na wana amani wale waliotubu dhambi zao na
Mungu amefuta mashtaka yao."
Kwa namna hii tunamwona
Nabii Yoha anajihukumu na kuchagua kufa kwa sababu ya kuhisi Mungu amemtenga na
kumwacha. Hata hivyo Nabii Yona anajua kwa uhakika Mungu anayemtumikia jinsi
alivyo, na kusema, “nalijua ya
kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi
wa rehema, nawe waghairi mabaya,” Yon 4:2c. Hata pamoja na kujua ukweli huu,
bado Yona haoni uwepo wa Mungu katika shida zake. Hivyo kwa kukata tamaa
anaamua afe. “Basi, sasa, Ee Bwana, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana ni afadhali
nife mimi kuliko kuishi,” Yon 4:3. Uhai huo ambao Yona anaotaka kuuondoa siyo
mali yake. Uhai ni mali ya Mungu na zawadi ya Mungu. Kujiua kwa kukimbia matatizo
siyo njia sahihi ya kufanya. Na kukata tamaa ni kumkufuru Roho Mtakatifu.
Dhambi hii haisamehewi. “Kwa sababu hiyo nawaambia, Kila dhambi na kila neno la
kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasamehewa,” Mt 12:31
Pamoja na hatia alizokuwa nazo mtu, Mungu hubaki kuwa HURUMA,
MSAMAHA, UPENDO NA AMANI yetu. Huruma hii na upendo huu wa Mungu, tunaiona
katika sala ya Baba yetu ambayo leo mmoja wa wanafunzi wa Yesu anamwomba Yesu
awafundishe namna ya kusali. Katika sala hii inatufundisha na kuweka wazi ni
nani aliyekimbilio letu la pekee, na mapaswa yetu tungali hapa duniani. “Akawaambia, Msalipo, semeni, Baba [yetu uliye
mbinguni], Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, [Mapenzi yako yatimizwe, hapa
duniani kama huko mbinguni.]” Lk 11:2. Jambo
lingine la msingi ni
huruma ya Mungu kwa msamaha wa makosa yetu inayotokana na kiwango kile kile cha
sisi kuwasamehe wale waliotukosea. “Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi
tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni [lakini tuokoe na yule
mwovu],” Lk 11:4. Wapendwa wana wa Mungu, kama kipimo cha kupenda ni kupenda
bila kipimo kama asemavyo Mt. Agustino, basi ni hivyo hivyo masharti ya
kusamehe ni kusamehe bila masharti.
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU TUJALIE NEEMA YA KUVUMILIA MATESO. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario