viernes, 16 de octubre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 29 YA MWAKA-B

JUMAPILI YA 29 YA MWAKA-B
18/10/2015
Somo I: Isa 53:10-11
Zab: 33:4-5, 18-19, 20, 22
Somo II: Ebr 4:14-16
Injili: Mk 10:35-45
Nukuu:
Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake,” Isa 53:10

“Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao,” Isa 53:11b

Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu,” Ebr 4:14

Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15

Wakamwambia, Utujalie sisi tuketi, mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika utukufu wako,” Mk 10:37

Yesu akawaambia, Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?” Lk 10:38

“Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari,” Mk 10:39b-40 

“bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10 43b-44

Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45

TAFAKARI: “Hakuna Utukufu pasipo Msalaba. Basi, tumika na siyo kutumikiwa ndani na katika Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 29 ya mwaka “B.” Masomo yetu ya leo yanatualika tutafakari juu ya Utukufu utupatao baada ya Msalaba. Na ili tuufikie ufalme wa Mungu yatupasa kutumika na siyo kutumikiwa ndani na katika Kristo. Utukufu ni tokeo la kukubali mateso katika mwono wa ukamilifu kwa kile tukitamanicho kuwa, au tusichokijua lakini chenye mwono wa wokovu kwetu na kwa wenzetu. Somo letu la kwanza na la pili yamezungumzia kwa kina juu ya dhana hii ya msalaba au mateso, na uhusianao wake na Utukufu. Nabii Isa anatuonyesha ni kwa namna gani mtu aweza kuteseka kwa ajili ya wengine kwa maridhio ya Mungu Mwenyewe.

Mtu huyo aliyetabiriwa na Nabii Isaya ndiye Kristo, neno aliyefanyika mwili, na hasa katika fumbo zima la Pasaka. Nabii Isaya anatoa sifa na mwelekeo wa huyu aliye ufia ulimwengu kwa sababu ya dhambi za watu ingawa yeye hakuwa na kosa lolote.Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake,” Isa 53:10. Tunapoyatazama mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo ni dhahiri kabisa hayakwenda tofauti na yale aliyoyatabiri Nabii Isaya. Tumehesabiwa haki kwa mateso ya Kristo na kurudishiwa hadhi yetu kama wanadamu na warithi wa ufalme wa Mbinguni ambapo uliondolewa kwa anguko la Wazazi wetu wa kwanza, Adam na Eva. Hivyo, “Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao,” Isa 53:11b. Ni ukweli usiotia shaka kwamba mimi na wewe tumekombolewa kwa gharama kubwa sana na yenye thamani isiyo elezeka. Ukweli huu anauthibitisha Mtume Petro kwa kusema, “Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19. Kulipa shukrani hii kwa Kristo aliyetufia ni kuwa tayari kutumika kwa ajili ya wengine bila kujibakiza kama alivyofanya.

Kuhani wetu huyu Mkuu Yesu Kristo, ndiye Hakimu wetu wa haki. Siku yaja na imekaribia kwa kila mwenye punzi sasa ambapo tutatakiwa kujibu ni kwa namna gani tumewapenda wengine na kujitoa kwao kama alivyofanya yeye, Kristo. Kulijibu swali hili vizuri yatupasa kujua tupo leo katika ulimwengu huu kwa lengo gani la muhimu. Ikiwa kwa miezi tisa tumboni ilikuwa maandalizi ya kuishi katika ulimwengu huu, basi tuelewa tupo hapa duniani kwa maandalizi ya maisha ya umilele. Hivyo kifo chake ni siku ya kuzaliwa katika maisha ya umilele endapo ulijiandaa vyema. Kwa maana hiyo, ili tukutane na Kuhani wetu Mkuu huko mbinguni yatupasa kuyashika vyema na kwa uaminifu maagano yetu tungali hapa duniani. Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu,” Ebr 4:14. Ni kweli pia katika kuyashika maagano haya ya maisha, iwe maisha ya ndoa, utawa, au ukleri hatuwe kukwepa misalaba. Tutakutana na Kristo aliyeushinda msalaba katika maagano yetu haya iwapo tutayaishi maagano hayo kwa uaminifu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15. Uaminifu katika agano lako na Mungu ndiyo salama yako katika maisha ya umilele.

Wapendwa wana wa Mungu, baada ya kuona uhusiano wa msalaba na utukufu tuupatao baada ya kuyaishi kwa uaminifu maagano yetu katika maisha, Yesu katika injili ya leo, anatupa changamoto ya msingi. Ni kweli hakuna mwanadamu anayependa shida kwa urahisi. Kila mmoja wetu angependa kuishi ndoto yake hata kama haitekelezeki. Binadamu yupo hivyo kwa sababu ndani yake Mungu amemwekea hali ya kutamani. Tatizo siyo kutamani, ila tatizo lipo tunapoyaelekezea matamanio yetu. Yakobo na Yohana wana wa Zebedayo wanaonyesha matamanio yao ya kuketi kuume na kushoto mwa Yesu katika utukufu wake. Ndugu hawa wawili wanamdai Yesu awafanyie lolote lile awezalo ili waikamilishe tamaa yao.

Tukizama zaidi katika maneno ya ndugu hawa wawili katika mtazamo wa jamii yetu ya leo Tanzania, tungeweza kusema kwamba, ndugu hawa wapo tayari hata kutoa rushwa ili tu katika ufalme wa Kristo wawe pembeni yake. Katika jambo hili, Yesu Kristo hayupo tayari kubomoa nguvu ya kimaadili aliyokuwa nayo hata kama angeona inafaa kufanya hivyo. Kristo Yesu ni KWELI, NJIA, UZIMA, HAKI, AMANI, UPENDO, na zaidi, hayo yote yamebebwa katika UNYENYEKEVU wake. Yesu anawauliza ndugu hawa swali la msingi baada ya kuona hawajui wakiombacho. “Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?” Lk 10:38. Yesu anawakumbusha ndugu hawa na sisi pia kwamba “ukiona vinaelea ujue vimeundwa.” Hivyo, kufikia hatua fulani kimaisha, iwe kimwili au kiroho inamapaswa yake. Ndugu hawa licha ya kutokujua kwao kwa kile wakiombacho, hawakuacha kushupalia matamanio yao. Yesu kwa mara nyingine haterereki katika misingi ya kweli na haki katika maadili. Naye anawajibu, “Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari,” Mk 10:39b-40. Hapa Yesu anagusa hatua ya pili katika makuzi ya kiroho.

Wapendwa katika Kristo, kama yote tulionayo na kile tulicho si mali yetu ni mali ya Mungu, basi ni kwa namna hiyo hiyo kwamba ni Mungu mwenyewe mwenye kutuhesabia haki. Tupo kama tulivyo kwa neema ya Mungu. Mtume Paulo anatuambia, Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10. Kumbe ni vyema kwanza kutimiza wajibu wetu katika kuwajibika na kutumika kwa ajili ya wengine bila kujibakiza ndipo tutakapo nyanyuliwa kadiri ya mapenzi ya Mungu na siyo yetu. Hii ndiyo hatua ya pili ya kukua kiroho. Hatupaswi kujihesabia haki kwa yale tulionayo au yale tuyafanyayo, bali tuwe tayari muda wote kutumika kwa ajili ya wengine bila kujibakiza. Huu ndio unyenyekevu katika kujitoa kama asemavyo Yesu, kwamba, “bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10 43b-44. Hili ndilo tunalopaswa kulifanya kama wafuasi wake Yesu, na watu wenye hofu ya Mungu. Tunaishi na kuyafanya aliyofanya Kristo tukitambua ukweli huu kutoka kwake mwenyewe. Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45.

Wapendwa katika Kristo, nimalize kwa mchapo huu. Alikuwepo mama mmoja aliyekuwa chongo na mwanae Zawadi alimchukia kwa sababu ya kuwa chongo. Zawadi alijisikia aibu kutembea na mama yake mwenye jicho moja na hakupenda watu wajue kuwa yule ni mama yake.

Hata alipokuwa shuleni Zawadi hakupenda mama yake amtembelee, na ilitokea mama yake akamtembelea basi watoto wenzie watamcheka siku nzima na kumtania. Hii ilimfanya Zawadi kujisikia vibaya sana na wakati mwingine kujuta kuwa na mama wa aina hiyo.
Lakini mama alimpenda mwanae na hakuonyesha kukasirika hata pale mwane alipomnyanyapaa waziwazi.

Baadaye Zawadi akakuwa akamaliza masomo yake na kupata kazi nzuri. Akafurahi kuwa sasa amepata kazi atakuwa mbali na mama yake “chongo” anayemtia aibu.

Zawasi akachagua kufanya kazi mji wa mbali na alipo mama yake. Akafanikiwa kazini kwa kupandishwa cheo na akawa mtu mashuhuri mwenye mali na mwenye heshima kubwa katika jamii yake.

Siku moja asubuhi Zawadi alisikia wanawe wakilia wakipokua nje wakicheza. Alipowaukiza wakasema kuna mtu anawatisha. Akatoka nje kujua nani anayewatisha wanawe. Kufika akamkuta mwanamke mmoja mzee mwenye jicho moja (chongo). Kumbe wale watoto walitishwa na chongo la yule bibi.

Zawadi alipomtizama vizuri yule mwanamke akamgundua ni mama yake mzazi. Alikuwa amechoka na amezeeka sana. Amedhoofika mwili na anaonekana mgonjwa

Zawadi kwa hasira akamuuliza, “Mama umejuja kufanya nini hapa? Kama una shida ungenipigia simu sio kuja. Kwanza nan kakuonyesha ninapoishi? Na nani kamruhusu mlinzi kukufungulia mlango? Ona sasa umewatisha wanangu kwa chongo lako.”

Mama yake akamjibu, “samahani mwanangu, sikujua naomba unisamehe.” Kisha Zawadi akamchukua mama yake akamtoa nje na kumpeleka kituo cha basi ili arudi kijijini.

Baada ya siku chache kupita, yule Zawadi akapata taarifa kuwa mama yake ni mgonjwa sana na anahitaji kumuona. Akaondoka kwa siri kwenda kijijini ili akasikie mama yake anataka kumwambia nini.

Zawadu alipofika akakuta watu wengi wamekusanyika nyumbani kwao. Alipouliza akaambiwa mama yake alifariki baada ya kuugua sana bila msaada wowote.

Alipoingia ndani Zawadi akakuta barua aliyoandika mama yake. Barua ilisomeka hivi:

“Kwako mwanangu mpendwa wa pekee Zawadi. Naandika barua hii nikiwa kwenye maumivu makali sana na sijui kama nitapona. Nimeugua nikakosa matibabu kwa kutokuwa na fedha. Sikuwa na mtu mwingine wa kumueleza shida yangu zaidi yako wewe mwanangu wa pekee. Lakini nilipojitahidi kuja kwako angalau unisaidie matibabu ulinifukuza na kudai nawatisha wanao kwa chongo langu! Uliniumiza sana mwanangu sitisahau maishani mwangu ila nimekusamehe.

Baba yako alifariki ukiwa mdogo sana. Nami sikubahatika kupata mtoto mwingine. Nilikulea kwa nguvu zangu zote na umasikini niliokuwa nao nilikuwa nikitegemea baadaye utanisaidia lakini umenitelekeza na kunitupa kwa sababu tu mimi mama yako ni chongo! Hivyo unaona aibu kuwa nami.

Nisamehe kwa kuwatisha wanao kwa chongo langu, nisamehe kwa kuja kwako bila taarifa, nisamehe kwa kukufanya uchekwe na wenzio kwa kuwa mimi mama yako ni chongo.

Lakini naomba nikupe siri ambayo hukua unaijua ewe mwanangu. Wewe ndiye uliyezaliwa ukiwa chongo. Ulikuwa na jicho moja tu. Nikaumia sana kuona mwanangu ana jicho moja, atawezaje kuishi na kukabiliana na changamoto za maisha. Nikaomba madaktari wanitoe jicho langu moja wakupe wewe. Niliona ni heri mimi niwe chongo kwa kuwa nimeshaona mengi sana duniani.

Zawadi, ulipowekewa jicho langu nilifurahi kukuona una macho mawili nikajua utaweza kuzikabili vema changamoto za dunia hii. Na hakika jicho langu limekusaidia kwani wewe ni mtu mashuhuri na tajiri sana kwa sasa.

Lakini kwa jinsi ninavyoumwa najua nitakufa. Ila nafurahi kwamba nakufa nikiwa nimetimiza haya ya moyo wangu. Kwa kutumia jicho langu umeweza kuwa msomi mzuri na tajiri unayeheshimika na jamii yote. Wasalimie wajukuu zangu na waambie wawe na amani hawataniona tena nikienda kuwatisha na chongo langu. Tafadhali litunze jicho langu.

Akupendaye,
Mama.”

Alipomaliza kuisoma barua hii akalia sana. Akatamani mama yake afufuke amuombe msamaha na amlipe kwa wema wake aliomtendea. Lakini haikuwezekana tena. Alikuwa kesha chelewa!

Wapendwa katika Kristo, mafanikio yako yanaweza kuwa ni matokeo ya Wazazi wako, mke wako, mume wako, dada yakeo au mchumba wako. Je, unatambua nafasi yao kati ya hao katika mafanikio yako au unapuuza tu?

Kwa namna ya pekee yawezekana wapo walijitoa sadaka sana ili uweze kuwa hapo ulipo. Jiulize kwa mfano wazazi wako wamefanya mangapi kukufikisha hapo ulipo? Leo kwa mfano akina Mama zetu ni wafia dini katika Kanisa la leo na jamii ya leo. Wanataabika sana juu ya familia na watoto wao. 

Wapo miongoni mwetu jicho lao ni wale ambao vibarua alivyokuwa anafanya ili wewe usome. Pengine jicho lake ni namna alivyokuwa akijinyima kwa kuvaa nguo moja mwaka mzima ili upate ada ya shule na mahitaji mengine. Wengine tumesoma na kufikia hapa tulipo kwa mama zetu kufanya biashara za kuuza ndizi na pombe kila kikicha. Je, umewahi kumshukuru mtu huyo kwa kwa kutoa jicho lake kwa ajili yako?

Kwa kifo na ufufuke wake Bwana wetu Yesu Kristo tumepewa jicho la kuuona na kuurithi ufalme wa Mbinguni. Ndugu yangu, shikamana naye katika kujitoa bia kujibakiza kama kielelezo cha kutumika kwako ndani na katika Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!


“Ee Bwana unifanye chombo cha Amani yako,” Mt. Franscisco wa Assis

No hay comentarios:

Publicar un comentario