JUMAMOSI WIKI YA 29 YA MWAKA-B
24/10/2015
Somo: Rum 8:1-11
Zab: 24:1b-2, 3-4ab, 5-6
Injili: Lk 13:1-9
Nukuu:
“Kwa sababu sheria ya
Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya
dhambi na mauti,” Rum 8:2
“Kwa maana wale waufuatao
mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya
roho,” Rum 8:5
“Kwa kuwa nia ya mwili
ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani,” Rum 8:6
“Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza
Mungu,” Rum 8:8
“Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani
yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote
asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake,” Rum 8:9
“Lakini, ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua
Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu
ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa
ndani yenu,” Rum 8:11
“Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya
kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata
wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2
“Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu,
ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:3
“Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka
huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo
uukate,” Lk 13:8-9
TAFAKARI: “Kwa
kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake.
Utukufu una yeye milele. Amina.”
Wapendwa wana wa Mungu, tunapotafakari
masomo ya leo ni vema kufahamu jambo hili la msingi kuhusiana na uumbaji wetu
na sababu ya kuishi kwetu. Napenda kuyachukua maneno haya ya Mtume Paulo
kwamba, “kwa kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea
kwake. Utukufu una yeye milele. Amina,” Rum 11:36. Jambo la msingi hapa ni
ukweli kwamba Mungu hakuhitaji kukuumba wewe, bali alichagua kukuumba kama
ulivyo kwa furaha na utukufu wake. Kwa maana hiyo, maisha yetu hapa duniani
yapaswa kuufunua, kuuonyesha Utukufu wa Mungu, na furaha yake.
Ndugu zangu katika Kristo, mwanadamu
angali akiwa hapa duniani utoa Utukufu wa Mungu na furaha yake kwa kufanya
mambo yafuatayo: Kwa kumwabudu Mungu, yaani maisha yake yote, kwa kuwapenda
watu wengine bila kubaguana, kwa kuishi na kuwa kama Kristo, kwa kutumia vipaji
kwake vyote kwa ajili ya wengine, yaani kufaidiana, na kwa kueneza habari njema
za Mungu kila pande za dunia. Hata hivyo licha ya ukweli huu, mwanadamu huyu
anaweza kuufunua utukufu wa Mungu na furaha yake kwa kutenda matendo ya roho,
Gal 5:22-23, na siyo yale ya mwili yasiyo na uzima ndani yake, Gal 5:19-21. “Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na
amani,” Rum 8:6. Mtu hawezi kumpenda Mungu
kama anafuata matendo ya mwili wake tu. Ni kweli kwamba kiini cha dhambi ni
pale mtu anapojipenda yeye zaidi kuliko Mungu. “Wale waufuatao mwili
hawawezi kumpendeza Mungu,” Rum 8:8. Hivyo
basi kama tunataka kuishi na kuwa kama Kristo lazima tufuata sheria ya roho,
yaani, matendo ya roho, ambayo ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu
wema, fadhili, uaminifu, upole,
kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria, Gal 5:22-23. Uzima huu tuupatao
kwa matendo ya roho upo ndani ya Kristo pale tunapotaka kuishi na kufanana
naye. “Kwa sababu sheria ya
Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya
dhambi na mauti,” Rum 8:2. Hivyo kwa kuishi
na kufanana kama Kristo tunaufunua Utukufu wa Mungu na furaha yake ya kutuumba.
Wapendwa wana wa Taifa la
Mungu, kwa upande mwingine, sheria ya dhambi ni matendo yale yasiyo na uzima
ndani yake, na kwayo kamwe hatuwezi kuurithi ufalme wa Mungu. Matendo haya ni
haya; uasherati, uchafu,
ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina,
faraka, uzushi, husuda, ulevi,
ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.
Mtume Paulo anasisitiza kwamba, “katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Je, hutaki kuurithi ufalme wa Mungu
na maisha ya umilele?
Kuishi na
kutenda kwetu ili kuwe kwa sifa na utukufu wake Mungu kwa tulazimu kufikiria
mambo ya roho. “Kwa maana wale
waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri
mambo ya roho,” Rum 8:5. Ndugu yangu, utawezaje basi kuishi na kufanana na
Kristo kama muda wote wa ufuata mwili na kufikiri mambo ya mwili? Hii ni
changamoto kwa kila mmoja wetu. Ni kweli kwamba hatuwezi kuyawaza ya roho kama
hatuna mwili. Jambo la msingi na la kufahamu hapa ni kwamba ‘vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena
vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele,’ Rum 11:36. Hivyo hakuna kilicho
chako katika maana ya umiliki halali zaidi ya dhambi zako. Sasa nifanye nini
katika hali hii?
Wapendwa katika Kristo, tunahitaji roho wa Kristo ndani
yetu ili tuyafuate matendo ya roho na mwisho tuwe mali ya Kristo. Roho huyu ni
zawadi kwetu kutoka kwa Mungu, na hufanya kazi ndani yetu kadiri apendavyo yeye
kututumia kadiri ya mpango mzima wa Mungu. Hivyo, “ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani
yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo
katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu,” Rum 8:11. Hapa ndipo
tunapoona Upendo na Huruma ya Mungu kwetu. Mungu hapendi hata mmoja wetu apotee
kwa sababu ya dhambi zake. Mimi na wewe tunapewa kila siku fursa ya kutubu na
kumrudia Mungu. Katika mantiki hii yanipasa kuzitazama dhambi zangu, kuzitubu,
na mwisho kuwa huru kutoka utumwa huu wa dhambi. Ni kwa namna hiyo hiyo sina
haki wala sababu ya msingi kuwanyooshea vidole wengine ilhali mimi mwenyewe
nahitaji Upendo na huruma ya Mungu.
Injili ya
leo inatuasa kutumia vyema fursa hii ya upendo na huruma ya Mungu kwa kuishi
matendo ya roho na kuachana na matendo ya mwili. Tusipoteze Muda mwingi
kuzitazama dhambi za watu wengine na hata maafa ya watu wengine tukafikiri
kwamba wao ni waovu kupita sisi. Yesu analiona hilo kwa wayahudi wanapomsimulia
tukio lile la Pilato kuchanganya damu za Wagalilaya na dhabibu zao. Yesu
akawaambia, “Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko
Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2. Je, nasi tunatofauti
na hao Wayahudi kwa fikra na matendo yetu? Ndgu yangu, mimi na wewe tunaambiwa
hivyo hivyo na Yesu. Kati yetu wapo watu hodari sana wa kuyasema maovu ya watu
wengine na wakati mwingine wayasemayo na kuyashuhudia hayana ukweli wowote juu
ya kile wakisemacho au kukishuhudia. Uzushi katika jamii yetu leo umekuwa ndiyo
wimbo tuupendao na uujazao vinywa vyetu. Je, tumepata nafasi ya kuyachunguza
maisha yetu kwa undani? Kama hatufanyi jambo hili hatuwezi kuepuka kuwa
wanafiki. Yesu anatukaripia kwa nguvu zote kuhusu unafiki wa mtindo huu na
kusema, “Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti
katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika
jicho la ndugu yako,” Mt 7:5. Hakuna njia ya kuepukana na unafiki huu kama
hatutafanya tafiti moyo na kufanya toba ya kweli. “Nawaambia, lakini
msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:3. Kilichowapata wengine kwa mtindo ule ule
kitatupata nasi tusipotubu na kumrudia Mungu.
Mungu wetu ambaye ni
Upendo na Huruma humjalia kila mmoja wetu nafasi na muda wa kutosha
kujirekebisha. Mungu huyu asingekuwa hivyo, tusingeendelea kuishi hata kwa
sekunde moja tungali na madhambi zetu. Ukimya wa Mungu juu ya dhambi zako siyo
kwamba haoni kinachoendelea ndani yako, bali anakupa muda wa kutosha kufanya tafiti moyo na toba
ya kweli. Mungu wetu ni huruma kama mtunza bustani alivyomjibu mmiliki wa mtini
kwa kutokuzaa matunda yake kwa miaka mitatu mfululizo. “Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda
baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9. Mungu wetu ni Mvumilivu
sana kwa sababu anatupenda sana. Ni kwa sababu ya Upendo wake Mungu alichagua
kutuumba kama tulivyo kwa sifa na utukufu wake. Ndugu yangu uliyesafiri nami
katika tafakari hii yatupasa kutumia vyema nafsi na muda tulionao kuyatenda
matendo ya roho.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bwana, kama
Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Zab 130:3
No hay comentarios:
Publicar un comentario