jueves, 8 de octubre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 27 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 27 YA MWAKA-B
9/10/2015
Somo: Yoe 1:13-15, 2:1-2
Zab: 9A:2-3, 6, 16, 8-9
Injili: Lk 11:15-26
Nukuu:
Jikazeni mkaomboleze, enyi makuhani; Pigeni yowe, enyi wahudumu wa madhabahu; Njoni mlale usiku kucha katika magunia, Enyi wahudumu wa Mungu wangu; Kwa kuwa sadaka ya unga na sadaka ya kinywaji Zimezuiwa katika nyumba ya Mungu,” Yoe 1:13

Naye akajua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba huanguka,” Lk 11:17

Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia,” Lk 11:20

Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya,” Lk 11:23

TAFAKARI: “Tuachane na yaliyo yetu na kibinadamu zaidi tushikamane na kweli ambaye ndiye Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mtume Paulo anatuasa jambo la msingi sana, na hasa maana ya  maisha ya ufufuko wa Bwana Wetu Yesu Kristo kwetu sisi wafuasi wake. Mtume Paulo anasema, Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Kuyatafuta yaliyo juu kwa maana nyingine ndiko kushikamana na kweli ambayo ndiyo Kristo. Kuyatafuta yale ya juu Kristo aliko, ni kuishi katika neema za ufufuo, yaani maisha ya utakaso na yasiyo na hatia. Ni kupiga vita kwa kweli kuushinda ubinadamu wetu kwa kufanana na kuwa zaidi kama Kristo.

Kila mbatizwa ni Kristo mwingine “Alter Christus.” Kwa sababu hii na kwa maana hiyo, yatupasa kila siku kuachana na yaliyo yetu na ya kibinadamu ili kushikamane na kweli ambaye ndiye Kristo. Tunaporejea katika somo la kwanza kutoka katika kitabu cha Nabii Yoeli, tunakutana na tatizo la wana wa Israeli la kutokufanana na kufanya yale atakayo Mungu. Kutokana na kuasi kwao na kufuata njia zao, na hasa Makuhani, Mungu hayupo tayari kupokea sadaka zao. Nabii Yoeli anawaasa Makuhani hao kufanya toba ya kweli na kujenga uhusiano tena na Mungu. Jikazeni mkaomboleze, enyi makuhani; Pigeni yowe, enyi wahudumu wa madhabahu; Njoni mlale usiku kucha katika magunia, Enyi wahudumu wa Mungu wangu; Kwa kuwa sadaka ya unga na sadaka ya kinywaji Zimezuiwa katika nyumba ya Mungu,” Yoe 1:13. Kwa mazingira haya ya kuasi hasa kwa Viongozi hawa wa dini, inaonyesha dhahiri kwamba hali ilikuwa mbaya sana kwa mtu mmoja mmoja. Tuelewe kwamba kile kilichokuwa kinatolewa sadaka kilitoka mikononi mwa kila Myahudi katika upekee wake. Ni dhahiri kama sadaka hiyo inakataliwa ni kwa namna hiyo hiyo Mungu hakupendezwa na maisha ya kila mmoja katika upekee wake.

Katika somo letu la Injili ikiwa ni mwendelezo ule ule wa kumkomboa mwanadamu, Yesu anapata shutuma za kutoa pepo kwa kutumia nguvu za Pepo Mkuu- Beelzebuli. Je, mawazo hayo ya kishirikina yanatoka wapi kwa wana hawa wa Israeli? Kama kweli walikuwa wanamwabudu Mungu mmoja, iweje wawe na mawazo kama hayo? Wapendwa wana wa Mungu, tusipoachana na yaliyo yetu na ubinadamu wetu hatutaweza kuondokana na hisia za kishirikina. Ni wazi kwamba licha ya kuwa walimwamini Mungu moja, watu hawa hawakuachana na yaliyo yao na ubinadamu wao. Hisia hizo mbaya juu ya uwezo wa Yesu wa kutoa pepo kwa nguvu walisiyoijua, zinakuja kwa sababu miongoni mwao walikuwa na mazoea ya kufanya hivyo. Mara nyingi  mtu humwekea hisia mbaya mtu mwingine kwa kile ambacho yeye huwa anakifikiri na kukitenda.

Kutokana na tuhuma hizo za Wayahudi juu ya uwezo wake Yesu wa kutoa pepo, Yesu akiyajua mawazo yao, anawafikirisha kidogo na kusema, Kila ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba huanguka,” Lk 11:17. Hoja hapa ni kwamba, kama Yeye, yaani Kristo, anayafanya hayo yote na watu wanapona kwa kuutoa utawala wa pepo, kuna sababu gani ya kufanya hivyo kwa maana ya kwenda kinyume cha yule aliyempa nguvu hizo yaani Beelzebuli? Kwa kufanya hivyo kama hoja yao inamshiko ni kujichanganya kwa utawala huo wenyewe. Ila Yesu anawaambia kwama hayo yote anayafanya kwa uwezo wa Mungu mwenyewe. Na kwa mantiki hiyo Ufalme wa Mungu huu kati yao tayari. Hawana sababu ya kuwa na hofu. Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia,” Lk 11:20. Ni mara ngapi tunapata nguvu na uponyaji kwa njia ya sala na maomba na mara tupatapo tena shida kama hiyo tunakosa imani na kwenda kwa waganga wa kienyeji? Kwa nini basi unatapatapa katika Imani?

Wapendwa wana wa Mungu, kujitenga kwetu na Mungu kwa kufuata mambo yetu na ubinadamu wetu ndiko kunakotunyima neema na baraka zake. Tunajifungia milango wenyewe na tunapokosa neema na baraka hizo tuna mtafuta mchawi aliyeturoga. Ni sawa na mlevi aliyepoteza ufunguo kwenye Kilabu cha pombe akawa usiku kucha anatafuta ufungua barazani mwa jirani yake eti kwa sababu tu pale kuna mwanga. Je, ataupata ufunguo huo? Ndiyo maana Yesu leo anatuambia maneno haya mazito, Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya,” Lk 11:23. Ndugu yangu, hakuna namna nyingine tuwezayo kupata neema na baraka kama hatutajisalimisha moja kwa moja kwa Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!


Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo,” Efe 2:13

No hay comentarios:

Publicar un comentario