JUMATANO WIKI YA 30 YA MWAKA-B
Sikukuu ya Simoni na Yuda, Mitume
28/10/2015
Somo: Efe 2:19-22
Zab: 19:2-3, 4-5
Injili: Lk 6:12-16
Nukuu:
“Mmejengwa juu ya
msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,”
Efe 2:20
“Katika yeye jengo
lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana,”
Efe 2:21
“Katika yeye ninyi
nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho,” Efe 2:22
“akachagua kumi na
wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; Simoni,
aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na
Filipo na Bartolomayo, na Mathayo
na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa
msaliti,” Lk 6:13b-16
TAFAKARI: “Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, Kristo ni
jiwe la pembeni.”
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu
ya Mitume Simoni na Yuda. Mitume kwa ujumla wao, yaani wale kumi na mbili, kwa
maisha yao na ushuhuda wao wa Imani ndiyo msingi Imara wa Kanisa letu kama
tunavyoliona hii leo. “Akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; Simoni, aliyemwita jina
la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na
Bartolomayo, na Mathayo na
Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa
msaliti,” Lk 6:13b-16. Sadaka yao kwa maisha yao ya Imani juu ya Kristo Yesu,
Kanisa linaendelea kutimiza wajibu wake kama sakramenti ya wokovu wetu. Kristo
Yesu mwenyewe ndiye jiwe kuu la pembeni.
Ukristo wetu na Imani yetu imejengwa juu ya msingi wa mitume
na manabii, na Kristo Yesu akiwa jiwe kuu la pembeni. “Mmejengwa juu ya
msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,”
Efe 2:20. Ni fahari ya kila aliyebatizwa kuishi ahadi zake za ubatizo na
kuendeleza msingi huu imara wa Imani. Hivyo kila mmoja wetu kwa njia ya Kristo
na kwa sadaka ya maisha yake na wito wake, ameunganishwa hekalu la Mungu. “Katika yeye jengo
lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana,”
Efe 2:21. Mitume tunaowasheherekea leo ni mfano wa kuingwa kwetu. Mitume hawa
walikuwa mashahidi na manabii katika kipindi chao. Maisha hayakuwa rahisi
tunapolitazama Kanisa la Mwanzo. Wengi wao walikufa kwa kuuwawa kikatili, ila
hakuna aliyemsaliti Kristo zaidi ya Yuda Eskariote. Leo miongoni mwetu akina
Yuda wapo wengi sana. Ni ni changamoto ya Kanisa na maisha yetu ya kijamii.
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Kanisa linachangamoto nyingi sana. Ili kuzikabili changamoto
hizi, yampasa kila mbatizwa kuishi ahadi zake za ubatizo. Pili, kila mmoja wetu
kadiri ya wito wake ajitahidi kila siku kufanana na Kristo ambaye ndiye jiwe
kuu la pembeni ambapo maisha yetu na sadaka yake upewa maana. Huu ni ushuhuda
tosha wa ukimya hata pale ambapo Kristo hakubaliki kutokana na mitazamo tofauti
ya Kiimani. Matendo yetu mema humwakilisha vizuri Kristo popote kuliko kile
tukiaminicho kwa nadharia tu. Mtume Yakobo anatupatia changamoto hii kwa
kusema, “Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo.
Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya
matendo yangu,” Yak 2:18.
Wapendwa
wana wa Mungu, tuwe waaminifu kwa wito wetu kila mmoja kadiri ya namna
yake, na upendo uliobeba matendo yetu
mema kwa watu wote.
Tumsifu
Yesu Kristo!
Watakatifu
Simoni, na Yuda Mitume, Mtuombee.
No hay comentarios:
Publicar un comentario