JUMATATU WIKI YA 29 YA MWAKA-B
19/10/2015
Somo: Rum 4:20-25
Zab: Lk 1:69-70,
71-72, 73-75
Injili: Lk 12:13-21
Nukuu:
“bali na kwa ajili
yetu sisi mtakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu
Bwana wetu katika wafu; ambaye
alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki,”
Rum 4:24-25
“Akamwambia, Mtu wewe,
ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” Lk 12:14
“Akawaambia,
Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu
vyake alivyo navyo,” Lk 12:15
“Lakini Mungu
akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu
ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo
alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21
TAFAKARI: “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.
Maisha ni dhamana.”
Wapendwa Taifa la Mungu,
masomo yetu ya leo na hasa Injili, yanatualika tutafakari kwa undani maisha
yetu na uhusiano wake na mali. Ndugu moja anamwendea Yesu mbele ya mkutano na
kumwamuru amwambie ndugu yake amgawie urith wao, Lk 12:13. Badala yake, Yesu
anamuuliza swali la msingi na la kushangaza. “Akamwambia, Mtu wewe,
ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” Lk 12:14. Swali hili linatutaka kuweka bayana
nini maana ya maisha yetu na mahusiano yake na mali. Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, elewa leo kwamba maisha yako ni dhamana hapa duniani,
na mali tulizo nazo tumeazimwa tu kwa muda. Mali ni za Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu,
muda wetu hapa duniani na nguvu zetu, akili, nafsi, mahusiano, na mali zetu
zote ni zawadi toka kwa Mungu ambazo ametukabidhi tuvitunze na kuvitumia
vizuri. Sisi ni mawakili wa yale Mungu atupayo. Wazo hili la uwakili huanza na
utambuzi wa kuwa Mungu ndiye mmiliki wa kila kitu na kila mtu duniani.
"Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, dunia na wote wakaao ndani
yake." Zab 24:1. Hivyo Yesu anamtahadharisha kijana yule na sisi pia kwa
kutuambia kwamba, “Angalieni, jilindeni na choyo,
maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo,” Lk 12:15.
Uzima wako na furaha yako ya kweli haitokani na wingi wa mbali ulizokuwa nazo.
Kwa maana nyingine, vitu hivyo kwa kuwa navyo kwa wingi havituhesabii haki
mbele za Mungu. Ndugu yangu, kama humwamini yule aliyefufuliwa kutoka wafu
yaani, Kristo Yesu, wingi wa utajiri wako ni bure kabisa kwa sababu mali zote
ni za Bwana ukiwa na wewe mwenyewe. Mtume Paulo anasema, “sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika
wafu; ambaye alitolewa kwa
ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki,” Rum 4:24b-25.
Hivyo wingi wa mali zako bila Imani juu ya Kristo mfufuka ni bure.
Hakika
"hatumiliki" chochote kwa wakati wetu mfupi wa kuishi duniani. Mungu
"hutukopesha" dunia tunapoishi hapa. Ilikuwa mali ya Mungu kabla
hujaja, na Mungu anamkopesha mtu mwingine ukifa. Je unabisha? Ndugu, ukweli ni
kwamba unaifurahia dunia hii kwa muda mfupi tu. Injili ya leo inatuambia kwamba
asiyefahamu ukweli huu ni MPUMBAVU kama mkulima yule tajiri aliyetaka kufurahisha
nafsi yake kwa kusema, ‘pumzika basi, ule, unywe,
ufurahi,” bila kujua ni nani aliye sababu ya uzima wake. “Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo
wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye
nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21. Ndugu yangu bado furaha yako ipo kwenye mali?
Mungu alipowaumba Adamu na Hawa,
aliwakabidhi uangalizi wa uumbaji wake na akawaweka kuwa wadhamini wa uumbaji
wa mali yake. "Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale
samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho
juu ya nchi," Mwa 1:28
Ndugu unayesafiri nami katika tafakari
hii, kazi ya kwanza ambayo Mungu aliwapa wanadamu ni kuangalia na kutunza
"vitu" vya Mungu duniani. Wajibu huu haujaondolewa kamwe. Ni sehemu
ya malengo yetu leo. Kila kitu tunachokifurahia yapasa tukione kama dhamana
ambayo Mungu ameiweka mikononi mwetu. "Hapo tena inayohitajiwa katika
mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu." 1Kor 4:2
Yesu mara kwa mara anaonyesha kuwa
maisha ni dhamana na anatoa mfano wa talanta, mfanya biashara alikabidhi
watumishi utajiri wake alipo safiri. Aliporudi alitathmini kazi ya kila
mtumishi na kumpa ujira sawasawa na kazi yake. Yule tajiri anasema, "vema, mtumwa mwema na mwaminifu;
ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya
Bwana wako," Mt 25:21.
Ndugu, mwisho wa maisha yako duniani
utatathminiwa kulingana na ulivyotumia yale Mungu aliyokukabidhi. Hii inamaana
kwamba mambo yote unayofanya, hata yale mambo madogo madogo ya kila siku, yana
matokeo ya umilele.
Kama utaona mambo yote kuwa dhamana,
Mungu anaahidi zawadi tatu katika maisha ya milele. Kwanza, utapewa
"uthibitisho". Atasema, "kazi nzuri! umefanya vyema." Kisha
"utapandishwa" daraja na utapewa jukumu kubwa katika umilele:
"nitakuweka uwe mwangalizi wa vitu vingi." Na mwisho utakaribishwa
katika "karamu." "Njoo ushiriki katika furaha ya Bwana wako.
Watu wengi wanashindwa kufahamu kuwa
pesa ni jaribu na dhamana toka kwa Mungu. Mungu anatumia pesa kutufundisha
kumtegemea; na kwa watu wengi fedha ni jaribu kuu kupita yote. “Maana shina moja la
mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo
wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim 6:10. Mungu
anaangalia jinsi tunavyotumia pesa ili kupima jinsi gani tunaaminika.
"Basi, kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu, ni nani
atakayewapa amana mali ya kweli?" Lk 16:11. Ndugu yangu, unapoelekea
kwenye uchaguzi mkuu, unampimaje yule leo anayekuja kwako nakuomba ridhaa ya
uongozi na kusimamia mali ya umma kwa
uaminifu? Je, historia yake huko nyuma inathibitisha ukweli wa hiki
anachokiomba leo? Tusiwakabidhi fisi zizi la kondoo. Hakika kondoo hawatakuwa
salama.
Huu ni ukweli wa muhimu sana. Mungu
anasema kuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya ninavyotumia pesa zangu na hali
yangu ya kiroho. Jinsi ninavyotawala pesa zangu "utajiri wa dunia" ni
kigezo cha kiasi gani Mungu anaweza kunikabidhi baraka za kiroho, "utajiri
wa kweli".
Hebu jiulize ndugu yangu, Je, namna
ninavyotumia fedha zangu yaweza kumzuia Mungu kufanya mambo zaidi maishani
mwangu? Je, ninaweza kuaminiwa katika utajiri wa kiroho? Wapo watu wachache
katika mazingira na maisha yetu, waliweza kuthibitisha uhusiano wa moja kwa
moja baina ya walivyotumia pesa zao na hali ya kiroho ya maisha yao. Pesa au
utajiri wao havikuwa kipao mbele katika maisha yao. Watu na maisha yao ya dhiki
ilikuwa kero zake na mara zote alijitahidi kutafuta suluhu ya kero hizo za
watu. Mtu wa namna hii ndiye tunayeweza kuumpa dhamana ya kusimamia mali ya
umma. Alilolisema ndilo alilolifanya. Dhima hii ndiyo iliyompa nguvu ya
Kimaadili. Mfano wa mtu huyu ni Baba yetu wa Taifa; Julius Kambarage Nyerere,
aliyetutangulia katika haki. Mungu amlaze mahali pema peponi. Sina shaka katika
maisha yake. Ipo siku atapewa uangalizi mkubwa zaidi na Mama Kanisa na kuwa
Mwombezi wetu-Mtakatifu.
Yesu Kristo anasema, "na yule
asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa
vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake
huyo watataka na zaidi." Lk 16:48. Maisha ni dhamana. Na kadiri Mungu
anavyokupa zaidi, ndivyo anakutaka uwajibike zaidi.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mali hazifaidii kitu siku
ya ghadhabu; Bali haki huokoa na mauti.” Mit 11:4
No hay comentarios:
Publicar un comentario