viernes, 16 de octubre de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 28 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 28 YA MWAKA-B
17/10/2015
Somo: Rum 4:13, 16-18
Zab: 105:6-7, 8-9, 42-43
Injili: Lk 12:8-12
Nukuu:
Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa imani,” Rum 4:12 

Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ili apate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako,” Rum 4:18

Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:8

na mwenye kunikana mbele ya watu, huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:9 
Na kila mtu atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa,” Lk 12:10 +

“msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema,” Lk 12:11b-12

TAFAKARI: “Maisha yanayoongozwa na ushuhuda wa Imani ya kweli.”

Wapendwa wana wa Mungu, barua kwa Waibrania yatufundisha kwamba, “imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1. Kuwa na hakika na jambo ni kutokuwa na shaka na jambo au kitu hicho katika maana ya uwepo wake. Hali hii humpelekea mtu kuwa na MATUMAINI hata kama hajakipata ukweli wa jambo hilo au kukiona kitu hicho. Ukweli na hali hii hauwezi kumtia mtu shaka kwa vile avionavyo au asivyoviona. Matumaini haya humjaza mtu UPENDO wa ajabu wa kumpenda Mungu na kutambua uwepo wake katika maisha halisi ya kila siku ya mtu. Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao,” Ebr 11:6. Uwepo wa Mungu aliye hai humjengea mtu IMANI ya malengo thabiti katika maisha yake. Kuishi maisha yenye malengo na yaliyojengwa katika msingi thabiti wa imani ya kweli, msingi huo humpa mtu MAANA ya maisha yake.

Matokeo ya maisha haya yenye malengo humfanya mtu kutambua SIRI ya maisha yake hapa duniani na kutambua kwamba tumeumbwa ili tuishi milele. Imani ya mtu huonekana katika USHUHUDA wa maisha yake. Mtu huanza kutambua umuhimu wa muda, na hivyo hawezi kuchezea muda wake. Hali hii humfanya mtu awe KARIBU sana na Mungu kwa sababu jambo la msingi ni kuutafuta uso wa Mungu. Hivyo, “Mtakeni Bwana na nguvu zake; utafuteni uso wake siku zote,” 1Nya 16:11. Ni katika ukaribu huu na Mungu wenye msingi katika imani ya kweli, Mungu hufanya nasi mipango mikubwa kuhusu wokovu wetu na watu wengine. Hivyo Ibrahimu anahesabiwa haki na kushirikishwa mpango wa wokovu wa Mungu kwa sababu ya Imani yake. Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa imani,” Rum 4:12. Hili ndilo tunda la imani (KUHESABIWA HAKI) pasipo shaka juu ya uwepo wa Mungu.

Jambo la msingi la kutafakari hasa tunapoyatazama maisha ya Ibrahimu ni hasa pale tunapotazama ubinadamu wake. Mazingira na hali aliyokuwa nayo Ibrahimu, yaani Uzee wake, na aliyokuwa akiyapokea maagizo kutoka kwa Mungu ingekuwa vigumu kwake kuyapokea maagizo hayo na kuyaamini kama angejitazama jinsi alivyo na udhaifu aliokuwa nayo. Hata hivyo hakuona shaka kwa yale yaliyojidhihirisha katika maisha yake, na yale ambayo ilimpata kuyatazamia. Hivyo Ibrahimu aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ili apate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako,” Rum 4:18. Mara nyingi Mungu anashindwa kufanya mipango mikubwa kwangu na wewe kwa sababu tunajitazama sana katika udhaifu wetu na hivyo hatuoni sababu yoyote ya Mungu kufanya hayo makubwa kwetu. Mtume Paulo anatukumbusha jambo la msingi sana katika maisha yetu ya kiroho na hasa katika udhaifu wetu. “Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu,” 2Kor 12:10. Hivyo, historia yako mbaya na udhaifu wako kibinadamu, visiwe ukuta wa kutoyaona mema ya Mungu na kupokea neema zake. Huna sababu ya kutokufanya chochote kwa vile wajiona ovyo kupita vitu vyote. Mungu yupo tayari na muda wote kusubiri ukiri wako, yaani,  kuachana na dhambi au uovu wako huo na kuanza Naye upya.

Wapendwa wana wa Mungu, hatuna kitu chochote cha kumficha Mungu wetu. Mungu kesha tupatia namna ya kumfikia kwa kupitia uwepo wa Mwanaye Yesu Kristo. Yesu ananiambia mimi na wewe kwamba, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Je, ndugu yangu tunayesafiri pamoja katika tafakari hii wasadiki maneno hayo ya Yesu Kristo? Kusadiki maneno haya ya Kristo Yesu ni kukiri kwamba katika maisha ninayoishi leo na sasa Yesu Kristo yupo hai ndani yangu, na kwa wale wote wanaonizunguka. Nisipolifanya jambo hili nisijeshangaa siku ya mwisho napishana na Kristo Yesu katika maana ya kutokunitambua mbele ya Baba yake wa Mbinguni. Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:8. Ukiri wangu katika maisha na ushuhuda mbele za watu, ndiyo salama yangu mbele ya Mungu. Kinyume chake ni kwamba, na mwenye kunikana mbele ya watu, huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:9. Inasikitisha kwamba wapo miongoni mwetu ambao watakanwa milele kwa vile tu walishindwa kutambua uwepo wa Mungu katika maisha yao na kuuishi ukweli huo kwa Imani iliyo hai. Wakati mwingine matatizo yako yanaweza kuwa sababu ya kutokuona uwepo wa Mungu na hali hiyo ikakufanya ukate tamaa kabisa. Je, kunasababu ya kukata tamaa tukifikiri kuwa Mungu ametuacha? Ukimya wa Mungu juu ya matatizo yako siyo kwamba haoni wala hajali. Mungu anajua ni wakati gani unaofaa kukupa kile anachoona kitakufaa katika maisha yako ya umilele. Hivyo Mungu hawezi kukusahau kabisa kwasababu alikuumba kwa sura na mfano wake, na anampango madhubuti na maisha yako. Yesu anatuamba, “lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote,”Mt 10:30. USIOGOPE hasa pale mambo yanapoanza kwenda ndivyo sivyo. Huo nao ni mtihani wa imani yako. Mungu anajua utashinda tu ukimtumainia. Mungu utuwazia mema kila wakati. Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11. Ndugu yangu huna sababu ya kukata tamaa.

Kukata tamaa katika maisha ni kosa kubwa sana kulifanya kama unaishi kwa malengo. Kosa hili au dhambi hii ni kumkufuru Roho Mtakatifu. Kwa tendo hili hatuwezi kupata msamaha wake. Na kila mtu atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa,” Lk 12:10. Je, ni mara ngapi nimemkufuru Roho Mtakatifu kwa kukata tamaa? Roho Mtakatifu utuondolea mifadhahiko yote hasa pale tunaposhindwa kujitetea kutokana na mazingira yetu, hali zetu, na ubinadamu wetu. Tunapokuwa na Roho Mtakatifu, huyatakatifuza yote na kuyafanya mapya na yenye nguvu. HivyoYesu anatuambia, “msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema,” Lk 12:11b-12. Je, naitaji silaha gani zaidi ya kiroho kumshinda Roho Mtakatifu? 
TAFAKARI NA CHUKUA HATUA!

Tumsifu Yesu Kristo!


Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?” Zab 27:1

No hay comentarios:

Publicar un comentario