lunes, 26 de octubre de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 30 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 30 YA MWAKA-B
26/10/2015
Somo: Rum 8:12-17
Zab: 68:2, 4, 6-7, 20-21
Injili: Lk 13:10-17
Nukuu:
kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi,” Rum 8:13 

Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu,” Rum 8:14 
Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba,” Rum 8:15

na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye,” Rum 8:17 

Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako,” Lk 13:12

TAFAKARI: “Je, wataka kuishi?”

Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka tunapotazama historia ya uumbaji wa ulimwengu huu, na wokovu wa mwanadamu, utagundua kwamba Mungu anapenda mwanadamu huyu aishi milele. Mwanadamu huyu ili aishi milele, yampasa kutafuta na kutenda mema na kuishi kadiri ya mpango wa Mungu. Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi; hivyo Bwana, Mungu wa majeshi, atakuwa pamoja nanyi, kama msemavyo,” Amo 5:14. Mahusiano kati ya mwanadamu na Mungu hujengwa katika matendo mema.

Mungu kwa kutuumba kwa sura na mfano wake, na kama tulivyo wanadamu ni ushahidi tosha kwamba hana mpango wa kuvunja uhusiano wake na huyo aliyemuumb. Binadamu mwenyewe kwa utashi wake huvunja uhusiano wake na Mungu kwa kufanya ayapendayo na hasa kujipenda yeye zaidi na siyo Mungu. Kujipenda huku zaidi kuliko Muumba wake kunavutwa na matendo yake ya mwili. Huku ndiko kufa kusiko kwa makusudi ya Mungu, kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi,” Rum 8:13. Uzima wa mtu upo pale anapoongozwa na matendo ya roho. Matendo haya ya roho ndiyo yanayotufanya watoto wa Mungu kwa sababu ndani yake upo wema na uzuri wa Mungu. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu,” Rum 8:14.

Wapendwa wana wa Mungu, kadiri ya mpango mzima wa Kanisa, twampokea roho huyu tunaposhiriki vyema masakramenti yake na kuishi kadiri ya neema tuzipatazo kwenye sakaramenti hizo. Maisha haya ya hofu ya Mungu umwondolea mtu huyo hofu ya kibinadamu ambaye mwisho wake ni kuukosa ufalme wa Mungu. Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba,” Rum 8:15. Kwa maana hiyo, sisi si watumwa tena tunapoishi ndani ya Kristo na katika Kristo na kumpa nafasi Roho Mtakatifu afanye kazi ndani yetu. Huku ni kikiri tu hai ndani ya Kristo na kumwita Baba wa uzima wetu. Ukiri huu unatupa nafasi ya kuwa watoto wa Mungu na warithi pamoja na Kristo. Na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye,” Rum 8:17. Je, unashaka juu ya jambo hili?

Injili ya leo inatupa maisha mapya ndani ya Kristo pale tunapomwamini. Maisha ni mali na zawadi ya Mungu kwetu. Hakuna mbadala kuhusu uhai wa mtu. Yesu analithibitisha hili kwa kuvunja taratibu za kisinagogi na kisabato kwa kumponya  mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa. Mateso na mahangaiko yetu ufikia kikomo chake tukiwa na imani pasipo shaka juu ya Mwana wa Mungu. Yesu hakuweza kukaa kimya anapoona udhaifu wa mama yule licha ya kwamba taratibu za kisinagogi na kisabato hazikumruhusu kufanya aliyoyafanya. Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako,” Lk 13:12. Tendo hili linaibua mjadala mkubwa kuhusu uhalali wa Yesu kutoa huduma ile. Jambo la ajabu Wayahudi waliheshimu taratibu zao hizo, bila kuona upendo na huruma ya Mungu kwao na watu wengine. Je, kwa nini basi mimi na wewe tunajisikia vibaya mmoja wetu atendapo jambo jema na lenye kumpendeza Mungu? Ndugu uliyesafiri nami katika tafakari hii kama unataka kuishi ndani na katika Kristo fuata lililo jema na tenda mema siku zote.

Tumsifu Yesu Kristo!


Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24

No hay comentarios:

Publicar un comentario