martes, 1 de noviembre de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 31 YA MWAKA-C


ALHAMISI WIKI YA 31 YA MWAKA-C

Somo: Flp 3:3-8a

Zab/kit: 105:2-3, 4-5, 6-7

Injili: Lk 15:1-10

Nukuu:

“Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili,” Flp 3:3

“Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo,” Flp 3:5

“Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo,” Flp 3:7

“Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu,” Flp 3:8

Nawaambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7 

Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye,” Lk 15:10 

TAFAKARI: “Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu.”

Wapendwa wana wa Mungu, imani yetu na mwelekeo wake msingi wake ni Kristo Yesu. Kristo ndiyo msingi kwa sababu kwake twaiona njia, kweli, na uzima kwa kule tunapokutamani yaani, uzima wa milele, Yoh 14:6. Hivyo kile tulicho, na yote tuliyo nayo na tunayojivunia katika ukamilifu wake bila Kristo bado yana upungufu mkubwa. “Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili,” Flp 3:3.

Wapo kati yetu waaminifu sana na wakweli katika kutimiza yale yaliyokuwa yakifanyika katika mila na desturi zetu bila hata kuhoji ukweli wake. Mara zote tumepelekwa katika mambo hayo kwa hofu kubwa, na wakati mwingine ni vigumu kuelewa faidha ya elimu yako katika hatua ya kukukomboa kutoka katika giza. Na hili ndilo alilolishikilia Mtume Paulo kabla ya ufahamu wake juu ya kweli katika Kristo Yesu. Naye anatuambia, “Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo,” Flp 3:5. Kuzishika sheria na kudumisha mila na desturi za kabila lake na utaifa wake aliupa nafasi ya kwanza bila kuhoji kweli iliyopo ndani yake.

Hapa si semi kwamba hatupaswi kuzishika na kuziheshimu mila na desturi zetu, bali nachokazia hapa ni kwamba tuziheshimu mila hizo na kuzishika endapo zina kuweka huru katika kweli na haki. Ni baada ya Paulo kugundua  hakukwa huru katika mila na desturi hizo za kiyahudi anatoa ushuhuda na kusema,  “Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo,” Flp 3:7. Huyu sasa ni Paulo anayeufahamu ukweli kama ulivyo, na siyo maswala ya ushabiki usio na maana kama tunavyoona kwa wapenzi wa soka hata siasa.

Hakuna jambo zuri na furaha ya kweli unapotambua kweli kwa kile ukiaminicho na kukifuata. Faida kubwa katika jambo hili ni kuishi bila hofu hata kama katika uhalisia wa jambo hili umegubikwa na mazingira hatarishi. Ni katika kiwango na hali hii, Mtume Paulo anasema, “Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu,” Flp 3:8. Huyu ni Paulo asiyekuwa na hofu yoyote ile kwa kweli aliyoigundua ndani na katika Kristo Yesu. Na hapa ndipo tunapopata furaha ya kweli, na kushiriki fuhara ya Mungu katika upendo na huruma yake. Na furaha hii tunaipata pale tu tunapojisalimisha kwake pasipo shaka licha ya udhaifu wetu unaotokana na hali yetu katika ubinadamu wetu. Mtume Paulo ambaye alilitesa Kanisa la mwanzo na sasa hupo huru ndani na katika Kristo Yesu, ni mfano wa kuigwa.

Wapendwa wana Mungu, Injili ya leo, Yesu anatoa mifano miwili yenye kuonyesha furaha ya Mungu tunapomrudia baada ya kutambua njia ya uzima aliyotuandalia.  Mfano wa kwanza, ni mtu mwenye kondoo mia na kumpoteza mmoja. Naye Yesu anatuambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7. Mfano wa pili ni huu wa mwanamke yule mwenye shilingi kumi akapoteza moja. Naye Yesu anatuambia, “Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye,” Lk 15:10.

Shauku hii ya kutafuta kimoja kilichopotea itusukume kujiweka karibu zaidi na Mungu. Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa,” Isa 55:7. Mungu wetu anamaanisha kweli hili alisemalo, yaani kutusamehe kabisa tunapofanya toba ya kweli na majuto.

Mzaburi anatuambia ukweli huu kwa kusema, Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni; Nawe utanijulisha hekima kwa siri, Unisafishe kwa hisopo nami nitakuwa safi, Unioshe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji,” Zab 51:6-7. Huyu ndiye Mungu anayependa kuanza upya nawe katika yote  licha ya historia yako mbaya ya huko nyuma. Je, upo tayari kuanza upya na Mungu?

Wapendwa katika Kristo, usipoteze muda wako mwingi kwa kuziangalia dhambi na uovu wa wenzako ilhali nawe upo kwenye mtego huo huo. Yesu kuwa karibu na wadhambi kwa mfano daraja na mpatanishi wetu na Mungu, anaonekana naye mdhambi kadiri ya mitazamo ya Mafarisayo ambao walipenda kujionyesha wasafi nje ila ndani ni ubatili mtupu. Basi watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia wamsikilize. Mafarisayo na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao,” Lk 15:1-2. Mimi na wewe hatuna tofauti na watoza ushuru na wenye dhambi. Tunahitaji huruma ya Mungu na msamaha wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye,” Lk 15:10

Tusali:-Ee Yesu, yatengeneze maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario