sábado, 5 de noviembre de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 32 YA MWAKA-C


JUMATATU WIKI YA 32 YA MWAKA-C

Somo: Tit 1:1-9

Zab/kit: 24:1-2, 3-4ab, 5-6

Injili: Lk 17:1-6

Nukuu:

“ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii,” Tit 1:6

“Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno,  kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu,” Tit 1:7

 “Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe,” Lk 17:3

“Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe,” Lk 17:4

“Mitume wakamwambia Bwana, Tuongezee imani,” Lk 17:5

“Bwana akasema, Kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii,” Lk 17:6

TAFAKARI: “Tuongezee Imani Bwana.”

Wapendwa wana wa Mungu, Habari Njema yetu ya leo, yaani, Injili, tunaona utendaji wa hekima iliyo safi. Mtu anayeongozwa na yaliyomema kamwe hawezi kumwingiza mwingine kwa yaliyo mabaya. Kwa kufanya hivyo ni kuisaliti dhamiri njema ambayo Mungu ametupatia ili tuwe wawakilishi kwa yaliyo mema kama yeye alivyo mwema. Licha ya kwamba maisha hayakosi makwazo ya hapa na pale, Yesu anatupa angalizo kwa wale ambayo ndani yao Mungu kwa nia njema amewapa uwezo wa kuwa na dhamiri njema ila kwa ubinafsi wao wanakuwa vikwazo kwa wengine. Yesu anasema adhabu ya mtu huyo, Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa,” Lk 17:2. Je, ni mara ngapi unakuwa kikwazo kwa mwenzako ilhali tunajua?

Basi ndugu zangu katika ukweli huu, yaani, kuwa watu wanaongozwa na dhamiri safi si wakati wa kufanya ‘jino kwa jino.’ Je, upo tayari kutoa msamaha pale ambapo yule aliyekukosea yupo tayari kuomba msamaha? Je, wasimama tu katika kweli  iliyo ndani yako bila kuona ukunyufu wa anayekuomba msamaha? Tuelewe kwamba, wokovu wa mtu si kwa ajili yake peke yake, bali kwa ajili ya wengine pia. Kuna furaha kubwa sana mbingini na kwa Mungu wetu,  pale baadhi ya watu uliowajua wamepata kuiona mbingu kupitia kwako kwa tendo tu la kutoa msamaha. Hivyo Yesu anasema, Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe,” Lk 17:3. Tuonyane kindugu mara zote.

Ndugu yangu, lengo lako katika upatanishi liwe kumpata ndugu yako na wala siyo kumpoteza. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe,” Lk 17:4. Tusiwe tayari kuhesabu kushindwa kwake kwa kutimiza yale aliyoyahaidi, bali tutazame utayari wake kwa kuliona kosa na kuwa tayari kutubu. Mazoea yaliyokwisha kuwa tabia ya mtu ni vigumu kuachana  nayo kwa mara moja.

Tuwe tayari kutoa muda wa kutosha kwa mtu kujirudi na kujirekebisa. Hapa na katika hali hii, tumwombe Mungu atupe Imani dhamini ya kuamini kazi yake kwa wengine wanaovutwa kwake licha kwa polepole. Ni katika ukweli huu Mitume wa Yesu wanamwomba Yesu awaongezee imani ya kuyabeba hayo pale yatakapotokea, Lk 17:5. Naye Yesu akawajibu, “Kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii,” Lk 17:6. Kumbe ili mambo yaende vizuri hatunabudi ya kuwa na imani thabiti.

Uthabiti huu wa Imani pamoja na kuwa ndicho kigezo cha kukomaa kiroho, unabeba uzito zaidi kwa wale walio hesabiwa haki hiyo na Mama Kanisa kwa nafasi mbali mbali. Leo katika somo letu la kwanza tunaona sifa ya kuwa Askofu kadiri ya hitaji lile la Kanisa la mwanzo kama ifuatavyo; “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno,  kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu,” Tit 1:7. Kiongozi licha ya kubeba dhamana kadiri ya ofisi yake, Kiongozi ni kioo cha jamii.

Na zaidi ya hayo, Askofu ilimbidi “awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake,” Tit 1:8. Uwepo wa Askofu ni utimilifu, ukamilifu, na uwakilishi wa Kristo pale alipo. Askofu ni, mtetezi wa Imani, ikiwa ni pamoja na kufundisha imani ya kweli. Hivyo ni wajibu wetu kushirikiana vyema na Askofu wetu wa jimbo katika kukuza, kuimarisha, na kuikoleza imani ya kweli.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe,” Lk 17:3

Tusali:- Ee Yesu, tujalie neema ya kuishi imani ya kweli. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario