JUMATANO WIKI YA 34 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 15:1-4
Zab/kit: 98:1, 2-3ab, 7-8, 9
Injili: Lk 21:12-19
Nukuu:
“Nao wauimba wimbo wa
Musa, mtumwa wa Mungu, na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema, Ni makuu, na ya
ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki, na za kweli, njia
zako, Ee Mfalme wa mataifa,” Ufu 15:3
“Kwa kuwa wewe peke
yako u Mtakatifu; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa
kuwa matendo yako ya haki yamekwisha kufunuliwa,” Ufu 15:4b
Nanyi mtasalitiwa
na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha
baadhi yenu. Nanyi mtachukiwa na
watu wote kwa ajili ya jina langu,” Lk 21:16-17
“Walakini hautapotea
hata unywele mmoja wa vichwa vyenu,” Lk 21:18
TAFAKARI:
“Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina
langu,” Lk 21:17
Wapendwa wana wa Mungu,
katika Injili ya leo Yesu
anawaambia wafuasi wake nasi pia maneno haya mazito, ‘Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.’ Tutachukiwa kwa ajili ya jina la Yesu kwa sababu
ukiwa ndani na katika Kristo Yesu watangaza vita dhidi ya uovu. Ndani na katika
Kristo Yesu kuna kweli, haki, upendo, huruma, msamaha, na amani. Na zaidi ya
yote, ndani na katika Kristo Yesu kuna njia ya kweli, ukweli kamili, na uzima
wa milele, Yoh 14:6.
Lakini kustahimili hayo yote kutakugharibu subira na
uvumilivu. Naye Yesu anatuambia, “Nanyi kwa
subira yenu mtaziponya nafsi zenu,” Lk 21:19. Mwenye
subira ufikiri vyema tena kwa undani na upana wake. Mwenye subira huyatazama yote
katika jana yake, leo yake, kesho yake, na umilele wake.
Kuwa mfuasi hai wa Kristo kuna mapaswa yake. Yesu anatuambia
leo mapaswa ya kuwa mfuasi wake hai. Mapaswa yake ni kusalitiwa. “Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu,
na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. Nanyi
mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu,” Lk 21:16-17. Badala yake, katika hali hii Yesu anatuambia tuwe
na furaha. “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila
neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini,
na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo
walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:11-12.
Yatupasa kufurahi kwa sababu katika mateso na ugumu huu wa
kusimama katika kweli na haki, “hautapotea hata
unywele mmoja wa vichwa vyenu,” Lk 21:18. Ndugu yangu tunaye safiri pamoja
katika tafakari hii, elewa kwa hakika kabisa kama kweli huu mfuasi hai wa
Kristo, ipo siku ufuasi wako utapimwa.
Na hilo kama litatokea jiachie kwake
Kristo Yesu. “Basi, kusudieni mioyoni mwenu, kutofikiri-fikiri kwanza
mtakavyojibu; kwa sababu mimi nitawapa kinywa na
hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga,” Lk 21:14-15.
Kama isivyowezekana kula keki na wakati huo huo kutokuila kwa kuishikilia,
ndiyo lilivyo achilio la kweli katika mikoni ya Kristo Yesu.
Ukweli ni
kwamba yote yaliyo ya kibinadamu yana ukomo wake. Ila penye uhai hata kama uhai
huo una ukomo, nyuma yake kuna uhai mwingine, na wenye kuyashikilia hayo yote, yenye
ukomo na ya umilele. Hakikisho hilo kesha tupa Kristo mwenyewe kwamba, tusiwe na
shaka juu yake, na tusifikiri-fikiri na kupoteza tumaini la kweli.
Nguvu na
uwezo wa Mungu kwa namna yoyote ile mwanadamu hawezi kupima wala kujua kina
chake. Yohana anaonyeshwa baadhi tu katika maono. “Kisha
nikaona ishara nyingine katika mbingu, iliyo kubwa, na ya ajabu; malaika saba wenye
mapigo saba ya mwisho; maana katika hayo ghadhabu ya Mungu imetimia,” Ufu 15:1.
Mungu asingekuwa huruma na stahimilivu, hakuna hata mmoja kati yetu ambaye
angesalia bila kuipata ghadamu yake.
Ndiyo maana Malaika mbinguni
hawachoki kumwimbia Mungu na kumsujudia muda wote. “Nao wauimba wimbo wa Musa,
mtumwa wa Mungu, na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema, Ni makuu, na ya ajabu,
matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee
Mfalme wa mataifa,” Ufu 15:3. Je, kwa hali na mazingira yako hapo ulipo huna
sababu ya kumtukuza Bwana Mungu wako?
Malaika wa Mungu
wanatupa sababu ya kumwimbia Mungu na kumsujudu. Nao wanayatenda hayo “Kwa kuwa wewe (Mungu) peke yako u Mtakatifu;
kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako
ya haki yamekwisha kufunuliwa,” Ufu 15:4b. Na fungu lililo bora zaidi ni
kuyaachia yote mikoni mwa Mungu, yawe yale tuyawezayo kwa ufahamu wetu mdogo,
na hata yale yaliyo jificha nje ya uwezo wetu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu;
kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako
ya haki yamekwisha kufunuliwa,” Ufu 15:4b
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie subira. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario