lunes, 28 de noviembre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA MTAKATIFU ANDREA, MTUME


Sikukuu ya Mtakatifu Andrea, Mtume

30 Novemba

Somo: Rum 10:9-18

Zab: 19: 8-11

Injili: Mt 4:18-22


Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka,” Rum 10:9

Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu,” Rum 10:10 

 Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu,” Mt 4:19

Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mt 4:20

TAFAKARI: “Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata.”

Wapendwa wana wa Mungu, mtihani mkubwa kwa mtu yeyote yule siyo hii tuifanyayo mashuleni na hata vyuoni, bali ni mtihani huu wa “kuamua,” uwe nini katika maisha yako. Si rahisi kufanya maamuzi hayo na kuchukua njia nyingine mpya kabisa usiyojua kifuatacho huko mbeleni. Mtu huwa na uhakika kwa kile alichokiishi jana na anachokiishi leo na sasa. Huu ni mzunguko wa kawaida katika maisha ya kila mmoja wetu. Kuwekeza maisha yako yote kwa kile usichokijua humjengea mtu hofu.

Leo Kanisa linapofanya sikukuu za watakatifu na kwa maana ya pekee leo sikukuu ya Mt. Andrea Mtume, ni kusadifu yale waliyoyaamua na kuyaishi na ndiyo ukuaji wa Kanisa na uhai wake. Walifanya uamuzi wa kuacha yale waliyoyazoea na yaliyokuwa yanawapa usalama na kufuata kile wasichokijua wakijisalimisha kabisa katika hicho. Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mt 4:20.

Mtume Andrea akiwa na ndugu yake Simoni Petro walikuwa wavuvi. Kazi hii iliwapa usalama na mahitaji yao ya kila siku. Yesu anawaita wamfuate nao wanaacha pale pale waliyokuwa wanafanya na kumfuata. Uamuzi huu ni mzito sana.Naye alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya, aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi,” Mt 4:18. Kazi hii ndiyo iliyowapa mkate wao wa kila siku. Embu fikiri leo kwa kazi unayofanya hasa wale wanaopata kipato kilichonona, aje mtu tu na kukuambia nifuate. Nini kitakuwa kitu cha kwanza kufanya? Bila shaka utaanza kumpiga maswali mazito na mwisho kumchukulia kama mwendawazimu hivi.

Mitume hawa wanayaacha yote na kumfuata. Yesu Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu,” Mt 4:19. Kuwa wavuvi wa watu ni mabadiliko mazima ya mfumo na namna ya kutenda na kuishi. Hapa ndipo tunaposema Mitume hawa walikuwa majitu ya sifa. Mioyo yao ilikuwa na ushupavu wa hali ya juu. Ni vigumu sana mtu kuubadili mfumo wa maisha yake aliouzoea.

Yesu Kristo alikuwa kila kitu katika maisha yao. Walijua pia hakuna wokovu pasipo Kristo. Iliwezekanaje hivyo haraka? Bila shaka kwa Nguvu na Neema za Mungu iliwezekana pale walipoonyesha utayari wao wa kumsikia Yesu na kumfuata. Mtume Paulo anatuambia, kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka,” Rum 10:9. Jambo hili la kujisalimisha kabisa mikono mwa Yesu halikuwa na mashaka ndani ya mioyo ya hawa Mitume ingawa halikuwa jambo rahisi kufanya. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu,” Rum 10:10 

Wapendwa wana wa Mungu, sababu nyingine ya uwepo wetu hapa duniani licha ya kwamba ni kwa muda mfupi, ni kuwaelezea watu wengine habari njema ya wokovu wetu. Wewe uliyebahatika kuifahamu siri hii usibaki nayo mwenyewe. Ni furaha kubwa sana mbele ya Mungu kama watakuwepo baadhi ya watu waliofika mbinguni kwa sababu ulitumia muda wako kuwaelezea habari njema ya wokovu kwa maisha yao. Mitume waliona na kuupokea wajibu huu mkubwa. “Maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia,” Mdo 4:20. Neno hili sasa si kwa Wayahudi tu, ila lapaswa kusikika duniani kote.

Kwa kupitia Kristo sote tumeunganishwa na kuwa familia moja yenye mastahili sawa mbele ya Mungu, na warithi wa ufalme wake. Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao; kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka,” Rum 10:12-13. Mitume kwa namna ya pekee waliuona wajibu huu mkubwa wa kulihubiri neno la Mungu pasipo woga.

Msingi wa haya yote ni Imani ile waliyokuwa nayo Mitume, na kwa namna ya pekee leo Mama Kanisa anapofanya sikukuu ya Mt Andrea Mtume. Hivyo chanzo cha imani hiyo ni kusikia neno la Kristo. “Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo,” Rum 10:17. Je, watu watasikiaje bila kuambiwa? Kumbe leo pia tunakumbushwa mimi na wewe kwamba kwa Sakramenti ya Ubatizo tunafanywa wamisionari. Ni wajibu wa kila Mbatizwa kulitangaza neno la uzima na wokovu kwa watu wote. Lakini nasema, Je! Wao hawakusikia? Naam, wamesikia, Sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu,” Rum 10:18.

Hivi ndivyo walivyofanya Mitume, na leo Kanisa limesimama likiwa Kristo ndiye msingi wake Imara, na Mitume. Mimi na wewe tunadaiwa kuyatoa maisha yetu kama walivyofanya Mitume ili habari njema iwafikie wote ambao bado hawajasikia. Je, nifanye vipi? Anza hapo hapo ulipo! Kuwa chumvi na mwanga ili uso wa Kristo uonekana katika maisha yao na yako.

Tumsifu Yesu Kristo! 

Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!” 1Kor 9:16

Tusali: Ee Yesu, wajalie neema na nguvu wale wote wanaofanya kazi ya kimisionari, na hasa kwenye mazingira magumu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario