IJUMAA WIKI YA 34 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 20:1-4, 11-21:2
Zab/kit:
84:3, 4, 5-6a, 8a
Injili: Lk 21:29-33
Nukuu:
“Kisha nikaona viti vya enzi, wakaketi juu
yake, nao wakapewa hukumu; nami nikaona roho zao waliokatwa vichwa kwa ajili ya
ushuhuda wa Yesu, na kwa ajili ya neno la Mungu, na hao wasiomsujudia yule
mnyama, wala sanamu yake, wala hawakuipokea ile chapa katika vipaji vya nyuso
zao, wala katika mikono yao; nao wakawa hai, wakatawala pamoja na Kristo miaka
elfu,” Ufu 20:4
“Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa
maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari
tena,” Ufu 21:1
Wakati iishapo
kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha
kuwa karibu. Nanyi kadhalika,
mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u
karibu,” Lk 21:30-31
“Amin,
nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie. Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno
yangu hayatapita kamwe,” Lk 21:32-33
TAFAKARI:
“Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe.”
Wapendwa wana wa Mungu,
katika Injili ya leo, Yesu Kristo anatupa wosia
kwa yale yatakayojiri ikiwa ni hitimisho la nyakati. Yesu anatumia mifano ya
kawaida kulingana na mazingira ya watu wake. Katika jambo hili la kusoma alama
za nyakati, Yesu anatumia mfano wa mti aina ya Mtini. Naye anasema, “Wakati iishapo kuchipuka (Mitini), mwaona na
kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo
yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu,” Lk 21:30-31.
Ufalme huu wa Mungu ni ule aliofunuliwa
katika maono Yohana. Ni ufalme ambao utaushinda uovu kwa wema kama tulivyosoma
katika simulizi la ono la Yohana kuhusu lile joka-ibilisi wa zamani, na yule
mnyama-wale wote wanaojiinua na kujitananisha na Mungu. Hawa ni miungu watu. Ni
ufalme ulioshuka kutoka mbingu, yaani, neno kufanywa mwili, kumwilishwa na
kukaa kwetu, Yoh 1:14. Hivi ndivyo Yohana alivyofunuliwa katika maono: “Kisha
nikaona viti vya enzi, wakaketi juu yake, nao wakapewa hukumu; nami nikaona
roho zao waliokatwa vichwa kwa ajili ya ushuhuda wa Yesu, na kwa ajili ya neno
la Mungu, na hao wasiomsujudia yule mnyama, wala sanamu yake, wala hawakuipokea
ile chapa katika vipaji vya nyuso zao, wala katika mikono yao; nao wakawa hai,
wakatawala pamoja na Kristo miaka elfu,” Ufu 20:4
Ufalme
na utawala huu ushasimikwa kuanzia pale ilipoaanza safari nzima ya wokovu wa
mwanadamu, neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, mateso, kifo na ufufuko wa
Kristo Yesu. Huu ni ukweli usiopitwa na wakati. “Amin,
nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie. Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno
yangu hayatapita kamwe,” Lk 21:32-33. Ukweli
huu wa neno kutokupitwa na wakati ulishafunuliwa pia kwa njia ya maono
aliyofunuliwa Yohana.
Hapa
Yohana anamzungumzia Kristo Yesu, ambaye ndiye hakimu wetu wa upendo, haki na
kweli. Weupe wa kiti chake wasema yote kuhusu hukumu yake. “Kisha
nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi
na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana,” Ufu 20:11. Wale
wote wasioishi katika upendo wa kweli, haki, na kweli katika yote, hawatakuwa
majasiri kuuona uso wa hakimu huyu.
Ndugu
yangu unaye safiri nami katika tafakari
hii, utakuwa na ujasiri huo siku hiyo, kuutazama uso wa hakimu huyu aliye haki?
Jibu ni rahisi sana; ‘jitazame unavyoishi leo na sasa.’
Wapendwa
katika Kristo, kuwa katika ufalme wa
Kristo ni kufanana na Kristo katika kufikiri, kuona, kutenda, na kuishi. Yesu
anatuambia sote kwamba, “Mtu ye yote akitaka
kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate,” Lk
9:23. Zeozi au mtihani huu wa maisha si wa
mara moja tu, bali kila siku ya maisha yako na yangu.
Na
kuwa kweli mwanafunzi wa Yesu ni kuuchukua msalaba na kumfuata Yesu. Yesu
analisema jambo hili wazi kabisa bila kuficha kitu. Naye anasema, “Mtu ye yote
asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,”
Lk 14:27. Je, waufahamu msalaba wako? Hapa napo jibu ni rahisi tu; ‘Tazama
vilema vyako.’ ‘Tazama udhaifu wako!’ ‘Tazama changamoto zako katika maisha
agano unayoyaishi leo na sasa!’
Ni katika kuvijua
vilema vyake na kulenga katika ukamilifu ingawa udhaifu upo ndiyo pona na
salama yake. Ni katika kuujua udhaifu wako na kuchukua hatua kuelekea ukamilifu
ukilitazama tumaini la kweli katika Kristo mbele yako, ndiyo ongoka yako. Na,
ni katika kuishi maisha agano kila mtu kadiri ya wito wake ndipo ulipo mlango
wa mbinguni au kuzimu. Mlango wa mbinguni kwa kuishi utakatifu wa agano hilo
kadiri ya wito wako, na mlango wa kuzimu kwa kuishi kinyume au kulisaliti agano
hilo kadiri ya wito wako, na hasa kile
ulichoitiwa kuishi.
Yohana anatuambia jinsi
itakavyokuwa mwisho wa safari hiyo niliyoisema hivi punde kwa kila mmoja wetu
kuishi kile alichoitiwa katika utakatifu wake. Naye Yohana anasema, “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo,
wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu
kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika
mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao,” Ufu
20:12. Hapa tunafunuliwa hukumu ile ya mwisho ya kila mmoja kadiri ya matendo
yake.
Na hiki ndicho
kitakachotokea kadiri ya maona aliyofunuliwa Yohana, ambacho kwa uhakika Kristo
kesha tufunulia siri hiyo. Kwa lugha ya picha Yohana anasema, “Bahari ikawatoa
wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo
ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake,” Ufu 20:13.
Hukumu kadiri ya matendo inasema zaidi hukumu ile ya kila mmoja na inayolenga
maisha yako leo na sasa. Na swali la nafsi la kujiuliza ni hili; Je, maisha
yangu yanaakisi kile nilichoitiwa na kukiishi?
Na hukumu la jumla
yenye kulenga ‘kufanyika vyote upya,’ ndiyo anayoiongelea Yohana pia kwa lugha
hii ya picha, kwamba, “Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii
ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto,” Ufu 20:14. Na walioenenda vyema katika matendo yao
watauridhi uzima huo wa milele na kutawala pamoja na Mwana-Kondoo milele yote.
Kinyume chake ni kwamba, “iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu
cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto,” Ufu 20:15.
Kutokuwepo au kuandikwa
katika kitabu hiki cha uzima kwa maanisha kwamba ingawa maisha hapa duniani ni
jukumu la muda mfupi, hukufanya lolote jema kwa kipindi hicho cha kujiandaa.
Lolote jema ufanyalo leo na sasa licha ya udogo wake, na wakati mwingine
kutoonekana na watu, Malaika zake Mungu hulirekondi katika kitabu hiki cha
uzima. Je, Yesu anasema nini juu ya hukumu hii?
Yesu anatukumbusha
tukio hili na kusema, “Amin, amin,
nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa
Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai. Maana kama vile Baba alivyo na uzima
nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye
akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno
hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti
yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale
waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu,” Yoh 5:25-29. Wafu watakaoisikia sauti
ya Mwana wa Adamu na kuwa hai ni wale walioishi muda wote hofu ya Mungu.
Baada ya zoezi hili la
haki, upendo, na kweli kufanyika na Hakimu wetu huyu asiye na upendeleo, Yohana
anatuambia alichokiona. “Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana
mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena,”
Ufu 21:1. Huu ndio ule ukamilifu wa vyote kufanywa upya. “Nami nikauona mji ule
mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa
tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe,” Ufu 21:2. Je,
ushukapo mji huu mpya utakukuta katika hali gani?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kisha nikaona mbingu mpya na nchi
mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala
hapana bahari tena,” Ufu 21:1
Tusali:-Ee
Yesu, yatengeneze tena maisha yetu hasa pale tulipoikosea njia na kufuata
yaliyo yetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario