viernes, 25 de noviembre de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 1 YA MAJILI YA MWAKA-A


JUMAPILI YA 1 YA MAJILIO YA MWAKA-A

Somo I: Isa 2:1-5

Zab: 122:1-2, 3-4a, 8-9

Somo II: Rum 13:11-14

Injili: Mt 24:37-44

Nukuu:

Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana katika Yerusalemu,” Isa 2:3 

Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe,” Isa 2:4 

“Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu,” Mt 24:37

 “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42

 “Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia, basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru,” Rum 13:12

 “Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake,” Rum 13.14

TAFAKARI: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.”

Wapendwa wana wa Mungu, karibuni katika tafakari ya leo ikiwa Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kwanza ya majilio ya mwaka “A” wa Kanisa. Leo pia kwa namna ya pekee tunaanza mwaka “A” wa Kanisa. Masomo na tafakari zetu zitalenga katika kipindi hiki cha Kanisa. Kipindi hiki cha Majilio Kanisa linajifananisha na Taifa la Mungu la Agano la Kale linapotarajia kwa hamu kubwa ujio wa Mkombozi. Hivyo kipindi hiki Mama Kanisa anawaandaa wana wake kuwa tayari kumpokea Mkombozi.

Hata hivyo kipindi hiki cha Majilio kina sura nyingine, ambayo inaufunua ujio wa siku ya mwisho wa Bwana. Ni kwa namna hii Kanisa limegawa kipindi hiki cha Majilio katika sehemu kuu mbili nazo ni hizi zifuatazo: Sehemu ya kwanza inaanza leo hadi hapo tarehe 16 ya mwezi wa kumi na mbili. Mambo makuu katika kipindi hiki ni kutafakari juu ya ujio wa pili wa Kristo katika Utukufu wake. Sehemu ya Pili, Mama Kanisa atakuwa anatafakari juu ya  matayarisho ya Sikukuu ya Kuzaliwa kwake Yesu Kristo. Msukumo na wazo kuu katika kipindi hiki katika sehemu hii ya pili ni “Kristo yu karibu,” Yeye ni Mkombozi na Hakimu.

Wapendwa wana wa Mungu, Mwokozi tunayemtazamia kwa hamu kubwa ni Bwana wa Amani atakayetufundisha njia zake nasi kuenenda katika mapito yake. Sheria yake kuu ni UPENDO. Ni wakati wa kuyajenga upya mahusiano yetu na Bwana huyu wa Amani. Ni Bwana wa Amani wa wataifa yote, na ulimwengu mzima. Nabii Isaya anasema habari za Mkombozi huyu: Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana katika Yerusalemu,” Isa 2:3.

Amani ya Mkombozi huyu inaendana pia na haki. Hivyo ajapo lazima ipite hukumu ya haki, na ndipo atakapousimika utawala wake wa Amani, Haki, na Upendo. Ili mambo haya yatendeke katika utawala wake yatupasa kubadili namna yetu ya kufikiri na kutenda. Ulimwengu wa leo vita na hasa ugaidi vinashamiri kwa nguvu kubwa sana na uhai wa mwanadamu ikiwa ni pamoja na amani vipo reheni.

Nabii Isaya anasema, Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe,” Isa 2:4. Kwa mantiki hii, tunahitaji sana kwa sasa utawala wa Mkombozi huyu.

Lengo la Mungu kuumba ulimwengu pamoja na mambo mengine, aliuumba ili pawe sehemu salama kwa ajili ya uhai wa viumbe vyote alivyoviumba na kwa namna ya pekee Mwanadamu aliyemuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kwa mantiki hii, hakuna mwanadamu yeyote yule mwenye haki ya kuutoa uhai wa mwingine na hata kuudhuru. Leo, baadhi yetu kwa ulevi wa madaraka tunasahau kuwa nasi pia ni wanadamu, ipo siku tutakufa, na hukumu ya haki inatusubiri.

Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, Kristo mwenye haki bado anaendele kuteseka na kusulubiwa pale ninapowatenda vibaya wale wasiokuwa na sauti katika jamii yetu leo. Ninazidi kumtesa na kumsulubu Kristo, ninaposhindwa kutenda haki na kutoa haki kwa wale ambao hawana fursa sawa katika jamii yangu leo.

Kwa kosa hili, wewe na mimi tunayo njia moja tu ya kurejesha ushusiano huu. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe,” Mdo 3:19a. Tusianze kumtafuta mchawi wakati mchawi mwenyewe ni wewe na mimi. Yesu anasema, “Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi. Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele,” Mt 25:45-46. Ndugu yangu, wadogo anaowazungumzia Yesu hapa ni hawa wafuatao; wenye njaa, wenye kiu, wageni, walio uchi, wagonjwa, na wafungwa.

Kumbe kipindi hiki cha majilio, ambacho tunamsubiri Mkombozi wetu aliye upendo, haki, kweli, na amani, ni wakati mahususi wa kuyatafakari maisha yetu binafsi na makundi haya ya wahitaji katika jamii yetu. “Naam, tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini,” Rum 13:11. Hivyo, sasa ni wakati wa kuyavua matendo ya giza na kuzivaa sila za nuru, Rum 13:12. Na sila hizo za nuru ndizo hizi, “upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23.

Ndugu yangu, maisha ya hapa duniani ni jukumu la muda mfupi sana. Ndugu, ili kutimiza vizuri maisha yako hupaswi kusahau ukweli wa aina mbili: Kwanza, yakilinganishwa na umilele, maisha ni mafupi sana. Pili, dunia ni makazi ya muda tu. Hatuwezi kukaa hapa kwa muda mrefu, hivyo usijishikamanishe sana nayo.Fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa,” Mt 24:34. Tumwombe Mungu atusaidie kuyaona maisha ya duniani kama anavyoyaona yeye mwenyewe. Mfalme Daudi aliomba, "Bwana, nijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; nijue jinsi nilivyo dhaifu," Zab 39:4

Kwa maana nyingine, “Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia, basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru,” Rum 13:12. Matendo ya giza yako na yangu tunayopaswa kuyavua na bila kupepesa macho ni matendo haya ya mwili, nayo ni; uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21; Rum 13:13. Pona yako na yangu ni kumrudia Mungu, tukimvaa Yesu Kristo, Bwana wetu, na kutokuuangalia mwili hata kuwashwa tamaa zake, Rum 13:14.

Wapendwa katika Kristo, tusipende kujitenga katika kweli hii ya kupatanishwa na Mungu tungali hai. Mungu ameshatuwezesha vyakutosha katika hatua hii ya kupatanishwa naye. Kwa kupitia mwanaye mpenzi Yesu Kristo, yote yamerahisishwa. Naye Yesu anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” Yoh 14:6. Hatuna namna nyingine ya kupatanishwa na Mungu kama hatutamwelekea Yesu Kristo. “Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote,” 1Yoh 2:1a-2. Ndugu yangu, kinachokukwamisha kupatanishwa naye ni nini? Je, washuke malaika wakuambie mambo haya ndio uamini?

Injili ya leo ni mrejesho wa yale yote aliyokuwa akiyafanya Yesu, na ambayo anayafanya nasi katika hali hii ya ufufuko. Ni kumuishi Kristo katika ufufuko. Ni maisha ya ufufuko. Na ndiyo dhima ya Injili ya leo kwa maneno haya ya Yesu, Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42.

Ndugu yangu hapana shaka wa mfahamu vizuri "inzi!" Mdudu huyu kadiri ya utafiki wa kisayansi huishi siku saba tu. Ni wiki moja kati ya wiki 52 katika mwaka mmoja. Tazama fujo na papara za inzi. Hutua kila mahali kwa siku hizo saba; kwenye vyakula (vilivyo chacha na visivyo chacha), kwenye vinjwaji, kwenye vidonda, kwenye vinyesi, nk. Tazama anavyoongea kwa ishara akiwa amenyanyua miguu yake ya nyuma na kusema, "yaliyopita yeshapita." Na anapoinua miguu ya mbele husema hivi, "yajayo na yaje, ponda mali, furahia yote, haya ndiyo maisha."

Ndugu yangu, tulio wengi leo maisha yetu hayana tofauti na haya ya inzi. Hutaka kufanya yote na kujaribu yote katika maisha. Hakuna muda wa maandalizi wala tafakari kuhusu umilele wetu kama zawadi ya pekee tuliyopewa sisi wanadamu. Katika kweli hii Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja,” Mt 24:44

 Hata hivyo tunapewa kazi ya kufanya kuhusu Ufalme huu wa Mbinguni. Naye Yesu anasema,  “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42. Wajibu huu muhimu ni wa kila Mbatizwa na Kanisa kwa namna ya pekee. Haya ni maisha ya Kristo baada ya mateso, kifo na ufufuko wake. Ukeshaji ni mwitikio wa maisha ya ufufuko, na utayari wa maisha ndani na katika Kristo Yesu.

Jambo la kushangaza ni kwamba, licha ya mazoea yetu, kwamba mambo kwende kwa kiasi fulani kadiri ya mpango kazi wetu, ujio wa Kristo bado ni fumbo. Naye Yesu analithibitisha hilo kwa kusema, “kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu,” Mt 24:37. Jibu ni kwamba hakuna anayejua siku hiyo.

Kiama siku ya mwisho itakukuta katika hali uliyonayo sasa, yaani, kama utakuwa unajiboofusha kwa starehe na anasa, hodi ya pekee itapigwa kwako, na mwitikio huo ambao lazima uitikie utakuwa ndio mwisho wa pumzi yako. “Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu,” Mt 24:38-39. Nini maana ya neno hili?

Ukweli ni kwamba, leo shetani hawezi kutudanganya kwamba hakuna dhambi. Pia leo shetani hawezi kutudanganya kwamba hakuna hukumu ya mwisho.Na zaidi leo shetani hawezi kutudanganya kwamba hakuna mbingu. Ila leo shetani amechukua ufahamu wetu kwa kutusadikisha kwamba bado muda upo. Katika pumbaziko hilo kwamba, ‘bado muda upo,’ ndipo tunapopigwa na mshangao kwamba hakuna muda tena, na Mwana wa Adamu yupo mlangoni akipisha hodi. Hakutakuwa na maandalilizi! Na taswira ya kweli hii ni kwamba, “watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa,” Mt 24:40-41.

Ndugu yangu, kuepukana na kadhia hii ni KUKESHA ingali taa zetu zikiwa zinawaka na mafuta ya kutosha. Na kitendawili ni hiki; “Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa,” Mt 24:43. Je, upo tayari?

Pamoja na hayo yote tuliyoyatafakari siku ya leo, tusipofanya toba ya kweli na kuchukuwa wajibu huu muhimu katika maisha yetu kama Wafuasi wake Kristo, hata kama tukipewa “promotion” kwenda mbinguni hatutaona upekee wake, wala kufurahia ukweli huo, kwa sababu tu si mastahili yetu.

Mastahili ya kuurithi ufalme wa Mungu ni kuujenga kuanzia sasa; Kufurahia kuteseka na Kristo kwa ajili ya haki, kufa kwa ajili ya Kristo kila siku kwa ajili ya haki na upendo, na kufufuka naye kwa mastahili ya mateso na kifo chetu kitokanacho na haki, na upendo wa kweli. Hili ndilo badiliko túnalo hitaji kulifanya kipindi hiki cha majilio.

Miaka 15 iliyopita, mwenye hofu ya Mungu atokapo nyumbani mwake na kusafiri, kitu cha kwanza kukumbuka kubeba ilikuwa rozali, fedha, vitambulisho, na mambo mengine. Leo, kitu cha kwanza kukumbuka ni simu ya mkononi. Je, kuna ubaya katika hili? La hasha! Huu ni ujumbe kwamba tupo kwenye ulimwengu wa mawasiliano na ukaribu zaidi. Ndiyo maana kitokeacho leo Marekani, Bibi yangu Mzaa Baba pale Uru Mrawi anakipata kama kilivyo, yaani, ‘live.’ Je, kwa mabadiliko haya Mungu amepunguza upendo, huruma, na subira yake kwetu katika badiliko la kuyaacha maovu na kumwelekea? La hasha! Mabadiliko haya ni ufunuo wa upendo wake Mungu ndani yetu.

Na siri ya upendo huu ni kutupeleka katika ukamilifu ambao ndiyo Mungu mwenyewe. “Evolution is geared with love as an energe to wholeness.” Hata pamoja na mabadiliko haya ya sayansi na technolojia, Mungu hajapoteza uhasili wake, bali anazidi kujifunua katika mabadiliko hayo kwa sababu Yeye ndiye msukumo wa mabadiliko hayo kuelekea ukamilifu wake.

Siku mmoja watawa fulani katika monastery (maisha ya ndani ya kitawa, kujitenda katika ulimwengu huu kwa ajili ya Kristo) fulani, Kanisa lao lilipigwa radi na kuharibika isipokuwa altare ilibaki salama. Wakiwa katika sintofahamu hiyo, Mtawa mmoja aliyekuwa na umri kuliko wote aliwaambia wenzake, “afadhali radi hiyo imeipiga Kikanisa chetu. Mungu asingekuwa na huruma angepiga chumba chetu cha runinga. Hakika ingekula kwetu, na leo wote tungekuwa wafu hadi sasa!”

Ndugu yangu, embu fikiri, pamoja na maendeleo haya yote ya sayansi na teknolojia, Mungu wako akupaye uzima, unampa nafasi gani katika maisha yako? Tafakari tukio la watawa hao! Mungu wetu ni Upendo, Huruma, Msamaha, Haki, na Kweli. Tuwe karibu naye. Na hii ndiyo maana ya Majilio.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake,” Rum 13.14

Tusali:-Ee Yesu, azisha yote upya ndani yangu, kwako na ndani yako. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario