JUMAPILI YA 1 YA MAJILIO YA MWAKA-A
Somo
I: Isa 2:1-5
Zab:
122:1-2, 3-4a, 8-9
Somo
II: Rum 13:11-14
Injili:
Mt 24:37-44
Nukuu:
“Na
mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana,
nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda
katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana katika
Yerusalemu,” Isa 2:3
“Naye
atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao
watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua
upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe,” Isa 2:4
“Kwa maana kama vile
ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu,” Mt
24:37
“Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi
atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42
“Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia,
basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru,” Rum 13:12
“Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala
msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake,” Rum 13.14
TAFAKARI:
“Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
karibuni katika tafakari ya leo ikiwa Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya
kwanza ya majilio ya mwaka “A” wa Kanisa. Leo pia kwa namna ya pekee tunaanza
mwaka “A” wa Kanisa. Masomo na tafakari zetu zitalenga katika kipindi hiki cha
Kanisa. Kipindi hiki cha Majilio Kanisa linajifananisha na Taifa la Mungu la
Agano la Kale linapotarajia kwa hamu kubwa ujio wa Mkombozi. Hivyo kipindi hiki
Mama Kanisa anawaandaa wana wake kuwa tayari kumpokea Mkombozi.
Hata hivyo kipindi hiki
cha Majilio kina sura nyingine, ambayo inaufunua ujio wa siku ya mwisho wa
Bwana. Ni kwa namna hii Kanisa limegawa kipindi hiki cha Majilio katika sehemu
kuu mbili nazo ni hizi zifuatazo: Sehemu ya kwanza inaanza leo hadi hapo tarehe
16 ya mwezi wa kumi na mbili. Mambo makuu katika kipindi hiki ni kutafakari juu
ya ujio wa pili wa Kristo katika Utukufu wake. Sehemu ya Pili, Mama Kanisa
atakuwa anatafakari juu ya matayarisho
ya Sikukuu ya Kuzaliwa kwake Yesu Kristo. Msukumo na wazo kuu katika kipindi
hiki katika sehemu hii ya pili ni “Kristo yu karibu,” Yeye ni Mkombozi na
Hakimu.
Wapendwa
wana wa Mungu, Mwokozi tunayemtazamia kwa hamu kubwa ni Bwana wa Amani
atakayetufundisha njia zake nasi kuenenda katika mapito yake. Sheria yake kuu
ni UPENDO. Ni wakati wa kuyajenga upya mahusiano yetu na Bwana huyu wa Amani.
Ni Bwana wa Amani wa wataifa yote, na ulimwengu mzima. Nabii Isaya anasema
habari za Mkombozi huyu: “Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani
kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi
tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la
Bwana katika Yerusalemu,” Isa 2:3.
Amani ya Mkombozi huyu
inaendana pia na haki. Hivyo ajapo lazima ipite hukumu ya haki, na ndipo
atakapousimika utawala wake wa Amani, Haki, na Upendo. Ili mambo haya yatendeke
katika utawala wake yatupasa kubadili namna yetu ya kufikiri na kutenda.
Ulimwengu wa leo vita na hasa ugaidi vinashamiri kwa nguvu kubwa sana na uhai
wa mwanadamu ikiwa ni pamoja na amani vipo reheni.
Nabii Isaya anasema, “Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa
kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu;
taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena
kamwe,” Isa 2:4. Kwa mantiki hii, tunahitaji
sana kwa sasa utawala wa Mkombozi huyu.
Lengo la Mungu kuumba
ulimwengu pamoja na mambo mengine, aliuumba ili pawe sehemu salama kwa ajili ya
uhai wa viumbe vyote alivyoviumba na kwa namna ya pekee Mwanadamu aliyemuumba
kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kwa mantiki hii, hakuna mwanadamu yeyote yule
mwenye haki ya kuutoa uhai wa mwingine na hata kuudhuru. Leo, baadhi yetu kwa
ulevi wa madaraka tunasahau kuwa nasi pia ni wanadamu, ipo siku tutakufa, na
hukumu ya haki inatusubiri.
Ndugu yangu tunaye
safiri sote katika tafakari hii, Kristo mwenye haki bado anaendele kuteseka na
kusulubiwa pale ninapowatenda vibaya wale wasiokuwa na sauti katika jamii yetu
leo. Ninazidi kumtesa na kumsulubu Kristo, ninaposhindwa kutenda haki na kutoa
haki kwa wale ambao hawana fursa sawa katika jamii yangu leo.
Kwa kosa hili, wewe na
mimi tunayo njia moja tu ya kurejesha ushusiano huu. “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu
zifutwe,” Mdo 3:19a. Tusianze kumtafuta mchawi wakati mchawi mwenyewe ni wewe
na mimi. Yesu anasema, “Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao
walio wadogo, hamkunitendea mimi. Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu
ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele,” Mt 25:45-46.
Ndugu yangu, wadogo anaowazungumzia Yesu hapa ni hawa wafuatao; wenye njaa,
wenye kiu, wageni, walio uchi, wagonjwa, na wafungwa.
Kumbe kipindi hiki cha
majilio, ambacho tunamsubiri Mkombozi wetu aliye upendo, haki, kweli, na amani,
ni wakati mahususi wa kuyatafakari maisha yetu binafsi na makundi haya ya
wahitaji katika jamii yetu. “Naam, tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika
usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko
tulipoanza kuamini,” Rum 13:11. Hivyo, sasa ni wakati wa kuyavua matendo ya
giza na kuzivaa sila za nuru, Rum 13:12. Na sila hizo za nuru ndizo hizi,
“upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi;
juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23.
Ndugu yangu, maisha ya
hapa duniani ni jukumu la muda mfupi sana. Ndugu, ili kutimiza vizuri maisha
yako hupaswi kusahau ukweli wa aina mbili: Kwanza, yakilinganishwa na umilele,
maisha ni mafupi sana. Pili, dunia ni makazi ya muda tu. Hatuwezi kukaa hapa
kwa muda mrefu, hivyo usijishikamanishe sana nayo. “Fahamuni
neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja,
angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa,” Mt 24:34. Tumwombe Mungu atusaidie kuyaona
maisha ya duniani kama anavyoyaona yeye mwenyewe. Mfalme Daudi aliomba,
"Bwana, nijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani;
nijue jinsi nilivyo dhaifu," Zab 39:4
Kwa maana nyingine,
“Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia, basi na tuyavue matendo ya giza, na
kuzivaa silaha za nuru,” Rum 13:12. Matendo ya giza yako na yangu tunayopaswa
kuyavua na bila kupepesa macho ni matendo haya ya mwili, nayo ni; uasherati,
uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina,
faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika
hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao
mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21; Rum 13:13. Pona
yako na yangu ni kumrudia Mungu, tukimvaa Yesu Kristo, Bwana wetu, na
kutokuuangalia mwili hata kuwashwa tamaa zake, Rum 13:14.
Wapendwa
katika Kristo, tusipende kujitenga katika kweli hii ya kupatanishwa na Mungu
tungali hai. Mungu ameshatuwezesha vyakutosha katika hatua hii ya kupatanishwa
naye. Kwa kupitia mwanaye mpenzi Yesu Kristo, yote yamerahisishwa. Naye Yesu
anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia
ya mimi.” Yoh 14:6. Hatuna namna nyingine ya kupatanishwa na Mungu kama
hatutamwelekea Yesu Kristo. “Na kama mtu akitenda dhambi tunaye
Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye
ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa
dhambi za ulimwengu wote,” 1Yoh 2:1a-2. Ndugu yangu, kinachokukwamisha
kupatanishwa naye ni nini? Je, washuke malaika wakuambie mambo haya ndio
uamini?
Injili ya leo ni
mrejesho wa yale yote aliyokuwa akiyafanya Yesu, na ambayo anayafanya nasi
katika hali hii ya ufufuko. Ni kumuishi Kristo katika ufufuko. Ni maisha ya
ufufuko. Na ndiyo dhima ya Injili ya leo kwa maneno haya ya Yesu, “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi
atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42.
Ndugu yangu hapana shaka wa mfahamu
vizuri "inzi!" Mdudu huyu kadiri ya utafiki wa kisayansi huishi siku
saba tu. Ni wiki moja kati ya wiki 52 katika mwaka mmoja. Tazama fujo na papara
za inzi. Hutua kila mahali kwa siku hizo saba; kwenye vyakula (vilivyo chacha
na visivyo chacha), kwenye vinjwaji, kwenye vidonda, kwenye vinyesi, nk. Tazama
anavyoongea kwa ishara akiwa amenyanyua miguu yake ya nyuma na kusema,
"yaliyopita yeshapita." Na anapoinua miguu ya mbele husema hivi,
"yajayo na yaje, ponda mali, furahia yote, haya ndiyo maisha."
Ndugu yangu, tulio
wengi leo maisha yetu hayana tofauti na haya ya inzi. Hutaka kufanya yote na
kujaribu yote katika maisha. Hakuna muda wa maandalizi wala tafakari kuhusu
umilele wetu kama zawadi ya pekee tuliyopewa sisi wanadamu. Katika kweli hii
Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Kwa
sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana
wa Adamu yuaja,” Mt 24:44
Hata hivyo tunapewa kazi ya kufanya kuhusu
Ufalme huu wa Mbinguni. Naye Yesu anasema, ““Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi
atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42. Wajibu huu muhimu ni wa kila Mbatizwa na
Kanisa kwa namna ya pekee. Haya ni maisha ya Kristo baada ya mateso, kifo na
ufufuko wake. Ukeshaji ni mwitikio wa maisha ya ufufuko, na utayari wa maisha
ndani na katika Kristo Yesu.
Jambo la kushangaza ni
kwamba, licha ya mazoea yetu, kwamba mambo kwende kwa kiasi fulani kadiri ya
mpango kazi wetu, ujio wa Kristo bado ni fumbo. Naye Yesu analithibitisha hilo
kwa kusema, “kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake
Mwana wa Adamu,” Mt 24:37. Jibu ni kwamba hakuna anayejua siku hiyo.
Kiama siku ya mwisho
itakukuta katika hali uliyonayo sasa, yaani, kama utakuwa unajiboofusha kwa
starehe na anasa, hodi ya pekee itapigwa kwako, na mwitikio huo ambao lazima
uitikie utakuwa ndio mwisho wa pumzi yako. “Kwa kuwa kama vile siku zile
zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na
kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika
ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu,” Mt 24:38-39.
Nini maana ya neno hili?
Ukweli ni kwamba, leo
shetani hawezi kutudanganya kwamba hakuna dhambi. Pia leo shetani hawezi
kutudanganya kwamba hakuna hukumu ya mwisho.Na zaidi leo shetani hawezi
kutudanganya kwamba hakuna mbingu. Ila leo shetani amechukua ufahamu wetu kwa
kutusadikisha kwamba bado muda upo. Katika pumbaziko hilo kwamba, ‘bado muda
upo,’ ndipo tunapopigwa na mshangao kwamba hakuna muda tena, na Mwana wa Adamu
yupo mlangoni akipisha hodi. Hakutakuwa na maandalilizi! Na taswira ya kweli hii
ni kwamba, “watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa;
wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa,” Mt 24:40-41.
Ndugu yangu, kuepukana
na kadhia hii ni KUKESHA ingali taa zetu zikiwa zinawaka na mafuta ya kutosha.
Na kitendawili ni hiki; “Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba
angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba
yake kuvunjwa,” Mt 24:43. Je, upo tayari?
Pamoja na hayo yote
tuliyoyatafakari siku ya leo, tusipofanya toba ya kweli na kuchukuwa wajibu huu
muhimu katika maisha yetu kama Wafuasi wake Kristo, hata kama tukipewa
“promotion” kwenda mbinguni hatutaona upekee wake, wala kufurahia ukweli huo,
kwa sababu tu si mastahili yetu.
Mastahili ya kuurithi
ufalme wa Mungu ni kuujenga kuanzia sasa; Kufurahia kuteseka na Kristo kwa
ajili ya haki, kufa kwa ajili ya Kristo kila siku kwa ajili ya haki na upendo,
na kufufuka naye kwa mastahili ya mateso na kifo chetu kitokanacho na haki, na
upendo wa kweli. Hili ndilo badiliko túnalo hitaji kulifanya kipindi hiki cha
majilio.
Miaka 15 iliyopita,
mwenye hofu ya Mungu atokapo nyumbani mwake na kusafiri, kitu cha kwanza
kukumbuka kubeba ilikuwa rozali, fedha, vitambulisho, na mambo mengine. Leo,
kitu cha kwanza kukumbuka ni simu ya mkononi. Je, kuna ubaya katika hili? La
hasha! Huu ni ujumbe kwamba tupo kwenye ulimwengu wa mawasiliano na ukaribu
zaidi. Ndiyo maana kitokeacho leo Marekani, Bibi yangu Mzaa Baba pale Uru Mrawi
anakipata kama kilivyo, yaani, ‘live.’ Je, kwa mabadiliko haya Mungu amepunguza
upendo, huruma, na subira yake kwetu katika badiliko la kuyaacha maovu na
kumwelekea? La hasha! Mabadiliko haya ni ufunuo wa upendo wake Mungu ndani
yetu.
Na siri ya upendo huu
ni kutupeleka katika ukamilifu ambao ndiyo Mungu mwenyewe. “Evolution is geared with love as an energe to
wholeness.” Hata pamoja na mabadiliko haya ya sayansi na technolojia, Mungu
hajapoteza uhasili wake, bali anazidi kujifunua katika mabadiliko hayo kwa
sababu Yeye ndiye msukumo wa mabadiliko hayo kuelekea ukamilifu wake.
Siku mmoja watawa fulani katika monastery (maisha ya
ndani ya kitawa, kujitenda katika ulimwengu huu kwa ajili ya Kristo) fulani,
Kanisa lao lilipigwa radi na kuharibika isipokuwa altare ilibaki salama. Wakiwa
katika sintofahamu hiyo, Mtawa mmoja aliyekuwa na umri kuliko wote aliwaambia
wenzake, “afadhali radi hiyo imeipiga Kikanisa chetu. Mungu asingekuwa na
huruma angepiga chumba chetu cha runinga. Hakika ingekula kwetu, na leo wote
tungekuwa wafu hadi sasa!”
Ndugu yangu, embu fikiri, pamoja na maendeleo haya
yote ya sayansi na teknolojia, Mungu wako akupaye uzima, unampa nafasi gani
katika maisha yako? Tafakari tukio la watawa hao! Mungu wetu ni Upendo, Huruma,
Msamaha, Haki, na Kweli. Tuwe karibu naye. Na hii ndiyo maana ya
Majilio.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo,
wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake,” Rum 13.14
Tusali:-Ee
Yesu, azisha yote upya ndani yangu, kwako na ndani yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario