Kutabarukiwa
Basilika la Laterani
Somo
I: Eze 47:1-2, 8-9, 12
Zab:
46:2-3, 5-6, 8-9
Somo
II: 1Kor 3:9-11, 16-17
Injili:
Yoh 2:13-22
Nukuu:
“Tena
itakuwa, kila kiumbe hai kisongamanacho, kila mahali itakapofika mito hiyo,
kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa sababu maji haya yamefika huko
maana maji yale yataponyeka, na kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto
huo,” Eze 47:9
“Na
karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa
chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe;
utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali
patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni
dawa,” Eze 47:12
“Maana
sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la
Mungu,” 1Kor 3:9
“Maana
msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha
kuwekwa, yaani, Yesu Kristo,” 1Kor 3:11
“Kama
mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la
Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi,” 1Kor 3:17
“akawaambia
wale waliokuwa wakiuza njiwa, Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu
kuwa nyumba ya biashara,” Yoh 2:16
“Wanafunzi
wake wakakumbuka ya kuwa imeandikwa, Wivu wa nyumba yako utanila,” Yoh 2:17
“Yesu
akajibu, akawaambia, Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu
nitalisimamisha,” Yoh 2:19
“Lakini
yeye alinena habari za hekalu la mwili wake,” Yoh 2:21
TAFAKARI:
“Nasi ni shamba la Mungu Jengo la Mungu, Msingi wake ni Yesu Kristo.”
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa
anasheherekea siku ya Kutabarukiwa Basilika la Laterano. Historia fupi kuhusu
Basilika hii ya Laterano:
Laterano (kwa Kilatini Lateranus)
ni mtaa wa Roma maarufu hasa
kwa sababu kulikuwa na Ikulu mojawapo
la Kaisari Konstantino Mkuu.
Lakini pamoja na ukweli huo, inaonyesha kwamba Plautius Lateranus ilikuwa
familia moja tajiri katika Falme ya Roma. Plautius alituhumiwa na Mfalme Nero
kwa kula njama dhidi ya Mfalme. Matokeo ya tuhuma hii ilikuwa kunyang’anywa na
kugawanywa kwa mali za familia hii. Hivyo, Mfalme Constantino baada ya yeye
kuruhusu Ukristo katika Dola la Roma (Hati ya Milano 313) ikulu iligeuzwa kuwa
Kanisa ambalo liliwekwa
wakfu na Papa Melkiades (314),
na mpaka leo linaheshimiwa na Kanisa Katoliki kama
Kanisa kuu la Jimbo la Roma
na la ulimwengu mzima.
Tofauti na wanavyodhani wengi, Ukulu wa Papa ni katika Kanisa hilo, si
katika Basilika la Mt. Petro huko Vatikano. Jina rasmi ni Kanisa la
Kristo Mkombozi, lakini watu wanaliita kwa kawaida kanisa la Mt. Yohane
(Mbatizaji) kwa kuwa nyuma yake ipo batizio
kuu tena juu ya ukuta wake wa mbele kandokando ya sanamu ya marumaru ya Yesu, zipo zile za Yohane Mbatizaji na Mtume Yohane.
Ndani, juu ya altare kuu yanatunzwa mafuvu ya
vichwa vya Mtume Petro na Mtume Paulo. Ndani ya Kanisa hilo mara
tano ulifanyika mtaguso ambao
kila mmoja unahesabiwa na Kanisa Katoliki kuwa Mtaguso Mkuu. Mpaka uhamisho wa Avignon (karne ya 14) Mapapa
waliishi karibu na Kanisa hilo, na mpaka leo seminari kuu ya jimbo (pamoja na
chuo kikuu cha Kipapa cha Laterano)
iko nyuma yake. Eneo lote ni nje ya mamlaka ya nchi ya Italia na linahesabiwa kuwa
sehemu ya nchi huru ya Vatikano.
Wapendwa pamoja na
maelezo hayo mazuri kuhusu historia ya Kutabarukiwa kwa Basilika hii, masomo
yetu leo yote matatu yanatutaka kutafakari na kuona kuwa “Nasi ni shamba la
Mungu Jengo la Mungu, Msingi wake ni Yesu Kristo,” kwa Sakramenti ya Ubatizo.
Msingi wa Kanisa hili ni Kristo wenyewe aliyelisimamisha kwa mateso, kifo na
ufufuko wake. “Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni
ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo,” 1Kor 3:11. Kwa mateso, kifo,
na ufufuko wake Kristo miili yetu
imehuishwa na kuwa hekalu la Roho Mtakatifu.
Kwa kuwa tumehuishwa na
kuupokea huo Utakatifu hatupaswi kulibomoa hekalu hili kwa hatia yoyote ile, na
hasa dhambi. Yeyote yule atakayeliharibu hekalu hili, Mungu naye atamharibu.
Leo hekalu hili la Roho Mtakatifu linafanyiwa vituko vya aibu na vya
kusikitisha. Embu fikiri mtu anapomkata vipande vipande mwenzake kwa sababu ya
pesa na utajiri. Embu fikiri ni mimba ngapi zinaharibiwa na kutolewa kwa kila
sekunde. Embu tazama ni wazee wangapi na walemavu wa ngozi wanavyouwawa.
Hakika, “Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa
maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi,” 1Kor 3:17. Tuone
thamani na wajibu kuulinda uhai na kuutetea. Uhai ni mali ya Mungu na zawadi ya
Mungu kwetu.
Hekalu hili, yaani kila
Mbatizwa ni Takatifu. Na tunapoongelea Kanisa kwa maana ya kwanza kabisa siyo
Jengo bali ni kila aliyebatizwa. Na tunapoongelea Kanisa hai maana yake ni kila
aliyebatizwa na anayeishi ahadi zake za ubatizo vyema katika kujali na
kuwajibika ipasavyo. Kujali na kuwajibika huku kunachukua pande zote mbili,
yaani, Kanisa kama Wabatizwa, na Kanisa Kama Jengo. Sura na mtazamo huu wa
Kanisa la Mungu ni kama ilivyo shilingi. Mfuasi wa Kristo hawezi kujitenga na
kuchagua kuwa sehemu moja tu na kuacha nyingine. Akifanya hivyo atakuwa bado
hajakamilika.
Injili ya leo inatupa
ufafanuzi mzuri kuhusu mtazamo huu wa Kanisa niliouelezea hapo juu. Yesu
alipoingia hekaluni alikutana na mambo ya ajabu sana. Hekaluni watu waliokuwa
wakiuza ng'ombe na kondoo na njiwa, na wenye kuvunja fedha. Kwa hali aliyoikuta
na kuiona ilimbidi kuchukua hatua za haraka mara moja. Yesu “akawaambia wale
waliokuwa wakiuza njiwa, Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa
nyumba ya biashara,” Yoh 2:16. Hili ni Kanisa
Takatifu, na kama Jengo yapaswa
kufanyika yaliyo matakatifu. Yesu hakuona haya kuvitawanya vyote vilivyokuwa
ndani ya hekalu lile.
Wayahudi walipotaka kupewa Ishara ili
wajue ni kwa mamlaka gani anayafanya hayo, “Yesu
akajibu, akawaambia, Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu
nitalisimamisha,” Yoh 2:19. Hapa tunaona maana halisi ya Kanisa na Msingi wake,
yaani, Kanisa kama Wabatizwa wote, na Msingi wake ni Kristo mwenyewe. Kwa maneno hayo ya Yesu, kwamba, walivunje
hekalu naye katika siku tatu atalisimamisha, “yeye alinena habari za hekalu la
mwili wake,” Yoh 2:21.
Habari njema ya Kanisa
hili ni yale aliyokwisha yatabiri Nabii Ezekieli kama tulivyosoma na kusikiliza
somo la kwanza. Kwanza kabisa
katika habari njema hiyo, Kanisa ni sakramenti ya wokovu wetu. Kwa kupitia
Masakramenti yake tunapata neema na kujazwa uhai. Nabii Ezekieli anatumia lugha
ya picha, “mito yenye maji yaponyayo,” yaani, kwa tafsiri tungesema
‘Masakramenti.’ “Tena itakuwa, kila kiumbe hai kisongamanacho, kila
mahali itakapofika mito hiyo, kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa
sababu maji haya yamefika huko maana maji yale yataponyeka, na kila kitu
kitaishi po pote utakapofikilia mto huo,” Eze 47:9.
Mto
huu yaani, Kanisa kwa sasa upo duniani
kote, na Wabatizwa wote wenye kuishi ahadi zao za ubatizo wanazidi kuponywa na
kupata neema za Mungu. “Na karibu
na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa
chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe;
utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali
patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni
dawa,” Eze 47:12. Kwa vile Msingi wa Kanisa hili katika mfano huu wa mto na
maji yake yenye kuponya ni Kristo, kupata neema na baraka hizi yakupasa kuwa
ndani na katika Kristo Yesu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Maana
hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama
Kristo naye anavyolitendea Kanisa,” Efe 5:29
Tusali:-Ee Yesu, tufanya viungo hai
vya mwili wako, yaani, Kanisa kila mmoja wetu kadiri ya wito na nafasi yake.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario