miércoles, 2 de noviembre de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 31 YA MWAKA-C


IJUMAA WIKI YA 31 YA MWAKA-C

Somo: Flp 3:17-4:1

Zab/kit: 122:1-2, 4, 5

Injili: Lk 16:1-8

Nukuu:

“Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo,” Flp 3:18

“mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani,” Flp 3:19

“Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20

“atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake,” Flp 3:21

“Basi, ndugu zangu, wapendwa wangu, ninaowaonea shauku, furaha yangu, na taji yangu, hivyo simameni imara katika Bwana, wapenzi wangu,” Flp 4:1

Toa hesabu ya uwakili wako, kwa kuwa huwezi kuwa wakili tena,” Lk 16:2b

Yule bwana akamsifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru,” Lk 16:8 

TAFAKARI: Toa hesabu ya uwakili wako, kwa kuwa huwezi kuwa wakili tena.”

Wapendwa katika Kristo, Injili ya leo inatupatia hali halisi kuhusu hesabu yetu siku ya mwisho. Yesu analisema jambo hilo akitolea mfano wa Tajiri mmoja na Wakili wake dhalimu. Bila kujua siku wala saa, Wakili huyu dhalimu anatakiwa na Tajiri yake kutoa hesabu ya uwakile wake, baada ya Tajiri yake kupata habari ya kutapanywa kwa mali zake, Lk 16:1. Alichokifanya kwa haraka Wakili yule ni kurejesha uhusiano wa haraka na wateja zake ambao ndio hatma ya maisha yake kwa sasa.

Katika jambo hili ilimpasa kutoa msamaha wa madeni bila kuhathiri utajiri wa Tajiri yake. Hivyo, Yule bwana akamsifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru,” Lk 16:8. Kwa kuyasema haya, Yesu anatuacha na swali zito la kujibu. Swali hilo ni hili: Mimi na wewe tunasubiri nini kurejesha uhusiano wetu na Mungu kwa muda na nafasi tuliyonayo sasa tukiwa bado kwenye nuru, yaani, kwa ubatizo wetu na agano letu katika maisha, iwapo Wakili huyu na udhalimu wake aliweza kurejesha uhusiano wake na wateja zake? 

Somo letu la kwanza sote kama mawakili wa Bwana wetu Yesu Kristo tu na dhamana juu ya imani yetu. Hivyo Mtume Paulo anatufundisha wewe na mimi namna ya kuurejesha uhusiano huo ndani ya nafsi yako, jirani zako, na Mungu. Na kama tunashindwa namna ya kufanya tumtazame yeye (historia yake awali na maisha yake baada ya kuongoka, Flp 3:17; Gal 1:13-23). Hapo mwanza kabla ya kumjua Kristo alilihujumu Kanisa haswa kwa sababu alifikiri kufanya hivyo ni kulinda na kutetea mila na desturi za Kiyahudi ambazo kwa uwepo wa Kristo na Wakristo ilikuwa ni tishio katika ustawi wake.

Kwa maneno mengine kabla la kuongoka kwake, Paulo alikuwa mpinga Kristo si kwa maneno tu bali kwa matendo yake, Mdo 9:1-2. Hivyo leo akiwa huru ndani na katika Kristo Yesu anatoa mang’amuzi yake na kusema, “Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo,” Flp 3:18. Paulo sana yupo ndani ya nuru ya Yesu Kristo, na anaona faida kubwa ya kuwa na uhusiano naye. Kuna hasara kubwa kujua kweli hii na mwisho wa siku ukaacha kujenga uhusiano na Kristo aliye njia, kweli, na uzima.

Leo na kama ilivyokuwa nyakati za Mtume Paulo, yapo mambo mengi ambayo yanayoturudisha nyumba na hata kutokuwa tayari kuujenga uhusiano huo na Kristo. Wengi walishindwa kuujenga uhusiano huo na Kristo kwa sababu, “mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani,” Flp 3:19. Vishawishi hivi alivyovitaja Mtume Paulo licha ya kupita zaida ya miaka 2000 havijabadili  kwa kizazi cha leo. Ni kwa sababu ya tumbo-ubinfsi uliokidhiri, utukufu wa kutaka kuogopwa na kuabudiwa kama Mungu, fedha na utajiri, na kuupenda ulimwengu na mambo yake katika ufahari wake, leo wengi tumejikuta katika mtego huu. Maisha ni dhamana na ipo siku wewe na mimi tutatakiwa kutoa hesabu.

Ukweli ni kwamba, maisha ya hapa duniani licha ya vishawisho hivyo, ni ya muda mfupi sana. Hapa sipo mwisho na kusudi la kuumbwa kwetu. Tumeumbwa tuishi milele, na hapa sipo penye hayo kao ya milele. “Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20. Na katika mantiki hii, ni Kristo Yesu tu “atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake,” Flp 3:21. Haya yote tunayoyaangaikia usiku na mchana licha ya uzuri wake na mafaa yake, hayawezi kuubadili mwili wetu wa unyonge ufanane na mwili wa Kristo wa Utukufu.

Mwito wa Mtume Paulo kwako na kwangu leo ni huu: “simama imara katika Bwana,” Flp 4:1. Na kusimama katika Kristo Yesu ni kuenenda kama wana wa Nuru na siyo wa giza. Matendo yetu mema yawe chumvi pale tulipo, na maadili yetu mema yawe taa na mwanga pale tulipo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo,” Flp 3:20

Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wetu, tujalie mwanga na nuru katika maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario