JUMAMOSI WIKI YA 31 YA MWAKA-C
Somo:
Flp 4:10-19
Zab/kit: 112:1-2, 5-6, 8a, 9
Injili: Lk 16:9-15
Nukuu:
“Najua
kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote,
nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa,”12
“Nayaweza mambo yote
katika yeye anitiaye nguvu,” Flp 4:13
“Aliye mwaminifu
katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye
dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia,” Lk 16:10
“Hakuna
mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu na
kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia
Mungu na mali,” Lk 16:13
“Akawaambia,
Ninyi ndinyi mnaojidai haki mbele ya wanadamu, lakini Mungu awajua mioyo yenu;
kwa kuwa lililotukuka kwa wanadamu huwa chukizo mbele za Mungu,” Lk 16:15
TAFAKARI:
"Mshika mawili kwa pamoja, moja humponyoka.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Injili yetu ya leo yatutafakarisha juu ya kweli hii, ‘mshika mawili kwa pamoja,
moja humponyoka.’ Sehemu hii ya Injili ni mwendelezo wa Injili tuliyosoma jana
tulipotafakari neno hili, ‘Toa hesabu ya uwakili wako, kwa kuwa huwezi kuwa
wakili tena.’ Ndugu yangu, unapokuwa na malengo thabiti katika maisha yako
hukujengea msisitizo na uaminifu wa jambo hilo unalolifanya. Mafanikio ya mtu
ni moja ya tokeo la namna alivyojiwekeza katika kitu hicho. Mkusanyiko wa
pamoja wa nguvu zako, akili zako, na juhudi zako zisizo jigawagawa hukupatia
matokeo mazuri kwa kile ukifanyacho.
Katika jambo hili la
kujigawagawa Yesu anatupa angalizo na kusema, “Hakuna
mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu na
kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia
Mungu na mali,” Lk 16:13. Kama wataka kumtumikia Mungu fanya hivyo kweli pasipo
kujibakiza. Kufikia hatua hii katika mwono huu wa maisha, ni kufanya tathimini
ya kina juu ya maisha yako kama asemavyo Mtume Paulo, “Najua
kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote,
nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa,” Flp 4:12.
Matokea ya tathmini hii katika maisha ni makubwa sana, faida yake nikubwa sana,
yaani, hapa duniani na Mbinguni uzima wa milele.
Ila ukijitumikisha tu
kwa sababu ya mali, utapata faida ya muda mfupi hapa duniani na kukosa faida ya
milele Mbingu, yaani maisha ya uzima na umilele wake. Pamoja na hayo yote
niliyoyasema, mafanikio yako husukumwa
na uaminifu wako mwenyewe kwa kile unachofanya hata katika udogo wake. Katika
hili, Mtume Paulo anatoa ushuhuda wa uaminifu wake kwa jumuiya ile ya Wafilipi
na kusema, “Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa katika
mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa lingine lililoshirikiana
nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu,” Flp 4:15.
Mtume Paulo hakujibakiza katika ushiriki wake na watu wake. Aliwaona kama
alivyojiona yeye mwenyewe, na alikuwa sehemu ya jumuiya ile katika kufikiri,
kuamua, na kutenda pamoja. Naye anawaambia, “mlifanya vema, mliposhiriki nami
katika dhiki yangu,” Flp 4:14
Ndugu yangu,
tunapojitoa kwa watu na kwa ajili yao, kamwe hawawezi kutuacha katika yote.
Ushiriki wetu na watu katika shida zao kwa lengo la kufanya hali na mazingira
yale yawe sehemu nzuri zaidi ya kuishi, huwajengea ujari wale unaowaongoza na
kwako pia kwani matokeo yake huyaona na kuyaishi. Hivyo Wafilipi hawakumtupa
Mtume Paulo. Walimjali hata nyakati zile ambazo hakuwa nao. Naye Mtume Paulo
anawakumbusha ukarimu wao kwake na kusema, “hata huko Thesalonike mliniletea
msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja,” Flp 4:16. Ni vibaya sana pale
tunapokosa shukrani kwa yale watutendeayo watu kwa upendo wao. Na moyo usio na
shukrani ukausha mema yote. Hata kama watutendeayo watu ni madogo,
hatupungukiwi chochote kwa kusema neno “ASANTE.”
Ndiyo maana leo Yesu
anatuambia, “Aliye mwaminifu katika lililo
dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika
lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia,” Lk 16:10. Hapa Yesu
anatukumbusha kuwa maisha ni dhamana. Na kama maisha ni dhamana juu ya yale
tuliopewa uwakili, basi yatupasa kuthamini kama yalivyo katika ukubwa na udogo
wake. Leo Mtume Paulo anatufundisha namna ya uwakili baada ya kutambua thamani
ya yale tuliyo wekwa dhamana nayo. Naye anasema, “Lakini ninavyo vitu vyote na
kuzidi, tena nimejaa tele; nimepokea kwa mkono wa Epafrodito vitu vile
vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo
Mungu,”Flp 4:18. Ni yule tu mwenye hofu ya Mungu ndani yake anayeweza kuyasema
haya toka moyoni mwake kwa ujasiri. Mara nyingi na tulio wengi, ‘kwenye
mafanikio huzinyanyua nafsi zetu, na penye hasara au kushindwa huwalaumu
wengine.’
Wewe na mimi tukiwa tu wafuasi
wa Kristo na ndiyo maana tunaitwa Wakristo, hofu yetu katika kufikiri, kuamua,
na kutenda ni KRISTO anayeyajenga maisha yetu kila siku. Na hii ndiyo siri ya
mafanikio ya Mtume Paulo kama asemavyo, “Nayaweza
mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” Flp 4:13. Je, nguvu na jeuri yako
msingi wake ni nini? Je, ni umaarufu ulio nao? Cheo ulicho nacho? Utajiri na
fedha ulizo nazo? Je, ni afya uliyo nayo? Hayo yote ni upepo bila Mungu kwa
sababu yote ni mali ya Mungu. Tumeazimwa tu kwa muda, kwani tulivikuta, na
mwisho wa siku tutawaachia wengine kwa sababu hatukuja navyo. “Nchi na vyote
viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake. Maana ameiweka misingi yake juu ya
bahari, Na juu ya mito ya maji aliithibitisha,” Zab 24:1-2. Je, bado una jeuri?
Mtume Paulo
anatufundisha wewe na mimi leo kwamba
tuwapo ndani na katika Kristo Yesu yote mema na mazuri yanawezekana kwani huyo
ndiye Mungu anayemtumikia. Naye anasema, “Na Mungu wangu atawajazeni
kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo
Yesu,” Flp 4:19.
Hivyo
ndugu yangu ni kukumbushe tena neno hili kwamba, “Moyo usio na shukrani ukausha mema yote. Na mshika
mawili kwa pamoja, moja humponyoka.” Kristo Yesu ndiye jibu kwa sababu ndani na
katika Yeye ipo njia, kweli, na uzima, Yoh 14.6. Amina
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nayaweza mambo yote katika yeye
anitiaye nguvu,” Flp 4:13
Tusali:-Ee Yesu Mwema, yaongoze maisha yetu ili tuweze
kabiliana na changamoto
No hay comentarios:
Publicar un comentario