domingo, 13 de noviembre de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 33 YA MWAKA-C


JUMATATU WIKI YA 33 YA MWAKA-C

Somo: Ufu 1:1-4; 2:1-5a

Zab/kit: 1:1-2, 3, 4, 6

Injili: Lk 18:35-43

Nukuu:

 “Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu,” Ufu 1:3

“Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo,” Ufu 2:2

“Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza,” Ufu 2:4

“Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza,” Ufu 2:5a

Akapiga kelele, akisema, Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:38

Basi wale waliotangulia wakamkemea ili anyamaze; lakini yeye alizidi sana kupaza sauti, Ee Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:39

“Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia, alimwuliza, Wataka nikufanyie nini? Akasema, Bwana, nipate kuona,” Lk 18:40-41 

Yesu akamwambia, Upewe kuona; imani yako imekuponya,” Lk 18:42 

TAFAKARI: “Upewe kuona; imani yako imekuponya.”

Wapendwa wana wa Mungu, miongozo ya kibinadamu na mwonekano wake unaweza kutunyamazisha hapa na pale kwa kuikandamiza dhamiri iliyo hai na safi kuelekea lililo kweli na haki. Kelele hizo kamwe zisiwe kizuio cha kiu na kweli iliyopo ndani ya mioyo yetu. Leo katika Injili tunaona watu wachache wakijaribu kuzuia dhamiri iliyo hai na safi ya mtu mmoja kipofu aliyekuwa ameketi kando ya njia wakati Yesu akipita. Aliposikia habari ya Yesu alipiga kelele na kusema, “Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:38.

Jitihada za huyu kipofu zinajaribiwa na kuelekea kuzimwa na baadhi ya watu. Basi wale waliotangulia wakamkemea ili anyamaze; lakini yeye alizidi sana kupaza sauti, Ee Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:39. Dhamiri iliyo hai na safi ya Kipofu huyu ikiongozwa na imani aliyokuwa nayo, inakuwa sababu ya uponyaji wake. Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia, alimwuliza, Wataka nikufanyie nini? Akasema, Bwana, nipate kuona,” Lk 18:40-41. Imani hii iliyothabiti na yenye kuongozwa na dhamiri hai na iliyosafi juu ya Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, inakuwa uponyaji wake. Yesu akamwambia, Upewe kuona; imani yako imekuponya,” Lk 18:42.

Dhamiri hai na safi hukuzwa na kuelimishwa hasa pale tunapopenda kutenda mema kwa vile twatambua jambo jema ni jema kama lilivyo na linastahili kutendwa na kila mmoja wetu na hasa zaidi mwenye hofu ya Mungu.

Somo letu la kwanza tunaona mateso na kudhulumiwa wa Kanisa la mwanzo na wale wampingao Kristo. Falme nyingi na hasa zile zilizojichukulia nafasi ya Mungu, na kujifanya miungu watu hazikupenda kabisa kusikia au kuona habari njema za wokovu, na Ufalme wa Mungu ukishamiri. Katika hali na mazingira yale ilimpasa mmoja asema na kusimama katika kweli na haki. Na hapa ndipo Kanisa lilisimama imara kwa kile lilichokuwa likiamini na kuhubiri.

Na huu ndio unabii wa Yohana, “Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu,” Ufu 1:3. ‘Wakati u karibu’ kulimaanisha mwisho wa nyakati, na wakati huo huo kulimaanisha ni muda muhafaka wa kusimama imara katika imani kadiri ya mashambulio ya wampinga Kristo na Ufalme wake.

Yohana hakuona woga wowote zaidi ya hofu ya Mungu kusimama katika kweli na haki juu ya kile alichokiamini na kukuishi. Leo kati yetu pamoja na uhuru tulionao wa kuabudu na kuishi imani pasipo hofu, bado si mashuhuda wa imani hiyo. Huwezi kuwa shuhuda wa kile ukiaminicho kama huna uwezo wa kukishirikisha kile ukiaminicho kwa watu. Huwezi pia kukishirikisha ukiaminicho kwa sababu hujafanya tafakari ya kina kuhusu neno lile ya uzima. Na huwezi kulitafakari neno hilo kwa sababu hukulipokea. Hukulipokea neno hilo kwa sababu hukutaka kulisikia.

Ni dhahiri akisemacho Yohana na kukitolea ushuhuda ni neno lile la uzima alilolisikia, kulipokea, kulitafakari, kulishirikisha, na mwisho ndilo analolitolea ushuhuda pasipo woga zaidi ya hofu ya Mungu. Na hivi ndivyo mambo yalivyokuwa; “Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi,” Ufu 1:4. Kwa Kanisa lile la Efeso, Yohana analiona hili: “Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo,” Ufu 2:2. Hata pamoja na ukweli na juhudi hizo, bado wanaweza kufanya vizuri zaidi.

Na kufanya kwao vizuri ni kuurejea upendo ule wa kwanza, yaani, nguvu na neema zile walizokuwa nazo baada ya kulisikia na kulipokea neno la uzima. Na hivi ndivyo asemavyo Yohana, “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza,” Ufu 2:4. Na kurejea upendo ule wa kwanza ni kuangalia ni wapi waliojikwaa. “Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza,” Ufu 2:5a. Kufanya tathmini katika maisha ni jambo la muhimu kama kweli twataka kusonga mbele na kwenye mwanga zaidi.

Bila shaka jambo lolote lile liwe zuri au baya katika maisha ya kila siku, ni alama wazi ya kuyatafakari matendo yetu ikiwa ni pamoja na kuyahusisha na kusudi la kuumbwa kwetu, na uwepo wetu hapa duniani. Matukio hayo (mazuri na mabaya) katika jamii yetu yakufanye na kukupa uwezo wewe na mimi wa ‘kusikia, kupokea, kutafakari, kushirikishana, na mwisho kutoa ushuhuda katika kweli na haki.’ Huko tuendako pasipo sisi kupajua kwa asilimia 100% hapawezi kuwa salama kama hatutafanya zoezi hilo la dhamiri njema nililolisema. Maisha kila siku ni darasa. Hivyo tujifunze kadiri tunavyopewa pumzi hii ya bure na Mungu Mwenyezi. Na “tutapewa kuona tena” kama tupo tayari katika NENO-kusikia, kupokea, kutafakri, kushirikishana, na kutoa ushuhuda wa kweli na haki kama tokeo la ishi yetu katika hofu ya Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza,” Ufu 2:5a

Tusali:-Ee Yesu Mwema, niwezeshe kuona tena. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario