JUMAMOSI WIKI YA 33 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 11:4-12
Zab/kit: 144:1, 2, 9-10
Injili: Lk 20:27-40
Nukuu:
“Hao ndio ile mizeituni
miwili na vile vinara viwili visimamavyo mbele za Bwana wa nchi,” Ufu 11:4
“Hata watakapoumaliza ushuhuda wao, yule
mnyama atokaye katika kuzimu atafanya vita nao, naye atawashinda na kuwaua,”
Ufu 11:7
“Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya
uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu
ikawaangukia watu waliowatazama,” Ufu 11:11
“wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na
malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:36
“Naye
si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38
TAFAKARI:
“Wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa
sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo.”
Wapendwa wana wa Mungu, katika Injili ya leo Yesu anawatoa wasiwasi wale
waliomuuliza juu ya nani hasa atakaye kuwa mume baada ya maisha haya ya duniani
ikiwa mwanamke huyo aliolewa na kurithiwa na ndugu saba wa familia moja. Yesu
anawajibu na kuwaambia, “Wana wa
ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini,
wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka
katika wafu, hawaoi wala hawaolewi,” Lk 20:34-35. Tukiwa hapa duniani ni wakati
wa kuyafanya yote katika wema na haki. Hivyo, kesho yetu ni matokeo ya leo
yetu.
Mahitaji yetu tuwapo hapa
ulimwenguni ni tofauti na mahitaji yetu tukiwa mbingu kwenye uzima wa milele.
Hivyo walioko huko kwenye uzima wa milele, “wala hawawezi kufa tena; kwa sababu
huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa
ufufuo,” Lk 20:36. Kwa sababu hiyo mahitaji ya kimwili hayana nafasi tena kwani
tutakuwa na miili iliyotukuka na takatifuzwa, yaani, miili ya ufufuko.
Miili hii ya ufufuko inathibitisha
ukweli kwamba Mungu wetu, “si Mungu wa
wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38. Ndugu yangu,
kesho yako katika mikono salama ya Mungu inategemea leo yako katika mikono ya
Mungu iliyo salama. Hivyo mtafute Bwana ungali hai kwani anapatikana, Isa
55:6-7.
Hata hivyo ipo gharama yake ya
kuufikia mwili huo uliotuka na takatifuzwa, yaani, mwili wa ufufuko. Gharama
yake na hasa katika mazingira yetu ya leo ambayo walio na nguvu ujiinua na
kujifananisha na Mungu, ni kusimama katika kweli na haki. Ni kutokukubali
kuogelea katika mkondo wa maji yao. Ni kutokufurahia wanayofurahia kwa sababu
ni chukizo kwa Mungu mpenda haki, kweli, na mwenye kuthamini utu wa mtu kwa
sababu kwa upendo wake alimuumba mwanadamu kwa sura na mfano wake.
Na pale utakapo simama katika kweli
na haki dhidi ya utawala wowote ule wa giza na dhalimu uwe tayari kuteseka,
kuteswa, na hata kupoteza uhai wako. Na hili ndilo alisemalo Yohana katika somo
letu la kwanza kuonyesha mfanano wa watu hao walio tayari kuifia kweli na haki,
kwamba, “Hao ndio ile
mizeituni miwili na vile vinara viwili visimamavyo mbele za Bwana wa nchi,” Ufu
11:4. Watu hawa ishi yao, na hata kufa yao ni mpango wa Mungu kwa sababu kupia
wao mapenzi yake Mungu hutimia. Katika kweli hii Mtume Paulo anasema, “kwa
maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi
kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:8.
Na katika kuwa mikononi
mwa Mungu bila kujibakiza, kwayo usalama upo. Hivyo “Na mtu akitaka kuwadhuru,
moto hutoka katika vinywa vyao na kuwala adui zao. Na mtu akitaka kuwadhuru, hivyo
ndivyo impasavyo kuuawa,” Ufu 11:5. Lililo jema, na ambalo Mungu kalianzisha
ndani ya watu hawa, Mungu ulisimamia hadi mwisho. Hivyo binadamu jeuri na
asiyekuwa na hofu ya Mungu hatoweza zuiya mpango wa Mungu kwa watu wake. Na
moja ya mpango wa Mungu kwa watu wake ni ile hali ya uhuru aliwapa ambayo
hakuiondoa hata baada ya anguko la wazazi wetu wa kwanza. Je, wewe ni nani basi
mwenye kutaka kuwaweka wana wa Mungu katika mifuko yako?
Kwa vile watu hawa
walioyakabidhi maisha yao mikononi mwa Mungu, naye Mungu huwatumia kufikisha
ujumbe wake na takwa lake, watu hawa “wana amri ya kuzifunga mbingu, ili mvua
isinyeshe katika siku za unabii wao. Nao wana amri juu ya maji kuyageuza kuwa
damu, na kuipiga nchi kwa kila pigo, kila watakapo,” Ufu 11:6. Kwa maneno
mengine, Mungu huwapa nguvu na maono ya ajabu dhidi ya ufalme wa giza na
dhuluma.
Mara nyingi, na hasa
tuitazamapo historia ya Kanisa letu, mwisho wa wa watu hawa wasimamao katika
kweli na haki huwa wa mateso makubwa. Ukweli ni kwamba, penye upendo wa kweli
kuna mateso kwa sababu upendo utupeleka katika ukamilifu ambao wengi hatuutaka
kutokana na hali ile ya umimi. Hivyo,
“Hata watakapoumaliza ushuhuda wao, yule mnyama atokaye katika kuzimu
atafanya vita nao, naye atawashinda na kuwaua,” Ufu 11:7. Mnyama hapa
yamaanisha mtu jeuri, tawala dhalimu, au falme za giza. Kuuawa kwao siyo
kushindwa bali ni ushindi uliotukuka kama asemavyo Bwana wetu Yesu Kristo,
kwamba, “chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo
peke yake; bali ikifa, hutoa mazoa mengi,” Yoh 12:24.
Hivyo ukimya wao baada
ya kuondolewa pumzi yao na mnyama huyo kutoka kuzima ni swala la muda tu. “Na
mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule mkuu, uitwao kwa jinsi ya roho
Sodoma, na Misri, tena ni hapo Bwana wao aliposulibiwa,” Ufu 11:8. Hali na
mazingira haya ya ukimya kama siku ile ya Ijumaa Kuu ni muda wa kuzama katika
tafakari ya kina. “Na watu wa hao jamaa na kabila na lugha na taifa waitazama
mizoga yao siku tatu u nusu, wala hawaiachi mizoga yao kuwekwa kaburini,” Ufu
11:9. Ni tafakari yenye kutupeleka katika mabadiliko ya kweli. Ni wakati wa
kufanywa upya mwili, roho, na hata fikra zetu. Na ndio wakati wa kuona weupe na
weuzi wa mnyama huyu alitoka kuzimu.
Kwa upande mwingine
tendo la kuuawa hawa wasimamiao haki na kweli hutoa furaha kwa watesi wao kwa
sababu kwa kutokuwepo watetezi hawa kwao ni wakati wa kupumua na kuufurahia
udhalimu wao. Hata hivyo hili ni swala la muda mfupi sana. Mungu hawezi kamwe
kuliacho chozi la kweli na haki lipotee bure. Na ndiyo maana kusema, “Nao wakaao juu ya nchi wafurahi juu yao na
kushangilia. Nao watapelekeana zawadi wao kwa wao, kwa kuwa manabii hao wawili
waliwatesa wao wakaao juu ya nchi,” Ufu 11:10.
Ndugu yangu, mwisho wa
jambo jema hata katika hali ya mateso na kifo, ni mwanzo mpya na nuru mpya ya
kule tuendapo na kukutamani. Na hili ndilo linalomaanisha upya huo na ushindi
wa mwenye haki dhidi ya uovu na dhuluma, kwamba, “Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya
uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu
ikawaangukia watu waliowatazama,” Ufu 11:11. Naam, na mwisho wa mtu jeuri,
asiye na hofu ya Mungu, na mwenye kujiinua sawa na Mungu, kwake kiama ni
kikubwa!
Nao wateule wa Mungu
walioutoa ushuhuda wa kweli na haki kwa maisha yao ndipo watakapo sikia “sauti
kuu kutoka mbinguni ikiwaambia, Pandeni hata huku. Wakapanda mbinguni katika
wingu, adui zao wakiwatazama,” Ufu 11:12. Na hili ndilo taji na ile mede
tupasayo kuichuchumilia kila siku ya maisha yetu. Mede na taji hili ni tokeo la
gharama ile uitoayo ili kuupata mwili huo uliotukuka na takatifuzwa, yaani,
mwili wa ufufuko, hali ya Utakatifu, na ndicho cheo chako.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Na baada ya siku hizo tatu u nusu,
roho ya uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu
kuu ikawaangukia watu waliowatazama,” Ufu 11:11
Tusali:-Ee
Yesu tupiganie dhidi ya ufalme wa giza na uovu wake. Bila Wewe hatutoweza
chochote. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario