IJUMAA WIKI YA 33 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 10:8-11
Zab/kit: 119:14, 24, 72, 103, 111, 131
Injili: Lk 19:45-48
Nukuu:
“Na sauti ile
niliyoisikia kutoka mbinguni ilinena nami tena, ikisema, Enenda, ukakitwae kile
kitabu kilichofunguliwa katika mkono wa yule malaika, aliyesimama juu ya bahari
na juu ya nchi,” Ufu 10:8
“Kitwae, ukile, nacho
kitakutia uchungu tumboni mwako, bali katika kinywa chako kitakuwa kitamu kama
asali,” Ufu 10:9b
“Wakaniambia, Imekupasa kutoa unabii tena juu
ya watu na taifa na lugha na wafalme wengi,” Ufu 10:11
“Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala; lakini
ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Lk 19:46
“Naye
akawa akifundisha kila siku hekaluni. Lakini wakuu wa makuhani, na waandishi,
na wakuu wa watu walikuwa wakitafuta njia ya kumwangamiza; wasione la kutenda,
kwa kuwa watu wote walikuwa wakiandamana naye, wakimsikiliza,” Lk 19:47-48
TAFAKARI:
“Kwa Ubatizo wako nawe umetengwa kwa kazi maalum. Naam, umewekwa wakfu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
umuhimu wa kile kilichowekwa wakfu na kwa
ajili ya matumizi rasmi ndicho kisemacho katika Injili yetu ya leo. Yesu
anaingia hekaluni na kukuta yawiyoendana na hadhi ya Hekalu. Hekalu limegeuka
kuwa kituo cha uchuuzi, biashara. Naye anawaambia, “Imeandikwa, Nyumba yangu
itakuwa nyumba ya sala; lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Lk
19:46. Nyumba ya Mungu pamoja na kutolea sadaka na shukrani zetu ni nyumba ya
sala.
Yote
yale yasiyokuwa na uhusiano wa sala, shukrani, sadaka, na mengine kama hayo,
hayapaswi kufanyika mahali hapa. Kabla ya kuteswa, kufa, na kufufuka kwake
Bwana Yetu Kristo alijiweka wakfu kwa ajili yetu na kutufanya kuwa viungo vyake
akiwa yeye ndiye Mwili, yaani Kanisa. “Na
kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli,” Yoh
17:19.
Kanisa kama mwili wa
Kristo, ni kwa namna hiyo ya kutakaswa kupitia Sakramenti ya ubatizo nasi
tunakuwa viungo vya Kristo, na miili iliyowekwa wakfu kwa kushiriki ukuhani wa
kawaida wa Kristo. “Maana kama vile mwili
ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi,
ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Basi
ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake,” 1Kor 12:12,
27. Kwa maana hii, miili yetu imewekwa wakfu ndani na katika Kristo.
Hivyo matendo yote
machafu katika mwili ni kwenda kinyume na kutengwa huko kuliko wekwa wakfu kwa
ajili ya Kristo. “Je! Hamjui ya kuwa
miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo
vya kahaba? Hasha!” 1Kor 6:15.
Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na miili
yetu kuwa ni viungo vya Kristo na kuwekwa wakfu kwa ajili ya Kristo, mwili wa
mtu ni Hekalu la Roho Mtakatifu. “Au hamjui ya kuwa mwili
wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala
ninyi si mali yenu wenyewe; maana
mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu,” 1Kor
6:19-20. Ndugu yangu, na kilichowekwa wakfu na
kibaki kwa ajili hiyo daima.
Yohana
kwa maono yale juu ya Mbingu na Hukumu ya mwisho, kama chombo, anaandaliwa na
kuwekwa wakfu, yaani, kutengwa kwa kazi maalumu. “Na sauti ile
niliyoisikia kutoka mbinguni ilinena nami tena, ikisema, Enenda, ukakitwae kile
kitabu kilichofunguliwa katika mkono wa yule malaika, aliyesimama juu ya bahari
na juu ya nchi,” Ufu 10:8. Hili ndilo neno la uzima, na ndani yake twajifunza
kweli juu ya Mungu.
Hata hivyo ili kutoa
ushuhuda wa kweli juu ya neno hili la uzima, yakupasa kupitia hatua nne muhumu.
Nazo ni kama ifuatavyo, moja, KULISIKIA neno, mbili, KULIPOKEA neno, tatu,
KULITAFAKARI neno, na nne, KULISHIRIKISHA neno. Kwa mantiki hii, ni vigumu
kutoa ushuhuda wa neno kwa wengine kama huwezi kushirikisha NENO. Hutoweza
kulishirikisha NENO kama hujalitafakari. Huwezi kulitafakari NENO kama
ukulipokea. Na hutoweza kulipokea NENO kama hukulisikia.
Hivyo Malaika wa Mungu
anamwambia Yohana, “Kitwae, ukile, nacho kitakutia uchungu tumboni mwako, bali
katika kinywa chako kitakuwa kitamu kama asali,” Ufu 10:9b. Maana yake nini?
“Kukitwa kitabu” ni kulisikia Neno na kulipokea. “Kukila kitabu,” ni
kulitafakari Neno. Na “kutiwa uchungu,” ni kulishirikisha Neno. Na utamu wa
“kitabu,” yaani, ujumbe wa Neno, ni kutoa ushuhuda pasipo woga. Ni kuishuhudia
Imani bila woga. Ni kuishi Imani kwa sababu Neno sasa linakupa Uzima. Na habari
yenyewe ndiyo hii, kama asemavyo Yohana, “Nikakitwaa kile kitabu kidogo katika
mkono wa malaika yule, nikakila; nacho kikawa kitamu kama asali kinywani
mwangu, na nilipokwisha kukila tumbo langu likatiwa uchungu,” Ufu 10:10.
Na utoaji wa unabii,
ndiyo ushuhuda wa kile kikutiacho uzima na nguvu. Furaha ni kama kikohozi
huwezi kukizuia. Uzima huo siyo kwa ajili yako tu, bali yakupasa kuupasisha kwa
wengine pia. Na ndiyo maana ilimpasa Yohana “kutoa unabii tena juu ya watu na taifa
na lugha na wafalme wengi,” Ufu 10:11. Ujumbe huu siyo kwa yale tu wayapendayo
watu kuyasikia, bali hata yale wasiyoyapenda ila yanawapa uzima wa kweli. Hata
baadhi ya dawa huwa chungu, ila tokeo lake ni uponyaji. Na lengo msingi hapa ni
kufinyangwa na kuwa na umbo la kimungu; yaani, upendo wake, haki yake, kweli
yake, huruma yake, na msamaha wake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nyumba yangu
itakuwa nyumba ya sala; lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Lk
19:46
Tusali: Ee Yesu Mwema,
nijalie kuishi ahadi za ubatizo wangu kwa uaminifu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario