JUMATATU WIKI YA 34 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 14:1-3,4b-5
Zab/kit: 24:1-2, 3-4ab, 5-6
Injili: Lk 21:1-4
Nukuu:
“Kisha nikaona, na
tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na
arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake
limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao,” Ufu 14:1
“Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko
kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Na katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana
hawana mawaa,” Ufu 14:4
“Hakika
nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia
sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote
alivyokuwa navyo,” Lk 21:3-4
TAFAKARI:
Je, najitoa vya kutosha?
Wapendwa wana wa Mungu,
kusimama katika kweli na kujitoa bila kujibakiza
ndiyo mfumo aupendao Kristo hasa pale tunapoishi katika mazingira ya kubaguana
kutoka na hali na historia zetu. Katika utoaji wa sadaka, mwanamke mjane
anahesabiwa haki kwa tendo la kujitoa bila kujibakiza. Yesu “Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini
ametia zaidi kuliko wote; maana,
hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini
wake ametia vyote alivyokuwa navyo,” Lk 21:3-4.
Je ndugu yangu umejitoa vilivyo? Ni katika kutoa
bila kujibakiza kunakuwa kwako silaha za haki. Hivyo, “wala msiendelee
kuvitoa viungo vyenu kuwa silaha za dhuluma kwa dhambi; bali jitoeni wenyewe
kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa, na viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha
za haki,” Rum 6:13. Kama wafuasi wa Kristo nielewe kwamba pale nilipo
ninamwakilisha Kristo katika kweli na haki.
Na
tokeo la kujitoa kama ulivyo na bila kujibakiza ni kuhesabiwa haki pia baada ya
maisha yako hapa duniani. Naye Yohana anasimulia maono yake kuhusu yale
aliyoyaona huko mbinguni, “nikaona, na tazama, huyo
Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu
pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya
nyuso zao,” Ufu 14:1. Ujumbe ni kwamba, hapa duniani waweza kufanya ujanja wa
kila aina, ila hata ukifanikiwa kuingia mbinguni kwa ujanja ujanja hutofurahia
hali hiyo kamwe, na kama kutakuwa na nafasi ya kuchoropoka, basi utakimbia
haraka.
Sababu hasa ya
kuchoropoka haraka huko mbinguni ni kutokana na kutoendana na hali hiyo ya
Mbinguni. Elewa uwapo hapa duniani ndivyo unavyoiandaa hali hiyo. Maandalizi
yetu ya maisha ya uzima wa milele yanaanza hapa hapa duniani. Na kwa sababu
hiyo, Yohana katika maono yake anatuambia hivi, pamoja na watakatifu hao kuimba
wimbo mpya mbele ya kile kiti cha enzi, “wala hapana mtu aliyeweza kujifunza
wimbo ule, ila wale mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi,”
Ufu 14:3. Hivyo ikiwa kwa ujanja wako utafanikiwa kuingia mbinguni utajiondokea
mwenyewe kwa sababu utaonekana wazi kuwa ni mzamiaji.
Hivyo wataeule wa Mungu
katika mastahili yao hawatakuwa na shaka yoyote kwa sababu uwepo wao umekidhi
kiwango na mastahili yake. Ndugu yangu, wateule “Hawa wamenunuliwa katika
wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Na katika vinywa vyao
haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa,” Ufu 14:4. Mimi na wewe leo tunaoivuta
pumzi hii ya uhai tuelewe kwamba maandalizi ni leo na sasa kwa sababu hakuna
ajuaye nukta ijayo ya maisha yake hapa duniani.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Hawa wamenunuliwa katika wanadamu,
malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo,” Ufu 14:4a
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, nijalie nife kifo chema. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario