sábado, 5 de noviembre de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 32 YA MWAKA-C



 

Somo I: 2 Mak 7:1-2, 9-14

Zab/Kit: 17:1, 5-6, 8b, 15

Somo II: 2The 2:16-3:5

Injili: Lk 20:27-38

Nukuu:

 “Wewe, mdhalimu, unatufarikisha na maisha ya sasa, lakini Mungu wa ulimwengu attufufua sisi tuliokufa kwa ajili ya amri zake, hata tupate uzima wa milele,” 2Mak 7:9

 “Ni vema kufa kwa mikono ya wanadamu na kuzitazamia ahadi zitokazo kwa Mungu, kuwa tutafufuliwa naye. Lakini kwako wewe hakuna ufufuo,” 2Mak 7:14

 “Yesu akawaambia, Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi,” Lk 20:34-35

“wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:36

 “Naye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38

“Na Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema,” 2The 2:16-17

 “Bwana awaongoze mioyo yenu mkapate pendo la Mungu, na saburi ya Kristo,” 2The 3:5

TAFAKARI: “Mungu wetu si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 32 ya mwaka “C” wa Kanisa. Wazo Kuu la leo ni ‘uwepo wa Mungu wetu ambaye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake.’ Hivyo hatuna kitu chochote cha kupoteza hata kama katika hali ya mateso na dhiki nyingi uhai wetu utaondolewa kwa hila za mwanadamu. Mwanadamu kwa ulevi wa madaraka, nguvu, sifa, ufahari, na utajiri haweza kuibatilisha dhima ile aliyopewa na umma wa watu, na kuifanya shubiri kwao. Hapa ndipo mwanadamu anapojichukulia maumbile na ukuu wa Mungu.

Katika hali na mazingira kama haya, Yesu anatutaka tusimame katika kweli na haki, na wala hakuna cha kuogopa hata kama twafikwa na mauti. Naye anasema, “Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehenum,” Mt 10;28; Lk 12:5. Pale kunapokuwa na utawala kandamizi juu ya watu, na kujiinua kwa tawala hiyo mithili ya malaika walio hasi na mfano wa miungu, jamii husika hujawa na hofu, na hata wakati mwingine huweza kumwasi Mungu kwa kuzitii mamlaka hizi za giza. Jambo hili linapotokea ni chukizo kubwa sana mbele ya Mungu.

Somo letu la kwanza linatufundisha kuwa na hofu ya Mungu, na kusimama katika kweli na haki pasipo maasi. Ndugu wale watatu wa familia mmoja wanalazimishwa  kuonja nyama ya nguruwe ingawa kwetu leo lingetokea zoezi hilo lingekuwa heri kwa sababu kwa walio wengi ni kitoweo kipendwacho sana. Ila kinacholengwa katika somo hili la kwanza ni shuruti ile ya kulazimishwa kwenda kinyume cha dhamiri iliyo njema na safi kwa kumridhisha mwanadamu ambaye kwake yeye kama alivyo hana uzima huo wa milele ndani yake. Ndugu hawa wapo tayari kufa kuliko kwenda kinyume cha dhamiri zao. “Sisi tu tayari kufa kuliko kuzivunja amri za wazee wetu,” 2Mak 7:2b. Tupo kama tulivyo, yaani, jamii husika kutokana na mazingira, mila, na desturi tulizokulia. Na kwa asilimia kubwa mila na desturi hizi zimebeba uhai wa watu na ndiyo maana jamii husiku uendelea kuishi na kukabiliana na changamoto za maisha ya kila siku.

Jambo la kushangaza ni pale mmoja wa jamii husika kwa kulewa kilevi cha madaraka anajaribu kuvunja utaratibu ulio mzuri kwa kujiimairisha na kujitukuza kusiko kwa mafaa wala afya kwa jamii husika. Kuiokoa ama kuikomboa jamii husika kila mwenye hofu ya Mungu yampasa kusima katika kweli na haki kukemea uovu huu wa wazi na ulio moja kwa moja katika kuleta maumivu kwa watu pasipo sababu yoyote zaidi ya kujiinua kwa tawala dhalimu. Mmoja ya ndugu hawa watatu anatoa ujumbe sawiya kwa tawala hii dhalimu na kusema, “Wewe, mdhalimu, unatufarikisha na maisha ya sasa, lakini Mungu wa ulimwengu atatufufua sisi tuliokufa kwa ajili ya amri zake, hata tupate uzima wa milele,” 2Mak 7:9. Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, ni vyema ukajua wa kuogopwa na Mungu peke yake. Huyu ndiye mwenye mambo yote, yaani, “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:6-8

Historia ni mwalimu mzuri sana katika maisha. Hakuna tawala yoyote ile iwe ya kiustarabu au ya kiimla iyodumu katika umilele wake. Huu ni ujumbe kwetu kwamba mtawala katika umilele wake ni Mungu peke yake kwa sababu wote huishi kwake, Lk 20:38b. Ni kweli kunakupoteza ili kupata hata kama haki hiyo itacheleweshwa, ila ahadi ya Mungu kwa watu wake itasimama kama ilivyo mbele ya macho yake na kamwe haiwezi kupotezwa. Na huu ndio msimamo wa mmoja wa ndugu wale waliolazimishwa kuionja nyama ya nguruwe; “Kutoka mbinguni nalipewa hivi, na kwa ajili ya amri za Mungu navihesabu kuwa si kitu, na kwake natumaini kuvipokea tena,” 2Mak 7:11.

Leo pamoja na binadamu kuwa na ufahamu mkubwa juu ya mazingira yake, na uwepo wa binadamu mwenzake ambaye naye ana haki sawa na huyu anayoisimamia haki hiyo, lakini jambo la ajabu ni kwamba binadamu huyu amekuwa mwepesi kuikandamiza haki hiyo na kuwafanya mwenzake waishi kama panya na watumwa katika mazingira yao. Je, tuyafanyapo haya kwa wenzetu twakiona kifo mbele yetu? Na kama hatukioni kifo mbele yetu, Je, waifikiria kesho yetu? Ubatili hauwezi kudumu katika umilele wake kwa sababu hauna mfanano na Mungu wala ukuu wake. Hivyo “Ni vema kufa kwa mikono ya wanadamu na kuzitazamia ahadi zitokazo kwa Mungu, kuwa tutafufuliwa naye. Lakini kwako wewe (Mdhalimu) hakuna ufufuo,” 2Mak 7:14. Na ngoma ikiwamba sana ni ujumbe pia inakaribia kupasuka.

Yesu katika Injili ya leo anawatoa wasiwasi wale waliomuuliza juu ya nani hasa atakaye kuwa mume baada ya maisha haya ya duniani ikiwa mwanamke huyo aliolewa na kurithiwa na ndugu saba wa familia moja. Yesu anawajibu na kuwaambia, “Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi,” Lk 20:34-35. Tukiwa hapa duniani ni wakati wa kuyafanya yote katika wema na haki. Hivyo, kesho yetu ni matokeo ya leo yetu.

Mahitaji yetu tuwapo hapa duniani/ulimwenguni ni tofauti na mahitaji yetu tukiwa mbinguni kwenye uzima wa milele. Hivyo walioko huko kwenye uzima wa milele, “wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:36. Kwa sababu hiyo mahitaji ya kimwili hayana nafasi tena kwani tutakuwa na miili iliyotukuka na tukufuzwa. Miili ya ufufuko. Ukweli huu unathibitisha kwamba Mungu wetu, si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38. Ndugu yangu, kesho yako katika mikono salama ya Mungu inategemea leo yako katika mikono ya Mungu iliyo salama (katika kweli na haki). Hivyo mtafute Bwana ungali hai kwani anapatikana. Ni kuishi katika hofu ya Mungu.

Na tumaini letu katika nyakati hizi za sintofahamu ndilo hili; Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema,” 2The 2:16-17. Hakuna lisilowezekana kwa Mungu.

Tangu sasa ndani na katika Kristo Yesu, neema na baraka zimefunguliwa kwa watu wote. Mlango huu umefunguliwa hata kwa wale walioonekana ni wapagani kwa njia ya maono ya Petro alipokuwa akisali na mbingu zikafunguka, na chombo kikashuka kama nguo kubwa, wakiwemo aina zote za wanyama wenye miguu minne, watambaao, na ndege wa angani, Mdo 10:11-12. Kadiri ya maono haya Petro alisita kupokea maagizo ya Mungu kwa sababu ndani yake walikuwepo wanyama wale waliokatazwa kuliwa nao ni najisi, Mdo 10:14. “Pamoja na hayo, wanyama hawa hamtawala katika wale wenye kucheua, na katika wale walio na kwato; ngamia, kwa sababu yuacheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. Na wibari, kwa sababu yeye hucheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. Na sungura, kwa sababu hucheua, lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. Na nguruwe, kwa sababu yeye anazo kwato, ni mwenye miguu iliyopasuka kati, lakini hacheui, yeye ni najisi kwenu. Msiile nyama yao, wala msiiguse mizoga yao; hao ni najisi kwenu,” Law 11:4-8. Na hiki ndicho kisa tulichokiona katika somo letu la kwanza leo. Ndugu wale hawakuwa tayari kwenye kinyume cha dhamiri zao juu ya mapokeo na mafundisho ya wazee wao.

Kipindi cha Yesu na baada ya kufa na kufufuka kwake, Wapagani hawakuchangamana na Wayahudi, na mbaya kazaidi Wayahudi wale ambao kwa namna ya pekee ndio walikuwa Kanisa la Mwanzo. Hizi ni changamoto ambazo zilipelekea kuwepo kwa Mkutano/Mtaguso huko Yerusalemu, Mdo 15:1-41. Kuchangamana kwao ni najisi kama ilivyokuwa kula nyama za wanyama hawa au kugusa mizoga yake. Badala yake  “sauti ikamjia, kusema, Ondoka, Petro, uchinje ule. Sauti ikamjia mara ya pili, ikimwambia, Vilivyotakaswa na Mungu, usiviite wewe najisi,” Mdo 10: 13, 15. Neno “Ondoka uchinje ule,” linatupa uthibitisho wa kufunguliwa neema na baraka kwa watu wote wenye hofu ya Mungu.

Tendo hili linathibitishwa na Petro mwenyewe huko Kaisaria kwa ujumbe uliotumwa kwake na  Kornelio akida, mtu mwenye haki, mchaji wa Mungu, aliye na sifa njema kwa taifa lote la Wayahudi, Mdo 10:22. Mtume Petro kwa kuona tendo hili kubwa likitokea hata kwa wapagani kushukiwa na Roho Mtakatifu, anatoa hitimisho la Imani na kusema, “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye,” Mdo 10:34-35. Hivyo kumcha Mungu na kutenda haki ndicho kibali chakukubaliwa na Mungu.

Kibali hiki ndicho kielelezo cha utakatifu wetu. Na utakatifu huu ndio cheo chetu mbele ya Mungu licha ya utofauti rangi zetu, familia zetu, koo zetu, makabila yetu, na utaifa wetu. Haya yote yaliyo ya kibinadamu bila utakatifu wa Mungu katika kumcha na kutenda haki hayana fadhila yoyote mbele za Muumba wetu.

Ndugu yangu, hakuna asiyependa mwanga kunako giza nene. Kuyafanya mazingira yetu ya giza kuwa sehemu nzuri zaidi ya kuishi, yatupasa kujifunza kutoka Mshumaa. Kwa kuwaka mshumaa tunapata mwanga na giza linatoweka. Hata hivyo, kwa tendo hilo la pekee haliuachi mshumaa katika hali yake. Kadiri uwakavyo mshumaa ndiyo hivyo hivyo kutoweka, kujififisha, na kupungua kwa mshumaa huo. Bila kuwa na tabia ya mshumaa jamii yetu haitaweza kupiga hatua kutoka kwenye uovu na kwenda kwenye wema na uzuri.

Mimi na wewe, na kila mmoja wetu kadiri ya wito wake, na nafasi yake aliyonayo katika jamii, yampasa kuwa mshumaa pale alipo. Kutumia nguvu nyingine bila kubadilika sisi wenyewe kimtazamo na tabia, hakuna heri mbele zaidi ya majanga.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Ni vema kufa kwa mikono ya wanadamu na kuzitazamia ahadi zitokazo kwa Mungu, kuwa tutafufuliwa naye. Lakini kwako wewe hakuna ufufuo,” 2Mak 7:14

Tusali:-Ee Yesu Mwema na Mkombozi wetu, tujalie hofu yako ndani yetu, ili kuyatenda yote katika upendo, kweli, na haki. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario