JUMANNE WIKI YA 32 YA MWAKA-C
Somo:
Tit 2:1-8, 11-14
Zab/kit: 37:3-4, 18, 23, 27, 29
Injili: Lk 17:7-10
Nukuu:
“Lakini wewe nena mambo yapasayo mafundisho yenye
uzima; ya kwamba wazee wawe wenye kiasi, wastahivu, wenye busara, wazima katika
imani na katika upendo na katika saburi,” Tit 2:1-2
“Maana neema ya
Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na
tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu
huu wa sasa,” Tit 2:11-12
“Lakini, ni nani kwenu mwenye mtumwa
alimaye au achungaye ng'ombe, atakayemwambia mara arudipo kutoka shambani, Njoo
upesi, keti, ule chakula?” Lk 17:7
“Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya
yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu
yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10
TAFAKARI: “Mtakapokwisha kuyafanya yote
mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa
kufanya.”
Wapendwa
wana wa Mungu, lazima nielewe kwamba tendo lolote nilifanyalo lapaswa kuongozwa
na unyenyekevu wangu. Nielewe nayafanya haya kwa sababu yanipasa kuyafanya tena
kwa umakini mkubwa nikitimiza nafasi yangu kama initakavyo kufanya kwa sifa na
utukufu wa Mungu. Ni katika kweli hii Yesu anatuambia, “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote
mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa
kufanya,” Lk 17:10. Tutajisikia hali hii
pale tu tunaposhinda kujifananisha na kujilinganisha na yale tuyafanyayo.
Hivyo katika kweli
na haki simama katika dhamiri yako safi bila woga. Hupaswi kuwa na hofu
kulisema lile libebalo uzima ndani yako na kwa wengine. Hekima aliyonayo mtu
mara nyingine siyo tunda la umri wa mtu, bali ni uwezo ule alio nao mtu wa
kuliona jambo kama lilivyo na siyo kama alivyo. Hapa ndipo hekima ya mtu
kutoshahabiana na umri wake. Na hili likiwa ndani yako, “nena mambo yapasayo mafundisho
yenye uzima; ya kwamba wazee wawe wenye kiasi, wastahivu, wenye busara, wazima
katika imani na katika upendo na katika saburi,” Tit 2:1-2.
Ni kweli isiyo shaka
kwamba kuishi miaka mingi ni kuona mengi na kung’amua mengi katika maisha. Na
katika hali na mazingira kama haya, ndipo tunaposema kwamba mang’amuzi ni
mwalimu mzuri. Hapa ndipo kigezo cha umri huusishwa na hekima aliyokuwa nayo
mtu. Hivyo katika jamii yoyote ile wale walio kula chumvi nyingi, yaani, wenye
umri mkubwa zaidi ya wengine yawapasa kuwa mfano na darasa la maadili mema, ili
jamii iijue kweli, haki, usawa, na kuishi katika upendo kama ndugu. Kwa mantiki hiyo, “vivyo hivyo na wazee wa
kike wawe na mwenendo wa utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia
mvinyo nyingi, bali wafundishao mema; ili wawatie wanawake vijana akili,
wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi,
kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la
Mungu lisitukanwe,” Tit 2:3-5
Hata hivyo kumjua
mfugaji aliye hai na endelevu ni uwepo wa idadi ya ndama alio nao kwenye zizi.
Ikiwa kuna ndama wengi na wenye afya, basi hiyo ni dalili ya mfugaji mwenye
maono, malengo, na mwendelevu. Hivyo hivyo katika jamii yoyote ile uwepo wa
vijana wenye maadili mema ni uhai wa
jamii hiyo na taifa hilo. Ila kuwapata vijana wenye maadili mema leo hutegemea
sana shule yetu ya awali, yaani, familia. Familia zilizo hovyo ni tokeo la
jamii hovyo, kuanzia viongozi hadi waongozwa. Vijana ndiyo injini-“nguvu
sukuma” ya jamii husika na taifa pia. “Vivyo
hivyo na vijana waume uwaonye kuwa na kiasi; katika mambo yote ukijionyesha
wewe mwenyewe kuwa kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako
ukionyesha usahihi na ustahivu, na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa
makosa, ili yule mwenye kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena
juu yetu,” Tit 2:6-8
Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, ‘neema na baraka hufanya kazi katika uhalisia wa kitu
kama asemavyo Mt Thomasi wa Aquina.’ Kumbe palipo andaliwa vyema, yaani, katika
ufahamu na umaana wake, neema na baraka hiyo ya Mungu ujifunua na kufanya kazi
sawasawa. “Maana neema ya Mungu
iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa
za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu
wa sasa,” Tit 2:11-12.
Hata hivyo, kuwa na
uhakika na kule tuendapo tusipopajua twahitaji kielelezo cha kutufikisha huko.
Leo wewe na mimi ndani na katika Kristo Yesu, tunacho zaidi ya kielelezo cha
kule tusipokujua bado ingawa kupo. Hivyo “tukilitazamia
tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na
Mwokozi wetu; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi
yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi
katika matendo mema,” Tit 2:13.14. Kristo ndiyo Njia, Kweli, na Uzima, Yoh
14.6. Bila Kristo kwa Mkristo, hatuwezi kuufikia uzima huo wa milele ingawa
wasiomfahamu Kristo na wasio Wakristo wataufikia uzima huo wa milele kwa
dhamiri zao njema.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana neema ya Mungu iwaokoayo
wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia,”
Tit 2:11
Tusali:-Ee
Yesu tujalie neema ya kutumika kwa ajili ya wengine kwa sifa na Utukufu wako,
na siyo kutumikiwa. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario