ALHAMISI WIKI YA 32 YA MWAKA-C
Somo:
Flm 7-20
Zab/kit: 146:7, 8-9a, 9bc-10
Injili: Lk 17:20-25
Nukuu:
“lakini,
kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa
mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9
“Nakusihi
kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo;
ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika
vifungo vya Injili,” Flm 10, 13
“Ufalme
wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; wala
hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo
ndani yenu,” Lk 17:20b-21
“Lakini kwanza, hana budi kupata
mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki,” Lk 17:25
TAFAKARI: Kwa upendo sadaka, Mwana wa Adamu hana budi kupata mateso mengi, na
kukataliwa na kizazi hiki.”
Wapendwa
wana wa Mungu, maisha yako na makusudi ya kuumbwa kwako na Mungu ni kuishi
milele. Ufalme wa Mungu upo ndani yetu tangu kuumbwa kwetu. Mungu kwa kutuumba
kwa sura na mfano wake alianzisha rasmi ufalme wake ndani yetu. Kwa hiyo ni
jukumu lako na langu kuupokea kwa uhuru ufalme huu na kuwa sehemu ya maisha
mapya na Mungu au kuukataa. Hivyo pamoja na kwamba ufalme huu wa Mungu umo
ndani yako unayo hiari ya kuukataa pia kwa sababu Mungu haingilii uhuru wako.
Ni
kwa mantiki hii hatuwezi kusema ufalme wa Mungu waja kutoka upande gani wa
maisha yetu, bali yatupasa kujibiidisha kila siku kuuelewa na kuuishi. Yesu leo
anatuambia, “Ufalme wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; wala hawatasema, Tazama, upo huku, au,
kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo ndani yenu,” Lk 17:20b-21. Hii ni
sehemu ya kwanza kuhusu ufalme wa Mungu, yaani ni kufanya juu chini kuutambua
na kuuishi kila siku. Sehemu ya pili kuhusu
ufalme wa Mungu ni yale Kristo aliyojitolea kwa ajili yako, yaani mateso na
kifo cha msalaba. Hapa ndipo tulipohesabiwa haki na Mungu kwa kumtoa mwanaye
Mpendwa afe kwa ajili ya dhambi zetu nasi tuwe huru na warithi wa ufalme wake.
Je, unayo sadaka ya kutoa?
Wapendwa
wana wa Mungu, kama wewe ni mfuasi kweli wa Kristo elewa jambo hili: ‘hakuna
utukufu pasipo msalaba, na hakuna pasaka pasipo ijumaa kuu.’ Kristo alijitoa
kwa ajili yetu sisi na kukubali kuiendea njia ile ya mateso kwa ajili ya kweli
na haki. Naye Yesu anatuambia hayo yote yatatokea, “Lakini
kwanza, hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki,” Lk 17:25.
Nasi kama wafuasi wake Kristo tutaifuata njia itupelekayo kwenye utukufu na
ufufuko tunaposimama katika kweli na haki na hapo tutaonja mauti yake.
Pale
tunapoonja mateso yake pasipo shuruti ila kwa hiari yetu ndipo tutoapo sadaka
upendo kwa kile tukidhamiriacho katika kweli na haki. Hali hii ya kujitoa bila
kujibakiza kwa wengine na katika maana halisi ya upendo ndiko kunakotuelekeza
katika upendo sadaka. Ndgu yangu, kuufahamu ukweli huu wahitaji hekima ya Mungu
kuyachambua yote kwa busara, na kutenda katika kweli na haki. “Maana Mungu humpenda yeye tu
akaaye na Hekima,” Hek 7:28.
Ndugu yangu tunaye safiri sote pamoja katika tafakari
hii, tunahitaji sana hekima ya Mungu ili tuyaone mahangiko yetu na mateso yetu
kama sehemu muhimu ya wokovu wetu ambao tayari tunao ndani mwetu. “Hekima
huenea kwa nguvu nyingi toka pembe hii hata pembe hii ya dunia, na
kuyaratibisha mambo yote kwa jinsi ya ufaa,” Hek 8: Tuikubali hekima ili hekima
hiyo itufunulie siri za Mungu.
Ni kwa ajili ya upendo
sadaka Mtume Paulo haoni shaka kumtoa Onesimo kwa Filemoni kwa ajili ya vifungo
vya Injili. “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika
vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye mimi nalitaka akae kwangu,
apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili,” Flm 10, 13. Naye
anamwambia Filemoni, “kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama
nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9.
Kadiri ya mapokeo, Paulo anaandika Waraka kwa Filemoni
akiwa Rumi kunako mwaka 61-63 Baada ya Kristo (BK). Mtume
Paulo anampasha habari Filemoni kwamba mtumwa wake Onesimo aliyemtoroka
atarudi. “Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu
kama mimi mwenyewe,” Flm 17.
Waraka huu unafunua
moyo wa Paulo na mafundisho yake juu ya utumwa, Rum 6:15. Mtume Paulo hakatazi
utumwa kama ulivyokuwa zamani, bali anakazia sana kwamba Mkristo lazima amjali
mtumwa/mfanyakazi wake kama ndugu katika Kristo, Kol 3.22-4.1. “Lakini
sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako
usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari,” Flm 14. Ndani na katika Kristo Yesu
sisi sote ni ndugu licha ya historia zetu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ufalme wa Mungu
hauji kwa kuuchunguza; wala
hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo
ndani yenu,” Lk 17:20b-21
Tusali:-Ee Yesu Mwema,
tujalie neema na upendo wako ili tuchukuliane na kutaabikiana katika undugu wa
kweli. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario