Somo
I: Mal 4:1-2a
Zab/Kit: 98:5-6, 7, 8-9
Somo II: 2The 3:7-12
Injili:
Lk 21:5-19
Nukuu:
“Kwa maana, angalieni,
siku ile inakuja, inawaka kama tanuru; na watu wote wenye kiburi, nao wote
watendao uovu, watakuwa makapi; na siku ile inayokuja itawateketeza, asema
Bwana wa majeshi; hata haitawaachia shina wala tawi,” Mal 4:1
“Lakini kwenu ninyi
mnaolicha jina langu, jua la haki litawazukia, lenye kuponya katika mbawa
zake,” Mal 4:2a
“Haya
mnayoyatazama, siku zitakuja ambapo halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo
halitabomoshwa,” Lk 21:6
“Akasema,
Angalieni, msije mkadanganyika, kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu,
wakisema, Mimi ndiye; tena, Majira yamekaribia. Basi msiwafuate hao,” Lk 21:8
“Nanyi
mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao
watawafisha baadhi yenu. Nanyi
mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu,” Lk 21:16-17
“Walakini
hautapotea hata unywele mmoja wa vichwa vyenu,” Lk 21:18
“wala
hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na
mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote,” 2The 3:8
“Maana twasikia kwamba
wako watu kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini
wanajishughulisha na mambo ya wengine,” 2The 3:11
TAFAKARI:
“Fahari na mamlaka za kibinadamu zitapita,
utawala wa Mungu utadumu hadi mwisho wa nyakati. Subirá yako itaiponya nafsi yako.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 33 ya mwaka “C” wa Kanisa. Masomo yetu
yote matatu yanatutafakarisha mwisho wa nyakati; yaani, yatakayo jiri, mapaswa yake, na nini cha
kufanya leo na sasa. Njia iliyo salama kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu ni
KUJISALIMISHA. Je, wenye hofu ya Mungu wana
nafasi gani kwa kujisalimisha kwao?
Hakika
Mungu hataacha kamwe kuwanyeshea mvua ya neema na baraka wenye hofu Naye. Wenye
hofu ya Mungu kwa kuishi kwao kuliko kwa kweli na haki, watasitawi katika haki
na kweli ya Mungu. Mungu humwelekea mwenye hofu naye kwa sababu ndani yake kuna
unyofu wa moyo. Huku ndiko kusitawi
mbele za Mungu kuliko haki. Hivyo, “mwenye haki atasitawi kama mtende, atakua
kama mwerezi wa Lebanoni,” Zab 92:12. Mungu hawezi kukaa kimya kwa wonyofu wa
moyo.
Hakuna
alichaye jina la Mungu, naye Mungu akaziba masikio kwa kilio chake. “Lakini kwenu ninyi mnaolicha jina langu, jua la
haki litawazukia, lenye kuponya katika mbawa zake,” Mal 4:2. Yatupasa kudumu
katika sala na maombi yetu tukiwa na matumaini kwamba tumekwisha pata kile
tuombacho. Na kinyume chake ni dhahiri, yaani, “siku ile
inakuja, inawaka kama tanuru; na watu wote wenye kiburi, nao wote watendao
uovu, watakuwa makapi; na siku ile inayokuja itawateketeza, asema Bwana wa
majeshi; hata haitawaachia shina wala tawi,” Mal 4:1. Kwa maana nyingine, wewe
na mimi tusiotaka kujisalimisha kwa Mungu katika kweli na haki, tujiandae
kuuvuna upepo, majanga yasiyo koma.
Wapendwa
wana wa Mungu, licha ya kweli kwamba maisha yetu sisi wanadamu katika ulimwengu
huu ni ya muda mfupi, maisha hayo kama yalivyo ni fumbo. Mzaburi anasema, “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka
themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea
mara,” Zab 90:10. Nafikiri leo Mzaburi huyu angekuwa anaandika haya angesema
vingine, miaka 40, na mwenye nguvu miaka 50. Umri wa kuishi hasa nchi za
ulimwengu wa tatu ikiwemo na nchi yetu-Tanzania umeshuka sana.
Hata
hivyo maisha ni fumbo kwa sababu kifo kwa
kila mmoja wetu kimefichwa licha ya kwamba ipo siku na kwa wakati wake kila
mmoja atafikia kikomo chake hapa duniani. Ndiyo kusema kwamba, “Fahari na
mamlaka za kibinadamu zitapita, utawala wa Mungu utadumu hadi mwisho wa
nyakati.” Hivyo ni vyema kila mmoja wetu akajishughulisha na mambo yale
yatakayojenga uhusiano mzuri na Muumba wake, jirani yake, na mazingira yake.
Uzuri wa ulimwengu huu na fahari yake vyote vitapita na kusahaulika.
Licha
ya kwamba maisha ya mwanadamu hapa duniani kuwa na kikomo chake, mwanadamu huyu
hawezi sahaulika na Muumba wake kwa sababu kaumbwa kwa sura na mfano wa Muumba
wake, Mwa 1:26. Mungu hawezi kujisahau mwenyewe. Ni kwa maana hiyo na sababu
hii, ipo siku kila mmoja ataitajika kutoa hesabu yake mbele za Mungu. Kwa chapa
hii ya Mungu ndani yako, kamwe uwezi sahaulika. Jiandae kwa kutoa hesabu kwa
yale uliyo kasimiwa bure, ikiwa ni pamoja na vipaji na karama ulizo nazo.
Ndugu
yangu, wakati wa Yesu na hata kabla yake, wapo walio vutwa sana na ulimwengu
huu na fahari yake kama ilivyo leo. Wapo waliolitazama Hekalu la Yerusalemu na
kupambwa kwake wakaishia hapo tu wasione zaidi ya Hekalu hilo. Yesu anatutaka
tutazame zaidi ya kile tunachokiona, yaani, tuzame zaidi ya fumbo lenyewe
katika ufahamu na umaana wake. Naye Yesu aliwaambia watu wa nyakati zake, na
sisi pia kwamba, “Haya
mnayoyatazama, siku zitakuja ambapo halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo
halitabomoshwa,” Lk 21:6. Tunachotakiwa kukitazama ni uwepo wa ufalme wa kweli
wa Mungu na siyo fahari na mamlaka za kibinadamu tu. Nabii Danieli anatoa tafsiri kwa
mfalme kuhusu kubomoka kwa sanamu ile iliyojengwa kwa mikono ya wanadamu licha
ya uzuri iliyokuwa nayo.
Hii ni kutofautisha
falme na mamlaka za wanadamu na ufalme ule wa kweli wa Mungu, ufalme ambao
wadumu milele na milele. “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni
atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine
hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na
kuziharibu, nao utasimama milele na milele,” Dan 2:44. Kile kibebacho ufahari
wa kibinadamu na kisichotoka kwa Mungu hakina umilele.
Kutokana
na ukweli huo nilio usema, kuna hatari ya watu kuja na tafsiri zao kuhusu
mwisho wa nyakati kwa lengo hasa la kuwaogopesha watu kwa manufaa yao binafsi.
Yesu Kristo anatoa angalizo na kusema, “Angalieni, msije
mkadanganyika, kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ndiye;
tena, Majira yamekaribia. Basi msiwafuate hao,” Lk 21:8. Hawa ndio wale
wajulikanao kama manabii wa uongo kadiri ya Maandiko Matakatifu. “Kwa maana watatokea
makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu;
wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule,” Mt 24:24. Je, leo si
jambo la kawaida mtu kujiita nabii, askofu, mtume, n.k?
Mambo
haya, mfano uaskofu, ukasisi, mchungaji, mtumishi, nk, hakuna anayejitwalia,
bali hutwaliwa na Mungu peke yake, ikiwa ni hitaji la Kanisa mahalia kama Mwili
wa Kristo inapoonekana inafaa na mhusika anastahili kadiri ya mamlaka iliyopewa
Kanisa (Mwili wa Kristo) na Kristo mwenyewe (Kichwa cha Kanisa). “Maana kila
kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika
mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi,” Ebr
5:1. Hata Kristo hakujitwalia mwenyewe kuwa kuhani Mkuu. “Vivyo hivyo Kristo
naye hakujitukuza nafsi yake kufanywa kuhani mkuu, lakini yeye aliyemwambia,
Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa,” Ebr 5:5. Tujihadhari sana na manabii hawa
wa uongo. Kila kona wapo na wanajiinua kila kukichwa!
Mwisho
wa nyakati hauji upesi kama tusemavyo au kufikirivyo licha ya mwamba kabla ya
mwisho huo kutatokea matokeo ya kutisha. Yesu leo anatuambia ukweli wa jambo
hili, “Nanyi mtakaposikia habari za vita na fitina, msitishwe; maana, hayo
hayana budi kutukia kwanza, lakini ule mwisho hauji upesi,” Lk 21:9. Tunapoona
mtu anapanga hadi tarehe ya matukio haya ya mwisho wa nyakati yeye kaupata wapi
ukweli huo zaidi ya hiki anachotuambia Kristo? Ndugu yangu tunaye safiri sote
katika tafakari hii usisahau maneno haya ya wahenga wetu: “Wajinga ndio
waliwao.” Kristo kesho uweka sawa ukweli huu alipowajibu wanafunzi wake, Mdo
1:6, kabla ya kupaa mbinguni, kwamba, “si kazi yenu kujua nyakati wala majira,
Baba aliyeyaweka katika mamlaka yake mwenyewe,” Mdo 1:7. Kilichopo mbele yetu
leo na sasa ni kuihubiri habari njema hadi mwisho huo wa nyakati, Mdo 1:8. Na
katika kweli hii, tusichoke wala kukata tamaa katika kutenda mema, 2The 3:13
Leo
Yesu anawaambia wafuasi wake nasi pia maneno haya mazito, ‘subirá yako
itaiponya nafsi yako.’ Mwenye subira ufikiri vyema tena kwa undani na upana
wake. Mwenye subira huyatazama yote katika jana yake, leo yake, kesho yake, na
umilele wake. Kuwa mfuasi hai wa Kristo kuna mapaswa yake. Yesu anatuambia leo
mapaswa ya kuwa mfuasi wake hai. Mapaswa yake ni kusalitiwa. “Nanyi
mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao
watawafisha baadhi yenu. Nanyi
mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu,” Lk 21:16-17.
Badala yake, na katika hali hii ya
kusalitiwa, Yesu anatuambia tuwe na furaha. “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila
neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini,
na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo
walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:11-12. Yatupasa kufurahi kwa
sababu katika mateso na ugumu huu wa kusimama katika kweli na haki, “hautapotea
hata unywele mmoja wa vichwa vyenu,” Lk 21:18. Hakuna aliye wa bahati mbaya
katika ulimwengu huu “kwa maana kama tunaishi, twaishi kwa Bwana, au kama
tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,”
Rum 14:8
Mpendwa katika Kristo,
elewa kwa hakika kabisa kama kweli wewe ni mfuasi hai wa Kristo, ipo siku
ufuasi wako utapimwa. Na hilo kama litatokea jiachie-jisalimishe kwake Kristo
Yesu. “Basi, kusudieni mioyoni mwenu, kutofikiri-fikiri kwanza mtakavyojibu; kwa sababu mimi nitawapa kinywa na
hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga,” Lk
21:14-15. Kumbe kwa kujiachia-kujisalimisha kwake Kristo ni kwa namna hiyo hiyo
tayari tunaye mtetezi.
Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli pasipo shaka kwamba, ‘palipo na
utaratibu kuna akili.’ Ipo mifano mingi
yenye kuthibitisha ukweli huu wa uhusiano kati ya utaratibu na akili. Mfano
halisi ni uumbaji wa ulimwengu huu tunaoishi. Hata kama wengi wetu kwa sababu
zao hawaamini uwepo wa Mungu aliye hai, hatuwezi kupinga kwamba mpangilio mzima
wa ulimwengu huu tunaoishi haukuhusisha akili. Hivyo palipo na utaratibu kuna
akili. Ikiwa wewe na mimi tupo kwenye mpango huo na utaratibu huo, maisha yetu
yanatutaka tuenende katika utaratibu. Kila mmoja wetu yupo hapa ulimwenguni kwa
lengo. Huu ndio wito wa Mtume Paulo kwetu leo, kwamba tuenende kwa utaratibu. “Ndugu, twawaagiza
katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye
bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu,” 2The 3:6.
Pasipo utaratibu ni fujo. Na hukumu ya mwisho yategemea ishi yako na yangu leo
katika utaratibu.
Wanapoishi watu zaidi
ya mmoja, lazima kuwe na utaratibu, na utaratibu huu kuheshimiwa baina ya hao
walioweka huo utaratibu, kwa mafaa yao, na sifa kwa Muumba wao. Ni jambo la
kusikitisha sana tunapoona kwa wazi kabisa waliopewa dhamana ya kuulinda na
kuutetea utaratibu, Katiba, ndiyo vinara wa kuivunja Katibu hiyo kwa wao
kujihalalishia jeuri na ubatili wao. Huku ni kuusaliti umma wa watu, ambayo ni
sauti ya Mungu, na mwisho kuwa kikwazo kikubwa kwa UMMA na MUNGU MWENYEWE.
Mtume Paulo anashinda kishawishi hiki na kusema pasipo shaka kwamba, “Mwajua wenyewe jinsi
iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu,” 2The 3:7.
Mtume Paulo hakuishia
hapo tu, yaani, kutokuvunja utaratibu, bali alikuwa mstari wa mbele yeye na
wenzake katika kutimiza wajibu wao. Na hivi ndivyo anavyotoa ushuhuda wa maisha
yake na wenzake ya kila siku, na kusema, “wala
hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na
mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote,” 2The 3:8. Huu ni mfano mzuri sana wa kuigwa na
kupongezwa kwa kiongozi yeyote yule mwenye dhamana, na aliyepewa dhamana hiyo
na Mungu kupitia sauti ya watu. Maisha katika ujumla wake ni DHAMANA. Je, ugonjwa
wetu kama Taifa ni upi?
Wapendwa wana wa Mungu, saratani
angamizi ya Taifa hili letu la Tanzania ni UNAFIKI na UBABAISHAJI katika
kufikiri, kuamua, na kutenda. Tusitegemee maajabu hata kama tukimpata Rais
Malaika, kama hatutabadili mfumo huu wa maisha-Unafiki na Ubabaishaji. Tatizo
ni kwamba palipo na unafiki na ubabaishaji ni vigumu kutofautisha aliye soma na
aliye elimika. Palipo na unafiki na ubabaishaji, uhalisia wa jambo hauwi kama
ulivyo, bali kama tulivyo. Katika jambo hili, Mtume Paulo anatupa angalizo na
kusema, “twasikia kwamba wako watu kwenu waendao
bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini wanajishughulisha na mambo
ya wengine,” 2The 3:11. Huu ni utumiaji mbaya wa rasilimali muda, na malighafi
tuliyo kirimiwa bure na Mungu.
Badala yake, tunatumia
muda mwingi kutetea na kuufunika uovu. Wahenga katika hili wanasema, “mficha
uchi hazai, na mficha kidonda ndugu harufu umuumbua.” Kukiri udhaifu siyo
kushindwa bali ni mwisho wa mwanzo mpya wa kule utakako kufika. Ukweli wa jambo
uwezwa kufunikwa kwa wakati tu, bali kadiri ya muda uendavyo kweli hiyo
ujifunua yenyewe. Kweli ni asili ya Mungu, nayo
ni milele katika maana yake kama alivyo Mungu. Kwa misuli yetu na
ubinadamu wetu hatutoweza kamwe kuifunika kweli katika umilele wake. Badala
yake, na kama tutafanya hivyo, basi tujiandae kuanikwa na kuumbuliwa wakati
utakapo fika. Mtume Paulo analo jambo kwetu leo kama asemavyo, “Basi twawaagiza
hao, na kuwaonya katika Bwana Yesu Kristo, watende kazi kwa utulivu na kula
chakula chao wenyewe,” 2The 3:12. Kuwa kile ulicho, na fanya yote katika
ukamilifu wake kadiri ya; wito wako, uwezo wako, hali yako, na nafasi yako
katika jamii.
Ndugu yangu, bila shaka
wamfahamu vizuri Nyani. Pamoja na weledi wake nyani katika harakati zake za kila
siku, na kukweya kila aina ya miti kwa kujifurahisha na hata kujihifadhi, kamwe
hafanyi kosa katika jambo hili; “usiku awapo juu ya mti ujisaidia kwenye
kiganja chake na kupaka kinyesi chake kwenye mti.”
Nyani hufanya hivi siyo
kwa kupenda, bali kwa usalama wake mwenyewe. Mmoja ya wanyama hatarishi kwa
nyani ni chui. Hivyo nyani kukiacha kinyesi chake kudondoka chini ni kumpa
taarifa chui kwamba juu ya mti tena usiku kuna kitoweo, yaani, nyani. Na
nyakati za usiku nyani hana werevu wa kubembea kwenye matawi ya mti kwa jeuri
na majivuno. Kinyume chake, usiku kwa chui ndiyo muda muafaka kwa mawindo.
Ndugu yangu, ujumbe wa
simulizi hili ni kwamba, fanya yote
kadiri ya uwezo na maarifa yako, ila usisahau ukomo wako. Mungu kwa kukuumba
wewe na mimi kwa sura na mfano wake, na ndiyo tulivyo wanadamu, alijua na
anajua wazi kabisa kwamba kwa kuishi kama wanadamu ndipo ulipo ushindi wetu,
yaani, utakatifu wetu.
Kumbuka: Malaika walipo
muasi Mungu walibadilika kuwa mashetani. Nasi tunapoukataa ubinadamu wetu
katika ukomo wake, na kutaka kuwa sawa na Mungu, tunabadilika na kuwa wabaya
kuliko masheni kwa sababu tamanio hili hata malaika walilita na mwisho wakawa
mashetani.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana twasikia kwamba wako watu
kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini
wanajishughulisha na mambo ya wengine,” 2The 3:11
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie neema ya kuishi katika utaratibu ili uonekane kwa kila mmoja
wetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario