jueves, 10 de noviembre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 32 YA MWAKA-C


JUMAMOSI WIKI YA 32 YA MWAKA-C

Somo: 3Yoh 5-8

Zab/kit: 112:1-2, 3-4, 5-6

Injili: Lk 18:1-8

Nukuu:

 “Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa,” 3Yoh 7

“Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli,” 3Yoh 8

 “Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu,” Lk 18:3

“Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima,” Lk 18:4-5

 “Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” Lk 18:8

TAFAKARI: “Kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa. Hivyo yatupasa kumwomba Mungu sikuzote, wala tusikate tamaa.

Wapendwa wana wa Mungu, Kadhi kama tulivyosoma na kusikia Injili ya leo anampa mama mjane haki yake si kwa kupenda bali kwa kulazimika kutokana na usumbufu. Naye anasema, “Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima,” Lk 18:4b-5. Hivyo unaweza kutoa bila kupenda.

Tunapokuwa na mahusiano mazuri na Mungu kamwe hawezi kutuacha katika mahangaiko yetu. Bwana wetu Yesu Kristo anatupatia uhakikisho huyo. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao?” Lk 18:7. Uvumilivu wa Mungu kwetu ni Imani ile tuliyo nayo juu yake. Kwa imani dhabiti tunauhakika kwa kuyapata yale tumwombayo Mungu wetu aliye huruma na upendo.

Yesu anatupa pia uhakika wa jambo hili, ila imani ni moja ya kielelezo kikuu kwa kile tuombacho. Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” Lk 18:8. Je, unayoimani kwa hayo uyaombayo?

 Kwa upande mwingine huwezi kupenda bila kutoa. Yesu anasema, “Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:11. Yesu kwa kutupenda yupo tayari kutoa uhai wake kwa anjili yetu. Upendo ndiyo amri yenyewe. Kristo ndiye kielelezo chetu juu ya upendo na kupenda. Hili ndilo lile neno lililofanyika mwili nalo likakaa kwetu, Yoh 1:14. Kwa kupitia Kristo tunalo hakikisho la wokovu, na kwa jina lake kila tuombalo kwa imani tutapewa kwa wakati wake. Ni kwa matiki hiyo kwamba, “hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Kristo ndiye JIBU.

Hivyo ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, wewe kama ni Mbatizwa na unaishi ahadi zako za ubatizo kwa uaminifu, una wajibu mkubwa sana wa kufanya katika Kanisa la Kristo. Na kubwa kuliko yote ni kufanana na Kristo katika kufikiri, kuamua, na kutenda. Haya yote matatu yalidhihirisha upendo kamili wa Kristo ambaye ndiye maana halisi ya ufunuo na upendo wa Mungu kwetu. Kama Wakristo na wenye hofu ya Mungu, sote tu vyombo vya amani, upendo, haki, na huruma ya Mungu pale tulipo. Na lengo ni kuwasafirisha wote-wana wa Mungu, kwake Yeye aliye waumba kwa sura na mfano wake.

Hivyo “Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na hao wageni nao, waliokushuhudia upendo wako mbele ya Kanisa; utafanya vizuri ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu,” 3Yoh 5-6. Kupotezana njiani tena kwa agenda binafsi ni chukizo kubwa sana kwa Mungu ilhali twajiita Wakristo, Walei, Watawa, na Makreli. “Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa,” 3Yoh 7. Mimi na wewe ni watimiza wajibu wetu kwa uaminifu, ila awaitaye kwake ni Yule aliye waumba kwa sura na mfano wake. Mimi na wewe tusaidiane kuifikia taji na mede ile tuliyoandaliwa. Hali na mazingira hayo ya kusaidiana yanahitaji roho ile ya kutaabikiana. Twahiji fadhila ya unyenyekevu na burasa ili kufikia lengo lile la kufanana kama Kristo. Tusichoke kuomba neema ya Mungu, na fadhila hizo.

Mkristo na mwenye hofu ya Mungu siye mfunga mlango na mzuiya neema na baraka za Mungu kwa wateule wake. Kinyume chake Mkristo ni mtumika wa Mungu katika kweli na haki, na mwisho wa siku ni mtumishi asiye na faida, na aliye utimiza wajibu wake katika upendo, kweli, na haki ya Mungu, Lk 17:10. “Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli,” 3Yoh 8. Na palipo na upendo Mungu hujidhihirisha katika maisha ya watu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” Lk 18:8

Tusali:-Ee Yesu, tujalie ustahimilivu katika sala. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario