IJUMAA WIKI YA 32 YA MWAKA-C
Somo:
2Yoh 4-9
Zab/kit: 119:1, 2, 10, 11, 17, 18
Injili: Lk 17:26-37
Nukuu:
“Na huu ndio upendo:
tuenende kwa kuzifuata amri zake. Hii ndiyo ile amri, kama mlivyosikia tangu
mwanzo kwamba mwenende katika hiyo,” 2Yoh 6
“Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze
mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu,” 2Yoh 8
“Kila apitaye cheo,
wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika
mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia,” 2Yoh 9
“Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo
ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee
nyuma,” Lk 17:31
“Mtu
ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza
ataiponya,” Lk 17:33
Akawaambia, Ulipo mzoga, ndipo
watakapokutanika tai,” Lk 17:37b
TAFAKARI:
“Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai.”
Wapendwa wana wa Mungu,
kifo wakati mwingine uonekana
kipo mbali sana hasa pale tunapozama katika anasa na malimwengu. Wakati wa Nuhu
na hata Lutu habari za Mungu na uwepo wake hazikuonekana kama kitu cha pekee
kwa wengi hasa wale walioishi katika mfumo wa “ponda mali.” Ila hata kama
hatuna hisia na Mungu, Yeye hupo hai na anayaona yote tuyafanyayo. Siku ya
kuzungumza na kila mmoja wetu kwa wakati wake inakuja. Hivyo, “Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika
siku zake Mwana wa Adamu,” Lk 17:26. Itakapofika siku hiyo tutapigwa na
mshangao kwa vile hatutakuwa tumejiandaa vyakutosha kwa sababu tu ya kupuuzia
kama walivyompuuzia Nuhu kuitengeneza Safina ilhali hapakuwa na dalili yoyote
ya mvua, mto, ziwa wala baharí, ila Mungu aliinyeeshea duania kutoka chini.
Mshango
mwingine ni kwamba tukio hili la kifo litamkuta kila mtu pale alipo kwa
mshangao. Ni mara ngapi tunaondokewa na wapendwa wetu ilhali hatukuwa kumeagana
vizuri au kuongea nao kwa urefu? Mara nyingi tunabakiwa na ‘ninge…’ zisizo na
idadi. “Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya
nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma,” Lk
17:31. Hapa ni pale tunaposema, “lo! Nilikuwa naye leo asubuhi na sana hatunaye
tena!” Hata tukio kama hilo halisemi chochote kuhusu maandalizi yako?
Yesu
anatupatia jibu la mkwamo huu, na kutuweka mkono salama tusijepigwa na
mshangao. Naye anasema, “Mtu ye
yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza
ataiponya,” Lk 17:33. Kuiponya nafsi katika kuingamiza ni kuiridhia nafsi kwa
yale inayoyataka. Ni pale nafsi inapoegemea katika mwili na kufanya matendo ya
mwili. “Basi
matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui,
ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda,
ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Huku ni kuiponya nafsi katika
kuiangamiza.
Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, kuiangamiza nafsi katika kuiponya ni pale nafsi yako
inapoegemea roho, na kutenda matendo ya roho yenye tunda la roho. “Tunda la
Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria,” Gal 5:22-23. Huku ni kuiangamiza nafsi yako katika kuiponya. Je, mzoga
wako utakuwa wapi?
Baada ya mafundisho
haya mazito ya Injili ya leo, watu walitaka kujua hayo yatatendeka wapi? Yesu
anatujibu hivi, “Ulipo mzoga, ndipo
watakapokutanika tai,” Lk 17:37b. Kwa maana nyingine mwisho wako utategemea
ishi yako. Hivyo kama nafsi yako katika ishi yako itaegemea mwili, ndivyo hivyo
mwisho wako utakuwa katika matendo ya mwili. Tuna ambiwa watu watendao mambo ya
jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Vile vile kama nafsi yako itaegemea
roho yako, basi mwisho wako utakuwa tunda la roho. Tunaambiwa juu ya mambo kama
hayo hakuna sheria, kwani kwa kuishi hivyo ndiyo sheria yenyewe aipendayo
Mungu. Ni maisha ya kweli na haki.
Palipo
na upendo wa kweli, tokeo lake ni tunda la roho. Na twaudhihirisha upendo kwa
kuzishika amri za Mungu, “Na huu ndio upendo: tuenende kwa
kuzifuata amri zake. Hii ndiyo ile amri, kama mlivyosikia tangu mwanzo kwamba
mwenende katika hiyo,” 2Yoh 6. Uwepo wako na wangi leo ni tokea la upendo wangu
aliyeona na kumpendeza kutuumba kwa sura na mfano wake. Nasi ni furaha na
utukufu wake Mungu. Mungu kalifanya tendo hili la upendo siyo kwa sababu ya
hitaji, bali kwa uhuru wake na kupenda kwake.
Ni kwa upendo wake huu
Mungu, “Hata ulipowadia utimilifu wa
wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya
sheria, 5 kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate
kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Hivyo
ndugu yangu, baada ya Mungu kukuumba kwa sura na mfano wake hakukuacha
ujiendee mwenyewe kama saa ya mshale. Lengo na furaha yake Mungu ni mimi na
wewe tuishi milele. Na hili ndilo kusudi la NENO wa Mungu, yaani, Yesu Kristo,
kufanyika mwili-kumwilishwa, na kukaa kwetu. Ndugu yangu, kuwa macho kwa
sababu, pamoja na ukweli huu, wapo “wadanganyifu wengi wametokea duniani,
wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu
na mpinga Kristo,” 2Yoh 7. Hata kati yetu na hapo ulipo wampinga Kristo wapo.
Kuwa macho!
Pamoja na mpango huu
mzuri wa Mungu kwa kila mmoja wetu, ‘Mungu huyu aliyekuumba wewe pasipo wewe
hatoweza kukusaidia/kukuokoa wewe pasipo wewe,’ kama asemavyo Mtakatifu
Augustino wa Hippo. Hivyo Mtume Yohana anatuambi sote kwamba, “Jiangalieni
nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu,” 2Yoh 8.
Lengo la maisha yetu hapa duniani mwisho wa siku tuwe wakamilifu kama Baba yetu
wa Mbingu alivyo makamilifu, Mt 4:48. Bila ukamilifu/Utakatifu hatutaweza
kumwona wala kukutana na Mungu aliye Mkamilifu na Mtakatifu.
Hivyo ndugu yangu, uwapo hapa duniani licha ya
mbwembwe zako zote, majivuno yangu, kiburi, na jeuri ya hela na madaraka uliyo
nayo, ukomo wake ni mfupi sana. Ukweli ni kwamba, “Kila apitaye cheo, wala asidumu
katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho
hayo, huyo ana Baba na Mwana pia,” 2Yoh 9. Je, bila Kristo nawe wajiita
Mkristo, utatoboa, yaani, kuufikia ufalme huo wa Mbinguni?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mtu
ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza
ataiponya,” Lk 17:33
Tusali:-Ee Yesu na
Mkombozi wetu, tukumbushe mara zote ufupi wa maisha yetu hapa duniani. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario