JUMANNE WIKI YA 33 YA MWAKA-C
Somo:
Ufu 3:1-6, 14-22
Zab/kit: 15:2-3ab, 3bc-4ab, 5
Injili: Lk 19:1-10
Nukuu:
“Na kwa malaika wa
kanisa lililoko Sardi andika; Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa
hai, nawe umekufa,” Ufu 3:1ac
“Basi kumbuka jinsi
ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha,
nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako,” Ufu 3:3
“Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia
andika; 15 Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri
kama ungekuwa baridi au moto,” Ufu 3:14a,15
“Basi, kwa sababu una
uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu,”
Ufu 3:16
“Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia,
Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5
“Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa
sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9
“Kwa
kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea,” Lk 19:10
TAFAKARI:
Tazama, nasimama mlangoni, nabisha hodi.”
Wapendwa wana wa Mungu,
katika Injili ya leo tunaona upendo mkubwa na
wa ajabu wa Mungu katika kutano lile
kati ya Yesu na Zakayo. Zakayo hamwoneyi Yesu aibu pamoja na watu kuyajua
madhaifu yake ikiwa ni pamoja na ufupi aliokuwa nao. Bado anaona salama yake
ipo kwa Kristo tu na siyo mitazama ya wale walikuwa wanamzunguka. Ili amwone
Yesu, Zakayo alipanda juu ya mkuyu. “Na
Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi,
kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5.
Ni
wazi kwamba huwezi kuwa mrefu zaidi ya wewe mwenyewe. Na kwa kuwa huu ni ukweli
wa lazima, kumbe kuvijua na kuviona vile vilivyo nje ya uwezo na kimo chako
yakupasa kufanya juhudi ili kuujua ukweli ule ulio nje vya vimo vyako. Hivyo
Zakayo anatufundisha kwamba hata kama ulimwengu ushatuhukumu, na hali na
mazingira yetu yanatukwamisha, bado tunaweza kukutana na upendo na huruma ya
Mungu tufanyapo bidii. Mtakatifu Agustino wa Hippo katika kweli hii anasema,
“aliyekuumba wewe pasipo wewe, hataweza kukusaidia wewe pasipo wewe.” Hizo
Zakayo kwa juhudi zake, na mpango mahususi wa Mungu, anafanikisha ndoto yake,
na Yesu anakuwa mgeni wake.
Tendo
hili la Yesu linawashangaza wengi na wengine wananung’unika. “Hata
watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye
dhambi,” Lk 19:7. Hapa tunakumbushwa pia moja ya kazi ya Yesu Kristo katika
safari na historia hii ya wokovu kama asemavyo yeye mwenyewe kwamba, “sikuja
kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:32.
Kwa
utayari wa Yesu kwenda nyumbani kwa Zakayo, kwa furaha aliyokuwa nayo Zakayo
hakuweza kuificha. Hivyo Zakayo anayaweka yote wazi mbele ya Yesu. “Zakayo
akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini,
na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne,” Lk 19:8. Hii
ni toba ya kweli na maungamo ya wazi mbele ya Yesu aliye sasa njia, kweli na
uzima.
Maungamo
haya ya kweli toka moyoni mwa Zakayo yanaifunua furaha na upendo wa Mungu
kupitia mwanaye Yesu Kristo na kuonyesha kile hasa Yesu alichokijia
ulimwenguni. “Yesu akamwambia, Leo wokovu
umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9.
Wokovu ni kwa kila mmoja na hasa pale tunapouridhia wokovu huo kwa utashi wetu
wenyewe na kwa dhamiri iliyo hai na safi.
Mungu anatazama
utayari wako katika upya wa kuyaanza yote nawe na siyo historia ya maisha yako
mabaya yaliyopita. Tu wapya mbele ya Mungu siku na muda wowote. Ni wewe na mimi
tu kujisalimisha mbele ya uso wake wau pendo, huruma, na Mtakatifu. “Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile
kilichopotea,” Lk 19:10. Ndugu yangu, afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi
kwa unajisi.
Wakati
ndiyo sasa kusimama katika kweli na haki, na kuchukia uovu wa aina yoyote ile
kwenye maisha yako na jamii inayotuzunguka. Hivyo kwako na kwangu ni mwito
tunaopatiwa leo kila mmoja kadiri ya nafasi na wito wake pale alipo. Kwa yeyote
aliyepewa dhamana na umma kwake vitahitajika vingi pia. Naye Yesu anasema, “Na
kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu
vingi, kwake huyo watataka na zaidi,” Lk 12:48b
Somo
letu la kwanza limebeba ujumbe huo huo wa kubadilika na kuanza maisha mapya na
Mungu. Ni wazi kuwa Makanisa yale saba anayoyazungumzia Yohana yalighubikwa na
dhuluma na taabu nyingi kwa wampingao Kristo. Hata hivyo, kwa upande wa
wanakanisa, nao iliwapasa kuenenda katika uchaji na hofu ya Mungu. Na salama
yao ipo katika toba ya kweli na majuto. Na huu ndio ujumbe wa Yohana kwa Kanisa
la Sardi, “Na kwa malaika
wa kanisa lililoko Sardi andika; Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa
hai, nawe umekufa,” Ufu 3:1ac. Ni kweli kabisa kama waonekanavyo kuwa hai kumbe
ni wafu, nasi tunapo dondoka katika hali ya dhambi twaikumbatia mauti na mwisho
wa siku tunakosa uzima ndani yetu.
Wito kwa kila mmoja
wetu ni kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi. Ni kuyashika kwa uaminifu
mafundisha ya Kristo Yesu na kuyaishi. “Basi
kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu.
Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja
kwako,” Ufu 3:3. Kwa vile hakuna ajuaye kwa uhakika siku yake ya mwisho, kumbe
ni vyema kuwa tayari kila siku katika hali ya neema. Na kuwa katika hali ya
neema ni kujitahidi kila siku kutokuwa katika hatia ya mwili, nafsi, na roho
yako. Sakramenti ya kitubia/upatanisho utusafisha na kuturejesha katika hali ya
neema.
Kwa kuwatia moyo,
Yohana anatambua vile vile wale wachache walioweza kuishi bila hatia katika
hali ya uchaji na kuenenda kadiri ya mapenzi ya Mungu kwa Kanisa hili la Sardi.
“Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu.
Nao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili,”
Ufu 3:4. Hawa ndio watakatifu wa Mungu. Hawa ndio mfano wa kuigwa. Utakatifu
wawezekana kwa kila mmoja wetu. Ni utayari wako tu wa kuiacha njia ile mbaya na
kumfuata Kristo kwa uaminifu.
Ndugu yangu, maisha ni
jaribu na kila siku iendayo kwa Mungu twapaswa kulishinda jaribu hilo. Majaribu
mengine kwa nguvu zetu hatuweza kushinda kwa wepesi. Katika hali na mazingira
hayo twahitaji nguvu na msaada wa Mungu. Na watakatifu ni wale waliokuwa na
uhusiano wa karibu na Mungu, na hawakuwa na mashaka na uweza wake Mungu. Hivyo,
“Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake
katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na
mbele ya malaika zake,” Ufu 3:5. Mungu awezaye yote, huifanya njia pasipo njia,
kwa sababu majaribu hayo hayawezi kupita uwezo wa Mungu, isipokuwa lililo
kawaida ya wanadamu, IKor 10:13.
Tatizo kubwa la
wanakanisa wa Laodika ni kwamba hawakuwa imara katika Imani, na mwisho wa siku
walikosa msimamo kabisa kwa kile walichokiamini. Yohana anawapa karipio na wasio
huu; “Na kwa malaika wa kanisa lililoko
Laodikia andika; Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa
heri kama ungekuwa baridi au moto,” Ufu 3:14a, 15. Kuwa vuguvugu katika imani
ni hatari sana. Heri kuwa baridi au moto katika imani.
Mungu atakutapika,
yaani, kutoshughulika nawe kwa sababu umekosa msimamo katika imani ya kweli. “Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu
baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu,” Ufu 3:16. Leo kati
yetu, tu vinara wa kuhama hama kutoka nyumba moja ya sala na kwenda nyingine.
Tunachotafuta usiku na mchana ni ishara na miujiza. Hivi sivyo vielelezo vya
ukomavu wa imani, bali huwasaidia wale tu walio na imani changa.
Usalama wa wanakanisa
hawa wa Laodika ni kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi zao. Na huu ndio
ushauri wa Yohana; “Nakupa shauri,
ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi
meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka
macho yako, upate kuona,” Ufu 3:18. Kuinunua dhahabu ni ule utayari wa kumrudia
Mungu ulio wa thamani, toba ya kweli na
majuto. Mungu aliye Upendo na Huruma, yu tayari kumsamehe yeyote mwenye kutubu
na kuiacha njia yake mbaya na kumfuata. Naye
anasema, “Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na
bidii, ukatubu,” Ufu 3:19.
Ndugu yangu, subira ya
Mungu kwako na kwangu ni kubwa sana. Mungu wetu ni mvumilivu sana na mwenye
kutungoja tumrudie kwa uhuru wetu. Mungu kamwe hatumii shuruti kutulazimisha
jambo. Mungu anathamini sana uhuru wako. Naye anasema, “Tazama, nasimama
mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia
kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami,” Ufu 3:20. Huu ni upendo
mkubwa sana kwetu na wa ajabu.
Upendo huu wa Mungu
ulio wa ajabu, kwetu ni jaribu kubwa sana katika matumizi sahihi ya uhuru
aliotupatia Mungu kwa upendo wake. Tunapomrudia Mungu yeye anatuhaidia jambo
hili; “Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi,
kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha
enzi,” Ufu 3:21. Ni furaha kubwa iliyoje kuketi pamoja na Mungu katika kiti
chake cha enzi! Kila mmoja wetu anayo nafasi hiyo. Ni utayari wako tu kuiacha
njia yako mbaya na kumfuata katika kweli, haki, na uaminifu.
Tusifu Yesu Kristo!
“Kwa
kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea,” Lk 19:10
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, nipo hapa usinipite Bwana. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario