miércoles, 31 de agosto de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 22 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 3:18-23
Zab/Kit: 24:1-2, 3-4ab, 5-6
Injili: Lk 5:1-11
Nukuu
Mtu asijidanganye mwenyewe; kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu katika dunia hii, na awe mpumbavu, ili apate kuwa mwenye hekima,” 1Kor 3:18 

Maana hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, Yeye ndiye awanasaye wenye hekima katika hila yao,” 1Kor 3:19 

 “Akaingia katika chombo kimoja, ndicho chake Simoni, akamtaka akipeleke mbali kidogo na pwani. Akaketi, akawafundisha makutano ali chomboni,” Lk 5:3 

Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4 

 “Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8 

 “Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b

Hata walipokwisha kuviegesha pwani vyombo vyao, wakaacha vyote wakamfuata,” Lk 5:11 

TAFAKARI: Nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu. Tweka mpaka kilindini.”

Wapendwa wana wa Mungu, kwa uzoefu aliokuwa nao Simoni kama mvuvi wa samaki, isingekuwa rahisi kuuchukua ushauri wa Yesu wa kurudi tena ndani ya maji na kuvua samaki. Elewa kwamba usiku kucha Simoni na wenzake walikesha wakivua bila kupata chochote. Usiku ndio muda muhafaka wa kuvua samaki. Leo kwa namna ya kushangaza Yesu anamwambia Simoni azitupe nyavu zake ndani ya maji mchana kweupe, na kwenda kinyume kabisa na utaratibu wa uvuvi. Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4. Simoni akitambua alichokifanya usiku kucha bila kupata chochote, akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5. Maneno haya ya Simoni “lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” yanaonyesha kujisalimisha kwa Simoni pasipo shaka mbele ya Yesu. Ni kwa njia ya neno hili: Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu,” Yoh 1:3-4. Je, bado unamashaka na Neno wa Mungu, yaani Yesu Kristo?

Maneno hayo ya Simoni yenye kuonyesha kujisalimisha kwake, ndiyo roho na uzima. Katika hili Yesu anasema, Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,” Yoh 6:63. Na neno lile Yesu alilomwambia Simoni “tweka mpaka kilindini,” ndiyo uzima na ponya yake Simoni. Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, tuzame kidogo ndani na tuone maana halisi ya kujisalimisha kama siri na ufunguo wa mfanikio yote katika maisha yako.

Kujisalimisha ni neno lisilotumiwa sana, halipendwi kama vile neno kunyenyekea. Lina maana ya kupoteza, na hakuna mtu yeyote anapenda kupoteza. Kujisalimisha kunaonyesha picha isiyopendeza ya kukubalika kushindwa katika vita, kupoteza katika michezo, au kukubali kushindwa na mpinzani mwenye nguvu zaidi. Neno hili linatumiwa mara nyingi katika hali isiyokubalika. Wahalifu waliotekwa hujisalimisha kwa mamlaka.

Katika mila ya leo ya ushindani tunafundishwa kutokuacha au kutokukubali tu. Hivyo hatusikii sana kuhusu kujisalimisha. Kama kushinda ndiyo kila kitu, basi kujisalimisha hakupo. Labda tuongelee kushinda, kufanikiwa, kuzidi nguvu, na kushinda vita kuliko kujitoa, kunyenyekea, kutii, na kujisalimisha. Lakini kujisalimisha ni kiini cha kuabudu. Ni mwitikio wa asili wa huruma na upendo wa ajabu wa Mungu. Tunajitoa nafsi zetu kwake, si kwa hofu au kwa kuwa ni wajibu. Lakini kwa upendo, “kwa sababu alitupenda kwanza.” I Yn 4:9-10, 19.

Kujisalimisha kwa Mungu si kujiuzulu na kukaa tu kusubiri, au kuamini kuwa yote yameandikwa binadamu hana hiari, au kuwa na udhuru na wivu. Siyo kukubali hali hiyo hiyo uliyo nayo. Inaweza kumaanisha kinyume cha haya; kujitoa sadaka maisha yako au kuteseka ili kubadilisha yanahitajika kubadilishwa. Mara nyingi Mungu huwaita watu waliojisalimisha kwake kupiga vita kwa jina lake. Kujisalimisha sio kwa uoga au mazulia. Mungu asingependa kupoteza akili alizokupa! Mungu hapendi watu wawe kama mitambo (robots) ili kumtumikia.

Kujisalimisha siyo kukomesha utu wako. Badala ya kukomesha utu wako, kujisalimisha huutia nguvu. C. S Lewis alisema, “kadiri tunavyomruhusu Mungu atutawale ndivyo tunavyozidi kuwa sisi wenyewe-kwa sababu yeye ndiye aliyetuumba. Alibuni namna mbalimbali za watu wote tofauti ambao mimi na wewe tulikusudiwa kuwa…. Ni pale ninapomgeukia Kristo, ninapojikabidhi nafsi yangu kwake, ndipo ninapokuwa na ule utu wangu halisi.” Naye Mtume Paulo anasema, nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu,” 1Kor 3:23

Kujisalimisha kunadhihirika vyema katika kutii. Unasema ‘ndivyo, Bwana’ kwa chochote anachokueleza. Kusema “hapana, Bwana” ni kutamka vinyume. Hatuwezi kumwita Yesu Bwana na wakati huo huo hatutaki kumtii. Baada ya usiku kucha bila kupata samaki, Simoni alionyesha kujisalimisha pale Yesu alipomwambia kujaribu tena” “Bwana tumefanya kazi kwa bidii usiku wote na hatujakamata samaki yeyote. Lakini kwa sababu umesema, nitatia nyavu majini.” Lk.5:5. Watu waliojisalimisha hutii neno la Mungu hata kama linaonekana kutokuwa na maana.

Hapa Simoni Petro anauvua uelewa wake, anaweka pembeni uzoefu katika jambo analolijua tangu udogo wake, na kuruhusu hekima ya Mungu ifanye kazi ndani yake. Kwa maneno mengine, Simoni anaiweka pembeni hekima na busara yake ya kibinadamu na kuruhusu neema na hekima ya Mungu ifanye kazi ndani yake. Maana hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, Yeye ndiye awanasaye wenye hekima katika hila yao,” 1Kor 3:19. Kuiacha hekima ya dunia na kuruhusu hekima ya Mungu ndani yako kutakuhitaji ujisalimishe.

Jambo lingine katika kujisalimisha ni IMANI. Ibrahimu alifuata maelekezo ya Mungu bila kujua alikokuwa akienda. Hana alisubiri wakati wa Mungu bila kujua ni lini. Mariamu alitarajia muujiza bila kufahamu utatendekaje. Yusufu aliamini lengo la Mungu bila kujua kwa nini mazingira yalikuwa hivyo. Kila mmoja wa watu hawa alikuwa amejisalimisha kwa Mungu alipomtegemea. Katika kweli hii Mtume Paulo anatuambia, Mtu asijidanganye mwenyewe; kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu katika dunia hii, na awe mpumbavu, ili apate kuwa mwenye hekima,” 1Kor 3:18. Kuwa mpumbavu ili upate kuwa mwenye hekima kutakuhitaji kujisalimisha. 

Utafahamu umejisalimisha kwa Mungu unapomtegemea Mungu akutengenezee mambo yako badala ya kujaribu kuwafanyia hila wengine, ukapitisha jambo lako, na mwisho ukatawala mazingira hayo. Unamwachia Mungu afanye, Huhitaji wakati wote kuwa, “mwangalizi.” Maandiko matakatifu yanasema, “Jisalimishe nafsi yako kwa Bwana, na umsubiri kwa uvumilivu.” Zab. 37:7a. Baada ya kujaribu sana, umwamini zaidi. Pia unafahamu kwamba unajisalimisha unapokuwa huchukizwi na lawama na kukimbilia kujitetea. Mioyo iliyojisalimisha huonyesha mahusiano mazuri na wengine. Huwatupilii mbali wengine, hudai haki zako, na hutumikii nafsi yako kama umejisalimisha.

Na tazama huu ndio uzima juu ya neno lile la Yesu na kujisalimisha kule kwa Simoni: Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama,” Lk 5:6-7. Ndugu yangu, yawezekana umekata tamaa kabisa katika maisha yako kutokana na jambo fulani ambalo kwa uelewa wako na uzoefu wako hakuna pa kutokea. Leo Yesu anakuambia neno hili, “‘tweka mpaka kilindili,” yaani jaribu tena kile kilichobaki katika ukamilifu wake, na hadi mwisho wake kabisa, nawe utaona uwezo wangu.’ Hakika hakuna jambo lolote linaloweza kumshinda Mungu.

Yawezekana wakati fulani ulikuwa tajiri sana kwa kuwa na mali na pesa nyingi, na leo huna chochote. Usijifungie ndani kwa kuona aibu au kuchekwa na watu, na wala usiendelee kuishi jana ambayo ilishapita. Itazama kwa kina leo yako ambayo ndiyo uliyo nayo ili iwe tumaini lako la kesho. Jana yako ya ‘utajiri wa mali na pesa’ ibaki kuwa kumbukumbu tu na rejea ya kuwa karibu zaidi na Mungu. Jana yako iliyokuwa na mafanikio mengi ikukumbushe kiini halisi cha maisha, yaani, Maisha ni jaribu, Maisha ni dhamana, na Maisha ni jukumu la muda mfupi.

Matokeo ya nguvu na uwezo wa Yesu katika muujiza huu, unamfanya  Simoni kuyaona maisha yake ya ndani. Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8. Ndugu yangu, hutoweza kujiona ulivyo kama hutojiachia ndani na katika Kristo Yesu. Kuiona vizuri chunusi iliyoko kwenye paji la uso wako, yakupasa kusimama mbele ya kioo. Kumbe kujiachia mbele ya kioo kunakuwezesha kujiona vizuri. Yesu ni kioo kwetu, na ndivyo Simoni alivyojigundua kuwa yu mdhambi.

Pamoja na udhaifu ule aliokuwa nao Simoni bado Mungu anampango na maisha yake. Tena mpango mahususi kabisa. Naye “Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b. Yesu anaifanya njia katika maisha ya Simoni. Huyu ndiye baadaye aliyejulikana kama Simoni Petro, na juu yake ndipo lilipo jengwa Kanisa. Mtume Paulo anatuambia, Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13. Amina! Mruhusu Yesu ndani yako pasipo shaka naye atayatengeneza maisha yako upya.

Wapendwa wana wa Mungu, ukiyatazama maisha yako na jinsi Mungu alivyoendelea kuwa upendo na huruma kwako, hakika yote ndani yako ni kwa neema ya Mungu. Hakika, “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Zab 130:3. Ndugu yangu, mahangaiko katika maisha yako ya kila siku yasiwe ukuta wa kutokuona uwepo na nguvu ya Kristo Yesu ndani ya yale uyafanyayo hata kama uzoefu wako unathibitisha kutokuwezekana tena.

Kama kweli wasadiki Kristo ndiye Mwokozi, basi ni kwa namna hiyo hiyo huyaweza yote yaliyo chini ya miguu yake kwa sababu, “amevitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya Kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote,” Efe 1:22-23. Yesu Kristo analiweka jambo hili hadharani anapowakuta Simon Petro na wenzake waliokuwa mahodari wa kuvua samaki usiku kucha bila kupata chochote. Ni Kristo Yesu huyo huyo aliye hai atakayeyabadilisha maisha yako. Jisalimishe kwake mara!

Tumsifu Yesu Kristo!

Hata walipokwisha kuviegesha pwani vyombo vyao, wakaacha vyote wakamfuata,” Lk 5:11


Tusali:-Ee Yesu Mwema, yatengeneze upya maisha yangu. Naamini pasipo shaka yoyote, Wewe kwangu ndiye Njia, Kweli, na Uzima. Amnia

martes, 30 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 22 MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 3:1-9
Zab/Kit: 33:12-13, 14-15, 20-21
Injili: Lk 4:38-44
Nukuu
Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo,” 1Kor 3:1 

 “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu,” 1Kor 3:6

Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye,” 1Kor 3:7

 “Akasimama karibu naye, akaikemea ile homa, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia,” Lk 4:39 

 “Pepo nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo,” Lk 4:41

 “Akawaambia, Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa,” Lk 4:43 

TAFAKARI: Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye,” 1Kor 3:7

Wapendwa wana wa Mungu, uwepo wa Kristo katika maisha yetu ni habari njema ya ufalme wa Mungu. Habari hii njema ni wokovu na uzima wetu. Ujio wa Yesu kwetu, yaani, Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14, siyo ujio wa mwivi mwenye kupora na kuondoka. Naye Yesu anasema, Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele,” Yoh 10:10. Ujio wa Kristo ni uzima kwetu, na tena atutaka tuwe nao wa kutosha. Ukweli huu unajidihirisha katika uponyaji wa Mama mkwe wa Petro Mtume, Lk 4:38. Yesu akasimama karibu naye, akaikemea ile homa, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia,” Lk 4:39. Kama tendo la shukrani kwa uponyaji ule, kilichofuata ni kuwajibika kama sehemu ya kuyafanya mapenzi ya Mungu. 

 Kristo anatutaka pamoja na mambo yote tuyafanyayo kila siku tusiache kamwe kuutafuta ufalme wa Mungu. Ufalme huo umeshajidhihirisha hapa hapa duniani kwa matendo ya wokovu ya Kristo mwenyewe. Na jua lilipokuwa likichwa, wote waliokuwa na wagonjwa wenye maradhi mbali mbali waliwaleta kwake, akaweka mikono yake juu ya kila mmoja akawaponya,” Lk 4:40. Alama na ishara hizi zinaufunua Utukufu wa Mungu na Ufalme wake. Pepo nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo,” Lk 4:41. Uwepo wa Kristo unatikisa mfumo mzima wa shetani, na hiki ndicho kiama cha uovu na kushamiri kwa wema ndani na katika Kristo. Ni kwa sababu hiyo Kristo kaja kwetu. Tuushinde uovu kwa wema mara zote katika maisha yetu.

Mambo yote tuyapataya duniani hapa kwayo yenyewe siyo ukamilifu wa yale aliyotuandalia Mungu katika ufalme wake. Ni kwa mantiki hiyo, ishara au miujiza licha ya kuufunua Utukufu wa Mungu, kwayo kama ilivyo siyo mwisho wa kila kitu, bali utusaidia kukua katika Imani. Hata kulipokucha alitoka akaenda mahali pasipokuwa na watu; makutano wakawa wakimtafuta-tafuta, wakafika kwake, wakataka kumzuia asiondoke kwao,” Lk 4:42. Kutaka kumzuia Yesu abaki nao ni kupenda kugaagaa katika miujiza ambayo kwayo kama ilivyo siyo kusudi hasa la ujio wa Kristo kwetu.

Kupenda ishara na kubaki katika ishara ni alama ya kutokukua au kukomaa katika Imani.  Yesu anawaambia wale waliokuwa wanataka kukaa naye tu, “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa,” Lk 4:43. Na kauli mbiu ya Yesu kwako na kwangu ni hii; “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Wapendwa, yatupasa kuinjilishana ili kila mmoja ajue kusudi la Yesu hapa duniani.

Kielelezo cha kazi hii ya kuinjilishana ni Kristo mwenyewe na siyo kujiinua kwetu kuliko kwa kibinadamu. Nafasi yako katika uinjilishaji ni kama chombo cha udongo katika kutimiza wajibu wake kwa yale ipasayo kufanya. Hakika sote tu vyombo vya udongo kama asemavyo Mtume Paulo, Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu,” 2Kor 4:7. Hatuna cha kujisifia zaidi ya kumshukuru Mungu kwa kututumia vyema hata katika udhaifu wetu. Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo,” 1Kor 3:1. Leo na hasa tunapozungumzia uinjilishaji mpya, ni wito kwa kila mbatizwa kuifanya kazi hiyo kuanzia pale alipo.

Leo wengi wetu hatuweki tena mkazo katika mafundisha ya Kanisa na badala yake tumekuwa ‘vidakizi’ wa mambo na mwisho wa siku kukosa mwelekeo thabiti wa imani. Ndugu yangu, mkate usioiva vizuri ni hatari sana kwa tumbo. Wengi wetu leo twatambulika kama Wakrito kwa majina yetu tu. Hili ni jangwa la Imani katika familia. Ukweli ni kwamba, familia ndiyo shule ya kwanza kabisa tunapoweza kujifunza na kuishi imani yetu.

Baba na Mama ndiyo walimu wetu wa Imani. Mtume Paulo anatambua wajibu wake katika kweli hii, na kusema, Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?” 1Kor 3:2-3. Kumjua na kumuishi Kristo ni kuwa upande wa mabadiliko, yaani, kutoka kwenye giza na kuingia katika mwanga.

Mabadiliko hayo na katika ngazi tofauti tofauti yasiwe sababu ya mimi au wewe kujisifia na kujikweza. Udakuzi hapa si nani kafanya nini au kamzidi nini mwenzake, bali sote kwa pamoja tumelifikia lengo la kuihubiri habari njema? Maana hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je! Ninyi si wanadamu?” 1Kor 3:4. Je, hayo yote tuyaonayo pamoja na tofauti zetu katika utendaji yapo kama yalivyo kwa nguvu zetu binafsi?  Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani?” IKor 3:5a. Tofauti zetu katika utendaji ndiyo uzuri wa Mungu. Hatukuumbwa tuwe ‘maroboti,’ bali tuwe wamoja katika tofauti zetu. Hivyo Apolo na Paulo “ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa,” 1Kor 3:5b. Na ndivyo ilivyo mpendeza Mungu.

Uzuri wa umoja katika utofauti ukuza ubunifu na utofauti wa yale ya kawaida tuyafanyayo. Katika hili Mtume Paulo anasema, Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu,” 1Kor 3:6. Tunapozitanguliza nafsi zetu kwa kila jambo, tunazikwamisha neema za Mungu ndani yetu. Ni sawa na kubaki katika furaha ya kujichora kwako kusikobeba uhasili wako. Ukweli ni kwamba, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye,” 1Kor 3:7. Je, natambua nguvu hiyo ya Mungu ndani yangu na kwa mwenzangu? Kama natambua kweli hiyo, Je, namshukuru Mungu kwa uwepo wa mwenzangu na mafanikio yake? Ndugu yangu, yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe,” 1Kor 3:8. Kufurahia mafanikio ya mwenzako na kumshukuru Mungu ni ukomavu wa imani.

Wapendwa wana wa Mungu, kamwe tusisahau ukweli huu kwamba, sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu,” 1Kor 3:9. Umoja katika utofauti wetu ndiyo uzuri wa Mungu na wenye kuufunua Utukufu wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa,” Lk 4:43


Tusali:-Ee Yesu, tutumie vyema kama vyombo vyako vya udongo. Amina

lunes, 29 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 22 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 2:10b-16
Zab/Kit: 145:8-9, 10-11, 12-13ab, 13cd-14
Injili: Lk 4:34-37
Nukuu
akisema, Acha! Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu,” Lk 4:34 

Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati, akamtoka asimdhuru neno,” Lk 4:35 

 “Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu,” 1Kor 2:10b 

Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu,” 1Kor 2:11b 

 “Maana, Ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo,” 1Kor 2:16

TAFAKARI: “Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu.”

Wapendwa katika Kristo, uwepo wa Kristo na Jina lake, ni tishio kwa roho zile zilizo kinyume na mpango wa Mungu. Pepo wachafu huelewa na kuogopa uwepo wa Kristo. Hakuna roho chafu zinazoweza kuushinda uwepo wa Kristo. Pepo wachafu hawana amani mara litamkwapo jina la Yesu.  Uwepo wa Kristo ni tishio kwa wale wote wampingao Kristo. Mapepo yanasema, Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu,” Lk 4:34. Utakatifu wa Yesu na Ukamilifu wake ni kielelezo cha maisha yetu na yale yatupasayo kuishi ili kuurithi ufalme wa Mungu.

Ukamilifu na Utakatifu wa Yesu ndio unaompa mamlaka ya kukemea roho chafu na kuwaweka huru wale waliofungwa katika ulimwengu huo wa roho. Ukweli huo hata mapepo yenyewe yanakiri na kusema, “Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu,” Lk 4:34c. Hata baada ya ukiri huo wa hayo mapepo, Yesu anakemea roho hiyo chafu na kusema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati, akamtoka asimdhuru neno,” Lk 4:35. Ndugu yangu, kimbilio lako lipo wapi?

Ni wazi kati yetu mara tupatwapo na changamoto za imani ukimbia hapa na pale, na kushika hiki na kile ili kupata ulinzi. Kwa msukumo na woga huo, wengi ujikuta tumejiweka wenyewe wakfu kwa shetani kwa kupenda au kutokupenda kwa njia mbalimbali. Mfano: wengi wetu ni vinara wa ibada za mitambiko mara kwa mara na zisizo na kikomo.  Wapo pia baadhi yetu huzindika nyumba zao ikiwa ni pamoja na sehemu zao za kazi na biashara. Wengine na walio wengi, huziweka mali na fedha zao wakfu kwa shetani kabla ya kuzitumia, nk. Haya yote ni tokeo la hofu na ujinga.

Hofu na ujinga huu kamwe hauwezi ukawa ndiyo salama yako. Hofu na ujinga huu mwisho wa siku utakuingiza kwenye uovu mwingine na mkubwa zaidi. Ishinde hofu yako kwa kumwamini Kristo Yesu pasipo shaka. Kwa kuwa “hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Je, ndumba, hirizi, na haya mazindiko yako, yanasema chochote kuhusu wokovu wako? Tafakari na chukua hatua mapema!

Wapendwa wana wa Mungu, unavyo yakumbatia yaliyo ya shetani, yaani, ndumba, hirizi, mazindiko na hata wewe mwenyewe kujiweka wakfu kwa shetani na mali zako, Roho yule wa Mungu aliyeko ndani yako huondoka na kukuacha. Ukweli ni kwamba, miili yetu ni hekalu la Roho Mtakatifu, 1Kor 6:19. Na kwa mantiki hiyo, tunapolinajisi hekalu hili ndivyo hivyo hivyo tunavyomfukuza Roho huyo ndani yetu. Kazi ya Roho huyo ndani yetu “huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu,” 1Kor 2:10b. Utawezaje kuyajua mafumbo ya Mungu kama walinajisi hekalu la Roho huyo, yaani, mwili wako? Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu,” 1Kor 2:11b. Bila Roho wa Mungu ndani yako ni sawa na kapu tupu licha ya kwamba kapu hilo laweza kubeba chochote kile. Roho Mtakatifu ndani yako ni ulinzi tosha wa Mungu. Ikiwa mwili bila Roho Mtakatifu ndani yake hakuna ulinzi, ni sawa na kapu tupu licha ya uwezo wa kapu hilo kubeba chochote kile.

Pamoja na ulinzi huo wa Roho Mtakatifu ndani yetu, tusifananishe roho hiyo na roho ya dunia. Kwa maana nyingine sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu,” 1Kor 2:12. Utaithamini na kuitunza zawadi  ukijua thamani yake. Uthaminishwaji wa Roho ndani yetu  ndio utupao uwezo wa kusema zaidi ya hekima ya kibinadamu. Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni,” 1Kor 2:13. Na hili twalifanya siyo kwa nguvu zetu na werevu wetu, bali yote twawezeshwa kwa neema za Mungu.

Kwa mantiki hiyo ni wazi kwamba mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni,” 1Kor 2:14. Kwa maneno mengine ni kwamba, mtu yule awekaye matumaini yake yote kwenye nguvu nyingine, mfano, kujiweka wakfu kwa shetani, hatoweza kufahamu nguvu ya Roho Mtakatifu ndani yake. Badala yake, mtu wa rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu,” 1Kor 2:15. Mtu huyu ni yule anayeongozwa na Roho wa Mungu ndani yake, na mwenye hofu hiyo ya Mungu. Maana, Ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo,” 1Kor 2:16. Kristo ndiye kielelezo chetu kwa sababu ni katika Yeye tu twaweza kuokolewa Naye.

Tumsifu Yesu Kristo!

Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu,” 1Kor 2:12


Tusali:- Ee Yesu Mwema, tujalie Nguvu ya Roho wako Mtakatifu ili tuyawaze daima yaliyo Matakatifu. Amina

domingo, 28 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 22 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 2:1-5
Zab/Kit: 119:97, 98, 99, 101, 102
Injili: Lk 4:16-30
Nukuu
Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1 

Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5 

Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19 

Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21 

TAFAKARI:Lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake.”

Wapendwa wana wa Mungu, Yesu Kristo ndiye mfano hai na halisi kwetu wa kuiga na kufuata hata kama kwa hali yetu na ubinadamu wetu si rahisi. Leo Yesu katika Sinagogi huko Nazareti, wanapomjua vizuri anawaacha midomo wazi. Ni kweli walimfahamu Yesu katika maana ya historia yake. Mara zote tunajisikia vizuri na nyumbani pale tunapofikiri sawa, na kuwa na maisha yaliyowiyana. Kwa hali hii tunahitaji nguvu ya pekee kuwa tofauti. Yesu anatufundisha kuwa tofauti na kutokufanya mambo kimazoea. Yesu kama ilivyokuwa kawaida ya siku ya sabato, anaingia kwenye sinagogi na kulisoma neno la Mungu, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Hii ndiyo tofauti ya Yesu na kauli mbiu yake. Hiki ndicho kinachomtofautisha Yesu na wengine ingawa neno hili lilishasomwa na wengi waliomtangulia. Kwa kukazia Yesu anasema, “Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21. Maneno haya ndiyo msukumo wa mabadiliko yote na mtazamo mpya juu ya Yesu.

Mwana sayansi Isaac Newton wa Uingereza (1643-1727) alipolichukua jiwa na kulirusha juu na likarudi ardhini na kugundua nadharia “theory” ya mvutano “gravitation,”  hakuwa mwanadamu wa kwanza kurusha jiwe juu na likarudi ardhini. Ila kwa kwenda zaidi ya mazoea ya urushwaji wa jiwe na kurudi ardhini ndiko kunakomfanya leo tofauti na wengine waliomtangulia. Yesu anatualika kutokuishi kwa mazoea, bali tuende zaidi ya kile kilichozoeleka. Ukweli huu ni kwa hali zote za maisha na kwa namna ya pekee mahusiano yetu na wenzetu ambayo msingi wake ni Upendo, Kweli na Haki. Kwenda tofauti na yaliyozoeleka ni mshangao kwa wale wasiopenda kuwa tofauti katika kile kilichojificha. Hivyo, wakamshuhudia (Yesu) wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu?” Lk 4:22. Historia ya Mtu siyo kikwanzo cha yeye kuwa vizuri, mzuri, au kufanya vizuri zaidi hata kama historia ya kule alikotoka kuonekana kuwa mbaya.

Kwa msisitizo Yesu anatutaka tuione tofauti kati yake na wote waliomtangulia. Naye anasema, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni,” Lk 4:25-26. Leo pamoja na sintofahamu kama hizi tunalo tumaini ndani na katika Kristo. Yesu hatuponji tu majeraha yetu ya ndani na nje, bali hututakasa pia. Naye anasema, Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu,” Lk 4:27. Kristo kwa sasa ndiye utakaso wetu.

Kwa hali ya kawaida hasa kwa yale tuyoyazoea kuishi na kuyasikia, ujumbe huu wa Yesu hukuwapendeza Mafarisayo na waandishi walio kuwa vinara wa kudumisha desturi hizo. Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo,” Lk 4:28. Kwa vile saa yake ilikuwa bado kufika, ghadhabu ile haikumdhuru. Na mambo yalikuwa hivi; Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake,” Lk 4:29-30. Chuki na hila za mwanadamu haziwezi kufanikiwa palipo na mpango wa Mungu. 

Unyenyekevu wa Yesu uliobeba historia yake fupi hapa duniani unakuwa sababu ya hukumu yake. Mara nyingi tunawahukumu watu ndivyo sivyo kutokana na kujua historia zao, maeneo ya kijeografia walikotoka, historia za wazazi wao, mazingira ya makuzi yao, marafiki walioishi nao, na hata mtazamo wao kimaisha. Hili ni kosa kubwa sana kufanya. Hakuna aliyeko hapa duniani kwa bahati mbaya, au kuzaliwa kwa bahati mbaya. Sisi tu malengo na makusudi ya Mungu. Mungu anampango na kila mmoja wetu.

Baada ya Yesu kuwaambia ukweli Waandishi na Mafarisayo kwa kutokuamini kwao, hawapokei ujumbe ule wa ukweli na kubadilika, bali wanatafuta njia ya kumwangamiza. Katika hili Yesu anatujaza ujari kwa kusema, “Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Maana yake ni nini? Ukweli ni kwamba, tunaposimama katika kweli, na kuishi kweli hiyo, twatangaza vita kwa wale wasioipenda kweli hiyo. Kwa upande wa Imani ni vita, si tu ya nafsi, bali roho pia. Roho ambazo hazimwelekei Muumba wake zitakuwa kinyume na yote tusemayo na kuyaishi. Kuishi Ukristo na kumkiri Kristo leo ni vita kubwa ya kiroho. Tulizoea kusikia hadithi za Mashahidi wa Imani karne na nyakati za nyuma, lakini leo ni nafasi na wakati wetu kuwa mashahidi wa Kristo. Kuna kila dalili na sababu za kuutoa ushuhuda huo.

Tunachopaswa kuishi si maisha ya ushindani wa hoja katika majukwaa, bali zaidi ni kuishi na kutoa ushuhuda wa ukimya wa maisha ya kweli ya Ukristo wetu. Jambo hili ni muhimu sana, kwani katika utulivu Mungu yupo na kuonekana. “Na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:12. Huu ni wakati wa mitetemo ya Imani. Nasi tusienende kadiri ya mitetemo hiyo. Tuitafsiri hiyo mitetemo nako tutakutana na Mungu katika utulivu.

Ni wazi katika kutenda lililo la Mungu, yaani lenye kuongozwa na upendo wa kweli, tujiandae kupata upinzani. Yule mwovu shetani hafurahii yaliyo mazuri na mema yenye kuufunua Utukufu wa Mungu. Yesu Kristo mwenyewe alipata upinzani nyumbani mwake mwenyewe. Katika hili Yesu anasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Je, kama hatukubaliki nyumbani kwetu na watu wanaotufahamu iwe sababu ya kutokutenda mema? Jibu ni HAPANA! Tuendelee kutenda wema na upendo kwa wote, kwa sababu asili ya upendo ni Mungu, uwepo wa upendo ni Mungu, na Upendo ni Mungu. Kuyaona haya ya Mungu ndani yetu kwahitaji unyenyekevu na kuepuka kujiinua kusiko na sifa wala siha. Hali hiyo ndani yetu itatuwezesha kusema toka moyoni maneno haya ya Mtume Paulo; Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1. Mungu ndiye anaye wezesha yote ndani yetu. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5. Sifa na Utukufu ni kwa Mungu wetu. Amina

Tumsifu Yesu Kristo

“Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21


Tusali:-Ee Yesu tujalie ujasiri. Amina

sábado, 27 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 22 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 22 YA MWAKA-C
Somo I: YbS 3:17-20, 28-29
Zab/Kit: 68:4-5, 6-7, 10-11
Somo II: Ebr 12:18-19, 22-24
Injili: Lk 14:1, 7-14
Nukuu
“Mwanangu, wakati wa kufanikiwa uendelee katika unyenyekevu; hivyo utapendwa kuliko mwenye ukarmu,” YbS 3:17

Kadiri ulivyo mkuu uzidi kujinyenyekesha, nawe utapata kibali machoni pa Bwana; kwa maana rehema zake Bwana zi kuu, na siri yake ni kwa wanyenyekevu,” YbS 3:18-20

 “Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi,” Ebr 12:22 

mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika,” Ebr 12:23 

 “Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9 

Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10 

TAFAKARI: Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11 

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 22 ya mwaka “C” wa Kanisa. Masomo yetu yote matatu yamebeba ujumbe wa ‘UNYENYEKEVU.’ Hakika mtu ufanikiwa katika mambo yake mengi pale anapojinyenyekeza. Unyenyekevu ni msingi wa fadhila zote. “Mwanangu, wakati wa kufanikiwa uendelee katika unyenyekevu; hivyo utapendwa kuliko mwenye ukarimu,” YbS 3:17. Kujishusha hakumaanishi ‘UJINGA,’ bali kwa kufungulia ufahamu wa mengi yanayokuzunguka kadiri ya wito na nafasi yako katika jamii husika. Ni kwa mantiki hiyo kwamba, “kadiri ulivyo mkuu uzidi kujinyenyekesha, nawe utapata kibali machoni pa Bwana; kwa maana rehema zake Bwana zi kuu, na siri yake ni kwa wanyenyekevu,” YbS 3:18-20. Watu wote walioacha nyuma mazuri na kukumbukwa ni wale waliojinyenyekeza katika yote waliyokutana nayo kama jaribu.

Kinyume chake ni kwamba, “Msiba wa mwenye kiburi hauleti kupona, mche wa uovu umepandika ndani yake,” YbS 3:28. Kushindwa kwa wengi katika maisha na hata kile walicho kadiri ya wito na nafasi zao utokana na kiburi. Mshahara wa kiburi ni anguko lako mwenyewe. Kumbe nisichoke kuiomba hekima ya Mungu kila siku ili iniongoze katika busara. Na “moyo wa busara utatambua mithali, na sikio sikivu ni tama ya mtaalamu,” YbS 3:29. Unyenyekevu utuinua pale tunapojishusha pasipo shuruti. Naye Yesu ndicho anachotuambia, kwamba, “kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11 

Leo katika somo la Injili Yesu anatupa angalizo hasa tunapoalikwa kwenye tafrija mbalimbali. Tukizama ndani zaidi tunaona kwamba uhai tulionao na maisha tunayoyaishi ni sawa na kualikwa kwenye furaha ya Mungu na utukufu wake. Basi ni vyema mimi na wewe kutambua duniani hapa tunapita tu, na tupo kwa maandalizi ya maisha ya umilele. Ukweli huu wa maisha uniweke wazi kwa haya mambo matatu; maisha ni jukumu la muda mfupi, maisha ni dhamana, na maisha ni jaribu. Na katika Injili ya leo, Yesu anatuwasa hivi kuhusu ukweli huu wa maisha, na zaidi maisha kama jaribu. Naye Yesu anatuambi hivi; Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9. Kama sote tumealikwa harusini ni wazi tumepewa mastahili yaliyo sawa na yule aliyetualika. Je, kwa maanisha nini maisha ni JARIBU?

Mwelekeo huu wa maisha, yaani, maisha ni Jaribu, huonekana katika hadithi ya Biblia yote. Wakati wote Mungu huijaribu tabia ya watu, imani yao, utii, upendo,  ukamilifu na uaminifu wao. Mungu alimjaribu Ibrahimu kwa kumwambia amtoe sadaka mwanae Isaka. Mungu alimjaribu Yakobo alipopaswa kufanya kazi miaka ya ziada ili kumpata Raheli kama mkewe.

Adamu na Hawa walishindwa jaribio katika bustani ya Edeni, na Daudi alishindwa majaribu yake kutoka kwa Mungu mara kadhaa. Lakini Maandiko Matakatifu hutupa mifano mingi ya watu walioshinda majaribu makubwa mfano Yusufu, Ruthu, Esta na Daniel.

Wapendwa wana wa Mungu, ukweli ni kwamba majaribu hukuza tabia na kuiweka wazi, na maisha yote ni majaribu. Siku zote unajaribiwa. Mungu siku zote anatazama unavyoenenda kwa watu, matatizo, mafanikio, migongano, magonjwa, mambo ya kukatisha tamaa, hata hali ya hewa!

Mungu anaangalia hata matendo rahisi sana kama vile unapofungulia mlango wengine, unapookota kipande cha takataka, unapoonyesha upole kwa karani au mhudumu, unapomsikiliza mfanyakazi wako wa nyumbani, nk.

Ndugu yangu, ukweli ni kwamba hatuyajui majaribu yote ambayo Mungu anatupa lakini tunaweza kutabiri baadhi yake, kwa kuzingatia Maandiko Matakatifu. Utajaribiwa kwa mabadiliko makubwa, kucheleweshwa  ahadi, matatizo magumu, sala zisizojibiwa, lawama zisizostahili, na hata mikasa isiyo na sababu. Ndugu, katika maisha yangu nimetambua kuwa Mungu anajaribu imani yangu kupitia matatizo, anajaribu tumaini langu kwa njia ya mali, na anajaribu upendo wangu kwa njia ya watu.

Jaribu la muhimu sana ni jinsi unavyotenda unapoacha kuhisi uwepo wa Mungu katika maisha yako. Wakati mwingine Mungu hujiondoa kwa makusudi, na hatuoni uwepo wake. Mfalme Hezekia alipatwa na jaribu hili. "Walakini kwa Habari ya wajumbe wa wakuu wa Babeli, waliotumwa kwake kuuliza ajabu iliyofanywa katika nchi, Mungu akamwacha, ili amjaribu, ili kwamba ayajue yote yaliyokuwemo moyoni mwake." 2Nya 32:31. Hezekieli akikuwa amefaidi ushirika wa karibu na Mungu,  lakini kwa wakati wa muhimu sana Mungu alimwacha peke yake ili ampime tabia yake, adhihirishe udhaifu wake, na amwandae kwa MAJUKUMU ZAIDI. Kumbe lengo la majaribu si kutuangamiza, bali tunaandaliwa kwa mambo makubwa zaidi, na kwa malengo makubwa zaidi ya Mungu.

Wapendwa katika Kristo, ukielewa kuwa maisha ni jaribu, unatambua kuwa hakuna kitu kidogo katika maisha yako. Hata tukio dogo sana lina maana kubwa katika kukuza tabia yako. Kila siku ni siku ya muhimu, na kila dakika ni wasaa wa kukua kitabia, kuonyesha upendo, au kumtegemea Mungu. Majaribu mengine hata huyatambui. Lakini yote haya yana matokeo ya milele.

Habari njema ni kwamba Mungu anakutaka ushinde mtihani huo wa maisha, kwa hiyo haruhusu majaribu unayoyapata kuwa makubwa kuliko neema anayokupatia katika kukabili majaribu hayo."Jaribu haliwapati ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili." 1Kor 10:13

Mpendwa katika Kristo, kila unaposhinda jaribu, Mungu hutambua na kupanga kukupa tuzo la milele. Mtume Yakobo anasema, "heri mtu astahimikiye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao." Yak 1:12.

Basi ndugu yangu ninaye safiri nawe katika tafakari hii, yakupasa kujua kuwa sote ni waalikwa na siyo ‘mgeni rasmi.’ Kwa utaratibu wa kawaida mbele palipoandaliwa si mastahili yangu. Na kama nitakuwa mbele nielewe nipo hapo kwa kuhesabiwa haki na yule aliyenialika. Kama ni kiongozi katika taasisi yoyote ile, nielewe nipo hapa kwa kuhesabiwa haki hiyo na Mungu kupitia watu wake. Hivyo nifanye yote kadiri ya utaratibu uliopo wakati huo huo niheshimu mara zote kiapo changu kwa nafasi ile niliyohesabiwa haki na Mungu kwa kupitia watu wake kwa utaratibu tuliojiwekea.

Hali na mazingira haya yanifanye nizame ndani zaidi na kuyaona maisha kama jukumu la muda mfupi. Wito huu unikumbushe mara zote kufanya yale yanayo mpendeza Mungu kuelekea maisha yale ya milele. Pili, nione ukweli wa maisha na nafasi niliyopewa na watu kuwa ni dhamana. Ukweli huu unikumbusha mara zote niwapo mbele nipo kwa kuhesabiwa haki kama kiongozi katika taasisi yoyote ile. Nielewe nimepewa uwakili na siku ya mwisho itanipasa kutoa hesabu yake. La sivyo na kama hili silifahamu vizuri, ni vyema na busara kutafuta nafasi nyingine. Na ndivyo Yesu anavyotuambia ili kuwa sehemu salama zaidi, Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10. Huku ndiko kwa maneno mengine kupungua ili Mungu awe na nafasi juu ya maisha yako. Na huu ndiyo unyenyekevu utakao kupandisha pale unapojishusha.

Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii utakubaliana nami kwamba kati yetu kwa nafasi tulizokuwa nazo na madaraka tuliyonayo yaliyopitiliza hututia upofu na kutufanya kuwa ndiyo fimbo ya kuchapia wengine. Jeuri hii ndugu yangu tunaipata wapi wakati Maandiko Matakatifu yanatuambia, Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara,” Zab 90:10. Jinyenyekeshe basi na kuwa kile Mungu alichokusudia katika maisha yako. Kwa nini basi wajifananisha na Mungu asiye jaribiwa? Je, wajua idadi ya nywele zako kichwani? Kama hujui mipaka yako kitazame kifo. Na kama huna hofu ya kifo kwa kiburi chako, tafakari kwa kina tendo la usingizi/kulala. Hili ni zoezi la Kifo. Wengi wetu hulala kama kawaida na mara hukosa fursa ya kuamka tena. Je, hata usingizi siyo jaribu kwako kwamba wewe si lolote wala chochote?

Na swali la kujiuliza ni hili: Je, mwisho wa hayo yote ni nini? Kama mimi na wewe sioni maisha ni JARIBU, kujishusha itakuwa vigumu sana. Pasipo unyenyekevu nitegemee anguko langu binafsi. Na huku ndiko kupoteza lengo la Maisha kuelekea ule ukamilifu, Mt 5:48-(utakatifu) kama cheo chetu, na mwisho kutokuurithi ufalme wa mbinguni. Mwenye hofu ya Mungu ataweza kuepuka anguko lake binafsi. Na huu ndio wa Mungu kwako na kwangu. Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi,” Ebr 12:22. Hili ndilo Kanisa la wateule yaani, watakatifu. Ni  mkutano mkuu na Kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika,” Ebr 12:23. Ndugu yangu uwapo hapa duniani, “itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake?” Mk 8:36. Tumtazama Yesu aliye kielelezo chetu. Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili,” Ebr 12:24. Huyu ndiye kila kitu kwako na kwangu. Tujifunze kwake.

Tembo kwa umbo lake huweza kuyala majani yaliyo juu ya mti na hata yatambaayo chini ardhini. Kwa uwezo wa mdomo wake, Tembo huyafuruga maji kabla ya kuyanywa. Na sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kuvifukuza mbali vile vyote ‘atarishi’ kwa afya na maisha yake akiwemo chura.
Lakini pamoja na ukweli huu juu ya Tembo, ‘SISIMIZI’ kwa umoja wao huweza kumwangusha tembo na kumfanya kitoweo, na hata jumba la muda tu la kuishi. Kumbe pamoja na ukubwa alio nao Tembo, uwepo wa SISIMIZI umkumbusha namna ya kutembea vizuri.

Ndugu yangu, kama ilivyo kwamba hakuna lililo dogo katika maisha, ndivyo hivyo hivyo hakuna aliye mdogo kama sote tunaishi pamoja katika kweli na haki. Hawa wadogo katika udogo wao wanaweza kuwa sababu ya wewe kutolifikia lengo lako hata kama nia unayo. UNYENYEKEVU ndiyo msingi wa fadhila zote.  Na ndivyo Yesu anavyotutaka tufanye katika unyenyekevu na utu wa kweli, mwamba, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12. Tuwe tayari hata kuwaalika mahasimu wetu. Huku ndiko kukomaa kimwili na kiroho.

Na kwa namna nyingine Yesu anatuambi, Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14. Hawa ni wale wote wasio na sauti katika jamii. Nao wana haki ya kuishi kama wewe unavyoishi kwa kupenda mno starehe, anasa na tafrija. Kufikia kipimo hiki katika maisha kutakuitaji unyenyekevu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Moyo wa busara utatambua mithali, na sikio sikivu ni tama ya mtaalamu,” YbS 3:29

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie fadhila ya Unyenyekevu. Amina