lunes, 11 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 15 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 15 YA MWAKA-C
Somo: Isa 10:5-7, 13-16
Zab: 94:5-6, 7-8, 9-10, 14-15
Injili: Mt 11:25-27
Nukuu:
Nitamtuma juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani,” Isa 10:6 

 Je! Shoka lijisifu juu yake alitumiaye? Je! Msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? Ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti,” Isa 10:15 

 “Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga,” Mt 11:25 

 “Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia,” Mt 11:27 

TAFAKARI: “Bwana hatawatupa watu wake wanyenyekevu na wanyofu wa moyo.”

Wapendwa wana wa Mungu, mwanadamu anapokumbana na sintofahamu nyingi katika maisha yake, na kukosa mwanga na matumaini kwa kile akitazamiacho, huishia kukosa maana ya maisha ya maisha yale anayoyaishi. Pigana ya mwanadamu kila siku ni kuwa mahali pazuri zaidi na penye maana zaidi. Mwanadamu huyu ukosa mwelekeo na matumaini pale ambapo licha ya jitihada zake azifanyazo katika usahihi wake anashindwa kujikwamua. Je, tatizo lipo wapi? Kama tatizo halipo kwake binafsi, basi tatizo hilo lipo kwenye mfumo wa maisha anayoishi katika jamii husika. Hapa ndipo tunapoona dhambi ya jamii-‘social sin,’ au uovu katika jamii unavyokuwa sababu ya wengi kuteseka na kukata tamaa. Je, Mungu anaruhusu haya?

Ni vyema nikajua jambo hili kwamba, Mungu kaniumba kwa sura na mfano wake, na ndani yangu kanipa uhuru na utashi wa kupembua katika kujua lililo jema na baya. Hivyo ninavyoshindwa kutumia mizania hii vizuri, kifuatacho katika ubaya wake hujulikana kama ‘uovu wa kimaadili’ kwa sababu ni tokeo la kutokutumia uhuru na utashi wangu vyema. Hapa ndugu yangu, Mungu hausiki kabisaaa.

Ila tulitazamapo somo letu la leo tunaweza kuona kwa kiasi fulani Mungu huweza kuruhu lililo ovu ili mwisho wa suku liwe tunda la wema na mafaa. Mungu huweza kutumia njia hii kama tiba kwa mtu au jamii, somo kwa mtu au jamii hasa pale mtu au jamii inapokengeuka. Katika mazingira kama haya, agizo la Mungu huwa kama ifuatavyo; Nitamtuma (mtu au hali fulani katika maana ya kuruhusu) juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani,” Isa 10:6. Hapa Mungu anatumia tendo hili kama tiba na somo ili watu wajue uovu na sababu ya kuteseka kwao na mwisho wairudie njia ya kweli. Mungu analifanya hili, au kuruhusu jambo hili akijua na akiwa malengo chanya. Naye anasema, Kwa nguvu za mkono wangu nimetenda jambo hili, na kwa hekima yangu; maana mimi nina busara; nami nimeiondoa mipaka ya watu, nikaziteka akiba zao, nikawaangusha waketio juu ya viti vya enzi kama afanyavyo shujaa,” Isa 10:13. Hivyo kwa upande wangu na wewe ni hatari sana kufanya vitu kwa mazoea au ushabiki. Madhara yake kwa mtu mmoja au jamii ni makubwa sana.

Na hapa ndipo tunapoongelea juu ya upumbavu wa mtu au watu, na mwisho wa siku kinakuwa kilio cha wengi katika wingi wao (wapumbavu), na wachache katika uchache wao (walio simama katika kweli na haki). Je, Mungu katika uchache wa hawa waliosimama katika kweli na haki, na wakazidiwa na kundi kubwa la wapumbavu waliotumia vibaya uhuru na utashi wao kwa ushabiki, atakaa kimya? La hasha! “Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake, Wala hutauacha urithi wake, Maana hukumu itairejea haki, Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata,” Zab 94:14-15. Ukweli ni kwamba, ‘uovu hauwezi kudumu katika umilele kwa sababu hauna asili hiyo ya milele.’ Hivyo uovu kamwe hauwezi kujisifu kwa sababu hauna pa simimamia. Ila mtu mwenye kusimama katika kweli na haki anamahali pakusimamia kwa sababu kweli na haki hiyo ina umilele ambao ndiyo sifa ya Mungu. Na hii ndiyo maana ya maneno haya; Je! Shoka lijisifu juu yake alitumiaye? Je! Msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? Ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti,” Isa 10:15. Kumbe hakuna sababu ya kukata tamaa ikiwa umesimama katika kweli na haki, licha ya kuzungukwa na tufani la uovu na wasioona tena kweli na haki kwani hali hiyo (ovu) haina umilele. Kwa hiyo Bwana, Bwana wa majeshi, atawapelekea kukonda watu wake walionona; na badala ya utukufu wake kutawashwa kuteketea kama kuteketea kwa moto,” Isa 10:16. Tena kumbe hakuna sababu ya kukata tamaa pale mtu anapojiinua kwa uovu na wakati mwingine akijilinganisha na kujifananisha na Mungu. Mtu huyo au mazingira hayo ‘ovu’ ni ya leo na kesho tu. Hivyo, ‘Bwana hatawatupa watu wake wanyenyekevu na wanyofu wa moyo.’

Wapendwa wana wa Mungu, tuitazamapo historia ya wokovu wetu, tunagundua kwamba Mungu hufanya kazi na wale wajishushao na wanyenyekevu wa Moyo. Licha ya tabia na mwono huu wa Kimungu, wale wate wanoshirikishwa mpango wa Mungu katika tendo la Kimungu, huwa ni watu wa kawaida sana, na mara nyingine huwa wale waliodharaulika na jamii husika. Mama Bikira Maria ni mmoja wa wale walioshiriki mambo makuu ya Mungu katika unyonge na unyenyekevu wake. Naye Bikira Maria analitambua jambo hili na kusema, Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48.  Bikira Maria anatambua pia kile kinachotendeka kwake ni upendeleo wa Mungu ndani mwake, na hivyo kinamakusudi makubwa kadiri ilivyompendeza Mungu. Naye anasema, Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Mama Bikira Maria anayasema haya toka ndani ya mtima wake, na anamaanisha vivyo. Bikira Maria hayasema haya ili apate huruma kwa watu au ya watu. La hasha! Bikira Maria anayasema haya mambo mazito akitazama kuinuliwa kwake kusiko mastahili yake binafsi bali kwa kujinyenyekesha kwake, na hasa upendeleo aliopewa na Mungu wa kushiriki fumbo hili la wokovu wa mwanadamu. Hakika, Mama Bikira Maria kama mwanadamu ni mfano halisi wa yeyote yule mwenye kupewa dhama na umma wa watu.

Kujishusha huku na kuwa wanyenyekevu mbele ya Mungu mwenye kuyaweza yote, ndiko kunakotutafakarisha maneno na sala hii ya Yesu katika Injili ya leo: Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako,” Mt 11:25-26. Je, twatoa shukrani kwa Mungu hata kwa kile kidogo Mungu alichotuwezesha kukifanya? Je, mafanikio niyapatayo natambua ni mkono wa Mungu, au ni akili zangu na ujanja wangu? Ndugu yangu, ‘moyo usio na shukrani hukausha mema yote.’

Tumsifu Yesu Kristo!

Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia,” Mt 11:27


Tusali:-Ee Yesu na Mwalimu wangu, nipe macho na moyo wa unyenyekevu wa kuona yote niyafanyayo si kwa akili zangu tu, bali neema ile itokayo kwako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario