viernes, 15 de julio de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 16 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 16 YA MWAKA-C
Somo I: Mwa 18:1-10a
Zab: 15:2-3, 3-4, 5
Somo II: Kol 1:24-28
Injili: Lk 10:38-42
Nukuu:
Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako,” Mwa 18:3

Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:10a

Sasa nayafurahia mateso niliyo nayo kwa ajili yenu; tena nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua ya mateso ya Kristo, kwa ajili ya mwili wake, yaani, kanisa lake,” Kol 1:24

 “sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo,” Kol 1:28

Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie,” Lk 10:40 
 “lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa,” Lk 10:42

TAFAKARI:Kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.”

Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka si mgeni wa neno hili ‘ukarimu.’ Mtume Paulo anatupa maana halisi ya neno ukarimu.  “Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,” 2Kor 9:6-7. Ni kwa maana hii Ukarimu ujeuka kuwa baraka kwani ndivyo Mungu apendavyo tufanye.

Ibrahimu anabarikiwa na kuhaidiwa kutokana na ukarimu wake. Anapowaona wageni wale watatu, anawahudumia bila kujibakiza, Mwa 18:5-8. Naye anasema, Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako,” Mwa 18:3. Maneno haya; “usinipite sasa mimi mtumwa wako,” yanaelezea ni kwa kiasi gani Ibrahimu alivyo yaweka matumaini yake yote kwa Mungu kwa kile alichokuwa anakitamani, yaani, kuwa na Mtoto. Wageni hawa watatu ni fumbo zima la UTATU MTAKATIFU, Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Huu ni ugeni mkubwa sana. Tupatapo mgeni au wageni, yatupasa kuwahudumia kama walivyo kadiri ya kile wanachohitaji wakati ule. Tulifanye jambo hili bila kuwa na upendeleo au utofauti wa kulifanya kutoka na mwono wa yule tuleyekutana naye kama mgeni. Ibrahimu anajitoa bila kujibakiza kwa hali na mali alizokuwa nazo.

Ukarimu ni uwepo wa kimungu ndani yetu. Unapofanya tendo la ukarimu unaakisi uwepo wa Mungu ndani yako. Mungu ni MKARIMU! Tunapowakarimia wenzetu wenye mahitaji mbalimbali twafanya tendo la Kimungu, na tendo hilo Mungu usimama hapo. Mungu hutujibu mara moja tulifanyapo tendo hili bila kujibakiza. Mwenye jicho la ukarimu atabarikiwa; Maana huwapa maskini chakula chake,” Mit 22:9. Ibrahimu anapewa hakikisho hilo na baraka hizo mbele ya Mungu. Naye Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:10a. Ndugu yangu, unapomkarimu mtu usiangalie alikotoka, undugu uliokua nao naye, ukabila wako naye, ukanda wenu, na hata utaifa wenu. Yatupasa kulenga kwenye hitaji la mtu husika, na tulifanye jambo hilo bila kujibakiza.

Ni ukweli usiotia shaka kwamba kadiri ya mtazamo wetu wa kibinadamu, na hali tuliyonayo kibailoogia-elimu viumbe, ni vigumu kuamini kutendeka kwa yale ambayo kiualisia yeshapitwa na wakati wake. Hatuwezi kutegemea mwanamke mwenye umri mkubwa na hasa katika uzee wake kuwepo uwezekano wa kumpata mtoto. Maandiko Matakatifu yanatuambia kwamba Sara alikwisha fikia kikomo katika desturi ya wanawake. Habari kama hii inakuwa kichekesho kwa Ibrahimu ambaye alikuwa na umri wa miaka mia, Mwa 17:17. Hapa ilimaanisha kwamba kwa hali ya kawaida, ilikuwa vigumu kupata mtoto. Hivyo jambo hili kwa Sara mwenye umri wa miaka tisini ni kama kichekesho fulani. Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee?” Mwa 18:12. Pamoja na kihoja hiki, Mungu anasimama na kuonyesha Ukuu na Umungu wake pale mitazamo yetu, desturi zetu, na uwezo wa akili zetu unapofikia kikomo chake. Huyu ndiye Mungu!

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu wetu siyo wa kushindwa hata mara moja. Mungu wetu ni mweza wa mambo yote, na huyafanya mambo hayo si tu kwa kuonyesha Ukuu wake, bali ndivyo ilivyo asili yake. Kama yeye ndiye mwanzo na mwisho-‘alfa na omego’ ni kitu gani chini ya jua kitamshinda? Kama uwepo wetu leo na sasa ni kwa sababu yake, je, atashindwaje kuyarekebisha maisha na mfumo wetu? Hivyo Mungu anasimama katika ukweli huu na kumwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda Bwana? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:13-14. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Tunapoitafakari habari hii ya Ibrahimu na mkewe Sara inatupelea karibu zaidi kuelewa maneno haya ya Yesu kwa Martha, kwamba, “Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa,” Lk 10:42. Kitu hicho ni ‘kujisalimisha’ moja kwa moja bila kujibakiza katika mikono sala ya Mungu.

Biblia iko wazi kabisa kuhusu unavyoweza kufaidika unapojisalimisha kikamilifu kwa Mungu. Kwanza, unapata amani: “Acha kugombana na Mungu! Ukikubaliana naye, utapata amani hatimaye, na mambo yatakunyookea.” Ayu 22:21. Pili, unapata uhuru: “jitoeni nafsi zenu kuzifuata njia za Mungu na uhuru hautatoka kamwe….Amri zake zinawaweka huru kuishi kwa uwazi katika uhuru wake!” Rum. 6:17
Tatu, unapata nguvu za Mungu katika maisha yako. Majaribu makali na matatizo mazito yanaweza kushindwa na Kristo kama atakabidhiwa. Joshua alipoviendea vita vile vikubwa maishani mwake, Yosh. 5:13-15 alikutana na Mungu, akamsujudia, na akasalimisha mipango yake. Kujisalimisha huko kulileta ushindi mkubwa pale Yeriko.

Hiki ni kitendawili: Ushindi huja kwa kujisalimisha, kujisalimisha hakukudhoofishi wewe; kunakutia nguvu. Jisalimishe kwa Mungu, hauhitaji kuogopa au kujisalimisha kwa chochote kile. William Booth, wanzilishi wa Jeshi la wokovu, alisema, “ukuu wa nguvu za ubinadamu unapimwa kwa kiwango chake cha kujisalimisha.”

Watu waliojisalimisha ndio Mungu anaowatumia. Mungu alimchagua Mariamu kuwa mama wa Yesu, siyo wa sababu alikuwa na kipawa, au utajiri au uzuri wa umbile, lakini kwa sababu alikuwa amejitoa kikamilifu kwake. Malaika wa Bwana alipomwelezea mpango mgumu wa Mungu, alijibu kwa upole, “mimi ni mjakazi wa Bwana, na niko tayari kupokea chochote anachotaka.”Lk. 1:38 Hakuna kitu kikubwa kama maisha ya kujisalimisha katika mikono ya Mungu. “Hivyo zikabidhini nafsi zenu kikamilifu katika mikono ya Mungu.” Yak. 4:7a

Katika somo la Injili ya leo, Mariamu ndugu yake Martha anajielewa na kumfahamu yule anayemtumikia aliye kweli katika yote, na mwisho anajisalimisha kwake. Yawezekana mimi na wewe tumeyapa maisha yetu kipaumbele chake cha kwanza katika kujishughulisha katika mambo mengi yasiyo na mwelekeo. Maisha yetu hayajengwi kwa wingi wa vitu tunavyofanya, bali uelewa wa yale tunayoyafanya, na kwa nini tunafanya kama tunavyoyafanya. Martha kama tulivyo wengi, anajilinganisha na yale anayofanya na kukosa muda wa kujua chanzo ya yale yote anayoyafanya na kwa nini anayafanya kwa namna hiyo, na ni nani anayeyaratibisha. Martha anamlalamikia Yesu kwa nini Mariamu ndugu yake hamsaidii. Yesu anamkumbusha Martha jambo la muhimu na kusema, “Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi,” Lk 10:41. Furaha yetu haitokani na wingi wa vitu tuvifanyavyo. Tuyafanyayo yakikosa sababu na malengo yake husika, ni wazi kwayo kama yalivyo hayawezi kuwa sababu ya furaha yetu. Kujishughulisha huku katika maana ya kufanya hivyo tu, kutakuletea mfadhaiko mkubwa sana pale mambo hayo yatakapo kwenda ndivyo sivyo.

Maisha yetu yana maana kwanza kabisa tunapojitambua na mwisho kujisalimisha muda wote kwa Yule aliye sababu ya ishi yetu na atupaye uzima wa milele. Huyu ndiye chanzo cha furaha yetu na umilele wa maisha yetu. Kwake yatupasa kutumia muda mwingi naye. Huyu ndiye Kristo; njia, ukweli, na uzima wetu, Yoh 14:6. Kuwa na Kristo ni kuchagua fungu lililo jema ambalo kwalo hatuwezi ondolewa. Ukweli huu ndio Yesu anaomwambia Martha na sisi leo kwamba pamoja na yote tuyafanyayo, lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa,” Lk 10:42. Kukaa chini ya miguu ya Yesu ni ule utayari wa kulishwa neno la uzima, na kujazwa ufahamu na kufunuliwa siri ya uzima wa milele.

Kujisalimisha ndani na katika Kristo Yesu hukupa maana ya maisha yako. Mtume Paulo anathibitisha kweli hiyo kwa kusema,Sasa nayafurahia mateso niliyo nayo kwa ajili yenu; tena nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua ya mateso ya Kristo, kwa ajili ya mwili wake, yaani, Kanisa lake,” Kol 1:24. Kristo ndiye uzima ule uupiganiao kila siku. Na hii ndiyo siri iliyofIchwa kwa wamchao Mungu, yaani Watakatifu wake. Nisiri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake,” Kol 1:26. Na kwa siri hii, Mtume Paulo amefanywa  ‘mhudumu wake, sawasawa na uwakili wa Mungu, aliyopewa kwa faida watu, akilitimize neno la Mungu,’ Kol 1:25. Ndugu yangu, Kristo ndiyo njia ile sahihi unayoitafuta kila siku na mara nyingine kupotea kabisa. Na Kristo ndiye kweli yenyewe kwa sababu ndiye ufunuo wa kweli ya Mungu Baba. Ni katika kweli hii ambayo Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa Utukufu wa siri hii katika Mataifa, nao ni Kristo ndani yenu, tumaini la Utukufu,” Kol 1:27. Kumbe wito wako na wangu kama wabatizwa na wafuasi wa Kristo walio hai kama asemavyo Mtume Paulo ni kuhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo,” Kol 1:28. Na huu ndio ushuhuda wa kweli.
Wapendwa wana wa Mungu, hatutaweza kutoa ushuhuda huu wa Mungu kama hatupo tayari kulishirikisha kwa ukarimu neno la Mungu. Ushirikishaji huu wa Neno la Mungu kwa ukarimu tumeona leo ukifanyika kwa vitendo kutoka kwa Ibrahimu kwa wale watu watatu wageni, kutoka kwa Mariamu kwa kujisalimisha chini ya miguu ya Yesu, na kutoka kwa Mtume Paulo kwa kujitoa bila kujibakiza kwa Kanisa la Kristo na watu wake. Hata hivyo tutaweza tu kulishirikisha neno la Mungu kwa ukarimu kama tutaweza kulitafakari kwa kina Neno la Mungu. Kulitafakari kwa kina neno la Mungu kunahitaji utayari bila shuruti wa kulipokea Neno la Mungu. Na tutaweza kulipokea Neno la Mungu bila shuruti pale tu tutakapokuwa tayari kulisikia Neno la Mungu.

Familia ya Mzee Rajabu inatoka Kigango cha Kona Mbili. Familia hii ni ya kawaida kabisa lakini iliyojaa upendo na hofu ya Mungu. Kigango cha Kona Mbili kilikuwa na adhimisho la mwezi mzima kuutembeza Msalaba Mtakatifu.  Maandamano haya ya Msalaba Mtakatifu kila siku yalianza majira ya saa tisa alasiri ili kuwapa nafasi hata wale waliokuwa wameajiriwa kushiriki zoezi hili Takatifu. Na ilipofika saa mbili usiku Msalaba ulikesha kwenye mji wa mwaamini yeyote aliyetayari kufanya hivyo. Watu waliweza tena kupata nafasi ya kusali, kutafakari Neno la Mungu, na kuimba usiku kucha.

Siku moja ya alhamisi ilipofika saa mbili usiku ikiwa ni karibu na Familia ya Mzee Rajabu ambaye alikuwa safarini kwa siku saba, na siku hiyo ndiyo alikuwa ana rudi nyumbani, kulikuwa na ‘ukimya’ mkuwa wa nani atakaye uchukuwa Msalaba ule ukalale kwake hadi kesho. Hofu haikuwa kuuogopa Msalaba Mtakatifu, bali ni utayari katika maana ya ‘ukarimu wa wana familia’ husika kwa usiku ule ikiwa ni pamoja na kuwapatia watu maji na chai. Ndipo bila kusita Mke wa Mzee Rajabu aliomba Msalaba ule ulale kwenye familia yao. Kwenye mkusanyiko ule wa watu, wengine walisikia wakiguna kwa sababu waliijua familia ile katika umasikini wao. Hata hivyo wanafamilia ile wengine waliwahi nyumbani haraka na kuandaa mazingira ya watu kukaa na sehemu ya kuuweka Msalaba ule hadi asubuhi.

Kasukari kalichokuwepo chote kalitumia, na ajabu wote waliokuwa nyumbani pale walipata chai. Na ilipofika saa nne za usiku, Mzee Rajabu aliingia na boda boda akiwa na vifurushi vyake vya heshima. Mzee Rajabu akiwa anashangaa umati wa watu nyumbani mwake wakiimba kwa furaha, Mke wake alipigwa na butwaa kuona mme wake kuja na  mfuko wa sukari wa kilo 25. Haikuwahi kutokea katika familia hiyo. Mambo yalienda vizuri hadi asubuhi. Watu walifurahi sana na kila mtu alisema yake.

Ndipo Mama Rajabu alipotaka kujua ukweli wa ile Sukari kutoka kwa mme wake. “Hata mimi sijui nikuambiaje mke wangu. Kwa ufupi ni kwamba nilikutana na Mtani wangu ambaye tulikuwa tunafanya kazi kampuni moja na sasa yupo kampuni moja ya usafirishaji wa Sukari. Kwa furaha aliyokuwa nayo kwa jinsi nilivyomsaidia kwenye msiba wa mwanaye, akanipa sukari hiyo na kuniambia ‘ndugu yangu na Mtani wangu, kapate chai na watoto wangu,’ na nasema asante kwa ukarimu wako. Hivyo ndivyo ilivyokuwa. Maajabu!” Kwa furaha mke wake akamjibu, “Kwa kweli ni maajabu, sifa na shukrani kwake yeye ajuaye maisha yetu. Amina.”

Tumsifu Yesu Kristo!

Siri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake,” Kol 1:26


Tusali:-Ee Yesu tukirimie moyo wa utayari na ukarimu kujitoa bila kujibakiza na hasa tunapojisalimisha kwako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario