JUMANNE
WIKI YA 14 YA MWAKA-C
Somo: Hos 8:4-7, 11-13
Zab: 115: 3-4, 5-6, 7-8, 9-10
Injili: Mt 9:32-38
Nukuu:
“Wamesimamisha
wafalme, lakini si kwa shauri langu; wamejifanyia wakuu, lakini nalikuwa sina
habari; kwa fedha yao na dhahabu yao wamejifanyizia sanamu, kusudi wakatiliwe
mbali,” Hos 8:4
“Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani; nafaka
haina bua; machipuko yake hayatoi masuke; hata ikiwa yatoa, wageni watayameza,”
Hos 8:7
“Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni
mengi, lakini watenda kazi ni wachache,” Mt 9:37
“Basi
mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Mt 9:38
TAFAKARI: “Nia ovu haziwezi kuhalalisha lengo jema. Mungu hafananishwi na uovu.”
Wapendwa wana wa Mungu, ‘nia ovu haiwezi kamwe kusadifu lengo jema.
Mungu wetu hafananishwi na uovu.’ Bila shaka kwa matakwa na matarajio yetu
binafsi na kwa makundi yetu kiitikadi tungependa kumchonga Mungu kama
tunavyotaka awe. Ila ukweli ni kwamba, hatuwezi kumbeba Mungu katika mikomo
yetu na ubinadamu wetu. Hatuna uwezo huo wa kumshikilia ndani na katika
ubinadamu wetu. Aliyetuumba kwa sura na mfano wake anatujua vizuri kuliko sisi
tumjuavyo. Tangu lini kwa mfano, mashine ikawa na uwezo kuzidi ya yule
aliyeibuni na kuitengeneza? Ni ajabu!
Hivyo kufuru hujijenga pale tunapoyalazimisha yale ambayo hata kwa
uwezo wetu na mikomo yetu ni vigumu kufanyika. Huu ndio ujumbe wa Mungu kupitia
mtumishi wake Nabii Hosea, “Wamesimamisha
wafalme, lakini si kwa shauri langu; wamejifanyia wakuu, lakini nalikuwa sina
habari; kwa fedha yao na dhahabu yao wamejifanyizia sanamu, kusudi wakatiliwe
mbali,” Hos 8:4. Yote haya yamefanyika ili kukidhi matamanio ya watu, au kundi
la watu ambalo halitaki kuukubali ukweli wa mambo kama ulivyo. Mfano halisi ni huu: Nchi nyingi za Bara
letu la Afrika, na Tanzania ikiwepo “huwa tunafanya uchaguzi wa kidemokrasia,
kuruhusu uwepo wa vyama vingi, katika maana pia ya kuruhusu uwezekano wa fikra
tofauti.”
Lakini jambo la
kushangaza ni hili; “licha ya kwamba wengi huchagua fikra tofauti kama njia
mbadala ya kwenda pale tunapopatamani kwa sababu na mang’amuzi yatokanayo na
historia yetu, wapo wachache na tena wasiozidi wakati mwingine watu watano,
wanaopindisha matakwa ya walio wengi.” Mara hili linapotendeka kwa manufaa ya
kulinda kundi la watu wachache au historia ya walio na historia mbovu, halina
jina lingine zaidi ya UOVU. Kama sauti ya watu ni sauti ya Mungu, hakika Mungu
si wa kuchezewa katika mantiki hii. Na hii ndiyo maana ya maneno haya: “Maana
katika Israeli kimetokea hata na kitu hiki; fundi ndiye aliyekifanya, nacho si
mungu kamwe; naam, ndama ya Samaria itavunjika vipande vipande,” Hos 8:6.
Mateso tuyapatayo leo katika jamii siyo kusudi la kweli katika uhasilia wake,
bali ni matokeo ya tamaa ya watu wacheche waliopewa dhamana katika kundi kubwa
la watu.
Mengi
yawezekana kufanyika ili kuzima sauti za walio wengi, bali Mungu hachezewi hata
kidogo. Kifuatacho katika uovu huu uliofanywa kwa makusudi maalumu ni anguko
kubwa sana. Mtindo wa kulazimisha mambo katika bara letu la Afrika utokanao na wenye
uchu wacheche umekuwa sababu ya vifo vingi vya watu wasio na hatia. Damu hizi
hazipotei bure! Hakuna yeyote kati yetu aliyeko katika ulimwengu huu kwa bahati
mbaya hadi mwanadamu mwenzake autoe uhai wake kwa sababu tu ya kuyatetea
maslahi yake binafsi, au kundi lililomweka hapo alipo na kuwa na mamlaka hayo
maovu. Kufanya hivyo ni kupenda upepo na faida yake i waza kama asemavyo Nabii
Hosea, kwamba “Kwa
maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani; nafaka haina bua; machipuko yake
hayatoi masuke; hata ikiwa yatoa, wageni watayameza,” Hos 8:7.
Kama kile tupandacho
ndicho tukivunacho, kwa nini basi kutegemea miujiza katika uovu wetu? Yesu
anatuambia hivi; “Wapeni
watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa
hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile
kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa,” Lk 6:38. Je, tutegemee maajabu kwa lile
lililo ovu tena kukifanya huku tunajua? Mungu wetu si ‘mdoli’ wa kuchezea! Na
hii ndiyo maana ya maneno haya ya Mungu kupitia Mtumishi wake Nabii Hosea
kwamba, “Kwa kuwa Efraimu ameongeza madhabahu kwa dhambi,
madhabahu zimekuwa dhambi kwake,” Hos 8:11. Kwa maana nyingine tungesema hivi;
“kwa kuwa watawala wa watu wangu Tanzania wameongeza madhababu kwa dhambi,
madhababu hizo zimekuwa dhambi kwao.” Huu ni uovu kwa kiimaadili ufanywao na
mtu akijua na tena mwenye dhamira chanya.
Wapendwa,
kila siku tunaitwa kutenda na kuishi yale yanayompendeza Mungu. Tatizo kubwa
katika ukweli huu ni kwamba hatupo tayari kuyafanya hayo. Wazo lolote lenye
kutuhitaji kufanya kile kilicho cha pekee katika maisha yetu kinaitaji kujitoa
kusipo na kipimo. Pamoja na ukweli kwamba waitwayo ni wengi, ila wanaokubali
wito huu ni wachache. Ni wachache katika maana ya kwamba nguvu na akili zetu tuziwekazo
katika utume huu hazima majibu ya haraka na mepesi. Ndipo Yesu alipowaambia wanafunzi wake, “Mavuno ni
mengi, lakini watenda kazi ni wachache,” Mt 9:37. Sote tumeitwa kuwa watendaji
wa kazi ya Mungu bia kujibakiza. Hatuwezi kuona makusudia ya Mungu juu ya
maisha yetu yanapotea bure.
Hivyo
kila siku tunaalikwa kujitoa kwa ajili ya wito Mtakatifu. Kujitoa huku ni kuwa
na dhamira chanya ya kuiombea miito mitakatifu. Tusipolifanya jambo hili kwa
ukweli na umakini wake, yote hupotea kama moshi. “Basi mwombeni Bwana wa
mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Mt 9:38. Kama wewe ni Padre
unayefanya utume wako katika parokia, ni vyema ukayatazama kwa ukaribu makundi
haya: Kuwa na wakati ujayo mwema, unapaswa kuwa karibu sana na vijana. Kuyapata
mang’amuzi ya wakati uliopita yakupasa kuwa karibu sana na wazee. Kujua
mahangaiko ya familia ya kila siku, wewe kama mchungaji na padre yakupasa kuwa
karibu sana na wazazi. Kujua furaha ya kweli, wewe kama mchungaji mwema
yakupasa kujua furaha ya kweli iliyopo kwa watoto.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Maana
katika Israeli kimetokea hata na kitu hiki; fundi ndiye aliyekifanya, nacho si
mungu kamwe,” Hos 8:6a
Tusali:-
Ee Yesu mwema, tupe nguvu kuushinda uovu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario