martes, 12 de julio de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 15 YA MWAKA-C
Somo: Isa 26:7-9, 12, 16-17
Zab: 102:13-14ab, 15, 16-18, 19-21
Injili: Mt 11:28-30
Nukuu:
Njia yake mwenye haki ni unyofu; Wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki,” Isa 26:7 

Mtu mbaya ajapofadhiliwa, Hata hivyo hatajifunza haki; Katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu, Wala hatauona utukufu wa Bwana,” Isa 26:10 

Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29 

kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30

TAFAKARI: “Njia yake mwenye haki ni unyofu.”

Wapendwa wana wa Mungu, tuyatazamapo mazingira yetu leo na fursa azipatazo kila mmoja wetu, kutumika kumekuwa kudogo sana kuliko kufaidi na kufisadi fursa hiyo. Je, tuogelee katika wimbi hili lisilo na unyofu ndani yake? La hasha, Njia yake mwenye haki ni unyofu; Wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki,” Isa 26:7. Elewa pale ulipo wewe ni nuru na mwanga hata kama unazungukwa na giza tororo la ubatili na ufisadi. Yesu anasema hivi katika kweli hii, “ninyi ni nuru ya ulimwengu…vivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yetu aliye mbinguni. Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo!” Mt 5:14b, 16, Mt 6:22, 23b. Jambo lingine ni hili, katika mazingira ya kawaida kuna msemo huu, ‘aliye muhuni-mwenye kutembea na kila mtu katika maisha yake kamwe hawezwi kubadilishwa tu kwa siku ile ya tukio lake la kufunga ndoa.’ Hivyo, Mtu mbaya ajapofadhiliwa, Hata hivyo hatajifunza haki; Katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu, Wala hatauona utukufu wa Bwana,” Isa 26:10. Mtu huyu au kwenye hali hii anaitaji muda, na hasa utayari wa kuachana na hali hiyo.

Hata pamoja na hali na mazingira hayo, pale tunapokuwa tayari na kufanya maamuzi ya ndani na katika Kristo kutoka nafsini mwetu, vita hiyo ya nafsi inaushindi. Leo kwa yeyote yule mbatizwa na mwenye kumwamini Kristo, anapata kitulizo cha kweli ndani na katika Kristo. Ni kupitia Kristo wote twaweza kuiona nuru na kuishi katika nuru ya kweli. Hakuna jina lingine hapa dunia twaweza kuokolewa nalo nje ya jina hili, Yesu Kristo, Mdo 4:12. Yesu ndiye njia, kweli na uzima wetu, Yoh 14:6. Yesu anasema, Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Kiboko cha mahangaiko yetu kama watu waaminio na wafuasi wa Kristo ni Yesu mwenyewe. 

Mizigo yetu na taabu zake zote ni Kristo mwenyewe anayeweza kutubebea tukiwa naye. Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha,” Mt 11:28. Hakuna pumzisho la kweli nje ya Kristo. Mwongozo wa kweli katika mahangaiko yetu ni Kristo mwenyewe. Mwongozo wake ni UPENDO, na hii ndiyo nira yake. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29. Ndugu yangu kwa nini hupendi kupenda? Kwa nini humpendi huyo uliye weka mipaka naye? Je, Yesu angefanya hayo unayoyafanya leo ungekuwa wapi? Mbona bado anakupa nafasi na hilo bado haulioni katika maisha yako.

Ndugu yangu, ukipenda katika kweli yote, yote huwa mepesi. Kipimo cha kupenda kinawiana na kipimo cha kusamehe. Usipo kuwa mwepesi wa kusamehe bado hujaijua kweli ya Mungu. Katika hili Yesu anasema, kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:30. Ndugu yangu, ni mzingo upi ulio nao ni mzito ambao Yesu atashindwa kuubeba?

Tumsifu Yesu Kristo!
Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu,” Mt 11:29


Tusali:-Ee Yesu, wewe ndiye kila kitu kwangu. Amina!

No hay comentarios:

Publicar un comentario