ALHAMISI
WIKI YA 14 YA MWAKA-C
Somo: Hos 11:1-4, 8c-9
Zab: 80:2ac, 3b, 15-16
Injili: Mt 10:7-15
Nukuu:
“Naliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo;
nami nalikuwa kwao kama hao waondoao kongwa tayani mwao, nikaandika chakula
mbele yao,” Hos 11:4
“Moyo
wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja,” Hos 11:8d
“Sitatumia
ukali wa hasira yangu, sitarudi kumwangamiza Efraimu; kwa maana mimi ni Mungu,
si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia
ndani ya mji,” Hos 11:9
“Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni
pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 10:8
“Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo
ktika nyumba ile, au mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu,” Mt 10:14
TAFAKARI: “Mmepata bure, toeni bure.”
Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na ukweli kwamba ilimpendeza Mungu kutuumba
kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27, Mungu hakutuumba mithili ya ‘maroboti,’ bali
alituumba huru na ndivyo tulivyo. Ni kwa uhuru huu tunapoutimia vibaya tunakuwa waasi mbele ya macho
yake. Hata katika hali hiyo ya uasi, tunaweza kumrudia tena Mungu katika njia
ya toba na majuto ya kweli kwa uhuru huo huo. Ni katika hali hii ya kuwa huru
kwamba kila mmoja wetu anawajibika kwa makosa yake mbele za Mungu. Hata hivyo
kwa Sifa na Utukufu wake Mungu, yaani; Upendo, Huruma, Haki, Unyenyekevu,
Kweli, na Msamaha, hakuchoka kamwe kuturudisha pale tulipopotoka kwa kutumia
watumishi wake mbalimbali katika historia nzima ya wokovu wetu. Na hivi ndivyo
asemavyo Mungu, “Lakini nalimfundisha Efraimu kwenda kwa miguu; naliwachukua
mikononi mwangu; hawakujua ya kuwa naliwaponya,” Hos 11:3. Kwa nini Mungu
anayafanya haya yote? Bila shaka Mungu anayafanya haya yote kwa lengo hili
madhubuti, yaani, ‘katuumba ili tuishi milele.’
Hivyo
utambuapo lengo la kuumbwa kwako linakuwajibisha na kukunyenyekesha wakati huo
huo. Wajibu wetu mbele ya Mungu ni kama ifuatavyo; tumjue, tumpende,
tumtumikie, na mwisho turudi kwake na kuishi milele. Haya ambayo ni wajibu wetu wa kwanza mbele ya
Mungu siyo tokeo la nguvu zetu au juhudi zetu binafsi, bali uwezo huo umewekwa
ndani yetu na Mungu mwenyewe kwa sababu Yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza
kutupenda. Naye Yesu anatuambia, “Si
ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka
mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote
mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16. Kumbe ni jambo la msingi
sana kuujua lengo la kuumbwa kwako. Kujua lengo hii ni kuanza kuuonja upendo wa
Mungu kwako kwamba haupo ulimwenguni hapa kwa bahati mbaya. Hivi ndivyo Mungu
anavyolithibitisha jambo hili kwa wana wa Israeli, na kusema, “Naliwavuta
kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo; nami nalikuwa kwao kama hao
waondoao kongwa tayani mwao, nikaandika chakula mbele yao,” Hos 11:4. Hata pamoja na upendo huu kwa kutotambua lengo la
kuumbwa kwao, hawakuacha kutolea sadaka miungu ya Baali na kumwacha Mungu wa
kweli, Hos 10:2.
Katika hali na
mazingira haya, Mungu huyu wa kweli hakuacha kujinyenyekeza na kutoa fursa ya
sisi kumjua. Naye anasema, “Sitatumia
ukali wa hasira yangu, sitarudi kumwangamiza Efraimu; kwa maana mimi ni Mungu,
si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia
ndani ya mji,” Hos 11:9. Je, Mungu angekuwa ni hakimu wa kutoa adhabu za ‘papo
kwa papo,’ ni nani kati yetu angesalimika? Ni wazi hata mbinguni kusingekuwa na
Watakatifu. Hapa ndipo tunapoiona huruma ya Mungu. Naye anasema, “Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu
zimewaka pamoja,” Hos 11:8d. Huyu ndiye Mungu anayemtakia kila mmoja wetu
utakatifu kama yeye alivyo mtakatifu, na uzima wa milele.
Katika somo letu la Injili tunaona wosia wa Yesu
anapotuhimiza kutenda bila kujibakiza katika maisha yetu mara zote lile lililo
jema na lenye kumpendeza Mungu tukiwa kama viumbe shirikishwa pekee katika
uumbaji. “Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo;
mmepata bure, toeni bure,” Mt 10:8. Huu ni wajibu msingi kabisa. Na
tunawajibika kufanya hivyo bure kwa vile tumepewa bure. Kama wanadamu mali yetu
halali ni dhambi zetu. Hivyo, jambo la msingi la kuelewa juu ya kweli hii ni
kwamba tufanyacho ni kwa mkono wa Mungu nasi twafanya tu kama watumishi tena
wasio na faida, na tumefanya tu
yaliyotupasa kufanya, Lk 17:10. Ndugu yangu, tuyafanyavyo
mambo haya hatufanyi kwa kumpendezesha mtu, bali twayafanya kwa kutimiza wajibu
wetu na hasa kwa kufanya lile
linalompendeza Mungu. Hivyo, “Na mtu
asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au
mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu,” Mt 10:14. Kukung’uta mavumbi ya
miguu ni kutenda lililo jema na kutokutegemea shukrani yoyote. Kama wapo watakao
beza tendo hili la wema, adhabu yake ni hapa hapa duniani. Mfano wa adhabu hayo
ni kama asemavyo Yesu, kwamba, “itakuwa rahisi nchi ya Sodoma na Gomora
kustahimili adhabu ya siku ya hukumu, kuliko mji ule,” Mt 10:15
Ndugu yangu, usipompa
Mungu nafasi ya kwanza katika maisha yako chochote kile chaweza kuyaongoza
maisha yako, na mwisho wake ukawa mbaya kwa sababu kitu hicho kama kilivyo
hakina umilele. Maadili ya Mbatizwa yeyote yule ni kuwahubiria watu habari
njema ya wokovu na ufalme wa Mungu. Yesu anasisitiza jambo hili na kusema, “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme
wa mbinguni umekaribia,” Mt 10:7. Na kama lengo la kuumbwa kwetu, tumeumbwa
tuishi milele, na duniani hapa siyo makao yetu ya kudumu. Tupo hapa kwa
maandalizi tu huku tukijua maisha ya hapa duniani ni jukumu la muda mfupi. Kila
mmoja kadiri ya wito na karama zake, yampasa kutumia vyema karama hizo. Kwa
namna hiyo Yesu anatoa wito na kusema, “Pozeni
wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni
bure,” Mt 10:8. Kama ilivyokuwa wajibu
ule msingi, yaani viumbe shirikishwa pekee katika uumbaji, hapa msisitizo upo
katika matumizi sahihi ya karama na vipaji alivyotujalia Mungu. Pamoja na
wajibu huu, Yesu anatoa angalizo pia kuhusu tatizo la kushikamana na mali za
dunia hii. “Msichukue
dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu
mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake,” Mt
10:9-10. Kuambatana na mambo haya na kuyapa nafasi ya kwanza upunguza hari na
kasi ya kuyatimiza yale tupasayo kufanya.
Ni
vyema pia tukawa waangalifu kwa wale watukaribishao na kutupatia ukarimu wao na
hifadhi. Maisha ya kutangatanga pasipo mwelekeo sahihi ni hatari sana kwa
uchungaji na umisionari kwa ujumla wake. Hivyo “Na
mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu
mwaminifu; mkae kwake hata mtakapotoka,” Mt 10:11. Ni vyema kufanya kile
kilichokupeleka pale, na fanya hicho tu. “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu
na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi,” Mt
10:12-13. Tatizo kubwa hutokea pale tunapobadili nia na sababu ya kuwa pale
tulipopaswa kuwa. Tatizo hili ni sawa na “kubadili gia angani ilihali hujui
utaangukia wapi kwa maamuzi hayo.”
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Msichukue
dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu
mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake,” Mt
10:9-10
Tusali:-Ee
Bwana tufanya mara zote vyombo vya kuyatimiza mapenzi yako na siyo yetu, hata
pale itakapotubidi kutoa sadaka kubwa. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario