SIKUKUU YA MTAKATIFU YAKOBO MTUME
25/7
25/7
Somo:
2Kor 4:7-15
Zab:
126:1bc-2ab, 2cd-3, 4-5, 6
Injili:
Mt 20:20-28
Nukuu:
“Pande
zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa
chini, bali hatuangamizwi; siku
zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao
udhihirishwe katika miili yetu,” 2Kor 4:8-10
“Kwa
maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa
Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti,” 2Kor 4:11
“Akamwambia,
Wataka nini? Akamwambia, Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono
wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako,” Mt 20:21
“Yesu
akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea
mimi? Wakamwambia, Twaweza,” Mt 20:22
“Akawaambia,
Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono
wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba
yangu,” Mt 20:23
TAFAKARI:
“Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya
Mungu, wala si kutoka kwetu.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Mtakatifu Yakobo Mtume.
Mtume Yakobo kama walivyo kuwa Mitume wengine, alikuwa kielelezo halisi cha
upendo wa Kristo na mfano wake hasa katika kuisimamia na kuitetea imani ya
kweli bila kujibakiza na kuwa na hofu yoyote ile. Mtume huyu alisimama imara
hata pale ilipompasa kufa kwa ajili ya kweli, na imani ya kweli. Msingi wa
Kanisa ukiwa ndiye Kristo mwenyewe, Mtume Yakobo kama walivyokuwa Mitume
wengine ndizo nguzo za Kanisa la Kristo. Hili liliwezekana kwa Mitume pale
walipojichukulia kuwa hazina katika vyombo vya udongo, ili adama kuu ya uwezo
iwe ya Mungu, wala si kutoka kwao.
Hivyo
leo kwa namna ya pekee masomo yetu mawili yanamlenga mwanadamu katika uwezo
wake na mapungufu yake. Uwezo wa binadamu utiwa nguvu na kusimama imara endapo
kutakuwa na muunganiko wa kweli na wa haki kati yake na Muumba wake. Muunganiko
huu msingi wake mkubwa ni kujitambua kwake huyu mwanadamu kunakolenga kuweka
wazi mafanikio yake, na udhaifu wake. Msingi huu unawezekana kujengwa tu pale
ambako binadamu huyu atakubali kujinyenyekeza. Hivyo unapojinyenyeza unafungua
ufahamu mwingine wa kujiona kama ulivyo, na si kama watu wasemavyo ulivyo, au
mazingira yako unayoishi yanavyokuelekeza na kukutafsiri. Huku ndiko kujitambua
kama “u chombo cha udongo.”
Ndugu
yangu, ni pale tu unapojitambua kama u chombo cha udongo ndipo zile hazina
zilizojificha, mathalani vipaji vyako hujidhihirisha. Ni wakati wa kuishi kile
ulicho katika ukweli wake. Tulio wengi hatuishi kile tulicho, bali twaishi
vivuli vya wengine. Tunajivika vinyago vya wengine na mwisho wa siku tunabakia
kuwa vituko tu. Moja ya sababu kubwa ya watu wengi kutokuwa na furaha ya kweli
ndani yao ni kwamba hawajawahi kuishi kile walicho hata mara moja. Hupenda kuwa
kama mtu fulani muda wote. Unapoikataa nafsi yako, unajikataa wewe mwenyewe.
Je, ni kwa namna gani unaweza kuwa na furaha ya kweli katika mazingira kama
hayo? Ni lini basi utavijua vipaji na karama zako kama hukuwahi kuwa kile
alichokuumba Mungu? Utawezaje basi kuvithamini vipaji vya wengine kama vyako
huvijui? Hivyo, Mtume Paulo anatukumbusha jambo hili, na kusema, “Lakini tuna hazina hii
katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka
kwetu,” 2Kor 4:7
Ni
katika kujiona kama vyombo vya udongo twaweza kuyakabili yote katika maisha na
kuyachukulia bila woga kwa sababu tunajua anayetuimarisha na kutupa nguvu, ni
Kristo mwenyewe. Ni kwa sababu hii kwamba, “Siku
zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao
udhihirishwe katika miili yetu,” 2Kor 4:10. Hatuna hofu ya kufa wala kupata
mateso kwa sababu mwenye nguvu na mamlaka ya mwili na roho ni Mungu mwenyewe,
na kwa hali ya kibinadamu twa mtazama Kristo, neno aliyefanyika mwili na kukaa
kwetu. Hivyo Yesu anatutia nguvu na kutufanya imara kwa neno hili, “msiwaogope
wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye
kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum,” Mt 10:28. Nani kama Mungu? Wapo
wengi sana leo tunaishi kwa hofu, tena wakati mwingine hofu ya kurogwa na tunapoteza
wakati mwingi kuhangaika kwa waganga na kupoteza rasilimali nyingi sana kupitia
mlango huu wa shetani. Je, lipi lililo la heshima na baraka kwako; kufa
mikononi mwa Kristo, au kufa mikononi mwa mganga wa kienyeji? Mtume Paulo
anasema, “kwa maana sisi tulio hai, siku
zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe
katika miili yetu ipatikanayo na mauti,” 2Kor 4:11. Hii ndiyo heshima kubwa kwa
Mkristo na mfuasi wa Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu,
ndani na katika Kristo ndiko kwenye uhakika wa kweli kwa sababu pamoja na
kuyaonja mauti, Kristo yu hai milele. Je, hizo hirizi unazozivaa, na hayo
mazindiko uliyochimbia kwenye kuta za nyumba yako yanausalama zaidi ya usalama
ndani na katika Kristo? Ndugu yangu, “tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana
Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi,” 2Kor
4:14. Uzima wa kweli upo kwa Kristo tu, na si vinginevyo. Ni vyema kuanzia leo
ukafuta kabisa ziara zako hizo rasmi na zisizo rasmi kwa waganga wa kienyeji. Safari
hizo sinakukosesha neema na uzima wa Mungu na kujichumia wingi wa laama.
Injili yetu ya leo
inalizungumzia kwa mapana swala hili la kujitoa na kutumika kwa ajili ya ufalme
wa Mungu, na ndiyo sababu ya Ukristo wetu, na utambulisho wetu mbele ya Mungu. Utambulisho
wetu mbele ya Mungu hautokani na sababu ya kukaa kushoto kwake au kulia kwake,
bali ni kwa namna gani naishi kwa uaminifu na bila kujibakiza katika mapaswa
yake kile alichoniita leo na sasa. Tukiwa waaminifu katika hilo, Yesu anasema,
“kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali
watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu,” Mt 20:23b. Waliowekewa tayari kwa
maanisha wale walioyafanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu. Swala hili halipo
mwishoni mwa maisha yetu kama kupokea tunzo fulani, bali kila siku ya maisha
yetu twaishi tunzo hiyo, au kupokonywa tunzo hiyo. Kila siku ya maisha yetu
tupo darasani, na mtihani wetu ni
UPENDO. Upendo ndiyo mizania ya kila kitu tufanyacho.
Ndugu yangu
tunayesafiri pamoja katika tafakari hii, UTAMBULISHO wetu mbele ya Mungu, si
maisha ninayoishi, mfano; Maisha ya ndoa, Utawa, na Ukleri, au cho chote kile
ninachoishi kadiri ya wito wa Mungu, bali utambulisho wetu ni kwa namna gani
tunavyotumika kwa kuyatoa maisha yetu bila kujibakiza kwa upendo wake Mungu kwa
kile tulichoitiwa, na Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo kuwa kielelezo chetu. Bila
hivyo, maisha unayoishi au ninayoyaishi huwa ni maigizo tu. Utambulisho huu kwa
maana nyingine ni UTAKATIFU tunaojichotea kwa maisha tunayoyaishi hapa duniani
kila mmoja kadiri ya wito wake. UTAMBULISHO huu ndiyo tunzo na UTAKATIFU wetu
mbele ya Mungu. Na kwa mantiki hii ndiyo sababu leo Mama Kanisa kwa heshima
kubwa anaadhimisha Sikukuu ya Mtakatifu Yakobo Mtume, aliyeishi upendo wa
Kristo bila kujibakiza, na kuyatoa maisha yake kwa ushuhuda wa kweli hiyo kwa
watu wote.
Ndugu yangu, kwa Mungu
hatuendi na “CV” zetu, kama tulivyozoea kusikua historia fupi ya Marehemu. Huko
Mbinguni hakuna kazi tena zaidi ya kuishi umelele tulioandaliwa, au kuteseka
katika umilele tuliojiandalia kwa kuishi ndivyo sivyo. Vyeti vyako, na historia
yako kitaaluma ikuwezeshe kuupata utakatifu huo kwa kutumika vyema leo na sasa.
Kielelezo chetu kama wafuasi wa Kristo, ni Kristo Yesu Mwenyewe.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini kuketi mkono wangu wa kuume
na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari
na Baba yangu,” Mt 20:23
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tufanye vyombo vyako vya udongo, na katika udogo wetu tujitoe bila
kujibakiza. Amina
Mtakatikfu Yakobo Mtume, Utuombee.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario